ADABU ZA MSALANI

 

[Na Adam. Yemen]

Muislamu anatakiwa afuate mafunzo ya dini yake katika harakati zake zote,hata anapotaka kwenda haja basi atambue adabu na mafunzo ya Uiislamu kisha afuate.

Nijambo la msingi kufahamu kuwa sehemu za kufanya haja (choo) ni moja kati ya makaazi makuu ya Sheitani, hivyo muislamu anatakiwa achukue kila tahadhari na kufuata miongozo ya Uislamu ili asidhurike na viumbe hivi vibaya. Kuna adabu nyingi za kwenda haja, ambazo Uislamu umetufunza katika hali tofauti,miongoni mwa hizo nikama zifuatazo :

 

1).Kuhakikisha kuwa upo mbali na watu ikiwa unataka kufanya haja sehemu ya wazi, pia jiepushe na sehemu zifuatazo: sehemu yenye kivuli wanachotumia watu kwa mapumziko.

Amesema mtume (s.a.w);

"Jiepusheni na laana tatu (nazo ni) kufanya haja katika vianzio vya maji, njiani na kwenye kivuli.".

Pia chini ya mti wenye matunda, kwenye maji kidogo yaliyotuama.

Amesema mtume(s.a.w);

"Asifanye mmoja wenu haja ndogo katika maji yaliyotwama kisha akakoga ndani yake."

 

2) Wakati wa kuingia sehemu ya haja.Unapotaka kuingia tanguliza mguu wa kushoto huku ukisema maneno haya;

"Allahumma inniy audhu bika minal khubuthi wal khabaith."

Na maana yake ni; "Mola wangu, najilinda kwako na shari ya majini wa kiume na majini wa kike."

 

3) Baada ya kuingia chooni. Kabla ya kuanza kufanya haja ni vizuri kuhakikisha kuwa maji au mawe ya kujitoharisha yapo kwani alikuwa Mtume (SAW) akiandaa maji katika chombo kabla yakufanya haja. pia inakatazwa mtu kuzungumza au kuimba au hata kufanya zogo hadi kusikia walio nje.

 

4) Wakati wa kufanya haja. Utaegemea mguu wako wa kushoto wakati wa kufanya haja hali ya kuwa umechuchumaa kwani inasaidia kutoka uchafu kwa wepesi, na kwa hali yoyote ile jiepushe na kufanya haja ukiwa umesimama. Usiangalie utupu, wala kile kinachotoka, na asikichezee, pia usiangalie mbinguni au kugeuka kulia na kushoto, usielekee kibla wala usikipe mgongo ikiwa unakwenda haja sehemu ya wazi.

Amesema Mtume ( SA W);

"Anapotaka kufanya haja mmoja wenu asielekee kibla wala asikipe mgongo."

Na wala usilielekee jua pale linapozama au linapochomoza. Jihadhari na cheche za kile kinachotoka, kwani Mtume (SA W) amesema;

"Ataadhibikiwa ndani ya kaburi yule asiyejiepusha na cheche (za haja ndogo na kubwa)".

 

5) Baada ya kumaliza kufanya haja zako unatakiwa uhakikishe kuwa hakuna kitu kinachobaki, hivyo unatakiwa ufanye kila njia ili kuhakikisha kuwa uchafu umekwisha, kisha anza kujisafisha kwa kutumia mawe masafi kisha malizia kwa maji, na inatosha kutumia maji matupu bila ya mawe, na pindi ukikosa maji basi mawe yanatosha lakini kwa kutimiza shuruti zake ambazo zimetajwa kwenye vitabu vya fiqhi, pia jiepushe kujisafisha kwa kutumia mifupa au chakula kwani ni miongoni mwa kukufuru neema ya Mola wako, jisafishe kwa kutumia mkono wako wa kushoto na kuanzia sehemu inayotoka haja ndogo.

 

6) Baada ya kujitoharisha.Usikae kwa muda mrefu pale ulipofanyia haja kwani inasababisha ugonjwa wa ini kama ilivyopokewa kutoka kwa Lukman. Baada ya hapo vaa nguo zako kisha utawadhe kama udhu wa sala 7) Wakati wa kutoka. Unapotaka kutoka tanguliza mguu wako wa kulia huku unasema;

"Ghufraanaka - Ewe Mola nakuomba unisamehe, namshukuru Allah aliyeniondoshea yanayoniudhi na kunibakishia yanayoninufaisha"