NINI BAADA YA RAMADHANI?
MUHAMMAD FARAJ SALEM
AL SAIY
Ndugu zangu Waislam,
Assalaam aleikum wa Rahmatullahi wa Barakatuh
Mwezi
Mtukufu wa Ramadhani tumekwishauaga, zile siku njema na nyakati za usiku
zilizojaa baraka ndani yake tulokuwa tukiamka na kusoma Qurani na kujitahidi
katika kufanya kila amali za kumridhisha Mola wetu, ndiyo zishatutoka.
Lile kumi la mwanzo la mwezi mtukufu wa Ramadhani, kumi la Rahmah, na kumi la
pili la Maghfirah, na la tatu kumi la Kuepushwa na Moto, yoote hayo
tumekwishayamaliza.
Tumekiaga chuo cha Subira na ucha Mungu. Tumejisubirisha kutokana na matamanio
ya nafsi zetu mbali na ushawishi wa shetani. Misikiti ilijaa waumini, misahafu
iligawiwa na kusomwa kwa wingi, maji, tende, na vyakula vya aina mbali mbali
viligawiwa bure kwa nia ya kutaraji malipo mema kutoka kwa Mlipaji bila ya
hesabu.
Bila shaka yoyote tumeuaga mwezi huu Mtukufu baada ya kufaidika nao kutokana
na mafunzo yake mbali mbali pamoja na kufanya biashara na Mola wetu, biashara
isiyododa.
Mwenyezi Mungu anasema;
“Kwa yakini wale wanaosoma Kitabu cha Mwenyezi Mungu, na wakasimamisha Sala,
na katika yale Tuliyowapa wakatoa kwa siri na kwa dhahiri, hao wanatumai(faida
ya) bishara isiyododa (isiyobwaga)”.
[Fatir - 29
Bila
shaka tunategemea thawabu nyingi sana kutoka kwa Mola wetu Mkarimu, kwa ajili
ya kuupokea vizuri mwezi Wake Mkarimu.
Kwa ajili ya yote hayo inatupasa tumshukuru Mola wetu Mtukufu kwa neema zake
hizo na Ukarimu Wake huo.
Na ndiyo maana Mwenyezi Mungu Subhanahu wa Taala akasema;
“Na pia mtimize hisabu hiyo, na mumtukuze Mwenyezi Mungu kwa kuwa
amekuongozeni ili mpate kumshukuru”.
[Al Baqarah - 185
VIPI TUTAMSHUKURU MWENYEZI MUNGU?
Je! Tutamshukuru kwa kurudi kama tulivyokuwa kabla ya Mwezi wa Ramadhani au
tutamuonyesha Mola wetu matunda mema ya neema zake alizotuneemesha nazo katika
mwezi wake?
Maulamaa wanasema kuwa; Ukitaka kujuwa kiasi gani Ibada zako za Ramadhani
zimekubaliwa, basi itizame hali yako ilivyokuwa baada ya kumalizika mwezi huu
mtukufu, kisha uilinganishe na ilivyokuwa kabla yake. Ukiona kuwa imekuwa bora
kuliko pale ilivyokuwa kabla ya kuanza mwezi wa Ramadhani, basi mshukuru Mola
wako. Ama ukiona kinyume cha hivyo, basi usiilaumu isipokuwa nafsi yako.
IFICHE AKIBA YAKO KIBINDONI
Ikiwa umejitahidi kuzichuma thawabu zako ukaweza kujipatia akiba itakayotufaa
siku ambayo hazitofaa ndani yake mali wala watoto, basi ifiche akiba hiyo
kibindoni wala usianze kuwagawia watu na kuitupa huku na kule kisha ukaondoka
patupu ukiwa umefilisika.
Mtume(Swalla Llahu alayhi wa sallam) aliwauliza Masahaba wake (Radhiya
Llahu anhum):
“Mnamjuwa yupi aliyefilisika?”
Masahaba (Radhiya Llahu anhum) wakasema;
“Aliyefilisika tunayemjuwa sisi ni yule asiyekuwa na pesa wala kitu chochote”.
