NA WALE WATATU WALIONGOJESHWA

Muhammad Faraj Salem Al Saiy

Hiki ni kisa cha kusisimuwa juu ya Masahaba watatu (Radhiya Llahu anhum), waliofanya makosa, na walipomuendea Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) kumuomba msamaha, aliwataka wasubiri mpaka Mwenyezi Mungu Subhanahu wa Taala atakapoteremsha hukmu juu yao, wakati wenzao waliofanya kosa lile lile walipomuendea Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) hakuwataka wasubiri, bali aliwakubalia udhuru wao, akawaombea maghfira, kisha akamauchia Mwenyezi Mungu juu ya ukweli wa udhuru wao.

Hili ni fundisho kubwa kwetu Waislamu la kujifunza subira katika kutafuta radhi za Mwenyezi Mungu, pamoja na kujifunza namna gani Masahaba (Radhiya Llahu anhum) walikuwa watiifu kwa kiongozi wao na kipenzi chao Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam).

 

Masahaba watatu hawa (Radhiya Llahu anhum) walisubiri mpaka ardhi yote wakaiona dhiki, juu ya ukubwa wake, na mpaka wakatambua kuwa hapana pa kukimbilia isipokuwa kwake Subhanahu wa Taala.

 

Hiki ni kisa cha vita vya Tabuk, ambapo kwa mara ya mwanzo jeshi la Waislamu lilijitayarisha kupambana na jeshi kubwa la Warumi katika mwaka wa 9 Hijri wakati wa joto kali sana, katika vita vilivyojulikana kama ni  Vita vya Dhiki.

 

Watu wapatao themanini katika watu wa Madina hawakufuatana na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) kwenda Tabuk kushiriki katika vita hivyo, watu ambao wengi kati yao walikuwa ni wanafiki ambao aya za Qurani zilikwisha teremka juu yao kuwajulisha watu juu ya unafiki wao.

Walikuwepo pia wasioshiriki kwa sababu ya maradhi au udhaifu wa siha zao au kwa sababu ya kutokuwa na uwezo wa kumiliki wanyama wa kuwapanda kuwapeleka vitani. Na wengine hawakushiriki kwa sababu ya uvivu tu.

 

Kaab bin Maalik (Radhiya Llahu anhu), mmoja katika Masahaba waliojulikana kwa ucha Mungu ambaye pia alikuwa mmoja katika washairi maarufu sana wa Kiislamu hakushiriki katika vita hivyo.

Kaab alishiriki pamoja na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) katika vita vyote dhidi ya washirikina isipokuwa vita vya Badar, na hii ilikuwa kwa sababu Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) alipotoka na kundi dogo la Waislamu wapatao mia tatu na kidogo katika vita hivyo vya Badar hakuwa na nia ya kupigana vita vikubwa, bali alikuwa na nia ya kuuteka msafara mdogo wa Abu Sufiyan uliokuwa ukitokea nchi ya Sham.

 

Katika vita vya Uhud, Kaab (Radhiya Llahu anhu) alibadilishana nguo na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam). Yeye alivaa nguo za Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) zenye rangi ya manjano na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) alivaa nguo za Kaab (Radhiya Llahu anhu).

Katika vita hivyo Kaab (Radhiya Llahu anhu) alipata majeraha kumi na moja.

 

Hebu tumuache Kaab mwenyewe (Radhiya Llahu anhu) atuhadithie kisa chake cha kutokushiriki katika vita hivyo vya Tabuk.

Anasema Kaab (Radhiya Llahu anhu):

Sikupata kuwa katika hali nzuri kwa hali na mali kama nilivyokuwa wakati watu wakijitayarisha na vita hivyo. Wallahi sikupata kukusanya wanyama wawili wa kunipeleka vitani isipokuwa katika vita hivyo. Na ilikuwa kawaida ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) anapotaka kupigana vita vyovyote hutoa ishara kama kwamba anataka kupigana vita vingine, (Isipokuwa katika vita hivi hakufanya hivyo kwa sababu ya umbali wa Safari na ukali wa joto), mpaka ulipowadia wakati wa vita hivyo vilivyokuwa katika joto kali sana, safari ndefu, pamoja na maadui wengi sana.

 

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) alikuwa katika hali ya kujitayarisha, na Waislamu pia wakawa katika hali hiyo, na watu walikuwa wengi sana.

Nikasema:

'Kesho mimi nitajitayarisha nijiunge nao.'

