KWAHERI RAMADHANI

 

·        Enyi waja wa Mwenyezi Mungu! Mwezi wa Ramadhani ndio huo unatutoka, na hazikubaki isipokuwa siku chache sana. Aliyeutumia ipasavyo amefuzu, ama yule aliyepunguza ndani yake akacheza basi siku hizi chache zilizobaki azimalize kwa wema, kwani ubora wa amali ni mwisho wake. Kwa hivyo ongezeni juhudi katika siku chache hizi zilizobaki kwa kufanya amali njema ili Mola wenu akusifieni mbele ya Malaika wake.

·        Ewe mwezi wa Ramadhani! Pole pole, kwani machozi ya wanaokupenda yanazidi kumiminika, na kwa kufarikiana nawe nyoyo zao zinaumia na kuungulika.

Huenda katika kusali nyakati za usiku ndani ya siku zilizobaki huku ukiagwa, kukasaidia katika kuuzima moto wa shauku wa yale waliyopunguza ndani yako.

Huenda nyakati hizo za kutubu na kuacha maasi kukaziba pengo la yale yaliyopungua katika funga yako.

Huenda aliyechelewa na kuukosa msafara wa waliokubaliwa akawahi na kuwa pamoja nao.

Huenda mateka wa madhambi yake akawahi kujikomboa na kuwa huru.

Huenda anayestahiki kuingizwa Motoni akafanikiwa kuepushwa nao kwa toba ya kweli na kwa kushukuru.

Huenda Rehma za Mwenyezi Mungu zikamkumba mtu asi akaongoka na kujinusuru.

Wasalla llahu alaa sayiduna Muhammad wa Alaa aalihi wa Sahbihi wa sallam