Pamoja Na
Bwana Mtume
(Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)
Katika Ramadhaan
Imetayarishwa
Na Muhammad Faraj Salem Al Saiy
Shukrani zote ni zake Mwenyezi Mungu Mola wa viumbe
vyote. Tunamshukuru, tunamtegemea na tunajilinda kwake kutokana na shari za
nafsi zetu na amali zetu zilizo ovu. Atakayeongozwa na Mwenyezi Mungu hapana wa
kumpotosha na atakayeachwa, hatopata wa kumuongoza.
Ninashuhudia kuwa hapana anayestahiki kuabudiwa
isipokuwa Mwenyezi Mungu na kwamba Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi
wa sallam) ni mja wake na Mtume wake na kipenzi chake. Ameutimiza Ujumbe,
ameifikisha Amana, amewanasihi Ummah na amepigana Jihadi katika njia ya
Mwenyezi Mungu kama inavyopaswa. Mola wetu zifikishe swala na salaam zetu kwa
kipenzi chako huyu Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam).
Mola wetu, warehemu wazee wetu na walimu wetu na kila
aliyekuwa sababu katika malezi na elimu yetu. Walio hai na
waliokwishatutangulia.
Mola wetu, zijaze nyoyo zetu imani na utuingizie
matumaini na utulivu ndani ya nafsi zetu. Tuenezee kheri na baraka na
masikilizano majumbani mwetu. Wahifadhi watoto wetu, tujaalie wake zetu na
watoto wetu wawe pambo la macho yetu.
Mola wetu, tutunukie ucha Mungu ili tuweze kuepukana
na kukuasi. Tujaalie tuwe watiifu wa amri zako ili tustahiki kuingia ndani ya
Pepo yako. Tumiminie matumaini ndani ya nyoyo zetu ili tuwe na nguvu za
kuyapuuza masaibu ya dunia.
Mola wetu, zipe nguvu nyoyo za wapiganao Jihadi dhidi
ya adui wako kote ulimwenguni. Ziongoze risasi zao, zielekeze shabaha zao,
zithibitishe hatua zao na uwape nusura iliyo karibu Yaa rabbil ‘aalamiyn – Aamiyn.
Mwenyezi
Mungu Anasema:
ÔóåúÑõ
ÑóãóÖóÇäó ÇáøóÐöíó ÃõäÒöáó Ýöíåö ÇáúÞõÑúÂäõ åõÏðì áøöáäøóÇÓö æóÈóíøöäóÇÊò ãøöäó
ÇáúåõÏóì æóÇáúÝõÑúÞóÇäö Ýóãóä ÔóåöÏó ãöäßõãõ ÇáÔøóåúÑó ÝóáúíóÕõãúåõ æóãóä ßóÇäó
ãóÑöíÖðÇ Ãóæú Úóáóì ÓóÝóÑò ÝóÚöÏøóÉñ ãøöäú ÃóíøóÇãò ÃõÎóÑó íõÑöíÏõ Çááøåõ
Èößõãõ ÇáúíõÓúÑó æóáÇó íõÑöíÏõ Èößõãõ ÇáúÚõÓúÑó æóáöÊõßúãöáõæÇú ÇáúÚöÏøóÉó
æóáöÊõßóÈøöÑõæÇú Çááøåó Úóáóì ãóÇ åóÏóÇßõãú æóáóÚóáøóßõãú ÊóÔúßõÑõæäó.
{{Ni
mwezi wa Ramadhaan ambao imeteremshwa katika (mwezi) huo hii Qur-aan ili iwe
uwongozi kwa watu, na hoja zilizo wazi wa uwongozi na upambanuzi. Atakayekuwa
katika mji katika huu mwezi (wa Ramadhaan) afunge. Na mwenye kuwa mgonjwa au
safarini basi (atimize) hesabu (ya siku alizowacha kufunga) katika siku
nyingine. Mwenyezi Mungu anakutakieni yaliyo mepesi wala hakutakieni yaliyo
mazito.}} [Al-Baqarah: 185]
Mwezi wa Ramadhaan ndio huo ushaingia. Mwezi wa Rahmah,
mwezi wa Barkah, mwezi wa Maghfirah, mwezi wa kuepushwa na moto wa Jahannam.
