Mhammad Faraj Salem Al Saiy

 

 

Sala ya Idi imeanza kusaliwa katika mwaka wa mwanzo wa Al Hijra, mwaka ule Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alipohamia Madina akifuatana na Sahibu yake wa pangoni Al Siddique (Radhiya Llahu anhu), na hukmu yake Sala hiyo ni 'Sunnah Muakkadah'.

Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) hakupata kuiacha Sala hii na alikuwa akihimiza watu wote kwa pamoja, wanawake kwa wanaume kuisali Sala hiyo.

 

INAPENDEZA MTU KUKOGA, KUVAA NGUO NZURI NA KUJIPAKA MAFUTA MAZURI

Kutoka kwa Jaafar bin Muhammad, kutoka kwa babake, kutoka kwa babu yake, ameeleza kuwa;

"Siku ya Sikukuu, Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alikuwa akipenda kuivaa nguo yake nzuri aliyoletewa kutoka Yemen"

Imam Shafi

Anasema Ibnil Qayim;

"Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alikuwa akiwavalisha wajukuu zake nguo nzuri kabisa na alikuwa yeye mwenyewe ana guo lake zuri akilivaa kila Ijumaa na katika siku za Sikukuu.”

 

KULA CHOCHOTE KABLA YA KWENDA MSIKITINI

Siku ya Sikukuu ya Idd al Fitri ni Sunnah kula tende moja au tatu au tano nk. (kwa hesabu ya witri) kabla ya kwenda kusali.. Ama katika Sikukuu ya Idd al Adh-ha, tunatakiwa tule baada ya kurudi kusali.

Anasema Anas (Radhiya Llahu anhu);

"Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alikuwa hatoki kwenda kusali mpaka kwanza ale tende, na alikuwa akila kwa hesabu ya witri. (1 au 3 au 5 nk.)".

Ahmed na Bukhari

Na kutoka kwa Bureida (Radhiya Llahu anhu) amesema;

"Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alikuwa katika Sikukuu ya Idd al Fitri hatoki mpaka ale, na katika Idd al Adh-ha hali mpaka arudi".

Ahmed-Attirmidhy na Ibni Majah

 

BORA KUSALI UWANJANI

Sala ya Idi inaweza kusaliwa ndani ya msikiti, lakini kuisali nje penye uwanja ni bora zaidi, kwani Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alikuwa akisali Sala za Idi zote mbili (Sikukuu kubwa na Sikukuu ndogo) nje penye uwanja, isipokuwa panapotokea dharura kama vile mvua nk.

Abu Daud, Ibni Majah na Al Hakim

 

KUBADILISHA NJIA

Mtu anapokwenda kusali Sala ya Idi ni vizuri abadilishe njia. Ende kwa njia nyingine na arudi kwa njia nyingine.

Imesimuliwa katika Sahih Bukhari kuwa;

"Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alikuwa Siku ya Idi akenda kusali kwa kupitia njia nyingine na anaporudi akibadilisha njia".

Inajuzu pia kwenda na kurudi kwa njia ileile.

 

WAKATI WAKE

Anasema Imam Ibni Rushd al Qurtubiy;

"Sala ya Idi inasaliwa kuanzia pale jua linapochomoza mpaka wakati wa Zawal (jua linapokuwa utosini)."

Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alikuwa akiichelewesha kidogo Sala ya Idd al Fitri, ama Sala ya Idil al Adh ha alikuwa akisali mapema zaidi, huenda sababu ya kuichelewesha Sala ya Idd al Fitri ili watu wawahi kutoa Zakatul Fitri kabla hapajasaliwa, na akisali mapema zaidi Sala ya Idd al Adh-ha ili watu wapate kuwahi kwenda kuchinja wanyama wao.

Maulamaa wamekhitalifiana juu ya watu waliochelewa kupata habari za kuonekana kwa mwezi. Je, watasali wakati wowote pale itakapowafikia habari, hata wakizipata habari hizo wakati wa Alasiri?

Imepokelewa kuwa Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) aliwaamrisha watu waliochelewa kupata habari ya kuandama kwa mwezi wasiendelee kufunga (wale), na washerehekee kama wenzao lakini waisali Sala hiyo siku ya pili yake wakati wa asubuhi".

Abu Daud

 

SIKUKUU IKIANGUKIA SIKU YA IJUMAA

Wamekhitalifiana ikiiwa Sikukuu itaangukia siku ya Ijumaa, je, inatosha watu wakisali Sala ya Idi peke yake au wanatakiwa pia wasali Sala ya Ijumaa?

