|
|
|
|
Mhammad Faraj Salem Al Saiy
Sala ya Idi imeanza kusaliwa katika mwaka wa mwanzo wa Al Hijra, mwaka ule Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alipohamia Madina akifuatana na Sahibu yake wa pangoni Al Siddique (Radhiya Llahu anhu), na hukmu yake Sala hiyo ni 'Sunnah Muakkadah'.
Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) hakupata kuiacha Sala hii na alikuwa akihimiza watu wote kwa pamoja, wanawake kwa wanaume kuisali Sala hiyo.
INAPENDEZA MTU KUKOGA, KUVAA NGUO NZURI NA KUJIPAKA MAFUTA MAZURI
Kutoka kwa Jaafar bin Muhammad, kutoka kwa babake, kutoka kwa babu yake, ameeleza kuwa;
"Siku ya
Sikukuu, Mtume (Swalla Llahu alayhi
wa sallam)
alikuwa akipenda kuivaa nguo yake
nzuri aliyoletewa kutoka Yemen"
Imam Shafi
Anasema Ibnil Qayim;
"Mtume (Swalla Llahu alayhi
wa sallam) alikuwa akiwavalisha wajukuu zake nguo
nzuri kabisa na alikuwa yeye
mwenyewe ana guo lake zuri akilivaa
kila Ijumaa na katika siku
za Sikukuu.”
KULA CHOCHOTE KABLA YA KWENDA MSIKITINI
Siku ya Sikukuu ya Idd al Fitri ni Sunnah kula tende moja au tatu au tano nk. (kwa hesabu ya witri) kabla ya kwenda kusali.. Ama katika Sikukuu ya Idd al Adh-ha, tunatakiwa tule baada ya kurudi kusali.
Anasema Anas (Radhiya Llahu anhu);
"Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alikuwa hatoki kwenda kusali mpaka kwanza ale tende, na alikuwa akila kwa hesabu ya witri. (1 au 3 au 5 nk.)".
Ahmed na Bukhari
Na kutoka kwa Bureida (Radhiya Llahu anhu) amesema;
"Mtume (Swalla
Llahu alayhi wa sallam)
alikuwa katika Sikukuu ya Idd
al Fitri hatoki mpaka ale, na katika
Idd al Adh-ha hali mpaka arudi".
Ahmed-Attirmidhy na Ibni Majah
BORA KUSALI UWANJANI
Sala ya Idi
inaweza kusaliwa ndani ya msikiti,
lakini kuisali nje penye uwanja
ni bora
zaidi, kwani Mtume (Swalla Llahu
alayhi wa sallam) alikuwa akisali Sala za
Idi zote mbili (Sikukuu kubwa na Sikukuu
ndogo) nje penye uwanja, isipokuwa
panapotokea dharura
Abu Daud, Ibni Majah na Al Hakim
KUBADILISHA NJIA
Mtu anapokwenda kusali Sala ya Idi ni vizuri abadilishe njia. Ende kwa njia nyingine na arudi kwa njia nyingine.
Imesimuliwa katika Sahih Bukhari kuwa;
"Mtume (Swalla
Llahu alayhi wa sallam)
alikuwa Siku ya Idi akenda
kusali kwa kupitia njia nyingine
na anaporudi akibadilisha njia".
Inajuzu pia kwenda na kurudi kwa njia ileile.
WAKATI WAKE
Anasema Imam Ibni Rushd al Qurtubiy;
"Sala ya
Idi inasaliwa kuanzia pale jua linapochomoza mpaka wakati wa
Zawal (jua linapokuwa utosini)."
Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alikuwa akiichelewesha kidogo Sala ya Idd al Fitri, ama Sala ya Idil al Adh ha alikuwa akisali mapema zaidi, huenda sababu ya kuichelewesha Sala ya Idd al Fitri ili watu wawahi kutoa Zakatul Fitri kabla hapajasaliwa, na akisali mapema zaidi Sala ya Idd al Adh-ha ili watu wapate kuwahi kwenda kuchinja wanyama wao.
Maulamaa wamekhitalifiana juu ya watu waliochelewa kupata habari za kuonekana kwa mwezi. Je, watasali wakati wowote pale itakapowafikia habari, hata wakizipata habari hizo wakati wa Alasiri?
Imepokelewa kuwa Mtume (Swalla Llahu
alayhi wa
sallam) aliwaamrisha watu waliochelewa kupata habari ya
kuandama kwa mwezi wasiendelee kufunga (wale), na washerehekee
Abu Daud
SIKUKUU IKIANGUKIA SIKU YA IJUMAA
Wamekhitalifiana ikiiwa Sikukuu itaangukia siku ya Ijumaa, je, inatosha watu wakisali Sala ya Idi peke yake au wanatakiwa pia wasali Sala ya Ijumaa?