Mwenyezi Mungu ametutunukia mwezi huu kama ni zawadi
kutoka Kwake kwa ajili ya kututakasa, kuturehemu, kutughufuria madhambi yetu,
kuzinyanyua darja zetu na kuzilainisha nyoyo zetu.
Kwa ajili hii, inatupasa kuukabili ukarimu huu utokao
kwa Mola wetu Mkarimu (Subhaanahu wa Ta’ala) kwa kujitakasa na kutubu kutokana
na madhambi tuliyoyachuma miezi kumi na moja iliyopita, huku tukimuomba
atughufurie na huku tukimuahidi kutoyarudia tena madhambi hayo.
Mwenyezi Mungu Anasema:
æóÇáøóÐöíäó ÅöÐóÇ ÝóÚóáõæÇú ÝóÇÍöÔóÉð Ãóæú ÙóáóãõæÇú
ÃóäúÝõÓóåõãú ÐóßóÑõæÇú Çááøåó ÝóÇÓúÊóÛúÝóÑõæÇú áöÐõäõæÈöåöãú æóãóä íóÛúÝöÑõ
ÇáÐøõäõæÈó ÅöáÇøó Çááøåõ æóáóãú íõÕöÑøõæÇú Úóáóì ãóÇ ÝóÚóáõæÇú æóåõãú
íóÚúáóãõæäó
{{Na ambao pindi wafanyapo uchafu au
wakajidhulumu nafsi zao humkumbuka Mwenyezi Mungu na wakamwomba msamaha kwa dhambi zao - na nani anaye futa dhambi isipo kuwa Mwenyezi
Mungu? - na wala hawaendelei na waliyo yafanya na hali wanajua.}} [Aali ‘Imraan: 135]
Sayidul-Istighfaar
Imepokelewa kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla
Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:
((Mwenyezi Mungu huifurahia toba ya mja
wake kuliko mmoja wenu anapokuwa juu ya mnyama wake jangwani akamuangusha na
kumkimbia.)) [Imepokewa na Bukhaariy]
Na katika riwaya ya Muslim na wengine:
((Mwenyezi Mungu huifurahia toba ya mja
wake kuliko mmoja wenu anapokuwa juu ya mnyama wake jangwani akamuangusha na
kumkimbia, akiwa amebeba chakula na maji yake (mtu huyo), kisha mtu huyo
akakata tamaa, akauendea mti na kuegemea chini ya kivuli chake akiwa keshakata
tamaa ya kumuona tena mnyama wake. Na anapokuwa katika hali hiyo, ghafla
anamuona mnyama wake mbele yake. Akazishika hatamu zake, kisha akasema kwa
furaha: "Mola wangu Wewe ni mja wangu na mimi ni mola wako". “Alikosea
kwa wingi wa furaha.”)) [Imepokewa na Muslim na wengine.]
Na sababu ya Mwenyezi Mungu kuifurahia toba hiyo ni
kuwa anaridhika na nia ya mja wake juu ya kuwa alikosea kutamka.
Ndugu zangu Waislamu, huu ndio wakati wa kuomba
maghfirah. Jitaabishe ndani ya mwezi huu upate kupumzika siku ile watu
watakapotaabika. Mche Mungu zaidi upate kuwa mwenye matumaini siku ile watu
watakapokata tamaa. Lia sana upate kucheka siku ile watu watakapokuwa na khofu.
Jisogeze kwa Mola wako kwa kustaghfiru, kwani Mtume
wetu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akiomba maghfira kwa
Mola wake kila siku mara mia moja.
Miongoni mwa dua za kuomba maghfirah ni hii inayoitwa 'Sayyid al Istighfaar' (Dua bora ya
kuomba Maghfirah kupita zote) aliyotuusia Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu
‘alayhi wa aalihi wa sallam).
Imepokelewa kutoka Shaddaad bin ‘Aus (Radhiya Allaahu
‘anhu) kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa
sallam) amesema:
"Bwana
wa kuomba maghfira ni kusema:
Çááøóåõãøó ÃóäúÊó ÑóÈøöí áÇ Åöáóåó ÅáÇ ÃóäúÊó
ÎóáóÞúÊóäöí æóÃóäóÇ ÚóÈúÏõßó æóÃóäóÇ Úóáóì ÚóåúÏößó æóæóÚúÏößó ãóÇ ÇÓúÊóØóÚúÊõ
ÃóÚõæÐõ Èößó ãöäú ÔóÑøö ãóÇ ÕóäóÚúÊõ ÃóÈõæÁõ áóßó ÈöäöÚúãóÊößó Úóáóíøó
æóÃóÈõæÁõ áóßó ÈöÐóäúÈöí ÝóÇÛúÝöÑú áöí ÝóÅöäøóåõ áÇ íóÛúÝöÑõ ÇáÐøõäõæÈó ÅöáÇ
ÃóäúÊó.
