1)   Muwaddau Ramadhani, mgeni wetu azizi,
      Waja tuko hamkani, la kheri hatumaizi
      Tumejaa nuksani, usiondoke barizi
      Muwaddau Ramadhani, mgeni wetu azizi.


2)   Waja tuko hamkani, bakia wetu mpenzi
       Tumedhofu nafusini, keleshi tunu tuenzi
       Tutazama madhambini, ukiuka mwana enzi
       Muwaddau Ramadhani, mgeni wetu azizi.
 
3)   Tutazama madhambini, utatushinda uhunzi
      Auni Rabbi Muini, tusijegeuka panzi
      Misumeno muilini, kuchonga kwetu vibanzi
      Muwaddau Ramadhani, mgeni wetu azizi.
 
4)   Auni Rabbi Muini, sasa kwetu ndio kazi
      Vishawishi vya shetani, bayani vyawekwa wazi
      Vioja vya runingani, sumile havimaizi
      Muwaddau Ramadhani, mgeni wetu azizi.

 
5)   Vioja vya runingani, mrama lenda jahazi
       Alotufunza mgeni, dawamu maendelezi
       Etualika ugeni, Rabbana Mola Mlezi
       Muwaddau Ramadhani, mgeni wetu azizi.
 
6)   Alotufunza mgeni, utamu wa tunda lozi
       Tutakuwa punguwani, kukacha hayo malezi
       Wendapo hadi mwakani, tuwe hai maombezi
        Muwaddau Ramadhani, mgeni wetu azizi.
 
7)   Wendapo hadi mwakani, kuja tena l'azizi
       Sote minalfaizini, nabubujika machozi
       Hujaja wauka kwani, mgeni wetu mwombezi?
       Muwaddau Ramadhani, mgeni wetu azizi.
 
8)    Sote minalfaizini, idi fitri muizzi
        Si kuvaa nguo ngeni, na wala bora mchuzi
        Ni kumkwepa shetani, nasaha nazibarizi
        Muwaddau Ramadhani, mgeni wetu azizi.
 
9)   Ni kumkwepa shetani, Allah katupa malezi
      Tisia si asharani, witiri beti ni hizi
       Natudumu ibadani, hili ni langu ombezi
       Muwaddau Ramadhani, nabubujika machozi
.
 

Nakutakieni nyote sikukuu njema.
 Ndugu yenu,
 Ahmed.Rashid