Amesema Ataa;;
"Siku hiyo
haisaliwi Ijumaa wala adhuhuri, bali inasaliwa
Sala ya Idi
tu, kisha Sala ya Alasiri
pale unapoingia wakati
wake".
Ama Ibni Jariyr amesema;
"Walioruhusiwa kufanya hivyo ni watu wanaokaa mbali na miji tu, ili wasihangaike kuja mjini asubuhi kwa ajili ya kusali Sala ya Idi kisha waje tena mchana kusali Ijumaa, kama ilivyopokelewa kuwa Uthman (Radhiya Llahu anhu) aliwahutubia watu siku ya iliyosadifu Sikukuu kuwa siku ya Ijumaa akawaambia;
"Enyi watu mnaokaa sehemu
za mbali, ikwa mnataka kubaki
na kusali Ijumaa pamoja na
sisi basi bakini, ama mkitaka
kurudi makwenu mnaweza kurudi".
Malik katika 'Muwataa'.
ADHANI NA IQAMA
Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alikuwa mara baada ya kuwasili uwanja wa Sala anaanza kusalisha, na alikuwa akenda huko kwa miguu yake na wala hakuwa akipanda mnyama.
Mara anapowasili hapo, alikuwa akianza kusali bila ya Adhana wala Iqama, na wala hakuwa akisema;'Assalaatu jaamiah'.
'Hakuwa akiadhini wala hakuwa aqiqimu katika Sikukuu zote mbili'
Bukhari na Muslim
TAKBIYR KATIKA SALA YA IDI
Sala ya Idi ni raka-a mbili, na imesuniwa mtu katika raka-a ya mwanzo kukabir mara saba baada ya Takbiratul Ihram, na katika raka-a ya pili akabir mara tano na awe ananyamaza kidogo baada ya kila takbira kama alivyokuwa akifanya Mtume wetu (Swalla Llahu alayhi wa sallam).
Takbira ni Sunnah, na haibatiliki Sala mtu akiacha kwa kusahau au kwa makusudi.
Imam Al Shoukani anasema;
"Mtu akiiacha kwa kusahau
hatakiwi kusujudu Sajdatu sahau".
Wamekhitalifiana maulamaa katika kunyanyua mikono katika Takbira zote, baadhi yao wakasema hainyanyuliwi isipokuwa katika Takbiratul Ihram peke yake, ama Imam Shafi amesema kuwa inyanyuliwe mikono katika takbira zote.
KUSALI SALA YA SUNNAH KABLA YA SALA YA IDI AU BAADA YAKE
Hapana dalili yoyote ile kuwa pana Sala ya Sunnah kabla ya Sala ya Idi wala baada yake, na hakuwa Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akisali sala yoyote ile kabla ya Sala ya Idi wala baada yake, na Sahaba zake (Radhiya Llahu anhum) pia hawakuwa wakifanya hivyo.
Amesema Ibni Abbas;
"Mtume (Swalla
Llahu alayhi wa sallam)
alitoka siku ya Idi kuelekea
uwanjani akasali Raka-a mbili (za
Idi) na wala
hakusali sala yoyote ile kabla
yake wala baada yake".
Imepokelewa na maimam wote wa hadithi
Wapo baadhi ya maulamaa wanaosema kuwa ni Makruh mtu kusali Sala yoyote ile kabla au baada ya Sala ya Idi lakini hapana dalili ya kukataza kusali, muhimu isiwe katika zile nyakati zinazokatazwa mtu kusali.
HOTUBA YA IDI
Kutoa hotuba baada ya Sala ya Idi ni Sunnah, na kuisikiliza pia ni Sunnah.
Kutoka kwa Abu Said (Radhiya Llahu anhu) amesema;
"Alikuwa Mtume
(Swalla Llahu alayhi wa sallam)
katika Sikukuu ya Idi al Fitri
na Idi al Adh-ha akitoka kuelekea mahali panaposaliwa, na jambo la mwanzo analofanya mara baada ya kuwasili
hapo ni kusalisha
watu, na baada ya kutowa
salamu anawakabili watu wakiwa bado
wamekaa katika safu zao na
kuanza kuwapa mawaidha huku akiwausia
na kuwaamrisha mema, na alikuwa
katika hutoba yake akikithiri katika kusema 'Allahu Akbar', na alikuwa kama anataka
kuchaguwa ujumbe wa kwenda mahala
au kuchagua jeshi au kutoa amri yoyote
ile, basi alikuwa akifanya wakati huo kisha
anaondoka"
Anaendelea kusema Abu Said (Radhiya Llahu anhu);
"Mtume (Swalla
Llahu alayhi wa sallam) alikuwa
akeshasalisha akisema;
"Sasa nitatowa hotuba, anayetaka kubaki na abaki na anayetaka kuondoka anaweza kuondoka".
Annasai, Abu Daud na Ibni Majah.