((Allahumma anta Rabbiy laa ilaaha illa anta,
khalaqtaniy wa ana ‘abduka, wa ana ‘alaa ‘a-hdika wa wa’adika ma statwa’atu. A’udhu
bika min sharri ma sana’atu, abuu laka bini’imatika ‘alayya wa abu'u laka
bidhanbiy, faghfirliy, fainnahu laa yaghfiru dhunuuba illa anta.))
Akasema: ((Atakayesema hayo wakati wa
mchana akiwa na yakini juu yake, kisha akafa siku hiyo kabla ya usiku kuingia,
huyo ni katika watu wa Peponi. Na atakayesema hayo wakati wa usiku akiwa na
yakini juu yake, akafa kabla ya asubuhi kuingia, huyo ni katika watu wa Peponi.))
[Imepokewa na Bukhaariy,
Attirmidhy, Annasai na wengine]
Maana yake (Dua ya Sayidul-Istighfaar)
|
Ewe Allaah. Wewe ni Mola wangu mlezi hapana anayestahiki kuabudiwa
isipokuwa Wewe |
Çááøóåõãøó ÃóäúÊó ÑóÈøöí áÇ Åöáóåó ÅáÇ
ÃóäúÊó |
|
Umeniumba na mimi ni mja Wako |
ÎóáóÞúÊóäöí æóÃóäóÇ ÚóÈúÏõßó |
|
Na mimi nimo katika kutekeleza maamrisho Yako na wa’adi Wako niwezavyo |
æóÃóäóÇ Úóáóì ÚóåúÏößó æóæóÚúÏößó ãóÇ ÇÓúÊóØóÚúÊõ |
|
Ninajikinga Kwako na kila shari niliyoitenda |
ÃóÚõæÐõ Èößó ãöäú ÔóÑøö ãóÇ ÕóäóÚúÊõ |
|
Ninakiri Kwako kwa neema Zako juu yangu |
ÃóÈõæÁõ áóßó ÈöäöÚúãóÊößó Úóáóíøó |
|
Na ninakiri Kwako juu ya dhambi zangu |
æóÃóÈõæÁõ áóßó ÈöÐóäúÈöí |
|
Kwa hivyo unisamehe kwa sababu hapana mwenye kusamehe madhambi
isipokuwa Wewe |
ÝóÇÛúÝöÑú áöí ÝóÅöäøóåõ áÇ íóÛúÝöÑõ ÇáÐøõäõæÈó ÅöáÇ ÃóäúÊó. |
Namtakia kila Muislamu Ramadhaan njema ya mwaka huu na
kila mwaka, huku nikimuomba Mwenyezi Mungu Atujaalie tufaidike na Ramadhaan hii
na nyingi zijazo, miaka baada ya miaka -
Aamiyn.
Kutoka
kwa Ka’ab bin Ujarah (Radhiya Allaahu ‘anhu) alisema kuwa siku moja Mtume wa
Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alipanda juu ya
membari yake na alipoikanyaga ngazi ya mwanzo alisema 'Aamiyn', kisha akapanda
ngazi ya pili akasema tena 'Aamiyn' na juu ya ngazi ya tatu pia alisema 'Aamiyn'.
Alipoteremka tulimuuliza: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, tumekusikia leo
ukitamka maneno si kawaida yako?" Mtume wa Mwenyezi Mungu akasema:
((Alinijia
Jibriyl nilipokuwa juu ya ngazi ya mwanzo akaniambia: 'Ametengwa mbali mtu
aliyeiwahi Ramadhaan kisha asighufuriwe madhambi yake, sema 'Aamiyn', nikasema:
'Aamiyn'. Nilipopanda ngazi ya pili akaniambia: ‘Ametengwa mbali yule ambaye
umetajwa mbele yake kisha asikuswalie, sema 'Aamiyn', nikasema; 'Aamiyn'.