Mtume(Swalla Llahu alayhi wa sallam) akasema;
“Aliyefilisika katika umati wangu ni yule atakayekuja Siku ya Kiama akiwa na
Sala zake, Funga zake, Zaka zake, anakuja (na vyote hivyo), akiwa amemtukana
huyu, amemsingizia uwongo huyu, amekula mali ya huyu, amemwaga damu ya huyu na
amempiga huyu, kisha zinachukuliwa thawabu zake na kupewa huyu na yule, na
zikeshamalizika thawabu zake kabla ya kumaliza madeni ya watu, zinachukuliwa
dhambi zao, na kutwishwa nazo yeye, kisha akaingizwa Motoni”
(Huyo ndiye aliyefilisika).
Ndugu zangu Waislam, Siku ya Kiama hakuna kitakachokufaa isipokuwa thawabu
zako ulizojikusanyia hapa, na hakuna huko mahali pengine isipokuwa Peponi au
Motoni. Basi zizuwie vizuri thawabu zako na usiwagawie watu na kuzipoteza bure
kutokana na kuwasengenya watu, kuwatukana, kuzungumza juu ya mabaya yao,
kuwadhulumu, nk.
Hassan al Basry (Radhiya Llahu anhu), alipoambiwa kuwa pana mtu anayependa kumsema vibaya
mbele ya watu, alimwambia mkewe apike chakula kizuri, kisha akampa chakula
hicho mtumishi wake na kumtaka ampelekee mtu huyo anayemsema vibaya.
Alipoulizwa kwa nini umetenda hivyo, akajibu;
“Mimi nina madhambi mengi, na mtu huyu kila anaponisema vibaya kwa watu, huwa
ananipunguzia madhambi yangu. Kwa ajili hiyo, nikaona ni bora nimpe tunza
nzuri ninayoweza kumpa”.
Maulamaa wanasema;
“Mfano wa mtu aliyehangaika kuchuma thawabu nyingi kisha akawagawia watu
kutokana na kuwasengenya na kuwatukana na kuwadhulumu, ni mfano wa mtu
aliyeshona nguo nzuri, kisha baada ya kuimaliza na kuipamba, akachukua mkasi
na kuanza kuikata kata nguo hiyo”.
SALA
Ndugu zangu Waislam, kama tulivyokuwa tukiijaza misikiti katika mwezi wa
Ramadhan, basi tuendelee hivyo hivyo katika miezi yote, kwani Mungu wa
Ramadhani ni Yule Yule Mungu wa miezi iliyobaki. Na Mtume wenu (Swalla Llahu
alayhi wa sallam) hakupata
kuacha kusali jamaa isipokuwa penye udhuru mkubwa kabisa usioweza kuepukwa.
Hata wakati wa vita alikuwa akisali jamaa, wakati wa vita, vichwa vinakatwa
katwa kwa mapanga, mikuki inazama ndani ya miili ya watu huku farasi wakipiga
kelele na vumbi likitimka, yeye (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alikuwa akiisimamisha Sala ya jamaa.
Huu ndio mwenendo wake, na anayekwenda kinyume na mwenendo wake, basi aipime
tena imani yake.
Hebu tumsikilize Abdillahi bin Masaood (Radhiya Llahu anhu) akituelezea mambo yalivyokuwa
wakati wa Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam);
Abdillahi bin Masaood anasema;
“Anayetaka kuonana na Mola wake kesho akiwa na furaha, basi azitunze Sala hizi
kila zinaponadiwa (anapoadhini), kwani Mola wenu amemwekea Mtume wenu mwenendo
wa uongofu, na hizi (Sala) ni katika mwenedo wa uongofu. Na kama nanyi pia
mtasali majumbani mwenu kama anavyosali mtu huyu aliyechelewa (anavyosali)
nyumbani kwake, mtakuwa mumeuacha mwenendo wa Mtume wenu, na mkiuacha mwenendo
wa Mtume wenu, basi mtapotoka. Tulikuwa wakati wa Mtume(Swalla Llahu alayhi
wa sallam), hakuna anayeacha
kusali (jamaa) isipokuwa mnafiki anayejulikana (na kila mtu) kwa unafiki wake.