Nikawa nakwenda nikirudi bila ya kufanya chochote, huku nikijisemesha nafsini mwangu:

'Wakati wowote ninapotaka nitaweza kujitayarisha nijiunge nao'.

Nikaendelea na hali hiyo mpaka mambo yalipoanza kupamba moto, na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) alipoamua kuondoka asubuhi ya siku ya pili yake pamoja na Waislamu, na mimi bado sikuwa nimejitayarisha kwa chochote.

Nikasema:

'Nitajitayarisha siku ifuatayo baada ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) kuondoka, au hata baada ya siku mbili kisha nitakutana nao njiani kabla ya wao kuwasili Tabuk.'

Nikatoka asubuhi ya siku ya pili ili nianze kujitayarisha na kununua mahitajio yangu ya vitani, hatimae nikarudi nyumbani bila kufanya chochote.

Nikawa katika hali hiyo mpaka zikatufikia habari kuwa Waislamu wamekwishawasili Tabuk na kwamba vita vishaanza, ndipo iliponipitikia niondoke ili niwawahi.Yareti ningefanya hivyo. Lakini sikujaaliwa.

Nikawa kila ninapotoka nje ya nyumba yangu na kuonana na watu, ninahuzunika sana na kuona uchungu kwa sababu sikuwa nikimuona mtu yeyote aliye kufu yangu. Sikuwa nikiwaona isipokuwa wale watu waliokuwa wakijulikana kuwa ni wanafiki, au wale waliokuwa na udhuru wa kutokwenda vitani kwa sababu ya umasikini, udhaifu wa hali zao au maradhi.

 

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) hakuuuliza juu yangu mpaka walipowasili Tabuk, akasema huku akiwa amekaa pamoja na watu:

"Amefanya nini Kaab?"

Mmoja katika watu wa Bani Salama akasema:

"Limemzuwia tandiko lake na kuwatizama awapendao."

Muadh bin Jabal (Radhiya Llahu anhu) akasema:

"Maneno mabaya yaliyoje uliyosema; Wallahi ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu sisi tunavyomjua ni mtu anayependa kheri tu".

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) akanyamza.

 

Kaab (Radhiya Llahu anhu) anaendelea kuelezea:

"Niliposikia kuwa misafara inaanza kurudi nikaanza kujisemesha huku nikifikiri uongo upi niuseme hata Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) (anisadiki na) asighadhibike nami? Nikawaendea jamaa zangu wale wenye hekima kutaka ushauri wao.

Wakati Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) alipowasili Madina, mimi nilikuwa nishafikia uamuzi kuwa sina budi kumuambia ukweli, na kwamba nikisema uongo sitoweza kuokoka nao. Nikaamua kuwa lazima niseme kweli tu.

Asubuhi iliyofuata Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) aliwasili, na ilikuwa kawaida yake anapowasili kwanza huenda msikitini kusali rakaa mbili, kisha hukaa hapo muda kidogo kwa ajili ya kusikiliza matatizo ya watu.

Wale waliobaki Madina wasiende vitani wakaanza kumuendea huku wakimtolea (kila aina ya) udhuru, na walikuwa kiasi cha watu themanini na kidogo hivi.

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) aliwakubalia wote udhuru wao na kuwaombea maghufira na kumuachia Mola wao ukweli wa udhuru walioutoa. Nilipomsogelea mimi na kumsalimia alitabasamu huku akionyesha dalili ya kughadhibika nami, kisha akaniambia:

"Njoo."

Nikamuendea mpaka nikakaa mbele yake.

Akaniuliza:

"Nini kilichokufanya ubaki nyuma, si ulikuwa ushajitolea kupigana?"

Nikamuambia:

"Ndiyo, Wallahi ningeulizwa suali hili na mwengine asiyekuwa wewe katika watu wa dunia ningeweza kusalimika kwa kutoa udhuru wowote ule. Lakini nilijishauri sana nikaona kuwa ikiwa nitakutolea udhuru wowote wa uongo leo ukaridhika nami, Mwenyezi Mungu atakujulisha na utakuja kunichukia. Na iwapo nitakuambia ukweli, ukaujua ukweli juu yangu, mimi nategemea msamaha wa Mwenyezi Mungu. Wallahi sikuwa na udhuru wowote, Wallahi sikupata kuwa na nguvu na uwezo wa kifedha kuliko siku niliyokuacha na kubaki nyuma.'