Amesema Ataa;;

"Siku hiyo haisaliwi Ijumaa wala adhuhuri, bali inasaliwa Sala ya Idi tu, kisha Sala ya Alasiri pale unapoingia wakati wake".

Ama Ibni Jariyr amesema;

"Walioruhusiwa kufanya hivyo ni watu wanaokaa mbali na miji tu, ili wasihangaike kuja mjini asubuhi kwa ajili ya kusali Sala ya Idi kisha waje tena mchana kusali Ijumaa, kama ilivyopokelewa kuwa Uthman (Radhiya Llahu anhu) aliwahutubia watu siku ya iliyosadifu Sikukuu kuwa siku ya Ijumaa akawaambia;

"Enyi watu mnaokaa sehemu za mbali, ikwa mnataka kubaki na kusali Ijumaa pamoja na sisi basi bakini, ama mkitaka kurudi makwenu mnaweza kurudi".

Malik katika 'Muwataa'.

 

ADHANI NA IQAMA

Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alikuwa mara baada ya kuwasili uwanja wa Sala anaanza kusalisha, na alikuwa akenda huko kwa miguu yake na wala hakuwa akipanda mnyama.

Mara anapowasili hapo, alikuwa akianza kusali bila ya Adhana wala Iqama, na wala hakuwa akisema;'Assalaatu jaamiah'.

'Hakuwa akiadhini wala hakuwa aqiqimu katika Sikukuu zote mbili'

Bukhari na Muslim

 

TAKBIYR KATIKA SALA YA IDI

Sala ya Idi ni raka-a mbili, na imesuniwa mtu katika raka-a ya mwanzo kukabir mara saba baada ya Takbiratul Ihram, na katika raka-a ya pili akabir mara tano na awe ananyamaza kidogo baada ya kila takbira kama alivyokuwa akifanya Mtume wetu (Swalla Llahu alayhi wa sallam).

Takbira ni Sunnah, na haibatiliki Sala mtu akiacha kwa kusahau au kwa makusudi.

Imam Al Shoukani anasema;

"Mtu akiiacha kwa kusahau hatakiwi kusujudu Sajdatu sahau".

Wamekhitalifiana maulamaa katika kunyanyua mikono katika Takbira zote, baadhi yao wakasema hainyanyuliwi isipokuwa katika Takbiratul Ihram peke yake, ama Imam Shafi amesema kuwa inyanyuliwe mikono katika takbira zote.

 

KUSALI SALA YA SUNNAH KABLA YA SALA YA IDI AU BAADA YAKE

Hapana dalili yoyote ile kuwa pana Sala ya Sunnah kabla ya Sala ya Idi wala baada yake, na hakuwa Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akisali sala yoyote ile kabla ya Sala ya Idi wala baada yake, na Sahaba zake (Radhiya Llahu anhum) pia hawakuwa wakifanya hivyo.

Amesema Ibni Abbas;

"Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alitoka siku ya Idi kuelekea uwanjani akasali Raka-a mbili (za Idi) na wala hakusali sala yoyote ile kabla yake wala baada yake".

Imepokelewa na maimam wote wa hadithi

Wapo baadhi ya maulamaa wanaosema kuwa ni Makruh mtu kusali Sala yoyote ile kabla au baada ya Sala ya Idi lakini hapana dalili ya kukataza kusali, muhimu isiwe katika zile nyakati zinazokatazwa mtu kusali.

 

HOTUBA YA IDI

Kutoa hotuba baada ya Sala ya Idi ni Sunnah, na kuisikiliza pia ni Sunnah.

Kutoka kwa Abu Said (Radhiya Llahu anhu) amesema;

"Alikuwa Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) katika Sikukuu ya Idi al Fitri na Idi al Adh-ha akitoka kuelekea mahali panaposaliwa, na jambo la mwanzo analofanya mara baada ya kuwasili hapo ni kusalisha watu, na baada ya kutowa salamu anawakabili watu wakiwa bado wamekaa katika safu zao na kuanza kuwapa mawaidha huku akiwausia na kuwaamrisha mema, na alikuwa katika hutoba yake akikithiri katika kusema 'Allahu Akbar', na alikuwa kama anataka kuchaguwa ujumbe wa kwenda mahala au kuchagua jeshi au kutoa amri yoyote ile, basi alikuwa akifanya wakati huo kisha anaondoka"

Anaendelea kusema Abu Said (Radhiya Llahu anhu);

"Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alikuwa akeshasalisha akisema;

"Sasa nitatowa hotuba, anayetaka kubaki na abaki na anayetaka kuondoka anaweza kuondoka".

Annasai, Abu Daud na Ibni Majah.