Subhaanallah

 

Imekusanywa na kutafsiriwa na Muhammad Faraj Salem Al Saiy

 

 

Tunapotufu, tunaizunguka Al Kaaba kuanzia jiwe jeusi tukiliwacha upande wetu wa kushoto, na maana yake ni kuwa; tunaizunguka kwa njia hiyo mara saba kinyume na mishale (mikono) ya saa (anti clockwise).

 

Wataalamu wa sayansi wanasema kuwa kila chembe ya atomi (atom), ambazo ni viduchu vya kila kitu, ndani yake mna electrons, protons na neutrons. Electron iliyomo ndani ya atom, nayo pia inazunguka kinyume na inavyozunguka mishale ya saa (anti clockwise). Mzunguko ule ule tunaozunguka sisi tunapotufu Al Kaaba.

 

Sayari, kama vile Ardhi (Earth), Mercury, Venus, Jupiter n.k. zinajizunguka zenyewe mzunguko ule ule kama tunavyoizunguka Al Kaaba kinyume na inavyozunguka mishale ya saa. Wakati huo huo sayari hizo zinalizunguka jua kwa mzunguko huo huo wa kinyume na inavyozunguka mishale ya saa.

 

Jua lenyewe nalo linajizunguka mzunguko huo huo kama tunavyoizunguka sisi Al Kaaba, na haya yanatokea katika sayari zote ulimwenguni.

Kila kitu kinatii amri ya Mwenyezi Mungu na kuzunguka kama kilivyoamrishwa.

 

Dr. Mohammed Ali Albar, Mshauri wa Matibabu ya Kiislamu katika King Fahad Medical Research Center na Mwalimu katika Chuo kikuu cha Mfalme Abdul Aziz - Jeddah, na ambaye ameandika vitabu vingi vikiwemo; Aids, Drugs, Waislamu katika Urusi nk. na ambaye pia ni mjumbe mtendaji katika Halmashuri kuu ya Miujiza ya Sayansi katika Qurani, anasema:

"Mwenyezi Mungu Anasema:

إِنَّا خَلَقْنَا الاِنسَانَ مِن نُّطْفَةٍ أَمْشَاجٍ

"Kwa hakika tumemuumba mtu kutokana na mbegu ya uhai iliyochanganyika (ya mwanamume na mwanamke)."

Suratud Dahar- 2

 

"Wadudu wa mbegu ya uhai (sperms) ambayo ni maji ya uzazi ya mwanamume, mnajua kiasi gani ukubwa wake?" Aliendelea Mwanachuoni huyo , "Nyinyi mnatumia Meter katika vipimo vyenu, au Centimeter (moja katika mia), na Millimeter (moja katika elfu), lakini vidudu hivi vya uzazi kwa sababu ya udogo wake vinapimwa kwa 'Micron', yaani (moja katika milioni) na ukubwa wa kila mdudu katika hao ni Micron 5 hadi 6.

Wadudu hawa juu ya udogo wao, mara wanapoingia ndani ya tumbo la uzazi wanakwenda mbio kuelekea katika yai la mwanamke (Ovam) kwa kasi inayoshinda kasi ya bingwa wa kukimbia ulimwenguni mara mbili, iwapo itakisiwa kwa ukubwa wake mdudu huyo.

Yai hilo la mwanamke, 'Ovam', ni kubwa kuliko wadudu hao wa uzazi,  Yai ni zuri, lenye kupendeza sana, na ukubwa wake ni kiasi cha Micron 120. Juu yake pana mfano wa taji ambalo wataalamu wa uzazi wanaliita 'Taji linalongaa', linalotoka katika mfuko unaohifadhi na kuyapevusha mayai hayo huku likivutwa kuelekea penye Ovam kupitia ndani ya mirija ya Falopi (Fallopian tubes).

Mirija hiyo inalivuta yai hilo kwa nguvu za nywele nywele zilizojaa ndani ya tube hizo, huku likiingia humo pole pole, tena kwa maringo huku liking'aa ili kuwavutia wadudu hao walikimbilie.

 

Idadi ya wadudu wanaopatikana katika mchupo mmoja wa maji ya uzazi (sperms) wanakadiriwa kufikia milioni mia tatu hadi milioni mia tano, na wote hao wanalikimbilia yai hilo, na karibu wote wanakufa njiani kabla ya kulifikia, isipokuwa kiasi cha mia tano tu wanaobaki, na mwisho wao wanafika nje tu ya yai hilo.