Nilipokuwa juu ya ngazi ya tatu akaniambia: 'Ametengwa mbali aliyeishi na
wazazi wake wawili wakiwa katika umri mkubwa au mmoja kati yao kisha
wasimuingize Peponi (wasiwe sababu ya kumuingiza Peponi)' sema; 'Aamiyn'.
Nikasema: ‘Aamiyn.’))
Maana ya Hadiyth:
Ramadhaan
ni mwezi mtukufu tuliotunukiwa na Mola wetu (Subhaanahu wa Ta’ala) kwa ajili ya
kutumiminia Rahmah na Maghfirah na kutuepusha na Moto. Muislamu wa kweli
haiachi fursa kama hii ndani ya mwezi kama huu uliojaa khayr nyingi ndani yake
na Barkah. Bali huongeza jitihada katika kujikaribisha kwa Mwenyezi Mungu na
kujiepusha na kumuasi. Mwenye kuipuuza neema kama hii, huyo anastahiki
kutengwa.
Mtume wa
Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ametufundisha kuwa
kumswalia ni katika matendo adhimu na yenye kusababisha kupata Rahmah za
Mwenyezi Mungu.
Mtume (Swalla
Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alisema:
((Atakayeniswalia mara moja, Mwenyezi Mungu atamswalia (atamtakia rahmah)
mara kumi.)) [Imepokewa
na Muslim]
Na akasema:
((Wenye
kustahiki zaidi kuwa nami siku ya Qiyaamah ni wale wenye kuniswalia kwa wingi.))
[Imepokwa na Attirmidhy]
Na
akasema:
((Isugulike
juu ya mchanga pua ya yule niliyetajwa mbele yake kisha asiniswalie.)) [Imepokewa na Attirmidhy]
Kuwatendea
mema wazazi ni katika matendo anayoyapenda Mwenyezi Mungu (Subhaanahu wa
Ta’ala).
Kutoka kwa
Abdullahi bin Mas’uud (Radhiya Allaahu ‘anhu) alisema: "Nilimuuliza Mtume
wa Mwenyezi Mungu; matendo yepi yanayopendwa zaidi na Mwenyezi Mungu?” Akasema:
((Swala katika wakati wake.)) Nikamuuliza:
"Kisha ipi?" Akaniambia: ((Kisha kuwatendea
mema wazazi wawili.)) Nikamuuliza: “Kisha ipi?” Akaniambia: ((Jihadi katika njia ya Mwenyezi Mungu.)) [Imepokewa na Bukhaariy na Muslim]
Na kinyume cha hayo ni kutowatendea mema wazee wawili. Mtume wa Mwenyezi
Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:
((Watatu
hawafaidiki na amali zao (hawazipatii thawabu amali zao). Mwenye kumshirikisha
Mwenyezi Mungu, asiyewatendea wema wazazi wake wawili, na mwenye kukimbia akawaacha
wenzake uwanjani siku ya vita.)) [Imepokewa na Attabarani]
Ndani
ya mwezi huu
Ndani ya mwezi huu mna Maghfirah na kunyanyuliwa Darjah na thawabu nyingi. Na
ndani ya kila usiku wa mwezi huu Mwenyezi Mungu, huwaepusha na Moto wengi
miongoni mwa waja wake.
Ndani ya
mwezi huu du’ah zinatakabaliwa wakati wa kula futari, nyakati za usiku,
tunaposoma Qur-aan, ndani ya Swalah na wakati wowote mtu anapoamua kunyanyua
mikono yake na kumuomba Mola wake.
Usiku
mmoja peke yake wa 'Lailatul Qadar' ni bora kuliko miezi elfu.
Milango ya
Moto inafungwa na ya Pepo inafunguliwa, na mashetani wanakomelewa.
Mtume wa
Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:
((Atakayefunga
Ramadhaan kwa imani na kwa kutarajia, hufutiwa dhambi zake zilizotangulia.)) [Imepokewa na Bukhaariy na Muslim]
Na
akasema:
((Mwenyezi
Mungu anao anaowaepusha (na Moto) kila mchana na usiku.)) [Sahih At-Targhiib-988]
Kwa hivyo
Mola wetu Mkarimu tutakabalie na sisi du’aah zetu, tujaalie tuwe katika
watakaohitimisha Qur-aan mara nyingi ndani ya mwezi huu na miezi mingine.