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) akaniambia:

"Ama huyu amesema kweli. Inuka na ungoje mpaka Mwenyezi Mungu atakapotoa uamuzi wake juu yako."

Nikainuka na kuondoka hapo, na watu wa kabila la Bani Salamah wakainuka kunifuata, wakaniambia:

"Wallahi sisi tunavyokujuwa ni kuwa hujapata kufanya kosa kabla ya hili, kwa nini umeshindwa kutoa udhuru (wowote) kama walivyofanya wengine? Ingelitosha kufuta dhambi yako kwa maghfira atakayokuombea Mtume kwa Mwenyezi Mungu.

Wakawa wanaendelea kunilaumu mpaka nikafikiria nirudi tena kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) na kutoa udhuru wowote na kujidanganya nafsi yangu.

Kisha nikawaambia:

"Yuko mwengine aliyekuwa kama mimi?"

Wakasema:

"Wawili, wamesema kama ulivyosema na wakaambiwa kama ulivyoambiwa".

Nikauliza:

"Nani hao?"

Wakaniambia;

"Mirara bin Rabial Umariy na Hilal bin Umayyah Al Waqii-y."

Hawa ni watu wawili wacha Mungu waliopigana vita vya Badar na walijulikana kuwa ni wenye mfano mwema.

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) akaamrisha sote watatu tusisemeshwe na mtu.

 

Tukawa tunawaepuka watu na wao wanatuepuka. Haukupita muda watu wakaanza kutubadilikia hata nikaichukia ardhi ikawa kama nisiyoijuwa. Tukaendelea katika hali hiyo muda wa siku hamsini. Wenzangu walijikalia majumbani mwao wakilizana, lakini mimi nilikuwa kijana zaidi kupita wao na mwenye ustahamilivu zaidi. Nikawa natoka na kusali msikitini pamoja na Waislamu, huku nikitembea sokoni, lakini hakuna mtu anayenisemesha. Nilikuwa nikimkabili Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) na kumsalimia akiwa amekaa mahali pake baada ya Swala, kisha hujiuliza nafsini mwangu:

'Mdomo wake ulitikisika kuijibu salamu au haukutikisika?'

Mara nyingi huswali karibu yake, na baada ya swala, humtizama kwa kuibiaibia huku nikijishughulisha na dua baada ya Swala, na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) alikuwa mara nyingine akiniangalia, lakini ninapomuangalia mimi, yeye huugeuza uso wake.

 

Dhiki ya kupigwa pande ilipozidi nikaamua siku moja kwenda nyumbani kwa Abi Qatadah ambaye ni mtoto wa ami yangu, na nilikuwa nikimpenda sana. Nikaparamia ukuta, nikaingia uani na kugonga mlango wa nyumba yake, nikaingia ndani na kumsalimia. Wallahi hakuijibu salamu yangu.

Nikamuambia:

"Aba Qatada! Unavyonijua mimi kuwa simpendi Mwenyezi Mungu na Mtume wake?"

Akanyamaza asinijibu kitu. Nikamuuliza tena suala hilo hilo, akanijibu:

'Mwenyezi Mungu na Mtume wake ndio wanaojua.'

Machozi yakanitoka. Nikaondoka na kuruka ukuta nikatoka nje.

 

Siku moja nilipokuwa nikitembea sokoni nikamsikia mmoja katika watu wa Sham aliyekuja kufanya biashara ya vyakula akisema:

'Nani atakayenipeleka kwa Kaab bin Maalik?'

Watu wakamuelekeza kwangu. Akanijia na kunipa barua iliyotoka kwa mfalme Ghassan iliyoandikwa yafuatayo:

'Nimepata habari kuwa sahibu yako amekupiga pande, na Mola wako amekufanya usiwe na raha, kwa hivyo njoo kwetu tutakuliwaza.'

Nikasema moyoni mwangu:

'Huu pia ni mtihani mwengine.’

 

Nikaitumbukiza barua ile ndani ya tanuri la moto na kuiunguza, na ilipofika siku ya arubaini katika zile siku hamsini, mjumbe kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) alinijia na kuniambia:

"Kwa hakika Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) anakuamrisha usimkaribie mkeo."

Nikamuuliza:

'Nimtaliki au nifanyeje?'

Akaniambia:

'Bali uwe mbali naye na usimkaribie.'