Mara baada ya wadudu hao ambao idadi yao inakaribia mia tano wanapolifikia yai hilo, panatokea jambo la ajabu sana, jambo ambalo halijagunduliwa isipokuwa katika mwisho wa mwaka elfu moja mia tisa na sabini katika karne hii.

Yai hilo 'Ovum' linaanza kuzunguka mzunguko ule ule kama tunavyoizunguka Al Kaaba kinyume na inavyozunguka mishale ya saa, na wadudu waliobaki nao wanaanza kuzunguka mzunguko ule ule, tena mara saba, kisha mdudu mmoja tu ndiye anayeingia ndani ya yai hilo na wote waliobaki wanakufa wakiwa nje ya yai."

Dr. Mohammed Ali Albaar anaendelea kusema:

"Ipo filamu juu ya tukio hilo, niliiona na kumsikia mtangazaji wa kizungu, akipiga ukelele akisema:

"Sielewi kwa nini wadudu hawa wanalizunguka yai hili kabla ya kufa?"

 

Angalia namna gani ulivyomtukuza Mola wako kabla ya kuingia ndani ya yai lako ewe mwanadamu kabla hata hujazaliwa. Unalizunguka yai ukiwa tumboni mwa mama yako kama tunavyoizunguka Al Kaaba, tena mara saba. Kisha Mola wako anachagua mmoja tu kati ya wadudu hao, ambaye ni wewe uliyesalimika miongoni mwa mamilioni waliokuwemo humo ukaweza kuingia ndani ya yai hilo, kisha yai likafungika na wadudu wa uzazi wote waliobakia wakafa.

Kisha baadaye wanakuja wadudu wa uzazi wengine wengi, kwa mamilioni, lakini wote hao wanaishia mlangoni tu, wanakufa, haruhusiwi kuingia ndani ya yai zaidi ya mmoja tu aliyekwishatangulia kuingia".

 

سُبْحَانَ الَّذِي خَلَقَ الازْوَاجَ كُلَّهَا مِمَّا تُنبِتُ الارْضُ وَمِنْ أَنفُسِهِمْ

وَمِمَّا لَا يَعْلَمُونَ

"Ametukuka Mwenyezi Mungu ِAliyeumba dume na jike katika(vitu) vyote; katika vile ioteshavyo ardhi, na katika nafsi zao (wanadamu) na katika vile wasivyovijua".

Ya Sin - 36

 

Na katika Suratul Israa (Bani Israil) aya ya 44 Mwenyezi Mungu anasema:

تسبح له السماوات السبع والأرض ومن فيهن وإن من شيء إلا يسبح بحمده ولكن لا تفقهون تسبيحهم إنه كان حليما غفورا

"Zinamtukuza zote mbingu saba na ardhi na vilivyomo ndani yake. Na hakuna chochote ila kinamsabihi (Mwenyezi Mungu) kwa sifa Zake njema. Lakini nyinyi hamfahamu kusabihi (kutukuza) kwake. Hakika Yeye Mwenyezi Mungu ni Mpole (na) Mwingi wa kusamehe."

 

Na Akasema:

وَيُسَبِّحُ الرَّعْدُ بِحَمْدِهِ وَالْمَلاَئِكَةُ مِنْ خِيفَتِهِ وَيُرْسِلُ الصَّوَاعِقَ فَيُصِيبُ بِهَا مَن يَشَاءُ وَهُمْ يُجَادِلُونَ فِي اللّهِ وَهُوَ شَدِيدُ الْمِحَالِ

"Na radi inamsabihi Mwenyezi Mungu kwa kumshukuru na (pia) Malaika (humsabihi) kwa kumuogopa . Na (Mwenyezi Mungu) hupeleka mapigo ya radi na kumpiga nayo amtakaye.

Na hao (makafiri) wanabishana juu ya MwenyeziMungu (kuwa yuko kweli au hayuko) na hali (ya kuwa yuko na) Yeye ni Mkali wa kuadhibu".

Ar Raad -13

 

Imesimuliwa na Abi Huraira (Radhiya llahu anhu) kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wasallam) amesema:

 

"Maneno mawili mepesi ulimini na mazito katika mizani na yanapendwa sana na AlRahmani (Mwenyezi Mungu) (nayo ni):

سبحان الله وبحمده سبحان الله العظيم

"Sub haana Llah Wabihamdihi Sub haana Llahul Adhiym".

Bukhari na Muslim.