Tufutie dhambi zetu na utujaalie tuwe miongoni mwa hao utakaowaepusha na Moto –
Aamiyn.
Sharti Za
Kukubaliwa Amali
Sharti la
mwanzo la kukubaliwa kwa amali, ni kuihusisha amali hiyo iwe halisi kwa ajili
ya Mwenyezi Mungu (Subhaanahu wa Ta’ala), na sharti la pili ni amali hiyo
ikubaliane na mafundisho aliyokuja nayo Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu
‘alayhi wa aalihi wa sallam).
Hapana
amali inayokubaliana na mafundisho ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu
‘alayhi wa aalihi wa sallam) kupita ile aliyokuwa akiitenda mwenyewe (Swalla
Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam).
Yafuatayo
ni baadhi ya matendo aliyokuwa akiyatenda ndani ya mwezi mtukufu wa Ramadhaan. Nakuleteeni
ili yawe dira itakayotumulikia na kutuongoza njia, huku tukifunga kama
alivyokuwa akifunga, na kufanya ibada nyingine kama alivyokuwa akizifanya.
Vipi Alikuwa
Akiukaribisha Mwezi?
Mtume wa
Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa haanzi
kufunga mpaka ahakikishe kuwa mwezi umeonekana. Alikuwa akiutafuta na
akiwaamrisha wengine wautafute, na anapojuulishwa na yeyote kati ya Swahaabah
zake (Radhiya Allaahu ‘anhu) kuwa ameuona mwezi, na yeye huamrisha umati wake
kufunga.
Mtume wa
Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:
((Fungeni
mnapouona na fungueni mnapouona, na mnaposhindwa kuuona kwa ajili ya mawingu
basi kamilisheni mwezi wa Shaaban siku thelathini.)) [Imepokewa na Bukhaariy na Muslim]
Alikuwa
akiwakataza watu wake kufunga siku moja au mbili kabla ya kuandama mwezi, na
aliwahi kusema:
((Msiutangulie
mwezi wa Ramadhaan kwa kufunga kabla yake siku moja au siku mbili isipokuwa
kama mtu anayo kawaida ya kufunga (ndani ya siku hizo) basi na afunge.)) [Imepokewa na Bukhaariy na Muslim]
Kutia Nia
Mtume wa
Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa katika
saumu za fardhi akitia nia tokea usiku kabla ya kuingia alfajiri na alikuwa
akisema:
((Asiyetia
nia tokea usiku hana swaum.)) [Imepokewa na Annasai
kutoka kwa Bibi Hafsah (Radhiya Allaahu ‘Anha), Sahiih-al-Jami’i 6535.]
Na katika
riwaya nyingine alisema:
((Asiyetia
nia kabla ya kuingia alfajiri hana swaum.)) [Imepokewa Al Bayhaqi na Addaraqutni Sahiih-al-Jami’i, 6534]
Na
alisema:
((Asiyetia
nia ya kufunga kabla ya kuingia alfajiri, huyo hana funga.)) [Imaam Ahmad na watatu wengine, Sahiih-al-Jami’i, 6538]
Hizi zote
zinahusiana na swaum za fardhi, kwa sababu katika swaum zisizokuwa za fardhi
mtu halazimiki kutia nia tokea usiku.
