

MISIKITI WA MAKKA NA MSIKITI WA AL AQSA
Anasema mwanachuoni Ibnul Qayim;
"Msikiti wa mwanzo kujengwa duniani ni msikiti wa Makka, na haya yametajwa katika Sahih Bukhari na Sahih Muslim kutoka kwa Abu Dhar (RA) kuwa amesema;
"Nilimuuliza Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) juu ya msikiti uliojengwa mwanzo kupita misikiti yote, akanijibu;
"Msikiti wa Al Haram (Msikiti wa Makka)."
Nikamuuliza;
"Kisha upi?"
Akanambia;
"Msikiti wa Al Aqsa." (Msikiti wa Baytul Maqdis - Palastina)
Nikamuuliza;
"Miaka mingapi baina yao?"
Akanambia;
"Miaka arubaini."
Na jambo hili limewatatanisha watu wengi kwa kutoelewa lililokusudiwa hapa, wakasema;
'Nabi Suleiman bin Daud (AS) alioujenga msikiti wa Al Aqsa aliishi miaka zaidi ya elfu baada ya kuja kwa Nabi Ibrahim'.
Wanaosema maneno haya hawakuelewa kuwa Nabi Suleiman (AS) hakuujenga msikiti huo, bali aliujadidi tu (alirudia kuujuenga ) lakini aloujenga msikiti huo kwa mara ya mwanzo ni Nabi Yaakub bin Ishaq (AS), aliyeujenga baada ya Nabi Ibrahim (AS) kuujenga msikiti wa Al Kaaba kwa miaka iliyotajwa.
Zadul Maad - Mlango wa fadhila za Makka Juz. 1 uk.8