Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuletea mwezi huu mtukufu wenye Rehma na Maghfira na kutuepusha na Moto, na pia tunamshukuru kwa kutupa fursa hii mara moja kila mwaka ya kujirekebisha, kutubu na kurudi kwake Subhanahu wa Taala.

Kule kuwaona Waislamu kwa furaha na hamu kubwa wakikimbilia kuuona mwezi ukiandama ili siku ya pili yake waanze kufunga, ni dalili ya kuupenda kwao mwezi huu mtukufu. Na kule kuwaona wakijaa misikitini kwa ajili ya kusali Sala zao za fardhi pamoja na Sala ya Taraweh ni dalili ya kuupenda na kuufurahikia kwao mwezi huu mtukufu.

Kule kuwaona Waislamu wakishikamana na misahafu na kuisoma kwa wingi, ni dalili ya kuyapenda maneno ya Mola wao Mtukufu Subhanahu wa Taala na kuupenda kwao wahyi alioteremshiwa Mtume wao Muhammad (Swallah Llahu alayhi wa sallam) ndani ya mwezi huu mtukufu.

Kule kuwaona Waislamu ndani ya mwezi huu mtukufu wakihudhuria kwa wingi katika madarsa, ni dalili kuwa nyoyo zao zimeuelekea sana mwezi huu mtukufu.

Na Mwenyezi Mungu ameufadhilisha mwezi huu mtukufu kupita miezi yote, na Yeye Subhanahu wa Taala ndiye Mwenye kufadhilisha anachokitaka juu ya kingine.

Ni mwezi wa Rehma, kama kwamba siku zake zimeteremka kutoka mbinguni. Ladha yake mwezi huu ni ya aina yake peke yake, harufu yake ni ya aina yake peke yake, hali ya hewa inabadilika, tabia za watu zinageuka, na kila kitu ndani ya mwezi huu kinakhitalifiana kabisa na miezi mingine. Rehma zinatawala ndani ya nyoyo za waumini, na roho ya uchaMungu inaivaa miili nyakati za mchana wanapokuwa wamefunga, wakati inapoingia magharibi wakawa wanaingiza vinywani mwao tende na maji huku wakimuomba Mola wao dua nzuri nzuri zenye kukubaliwa, na hata nyakati za usiku baada ya kumaliza kula futari zao kisha wakakimbilia misikitini kwa ajili ya kuwahi sala ya Tarawehe.

 

Hata thawabu zake mwezi huu zinakhitalifiana na miezi mingine.

Ibada zote Mwenyezi Mungu anawalipa waja wake moja kwa kumi, isipokuwa saumu na subira, hivi Mwenyezi Mungu analipa kupita kiasi.

Katika kufanya amali njema kwa mfano, Mwenyezi Mungu humlipa mja wake mfano wa amali hiyo Moja Kwa Kumi.

Mwenyezi Mungu anasema:

"Afanyae kitendo kizuri, atalipwa mfano wake mara kumi, na afanyae kitendo kibaya (kimoja) hatalipwa ila sawa nacho tu, nao hawatadhulumiwa".

AL AN- AM - 160

Katika kuwasaidia ndugu wa nasaba na katika kusaidia katika kila jambo la kheri, Mwenyezi Mungu humlipa mja wake mfano wa amali hiyo Moja Kwa Mia Saba, Na Humzidishia Amtakaye.

Mwenyezi Mungu anasema;

"Mfano wa wale wanaotoa mali zao katika njia ya Mwenyezi Mungu ni kama mfano wa punje moja iliyotoa mashuke saba; ikawa katika kila shuke pana punje mia. Na Mwenyezi Mungu humzidishia amtakaye (zaidi kuliko hivi) na Mwenyezi Mungu ni Mwenye wasaa mkubwa (na) Mwenye kujua".

Al Baqarah- 261

Lakini katika SAUMU na SUBIRA, Mwenyezi Mungu humlipa mja wake Pasipo Hisabu

Mwenyezi Mungu anasema;

"Na bila shaka wafanyao SUBIRA watapewa ujira wao Pasipo hisabu".

Al Zumar - 10

Na katika hadith al Qudusiy Mwenyezi Mungu anasema;

"Amali zote za mwanadamu ni zake, isipokuwa Saumu, hiyo ni Yangu, na Mimi ndiye nitakayemjazi. Anaacha chakula chake na kinywaji chake na matamanio yake kwa ajili Yangu…"

Na katika riwaya nyingine;

"Amali zote ninalipa moja kwa kumi, na nyengine zinafikia moja kwa mara mia saba, isipokuwa saumu, (Funga), hii Mimi Mwenyewe ninamlipa."

Maulamaa wameleta tafisiri nyingi katika kauli ya Mwenyezi Mungu aliposema;

"Isipokuwa saumu hiyo ni yangu."

Wakasema kuwa; juu ya kuwa amali zote ni kwa ajili Yake Subhanahu wa Taala, lakini saumu haina riyaa ndani yake kama matendo mengine.

Kwa mfano katika ibada ya Sala, mtu anaweza kujionyesha mbele ya watu kuwa anasali wakati moyoni mwake hana khushuu mbele ya Mwenyezi Mungu. Lakini saumu inakhitalifiana na ibada nyingine kwa sababu ni kitendo cha moyo, na mtu anapokuwa peke yake anaweza kula na kunywa bila kuonekana.

Aliyefunga anapata ujira mara mbili, ujira kwa ajili ya kufunga na mwengine kwa ajili ya kusubiri, maana aliyefunga anatakiwa awe na subira kubwa ya kujizuwia na matamanio ya nafsi, na pia kustahamili maudhi ya watu nk.

Kwa ajili hiyo Mwenyezi Mungu anamlipa pasipo hisabu, na wakati huo huo anakuwa amefunga na kwa ajili hiyo jaza yake analipwa na Mola wake Subhanahu wa Taala.

Mola wetu tutakabalie amali zenu njema na uzijaalie ziwe halisi kwa ajili yakoAamin.