Imepokelewa
kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)
alikuwa katika baadhi ya siku zisizokuwa Ramadhaani anapokwenda kwa wake zake
asipate chakula huuliza: ((“Kipo chakula
chochote?" na anapojibiwa: "Hapana", yeye husema: "Basi
mimi nimefunga.”)) [Imepokewa na Muslim]
Kula
Futari (Kuftari)
Mtume wa
Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa
akiharakisha kula futari na akilichelewesha daku. Alikuwa akisema: ((Umati wangu utakuwa katika khayr kama utaendelea
kuharakisha (kula) futari na kuchelewesha (kula) daku.)) [Imepokewa na Bukhaariy na Muslim]
Na katika Hadiyth
nyingine alisema:
((Usiku
ukianza kuingia upande huu na mchana kutoweka upande huu na jua kuzama, basi
aliyefunga (awe) kesha kula futari.)) [Imepokewa
na Bukhaariy na Muslim]
Na kutoka kwa
Abud-Dar-daa (Radhiya Allaahu ‘anhu) amesema:
((Matatu
ni katika matendo ya Mitume - Kuharakisha futari (kifungua kinywa),
kuchelewesha daku, na kuweka mkono wa kulia juu ya mkono wa kushoto ndani ya Swalah.)) [Imepokewa na Attabaraniy]
Na futari
ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ilikuwa
hafifu sana tofauti na yetu siku hizi. Alikuwa akila tende chembe 3 au 5 au 7
na kunywa maji. Anapokosa tende, hunywa maji kisha hukimbilia kuswali katika
wakati wake wa mwanzo. [Imepokewa na Ahmad
na Abu Daawud na Attirmidhy]
Na katika
riwaya nyingine Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa
sallam) alisema:
((Atakayepata
tende afungulie kinywa, na asiyepata tende afungue kinywa kwa (kunywa) maji.)) [Angalia Sahiih at-Targhiib, 1064]
Kuomba Du’aah
Mtume wa
Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akisisitiza
watu waombe du’aah wakati wa kula futari, kwa sababu du’aah ya wakati huo
hairudi patupu, na akipendekeza hivyo sana. Katika du’aah alizokuwa akiomba
ilikuwa:
"ÐåÈ ÇáÙãà æÇÈÊáÊ ÇáÚÑæÞ æËÈÊ ÇáÃÌÑ Åä ÔÇÁ Çááå"
Na maana
yake: ((Kiu imekatika na mishipa imerutubika na ujira
(thawabu) umepatikana kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu.)) [Imepokewa na Abu Daawuud – Addaraqutni na
Al Hakim]
Na alikuwa
akipendekeza kuwalisha futari waliofunga. Alikuwa akisema: ((Atakayemfutarisha aliyefunga anapata thawabu sawa na zake,
na thawabu za yule aliyefunga hazipungui kitu ndani yake.)) [Angalia Sahiih at-Targhiib, 1072]
Kula Daku
Mtume wa
Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) hajawahi hata siku
moja kuacha kula daku. Jambo lililowafanya baadhi ya wanavyuoni kutamka kuwa
kula daku ni kitendo cha wajibu.
Alikuwa (Swalla
Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akisema: ((Kuleni
daku kwa sababu katika kula daku mna barka.)) [Imepokewa na Bukhaariy na Muslim]
Na
akasema:
((Daku
lote lina barka, kwa hivyo msiache kula hata ikibidi kunywa fundo ya maji, kwa
sababu Mwenyezi Mungu na Malaika wake wanawatakia rahmah wanaokula daku.)) [Angalia Sahiih at-Targhiib, 1062 na Sahih al Jam Sahiih-al-Jami’i, 3577]
Katika
barka za kula daku ni kupata thawabu kwa ajili ya kufuata mafundisho ya Mtume
wa Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), na pia linakupa
nguvu za kufanya ‘ibaadah wakati wa mchana na katika kufanya shughuli za
kawaida.
Thawabu za
kula daku zinapatikana kwa kula chakula chochote kabla ya muadhini wa Alfajiri,
hata kama ni tende au maji. Bali Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu
‘alayhi wa aalihi wa sallam) aliwahi kusema:
((Daku
bora kwa Muislamu ni tende.)) [Imepokewa na Abu Daawuud
na Ibni Hibban na Al Baihaqy]
Alikuwa
akiendelea kula na kunywa mpaka alfajiri inapoingia na hii inatokana na kauli
ya Mwenyezi Mungu isemayo:
æóßõáõæÇú
æóÇÔúÑóÈõæÇú ÍóÊøóì íóÊóÈóíøóäó áóßõãõ ÇáúÎóíúØõ ÇáÃóÈúíóÖõ ãöäó ÇáúÎóíúØö
ÇáÃóÓúæóÏö
((Na
kuleni na kunyweni mpaka ukubainikieni weupe wa Alfajiri katika weusi wa usiku.))