Alikuwa mtu analetwa (msikitini akiwa anaumwa) akishikwa mikono na kuongozwa
mpaka anasimamishwa katika safu”
Muslim
Hadithi katika mlango huu ziko nyingi sana.
KUTOWA
Ndugu zangu Waislam, tuendelee kutowa kama tulivyokuwa tukitowa katika mwezi
mtukufu wa Ramadhani, kwani mali tuliyokuwa nayo na uwezo tuliokuwa nao ni
mtihani tuliopewa na Mola wetu, na Siku ya Kiama tutaulizwa juu ya kila senti,
vipi tumeichuma na katika nini tumeitumia.
Mwenyezi Mungu anawajulisha na kuwasahihisha wale wanaodhania kuwa hiyo mali
waliyopewa, walipewa kwa ajili kukirimiwa au kwa ajili ya ubora wao.
Mwenyezi Mungu anasema;
“Lakini mwanadamu, Mola wake anapomfanyia MTIHANI Akamtukuza na kumneemesha,
basi husema; “Mola wangu amenitukuza”
Na Anapomfanyia MTIHANI Akampunguzia riziki yake, husema; “Mola Wangu
Amenidhalilisha”.
Sivyo hivyo (mnavyodhania)! Bali nyinyi (matajiri) hamuwatazami mayatima kwa
jicho la huruma.
Wala hamujihimizi kulisha masikini
Na mnakula urithi kwa ulaji wa pupa
Na mnapenda mali pendo la kupita kiasi.”
[Suratul Fajr – 15 – 20
Na Mtume wetu(Swalla Llahu alayhi wa sallam) anasema;
"Kuna
kingine unachofaidika nacho katika mali yako isipokuwa kile unachokula kikaoza,
na unachokivaa kikachakaa na
unachotoa sadaka KIKABAKI?"
Masahaba (Radhiya Llahu anhum) wanasema;
“Mtume
wetu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alikuwa akitowa utowaji wa asiyeogopa kufilisika”.
FUNGA
Katika
mafundisho ya mwezi wa Ramadhani, tumejifunza pia ustahamilivu wa Funga. Kama
tulivyoweza kustahamili kuufunga mwezi mzima, basi tujaribu katika meizi
isiyokuwa Ramadhani kustahamili kufunga angalau siku tatu katika kila mwezi.
Na mtu akifunga siku tatu katika kila mwezi, basi thawabu zake ni sawa na yule
aliyefunga mwaka mzima. Na hii ni kwa sababu Mwenyezi Mungu hulipa kwa kila
jema moja mara kumi, kwa hivyo funga ya siku moja, mtu hulipwa kwa amali ya
siku kumi, na amali ya siku tatu malipo yake huwa ya siku thelathini.
Ama
ikiwa siku tatu kwa mwezi ni nzito, basi tujaribu kujizowesha kwa kufunga
angalau siku moja kila mwezi, hii ni kwa kujizowesha tu.
Mtume(Swalla Llahu alayhi wa sallam) anasema;
“Mtu
anapofunga siku moja kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, basi Mwenyezi Mungu
humbaidishia moto umbali wa miaka sabini”.
Imesimuliwa na Maimamu wote wa hadithi isipokuwa Abu Daud.
QURANI
Mwenyezi Mungu anasema;
“Mwenyezi Mungu ameteremsha hadithi nzuri kabisa (kwa kuteremsha) kitabu
chenye maneno yanayowafikiana, yanayokaririwa (bila kuchosha); husisimka kwayo
ngozi za wale wanaomwogopa Mola wao. Kisha ngozi zao na nyoyo zao huwa laini
kwa kumkumbuka Mola wao. Huo ndio uwongofu wa Mwenyezi Mungu, kwa huo
humwongoa amtakaye. Na anayeachiwa na Mwenyezi Mungu kuwa amepotea , basi
hakuna wa kumuongoa.”