Na wenzangu wale wawili wakapewa amri kama niliyopewa mimi.

Nikamuambia mke wangu:

'Nenda kwa wazee wako na ubaki kwao mpaka Mwenyezi Mungu atakapotoa amri yake.'

 

Mke wa Hilaal bin Umayyah alikwenda kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) na kumuambia:

'Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, kwa hakika mume wangu Hilal ni mtu mzima

asiyeweza kujitumikia mwenyewe na hana mfanya kazi wa kumsaidia, utachukizwa iwapo nitabaki kwake na kumhudumia?'

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) akamuambia:

'Hapana (sitochukizwa), lakini asikukaribie'.

Akasema:

'Wallahi yeye hana haja ya kufanya jambo lolote. Tokea yalipotokea yaliyotokea, mpaka leo hana isipokuwa kulia tu.'

 

Baadhi ya watu wangu wakaniambia:

'Na wewe ungelimuomba Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) amruhusu mkeo akutumikie kama alivyomruhusu mke wa Hilaal bin Umayyah.'

Nikawaambia:

'Wallahi mimi sitomuomba Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam). Sijui atanijibu nini nitakapomuomba, kwa sababu mimi ni kijana bado.'

Nikaendelea katika hali hiyo kwa muda wa siku kumi nyingine, mpaka zikakamilika siku hamsini tokea Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) alipowataka watu wasitusemeshe.

 

Baada ya kuswali swala ya alfajiri ya siku ya hamsini, nikapanda juu ya dari la mojawapo ya nyumba zetu na kukaa. Na wakati nilipokuwa katika hali ile aliyoisema Mwenyezi Mungu kuwa:

'Hata ardhi ikawa dhiki kwao, pamoja na wasaa wake'

Nikasikia sauti kali ikitokea juu ya jabali ikisema:

'Ewe Kaab pokea habari njema.'

Pale pale nilipo nikaporomoka na kusujudu, nikajua kuwa faraja imekwishawasili.

Baada ya swala ya alfajiri Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) aliwatangazia watu juu ya kusamehewa kwetu na Mwenyezi Mungu, na watu wakatoka na kuanza kutupa habari njema hizo. Wengine wakaja kwangu na wengine wakaenda kwa sahibu zangu.

Walikuja wakiwa wamepanda wanyama wao na wengine kwa miguu kwa ajili ya kutupongeza. Na aliponijia yule niliyeisikia sauti yake akinipa habari njema pale mwanzo, nilimvisha guo langu kama ni zawadi yake. Wallahi sikuwa nikimiliki isipokuwa nguo hiyo tu, na mimi nikaazima nguo nyingine za kuvaa, kisha nikaelekea msikitini kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam), huku watu wakinijia makundi kwa makundi wakinipongeza na kuniambia:

'Tunakupongeza kwa toba iliyokuja kutoka kwa Allah.'

'Nilipoingia msikitini, Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) alikuwa amekaa akiwa amezungukwa na watu, na Twalha bin Ubaydullah alikuwa wa mwanzo kunijia mbio na kunipa mkono na kunipongeza. Hakusimama na kunipongeza katika Muhajirin mahali pale isipokuwa Twalha, sitomsahau kwa tendo lake hilo.

 

Nilipomsalimia Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) huku uso wake ukiwa unang'ara kwa furaha, na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) anapofurahi, uso wake huwa unang'ara mfano wa kipande cha mwezi, akaniambia:

'Pokea habari njema za kufikiwa na siku bora kupita siku zote tokea ulipozaliwa.'

Nikamuuliza:

'Msamaha huu umetoka kwako ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, au kutoka kwa Mwenyezi Mungu?'

Akanijibu:

'Bali kutoka kwa Mwenyezi Mungu.'

Nikiwa bado nimekaa mbele yake nikamuambia:

'Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, kwa ajili ya kutubiwa kwangu huku, nataka kutoa mali yangu yote sadaka kwa ajili ya Mwenyezi Mungu.'

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) akaniambia:

'Zuwia mali yako, kwani hiyo ni kheri yako.'

Nikamuabia:

'Mimi nitazuwia sehemu yangu ya Khaibar'.