[Al-Baqarah: 187]
Na aliwahi
kumruhusu Sayyidna ‘Umar aendelee kula daku na kunywa maji yake huku akiusikia
muadhini. Pia imepokelewa kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla
Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alisema: ((Mtu
anapomsikia muadhini na chakula kimo mikononi, asikirudishe mpaka amalize haja
yake.)) [Imepokewa na Imaam Ahmad,
Abu Daawuud na Al-Hakim. Imesahihishwa na Al-Albaaniy katika Sahiih-al-Jami’i,
1394]
‘Ibaadah Zake
Mtume wa
Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akijitahidi
zaidi kufanya ‘ibaadah ndani ya mwezi wa Ramadhaan kupita miezi mingine. Na
katika mwezi huu Jibril (‘Alayhis Salaam) alikuwa akimsomesha Qur-aan. Kwa
ajili hii watu wema waliotangulia walikuwa wakishindana katika kusoma na
kuhitimisha Qur-aan ndani ya mwezi wa Ramadhaan.
Maulamaa
wakubwa kama vile Imaam Az-Zuhri na Imaam Maalik na wengine wengi (Rahimahumu Allaah) walikuwa
wakiacha kufanya darsi zao na pia wakisimamisha shughuli za kutoa fatwa katika
mwezi huu kwa ajili ya kujishughulisha na kusoma Qur-aan na kuihitimisha mara
nyingi.
Na Mtume
wa Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa
linapoingia kumi la mwisho akiukaza vizuri mkanda wake na akiwaamsha wake zake
na kukesha nyakati za usiku. Alikuwa akifanya Itikafu ndani ya kumi la mwisho
huku akiusubiri usiku wa Laylatul-Qadar, na alikuwa akiwahimiza watu
kukithirisha ‘ibaadah ndani ya usiku huo.
Mtume wa
Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alisema: ((Atakayesimama (kwa kuswali na kuomba dua usiku wa) Laylatul-Qadar
kwa imani na kwa kutarajia, amesamehewa dhambi zake zilizotangulia.)) [Imepokewa na Bukhaariy na Muslim]
Ndugu
zangu Waislam! Kumi la mwanzo limekwishamalizika, na la pili ndiyo hilo
linaanza kutupa mgongo. Kwa hivyo panieni vizuri, kwa sababu siku zinakwenda
haraka sana na wakati uliobaki ni mchache, na bidhaa ya Mwenyezi Mungu ni ghali
sana. Bidhaa ya Mwenyezi Mungu ni Pepo.
Mtume wa
Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) amesema: ((Mwenye kuogopa huianza mapema safari yake, na mwenye kuianza safari
mapema atawasili mapema. Hakika bidhaa ya Mwenyezi Mungu ni ghali sana. Hakika
bidhaa ya Mwenyezi Mungu ni Pepo.)) [Imepokewa na Attirmidhy na Al-Haakim katika Al-Mustadrak kutoka kwa
Abu Hurairah (Radhiya Allaahu ‘anhu)]
Ukarimu Wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa
aalihi wa sallam)
Alikuwa (Swalla
Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) mkarimu sana katika mwezi huu wa Ramadhaan.
Imepokelewa kuwa; ((Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla
Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa mkarimu sana, na ukarimu wake
ulizidi kupita kiasi ndani ya mwezi wa Ramadhaan.)) [Imepokewa na Bukhaariy]
Na kutoka
kwa Ibni ‘Abbaas (Radhiya Allaahu ‘anhu) amesema:
((Mtume
wa Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa mkarimu
sana, na alikuwa mkarimu zaidi ndani ya mwezi wa Ramadhaan wakati anapoonana na
Jibriyl (‘Alayhis Salaam). Na alikuwa akionana na Jibriyl ndani ya kila usiku
wa Ramadhaani anamsomesha Qur-aan. Na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu
‘alayhi wa aalihi wa sallam) anapoonana na Jibriyl huwa mkarimu kuliko upepo
uliotumwa (kueneza khayr kila mahali).)) [Imepokewa na Bukhaariy na Muslim]
Kusimama Nyakati
Za Usiku (Qiyaam)
Imepokelewa
kutoka kwa Abu Hurairah (Radhiya Allaahu ‘anhu) kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla
Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akiwahimiza Swahaabah zake (Radhiya
Allaahu ‘anhu) kuswali nyakati za usiku katika mwezi wa Ramadhaan bila
kuwalazimisha. Alikuwa akisema:
((Atakayeswali (Qiyaam) usiku
katika mwezi wa Ramadhaan kwa imani na kwa kutarajia, amesamehewa dhambi zake
zilizotangulia.)) [Imepokewa na Muslim, 759]
[Pia imepokewa kwamba] atakayeswali Taraawiyh, basi anahesabiwa kuwa
ameswali Qiyaam.
