SALATUL
GHAIB
Inajuzu mtu kumsalia maiti
asiyekuwepo, yote sawa ikiwa aliyekufa yupo nchi ya karibu au nchi ya mbali.
Mpaka lini maiti asiyekuwepo
anaweza kusaliwa?
Mtume (SAW) alimsalia Al
Najashi aliyefariki katika nchi ya uhabeshi (Ethiopia), na bila shaka
alijulishwa juu ya kifo chake kwa wahyi, kwa hivyo huenda ikawa aliarifiwa siku
ile ile aliyomsalia.
Ama yule bibi aliyefariki na
kuzikwa bila Mtume (SAW) kuarifiwa, kisha Mtume (SAW) alipokwenda makaburini
akalikuta kaburi lake likiwa bado jipya, kisha akauliza;
"Kaburi la nani
hili?"
Akajibiwa kuwa ni kaburi la Bi
Fulani, akatajiwa jina lake, kisha akasema;
"Kwa nini
msinijulishe?"
Akajibiwa;
"Ewe Mtume wa Mwenyezi
Mungu siku hiyo ulikuwa umefunga tena umelala, tukaona haina haja ya kukuhangaisha".
Kisha akawaambia;
"Msifanye hivyo. Mara
nyingine mtu yoyote akifa miongoni mwenu lazima muniarifu nipate kumsalia,
kwani Sala yangu juu yake ni rahma".
Kisha akaliendea kaburi hilo na
kumsalia.
Imam Ahmed - Annasai - Al Hakim
na Ibni Habban
Hapa pia hapakutajwa muda gani
ulipita tokea alipozikwa Bibi huyo mpaka pale aliposaliwa.
Katika kitabu cha Sahih al
Bukhari ipo hadithi inayosema kuwa Mtume (SAW) aliwasalia mashahidi waliokufa
katika vita vya Uhud baada ya kupita miaka minane tokea wazikwe.
VIPI INASALIWA?
Sala ya maiti asiyekuwepo
inasaliwa kama Sala ya maiti ya kawaida (maiti aliyekuwepo).
SHURUTI ZAKE
Shuruti zake pia ni sawa na
shuruti za Sala yoyote ya kawaida kama vile mtu kuwa na tohara pamoja na udhu,
(ametahirika katika hadathi ndogo na kubwa), kuelekea kibla, na awe amevaa nguo
za kujisitiri.
Inakhitalifiana na Sala ya kawaida katika
wakati, kwa sababu Sala ya maiti inaweza kusaliwa wakati wowote ule maiti
atakapoletwa, hata ikiwa katika zile nyakati zinazokatazwa kusali ndani yake, ingawaje
baadhi ya maulamaa kama vile Imam Ahmed na Ibn Al Mubarak wanaona kuwa haijuzu
kusaliwa pale juwa linachomoza na pale linapozama.
NGUZO ZAKE
1. Kutia nia - Nia ni kitendo cha moyoni na haina
uhusiano wowote ule na ulimi.
2. Kusali kwa kusimama kwa mwenye uwezo - Haijuzu mtu
kumsalia maiti akiwa amepanda mnyama au akiwa amekaa, ila kama hana uwezo wa
kusimama.
3. Takbira nne - Imepokelewa kutoka kwa Bukhari na
Muslim kuwa Mtume (SAW) alipomsalia Al Najashi alisoma takbira mara nne.
Anasema Sayed Sabeq katika Fiqhil Sunnah kuwa ni vizuri mtu kutonyanyua mikono
katika Sala ya maiti isipokuwa katika takbira ya mwanzo. - (Ipo khitilafu baina
ya maulamaa juu ya kunyanyua mikono katika takbira zilizobaki).
4. Na 5- Kusoma Alhamdu kimya kimya baada ya takbira ya
mwanzo na kumsalia Mtume (SAW) baada ya takbira ya pili. Imepokelewa kutoka kwa
Imam Shafi katika Musand yake na kutoka kwa Bukhari na Attirmidhiy kuwa kusoma
Alhamdu baada ya takbira ya mwanzo na kumsalia Mtume (SAW) baada ya takbira ya
pili ni katika nguzo za Sala ya maiti.
Sala ya Mtume
(SAW) inaweza kusomwa kwa sigha yoyote ile kama vile kusema (AllAhumma salliy
alaa Muhammad wa alaa aali Muhammad) au kama mtu ataisoma kwa ukamilifu;
(Allhumma
salliy alaa Muhammad wa alaa aali Muhammad kama sallayta alaa Ibrahima wa ala
aali Ibrahima wa barik ala Muhammad wa alaa aali Muhammad kama barakta ala
Ibrahima wa alaa aali Ibrahima fil aalamiyna innaka hamiydun majiyd).