[Azzumar
-23
Maulamaa wanasema;
“Mtu anapotamani kuzungumza na Mola wake, basi ende kusali, (kwa sababu ndani
ya Sala, yanapita mazungumzo baina ya mja na Mola wake), na mtu anapotamani
Mola wake azungumze naye, basi aisome Qurani, kwani Qurani ni maneno ya
Mwenyezi Mungu aliyowateremshia waja wake akitujulisha nini anachotutaka
kutoka kwetu, na maamrisho na makatazo Yake Subhaanahu wa Taala juu yetu.
Qurani ni kiungo baina yetu na Mola wetu, Qurani ni katiba yetu Waislam na
ndani yake mna pumzi ya Mola wetu Subhanahau wa Taala.
Mwenyezi Mungu anasema;
“Na namna hivi tumekufunulia Wahyi kwa amri yetu. Ulikuwa hujui Kitabu ni nini
wala imani. Lakini tumefanya kitabu hiki (Qurani) ni nuru…”
[Ash Shuura – 52]
Na akasema;
“(Na hiki) Kitabu; tumekiteremsha kwako chenye baraka nyingi; ili wapate
kuzifikiri Aya zake, na wenye akili wawaidhike”.
[Sad - 29
Kwa hivyo tusiihame Qurani na kuiacha, tusije tukaingia katika wale
watakaoshitakiwa na Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) kwa Mola wake, pale Mwenyezi Mungu aliposema;
“Na Mtume alikuwa akisema; “Ee, Mola wangu! Hakika watu wangu wameifanya
Qurani hii kuwa kitu kilichoachwa (kilichohujuriwa)”.
[Al Furqan – 30
Katika kuisherehesha aya hii anasema Ibni Kathir;
“Kutokuisoma Qurani na kushughulikia mengine ni katika kuihama. Kutokutafakari
juu ya Aya zake ni katika kuihama.
Kutoifanyia kazi Qurani ni katika kuihama.
Kupenda kusikiliza nyimbo na maneno mengine yasiyokuwa na maana huku
ukiisukuma upande Qurani, ni katika kuihama”.
Mtume(Swalla Llahu alayhi wa sallam) amesema;
“Isomeni Qurani, kwa sababu Siku ya Kiama itakuja kuwaombea shifaa wanaoisoma”.
Muslim
Na akasema;
“Mfano wa Mwislamu anayesoma Qurani ni mfano wa Balungi, harufu yake nzuri na
ladha yake nzuri, na mfano wa Mwislamu asiyesoma Qurani ni mfano wa Tende,
haina harufu yoyote lakini ladha yake nzuri, na mfano wa Mnafiki anayesoma
Qurani, ni mfano wa mrehani, harufu yake nzuri lakini ladha yake chungu, na
mfano wa Mnafiki asiyesoma Qurani, ni mfano wa Handhalah (tunda chungu sana
lililofanana na tango), halina harufu yoyote, na ladha yake chungu”.
Bukhari na Muslim
Allah Allah ndugu zangu Qurani musiiweke nyuma, kwani atakayeiweka nyuma, basi
itamsukumiza Motoni – Tunamuomba Mwenyezi Mungu atuepushe na Moto wake.
Na
atakayeiweka mbele Qurani, basi itamuongoza na kumuingiza katika Bustani za Al
Rahmani.
Tunamuomba Mwenyezi Mungu azikubali amali zetu zote njema tulizotenda katika
mwezi huu Mtukufu, atusamehe katika yale tuliyopunguza, na atujaalie tuufikie
mwezi wa Ramadhani ujao na mingi mingine tukiwa katika hali iliyo bora kuliko
hii, tukiwa sote tumerudi kwa Mola wetu kurudi kwa haki,
na Umma wetu urudishe heshima na utukufu wake. Aaamin
Wasslaam aleikum wa Rahmatullahi wa Barakatuh