HUKUMU YA
KUFUGA MBWA
Na Shamim Khamis
Dini ya kiislam imeweka misingi maalumu
kwa kila jambo na kuliwekea jambo
Katika ufugaji wa mbwa nako pia kumewekwa
sheria zake na taratibu maalumu. Jambo hili la ufugaji mbwa hivi sasa limeenea
sana katika jamii za kiislam kwa kuwaiga watu wa magharibi na wale wasiokuwa
waislam katika tabia zao mbaya na ulazima wa kuwa na mbwa ndani ya nyumba au
familia.
Kwa hakika watu hao hugharamika sana kwa
kuwatunza mbwa wao hata kuwanyima wanaadamu wenziwao, kiasi ambacho mbwa
amepewa sehemu maalumu ya huduma na matumizi pamoja na heshima yake na nafasi
yake katika familia.
Dini ya kiislam kupitia kwa Mtume wake
Muhammad (SAW), kufuga mbwa majumbani bila ya haja yoyote na vile vile kuwepo
mbwa katika nyumba za waislam bila ya haja ni kupelekea kunajisika vyombo na
vitu vyengine kama vile viti, makochi, meza na hata nguo kwa sababu ya miguso
ya mbwa na kuramba kwake sehemu hizo, kwani mbwa mara nyingi ana tabia ya
kuramba ramba na kujiegemeza na vitu kama hivyo vilivyomo majumbani.
Wakati mwengine hufika kuramba sahani na
vyombo vya matumizi ya jikoni na hapo husambaza najisi na virusi vyengine
vibaya sana na hatari sana kwa afya za binaadamu.
Lengo la hadithi hii ni kubaianisha ubaya
wa najisi ya mbwa na hatari zake, kwani najisi nyingi huondolewa mara moja tu
kwa maji, baada ya kuhakikisha imeondoka. Lakini, najisi hii ya mbwa kwa ukali
wake huondolewa mara saba kwa maji ikiwemo mara moja kwa mchanga.
Wamesema baadhi ya maulamaa kuhusu hekima
ya kuzuia ufugaji mbwa bila ya haja, ni kwamba mbwa huwakera wageni
wanaotembelea majumbani kwa kuwabwekea ovyo ovyo na kuwatisha wenye kuuliza na
kuomba msaada majumbani pamoja na kuwakera na kuwaudhi wapita njia.
Muislam duniani anatakiwa asiwakere na
kuwaudhi watu wala kusababisha maudhi kwa wenzake kwa kero na chagizo za mbwa
wake. Mbali na kero hilo na maudhi hayo yanayosababishwa na ufugaji mbwa
kiholela, pia kuna madhara mengine makubwa yanayotokana na jambo hilo ikiwemo
kutokuingia Malaika wa Rehma katika nyumba inayofugwa mbwa.
Ushahidi wa hayo ni kauli ya Mtume (SAW)
aliposema: "Alinijia Jibril (AS) akaniambia nilikuja kwako jana na
hakukuwa na kitu kilichonizuia kuingia nyumbani mwako ila kulikuwa na mbwa
ndani…..". Hadithi inaonesha kuwa Malaika Jibril hakuingia nyumbani kwa
Mtume (SAW) kwa sababu ya kuwepo mbwa ndani yake, hapo Mtume (SAW) akaamrisha
atolewe yule mbwa.
Katazo la kufuga mbwa majumbani bila ya
haja yoyote haina maana ya ruhusa ya kuwatesa mbwa na kuwapiga na kuwaua, bali
mbwa wamestahiki kuangaliwa kama wanyama wengine, kwani wao ni viumbe kama
walivyo viumbe wengine wote, Mtume (SAW) amesema: "Lau kama mbwa si viumbe
kama viumbe wengine, basi ningeamrisha wauliwe".
Mtume (SAW) anatueleza katika hadithi ya
mtu aliyempa msaada mbwa na kumuondoshea kiu iliyomshika sana hata kukurubia
kufa. Mwenyezi Mungu akamshukuru mtu huyo na kumghufiria madhambi yake. Hii ni
kuonesha jinsi uislam unavyojali wanyama wakiwemo mbwa pamoja na viumbe hai
vyengine. Mtume (SAW) amesema;
‘Asie na huruma harehemewi – Mrehemu aliye
ardhini atakurehemu aliye mbinguni’.
Uislam umejenga nidhamu ya kuwatendea
wema viumbe hai bila ya kujali hali zao na kufanya hivyo ni sawa na kutoa
sadaka. Mtume (SAW) amesema: "Na katika kila moyo wa kiumbe hai ni
sadaka".
Inafaa tuelewe kwamba pamoja na kuwa
uislam haupendelei watu kufuga mbwa na kufuga kiholela, lakini pia umeruhusu
watu kufuga mbwa kwa malengo maalum na kwa dharura khasa. Kwa hivyo mbwa
wanaofugwa kwa haja maalum, kama vile mbwa wa kuwinda au wa kulindia mazao au
wa kufugia wanyama au wa haja nyengine yoyote ile, basi hao wametolewa katika
katazo la kutofugwa.
Mbwa hawa walioruhusiwa kufugwa ni lazima
wawe wameelimishwa na kufunzwa vizuri sana, kiasi ambacho wataweza kupokea amri
na kuitekeleza ipasavyo na vile vile ni lazima kwa muislam anaefuga mbwa wa
namna hiyo, achunge sana najis na uchafu unaotokana na mbwa. Hivyo asiwaruhusu
kuingia nyumbani na kuharibu vyombo.
Tabia ya kuweka maduka maalum ya kuuza na
kununua mbwa haifai katika jamii ya kiislam, kwani jambo hilo litapelekea
biashara hiyo ihalalike na kugeuka kuwa ni kitega uchumi na hasa ukiangalia
kuwa baadhi ya Maulamaa wa kiislam wamesema kuwa mbwa yeye mwenyewe ni najis,
kwa hivyo hatofaa kuuzwa kwa hali yoyote ile, kwani najis haiuzwi.
Ingawa wako Maulamaa wengine wanaoruhusu
biashara ya mbwa wa kulindia na kufugia, lakini biashara ya mbwa haiko katika
sura hiyo, bali ni mtindo tu wa mazoea ya kuiga watu wa magharibi juu ya kuwa
na mbwa majumbani mwao.
Waislam tunatakiwa daima tuwe tunaangalia
jambo lenye mas-lahi kwetu kidunia na kidini. Tukiangalia suala la kufuga mbwa
kiholela tutakuta ni kupoteza wakati bure na kuharibu mali zetu kwa
kuwashughulikia mbwa pamoja na kuwahudumikia. Kwa hivyo, suala hili halifai
katika jamii ya kiislam.