ZAKAATUL FITRI. 1

HIKMA YAKE. 1

NANI MWENYE KUITOA?. 2

KIASI CHAKE. 2

WAKATI WA KUITOWA.. 2

KUITANGULIZA KABLA YA WAKATI WAKE. 2

 

ZAKAATUL FITRI

 

Kila aliyefunga Mwezi wa Ramadhaan na akawa anamiliki chakula cha kumtosha kwa muda wa siku moja, inamwajibikia kutoa Zakaatul Fitri, nayo ni pishi ya tende au pishi ya ngano au pishi ya shaiyri. Anatakiwa atoe kwa ajili yake na kwa ajili ya kila anayemtegemea kama vile wanawe, wakeze nk. na kuwapa masikini ili nao wapate kufurahi katika Siku ya Sikukuu.

Kwa vipimo vya kisasa, pishi moja ya mbao iliyokuwa ikitumika wakati wa Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) ni kiasi cha kilo 2.

Zakaa hii ni wajibu kwa kila Muislam mdogo na mkubwa, mwanamume au mwanamke.

 

Ibn ‘Umar  (Radhiya Llaahu ‘anhu) amesema:

"Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) amefaridhisha kwa kila mtu kutoa Zakaatul Fitri katika mwezi wa Ramadhaan, pishi ya tende (au) pishi ya shaiyri, ikiwa yeye ni mtumwa au mtu aliye huru, mwanamume au mwanamke, mdogo au mkubwa miongoni mwa Waislam".

[Al-Bukhaariy na Muslim]

Rudi juu

HIKMA YAKE

Zakaatul Fitri ilifaridhishwa katika mwezi wa Sha’abaan mwaka wa pili baada ya Hijra kwa ajili ya kumtwaharisha aliyefunga kutokana na makosa yoyote yale aliyotenda katika mwezi wa Ramadhaan pale alipokuwa amefunga, kutokana na mazungumzo ya upuuzi au madhambi, na wakati huo huo Zakaah hiyo itawafaa masikini na wahitaji ili nao wapate kufurahi pamoja na Waislam wenzao katika Sikukuu.

 

Ibn ‘Abbaas  (Radhiya Llaahu ‘anhu) amesema:

"Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) amefaridhisha Zakaatul Fitri kwa ajili ya kumtwaharisha aliyefunga kutokana na maneno ya upuuzi au madhambi madogo madogo na ili masikini nao wapate chakula. Atakayeitoa (Zakaah hiyo) kabla ya Swalah (ya ‘Iyd) inakubaliwa Zakaah yake, ama atakayeitoa baada ya Swalah (ya ‘Iyd), itahesabiwa kama ni Swadaqah ya kawaida tu".

Abu Daawuud na Ibn Maajah na Ad-Daaraqutniy

Rudi juu

NANI MWENYE KUITOA?

Anayeitoa Zakaah hiyo ni mtu aliyefunga. Anajitolea yeye mwenyewe, mkewe na watoto wake wanaomtegemea na anawatolea pia wote wale wanaomtegemea wakiwemo watumishi wake.

Rudi juu

 

KIASI CHAKE

Iliyowajibishwa katika Zakaatul Fitri ni pishi ya ngano au ya shaiyri au ya tende au ya zabibu au ya mchele au ya mahindi na vinginevyo vilivyo na mfano huo katika vyakula.

Imaam Abu Haniyfah peke yake amejuzisha kutoa pesa zenye thamani hiyo badala ya kutoa nafaka panapo udhuru.

 

WAKATI WA KUITOA

Ma’ulamaa wengi wamekubaliana kuwa Zakaatul Fitri itolewe katika Ramadhaan ya mwisho, lakini wamekhitalifiana juu ya wakati maalum unaowajibika kuitoa.

Wapo waliosema kuwa wakati unaowajibika kuitoa ni pale jua la Ramadhaan ya mwisho linapozama, na wengine wakasema kuwa wakati wake ni kuanzia baada ya kuingia alfajiri ya siku ya Sikukuu.

 

Kutokana na hitilafu hii tunapata faida ya kuwajibika kumtolea Zakaah hiyo mtoto aliyezaliwa kabla ya kuingia alfajiri ya siku ya Sikukuu na baada ya jua kuzama, je mtoto huyo anatolewa Zakaah?

 

Kwa wale wenye kufuata rai kuwa wakati wa kuitoa Zakaah hiyo ni pale jua la siku ya Ramadhaan ya mwisho kuzama, mtoto huyo hatolewi Zakaah kwa sababu amezaliwa baada ya kumalizika wakati wa kuwajibika, na kwa wenye kufuata rai ya pili, kwa sababu amezaliwa kabla ya wakati unaomwajibika.

Rudi juu

 

KUITANGULIZA KABLA YA WAKATI WAKE

Ma’ulamaa wengi wanakubali kuwa Zakaatul Fitri inaweza kutangulizwa na kutolewa kabla ya wakati wake kwa siku moja au mbili.

 

Hadiyth iliyopokelewa kutoka kwa Ibn ‘Umar  (Radhiya Llaahu ‘anhu) inasema;

"Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) ametuamrisha kuitoa Zakaatul Fitri kabla ya watu kutoka Msikitini (katika Swalah ya ‘Iyd)".

 

Anasema Nafi’  (Radhiya Llaahu ‘anhu):

"Ibn ‘Umar  (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa akiitoa kwa siku moja au siku mbili kabla ya Siku ya Sikukuu".

Ama zaidi ya hapo, Ma’ulamaa wamekhitalifiana.

Imaam Abu Haniyfah amesema:

"Inaweza kutolewa wakati wowote ule katika mwezi wa Ramadhaan".

Imaam Ash-Shaafi’iy amesema:

"Inajuzu kuitoa (hata) katika siku za mwanzo za mwezi wa Ramadhaan".

Imaam Maalik amesema:

"Inajuzu kutanguliza kwa siku moja au mbili kabla ya Sikukuu."

Lakini Ma’ulamaa wote wamekubalina kuwa haijuzu kuiahirisha na kuitoa baada ya ‘Iyd.