‘Umrah
Alikuwa
akipendekeza watu wafanye ‘Umrah ndani ya mwezi wa Ramadhaan. Alikuwa akisema:
((‘Umrah
ndani ya mwezi wa Ramadhaan (thawabu zake) ni sawa na Hijjah.)) Na katika
riwaya nyingine: ((Sawa na Hijjah pamoja nami.)) [Imepokewa na Bukhaariy na Muslim]
Tabia Njema
Mtume wa
Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa mbora wa
mwenendo na tabia njema kupita watu wote, na alikuwa akiwaamrisha umati wake
kuwa hivyo. Kutoka kwa Abu Hurairah (Radhiya Allaahu ‘anhu) amesema kuwa Mtume
wa Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:
((Kufunga
siyo kujizuwia kula na kunywa peke yake, bali kufunga ni kujizuwia na maneno pamoja
na vitendo viovu. Na kama mtu atakutukana au atakudharau, wewe muambie:
"Mimi nimefunga, mimi nimefunga.")) [Angalia
Sahiih-al-Jami’i, 88/5]
Na
akasema:
((Ikiwa
mtu hatoacha kusema uongo na kuufanyia kazi uongo huo, basi Mwenyezi Mungu hana
haja ya kuacha kwake kula na kunywa.)) [Imepokewa
na Bukhaariy, Attirmidhy, Al-Baihaqiy na wengine]
Kuunganisha
Nasaba
Mtume wa
Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa katika
mwezi huu akikithirisha kuwatembelea ndugu na jamaa zake na kuzidisha katika
kuwatendea mema kuliko ndani ya miezi mingine.
Alikuwa
akizidisha katika kuwatendea wema hata wake zake. Imepokelewa kuwa Mtume wa
Mwenyezi Mungu alikuwa usiku akiwaingilia wake zake na mara nyingine alfajiri
huingia akiwa bado mwenye janaba, kisha hufunga na kuendelea na swaumu yake. [Imepokewa na Bukhaariy na Muslim]
Alikuwa
akiwabusu baadhi ya wake zake huku akiwa amefunga na alikuwa akiimiliki nafsi
yake.
Mwenye Huruma
Kwa umati Wake
Alikuwa
mwingi wa huruma kwa umati wake, aliwaruhusu wanaokula kwa kusahau waendelee na
swaumu zao.
Mtume wa
Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alisema: ((Mmoja wenu anaposahau akala na kunywa basi akamilishe swaumu
yake kwa sababu Mwenyezi Mungu ndiye aliyemlisha na kumnywesha.)) [Imepokewa na Bukhaariy na Muslim]
Na
akasema: ((Aliyetapika bila kukusudia aendelee na swaumu,
lakini aliyejitapisha kusudi alipe.)) [Imepokewa na Abu Daawuud, Attirmidhiy, Ibni Maajah na Imaam Ahmad]
Zakaatul-Fitwr
Katika
mwezi wa Shaaban mwaka wa pili baada ya Hijrah (baada ya kuhamia Madiynah),
Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alifaradhisha
Zakaatul-Fitwr ili iitakase swaumu kutokana na dhambi ndogo ndogo
zilizopatikana ndani ya mazungumzo na matendo. Na wakati huo huo Zakah hiyo iwe
msaada kwa mafakiri na wasiojiweza katika kuisherehekea Sikukuu.
Imepokelewa
kutoka kwa Ibni ‘Abbaas (Radhiya Allaahu ‘anhu) kuwa amesema: ((Mtume wa Mwenyezi Mungu
(Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alifaridhisha Zakah ya Fitwr kwa
ajili ya kumtakasa aliyefunga kutokana na dhambi ndogo ndogo za mazungumzo na
matendo, na ili wafaidike masikini. Atakayeitoa kabla ya Swalah (ya ‘Iyd)
inakubaliwa kama Zakah ya Fitwr, na atakayeitoa baada ya Swalah inakubaliwa
kama Swadaqah ya kawaida.)) [Imepokewa
na Abu Daawuud, Ibni Maajah na Addaraqutniy]
Alikuwa (Swalla
Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akitoa Zakah ya Fitwr siku ya mwisho ya
mwezi wa Ramadhaan kabla ya Swalah ya ‘Iyd kuswaliwa. [Imepokewa na Abu Daawuud, Ibni Maajah na Al-Haakim]