 

Nikawa kila siku naiambia nafsi yangu:

'Mweyezi Mungu ameniokoa kwa ajili ya kusema kweli. Kwa ajili hiyo katika maisha yangu sitotamka isipokuwa kweli tu. Kwani Wallahi simjui Muislamu yeyote aliyepata mtihani mkubwa kutoka kwa Allah kwa ajili ya kusema kweli tokea siku niliyozungumza na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) mpaka leo hii, kuliko mtihani nilioupata mimi. Na mimi namuomba Mwenyezi Mungu anihifadhi katika siku zangu zilizobaki."

(Mwisho wa maneno ya Kaab bin Maalik (Radhiya Llahu anhu).

 

Kisa hiki ni sababu ya kuteremshwa kwa aya zifuatazo zilizomo katika Suratul Tawbah:

"Mwenyezi Mungu amekwisha pokea toba ya Nabii na Wahajiri na Ansari

walio mfuata katika saa ya dhiki, pale baada ya kukaribia nyoyo za baadhi

yao kugeuka. Basi akapokea toba yao, kwani hakika Yeye kwao wao ni Mpole na ni Mwenye kuwarehemu.

Na pia wale watatu walio achwa nyuma hata dunia wakaiona dhiki juu ya

ukunjufu wake, na nafsi zao zikabanika, na wakayakinika kuwa hapana pa

kumkimbia Mwenyezi Mungu isipokuwa kwake Yeye. Kisha akawaelekea kwa rehema yake ili nao waendelee kutubu. Hakika Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye kupokea toba na Mwenye kurehemu”.

Enyi mlio amini! Mcheni Mwenyezi Mungu, na kuweni pamoja na wakweli.

Haiwafalii watu wa Madina na Mabedui walio jirani zao kubakia nyuma

wasitoke na Mtume, wala kujipendelea nafsi zao kuliko yeye. Hayo ni kwa kuwa hakiwapati kiu, wala machofu, wala njaa, kwa ajili ya Njia ya Mwenyezi Mungu, wala hawendi mahali panapo waghadhibisha makafiri, wala hakiwapati chochote kutokana na maadui, ila huandikiwa kuwa ni kitendo chema. Hakika Mwenyezi Mungu haupotezi ujira wa wanao fanya mema.

Wala hawatoi cha kutoa kidogo wala kikubwa, wala hawalivuki bonde, ila

huandikiwa, ili Mwenyezi Mungu awalipe bora ya waliyo kuwa wakiya- tenda.”

At Tawbah -117- 121

 

Na haya ndiyo wanayostahiki Wahajir (Watu wa Makka) na Ma Ansar (Watu wa Madina), pamoja na makabila yanayokaa nje ya Madina, kwa sababu wao ndio walioubeba Uislamu juu ya vichwa vyao na wakapambana na kila aina ya dhiki, tabu mateso.

Watu hawa walikuwa wakati wote wakisubiri ishara tu kutoka kwa kiongozi wao Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) akiwataka kwenda kupigana Jihadi, na bila ya kurudi nyuma walikuwa wakiuitikia mwito wake.

Walistahiki maghfira na ujira mwema kutoka kwa Mola wao kutokana na kila bonde walilopitia na kila usiku waliokesha na kila njaa waliyostahamili huku wakiwaghadhibisha makafiri kwa kushikamana kwao na kwa ushujaa wao. Walistahiki maghfira kutokana na kila jeraha walilopata katika kupigana Jihadi, na kutokana na kila kidogo au kikubwa walichotoa kwa ajili ya Mola wao.

 

Ama kuhusu wale wanafiki waliobaki nyuma bila udhuru wowote kisha wakaenda kutoa  udhuru wa uongo kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa Sallam) Mwenyezi Mungu alisema juu yao:

"Watakutoleeni udhuru mtapo warudia. Sema: Msitoe udhuru; hatukuaminini.

Mwenyezi Mungu amekwisha tueleza khabari zenu. Na Mwenyezi Mungu na Mtume wake wataviona vitendo vyenu. Kisha mtarudishwa kwa Mjuzi wa ya siri na ya dhaahiri; naye atakuambieni mliyo kuwa mkiyatenda.

Watakuapieni kwa Mwenyezi Mungu mtakapo rudi kwao ili muwaachilie mbali.

Basi waachilieni mbali. Hakika hao ni najsi, na makaazi yao ni Jahannamu,

kuwa ni malipo kwa waliyo kuwa wakiyachuma.

Wanakuapieni ili muwe radhi nao. Basi hata mkiwa radhi nao nyiye,

Mwenyezi Mungu hawi radhi na watu wapotofu."

At Tawbah - .94-96