Baadhi ya
maulamaa wamesema kuwa hii itakuwa bora zaidi na kwa ukamilifu zaidi ingawaje
hapana dalili ya kulazimika kuisoma kwa ukamilifu huo.
5. Dua - Mtume (SAW) amesema;
"Mnapomsalia
maiti muombeeni dua kwa ikhlasi (kwa moyo wote)".
Zipo hadithi
nyingi zinazoelezea juu ya dua mbali mbali alokuwa akiomba Mtume (SAW)
anaposalia maiti, na hapa nitaitaja mojawapo;
(Allahumma
ghfir lahu warham-hu wa afu anhu wa afihi wa akrim nuzulahu wa wassia
madkhalahu wa aghsilhu bimaain wa thaljin wa barad, wa naqihiy minal khataya
kama yunaqa thawbu l abyadh mina ddanas)
Ni vizuri pia
kuomba dua baada ya takbira ya nne. Anasema Imam Shafi kuwa ni vizuri kuomba
dua ifuatayo;
(Allahumma laa
tahrimna ajrahu wala taftinna baadahu waghfir lana walahu).
KUTOA SALAM
Wamekhitalifiana
maulamaa juu ya salam ngapi zinatolewa baada ya kusali Sala ya maiti.
Anasema Imam
Ahmed kuwa salam moja tu ndiyo Sunnah. Amma Imam Shafi, yeye anasema kuwa
zinatolewa salam mbili.
VIPI INASALIWA
Unasimama
mbele ya maiti kisha unanyanyua mikono juu na kusema: "Allahu akbar",
kisha unaweka mkono wa kulia juu ya mkono wa kushoto na kusoma suratul fatiha,
kisha unasema tena;"Allahu Akbar", kisha unamsalia Mtume (SAW) kwa
sigha iliyotangulia kutajwa, kisha unasema tena; "Allahu akbar",
kisha unamuombea dua maiti, kisha unasema tena;"Allahu akbar", kisha
unaomba tena, kisha unatoa salam.
VIPI IMAM
ANASIMAMA MBELE YA MAITI MWANAMUME AU MWANAMKE?
Imam anasimama
sawa na kichwa cha maiti mwanamume, ama akiwa maiti mwanamke, basi anasimama
katikati yake.
BORA ZIWE SAFU
TATU
Ni vizuri safu
ziwe tatu au zaidi, Mtume (SAW) amesema;
"Muislam
akifa,kisha akasaliwa na watu wanaofika safu tatu, basi anaghufiriwa (maiti
huyo)".
MUHAMMAD
FARAJ SALEM AL SAIY
KUMSALIA MAITI BAADA YA
KUZIKWA
Assalaam alaykum wa
Rahmatullahi wa Barakatuh
Inajuzu kumsalia maiti hata
baada ya kuzikwa, tena wakati wowote ule hata kama alikwishasaliwa.
Imepokelewa kuwa siku moja
Mtume (SAW) aliuliza juu ya mwanamke mmoja aitwae Ummu Mahjan (RA) aliyekuwa
akifagiafagia msikitini;
"Yuwapi bibi huyu
mbona simuoni siku hizi?"
Wakamjibu;
"Keshafariki (na
keshazikwa)".
Mtume (SAW) akasema;
"Kwa nini
msinambie?"
Akenda mpaka penye kaburi
lake akawapanga msitari Masahaba wake (RA) na kumsalia.
Hadithi hii imetolewa na
Bukhari na Muslim na Ahmed na Al Hakim na wengineo kwa njia mbali mbali.
Anasema Ibni l Qayim kuwa;
"Baadhi ya watu
wanaipinga Sunnah hii kutokana na hadithi za Mtume (SAW) inayosema;
"Msiyakalie makaburi
wala msiyaelekee pale mnaposali".
Anaendela kusema Ibni l
Qayim;
"Hadithi hii ni
sahihi, na aliyetamka maneno haya ni yule yule aliyemsalia mwanamke yule na
alikwishawahi kuwasalia wengine pia makaburini pao baada ya kuzikwa.
Hii ni kauli yake na kile
ni kitendo chake, na wala hapana mgongano baina yao, kwa sababu Sala
iliyokatazwa kusaliwa makaburini si Sala iliyosaliwa pale makaburini, kwani hii
ni Sala ya maiti inayosaliwa mahali popote pale, bali kuisali Sala ya maiti nje
ya msikiti ni bora kuliko kuisali ndani yake, na kumsalia maiti akiwa ndani ya
jeneza lake ni sawa na kumsalia akiwa kaburini mwake"
Natumai itafahamika