Hadithi ya Al Jassaasah

Imetafsiriwa na Muhammad Faraj Salem Al Saiy

 

Utafiti mwingi uliofanywa na wazungu wenye kufuatilia mambo ya ulimwengu wa Mashariki (Orientalists) juu ya dini ya Kiislamu na juu ya Mtume wa Waislamu katika nadharia zao wanaitakidi kuwa mengi kati ya yaliyomo ndani ya mafundisho ya dini ni miongoni mwa itikadi zilizokuwepo wakati ule alioishi Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam).

Kwa maana nyingine ni kuwa kwa vile Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa sallam) aliishi karibu na Mayahudi na Manasara, akaingiliana nao, na wakaingia baadhi yao katika dini ya Kiislamu kumesaidia sana katika kuingiza itikadi zao na kuzifanya kuwa sehemu ya dini hii mpya.

Kusudi la nadharia yao hii ni kuingiza shaka katika utukufu wa ujumbe huu wa mwisho kwa njia ya kuwaambia watu kuwa; Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa sallam) hakuja na kipya katika mambo ya Ghaibu na mambo ya Imani, na kwamba yote anayofundisha ni katika itikadi na ibada zilizokuwepo tokea mwanzo.

Utayaona hayo kwa uwazi katika kamusi mbalimbali za maarifa na vitabu vilivyowekwa kwa ajili ya kuwafundisha watu juu ya dini ya Kiislamu, elimu yake na viongozi wake likiwemo kamusi maarufu 'Daairat al maarif al Islamiyah', walioshirikiana kuliandika wengi katika watu maarufu wenye kushughulikia mambo ya ulimwengu wa Mashariki.

Tutakuta kwa mfano waliyoandika kuhusu 'Tamiym al Daariy', ambaye yumo katika maudhui yetu haya.

Anasema mtaalamu wa mambo ya ulimwengu wa Mashariki kutoka Italia Levy Dalavida:

"Na Tamiym alikuwa mfuasi wa dini ya Kinasara kama walivyokuwa wengi kati ya waarabu wa Syria, akafanikiwa kumfundisha Mtume juu ya ibada nyingi alizojifunza katika dini ya kinasara…. Na inasemekana kuwa Tamiym ndiye wa mwanzo kumhadithia Mtume visa mbalimbali vya dini, Mtume akavisadiki na kuwahadithia watu."

(Mwisho wa maneno ya Levy)

Wakaja wapungufu wa elimu waliofuata maneno haya ya wataalamu hawa wa ulimwengu wa Mashariki na kuyakubali maneno yao kama kwamba ni ukweli usiopingika. Wakazitilia shaka hadithi sahihi zilizoandikwa na kuthibitishwa katika vitabu sahihi kupita vyote, na zilizopokelewa kupitia masdari sahihi, kwa hoja kuwa eti watu wa kitabu 'Ahlul Kitab' wameingiza maneno yao ndani yake.

Sisi hatukanushi kuwa zipo hadithi nyingi za watu wa kitabu, pamoja na tafsiri zao zilizojipenyeza ndani ya vitabu vyetu, na hizi ni habari na visa maarufu ziliokwishatajwa na maulamaa na kuzibainisha kwa watu. Lakini kutumia kisingizio hiki kwa ajili ya kuzikataa hadithi sahihi zilizothibiti, au kuzitumia kwa ajili ya kuwatuhumu Masahaba (Radhiya Llahu an'hum), walioisimamia na kuisimamisha dini hii, ni jambo lisilokubaliwa na Muislamu yeyote.

Mjadala uliozushwa zaidi kuhusu riwaya za Tamiym ni juu ya kisa cha Al Jassasah kilichomo ndani ya Sahih Muslim.

Kisa hiki kilisimuliwa na Fatima binti Qays (Radhiya Llahu an'ha) kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa sallam) aliyekuwa akiwahadithia watu juu ya kisa cha Ad Dajjal kama alivyokisikia kutoka kwa Tamiym aliyekuwa katika dini ya Kinasara kisha akasilimu. Alimhadithia Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa sallam) hadithi iliyokubaliana na aliyokuwa akiwahadithia Sahaba zake (Radhiya Llahu an'hum) juu ya Ad Dajjal na wasfu wake.

Na kisa chenyewe ni kama ifuatavyo:

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa sallam) alikaa juu ya membari huku akicheka akasema: "Kila mtu aushikilie vizuri mswala wake. Kisha akasema: "Mnajua kwa nini nimekukusanyeni (nimekuiteni)?" Wakasema: "Mwenyezi Mungu na Mtume wake ndio wanaojua." Akasema: "Mimi wallahi sikukuiteni kwa ajili ya kukupendezesheni wala kukutisheni, lakini nimekuiteni kwa sababu Tamiym Al Daariy aliyekuwa akifuata dini ya kinasara amekuja kufungamana na mimi na kusilimu. Na amenihadithia hadithi inayokubaliana na niliyokuwa nikikuhadithieni juu ya Masiyh Ad Dajjal. Amenihadithia kuwa:

"Tulipanda merikebu baharini pamoja na wanaume thelathini wa kabila la Lakhm na Judham, na mawimbi yakatuchezea baharini mwezi mzima, mpaka tulipokifikia kisiwa wakati wa magharibi na watu wakakaa ukingoni mwa merikebu (au juu ya ngalawa ya kushushia watu). Wakaingia kisiwani wakamkuta mnyama mwenye nywele nyingi sana, kwa wingi wa nywele hajulikani wapi mbele wapi nyuma.

Wakasema: "Ole wako! Nani wewe?"

Akasema: "Mimi ndiye Jassaasah."

Wakasema: "Nini Jassaasah?"

Akasema: "Enyi watu, nendeni kwa huyu mtu kijijini hakika yeye atakuwa na hamu kubwa ya kujua habari zenu." Akasema: "Alipotutajia jina lake tukahofia asije kuwa shetani." Akasema: "Tukaondoka haraka mpaka tulipowasili kijijini, na hapo tukamuona mtu mkubwa hatukupata kuona mfano wake kimaumbile. Mikono yake imefungwa shingoni pake, na amefungwa kwa vyuma kuanzia magotini mpaka visigino vya miguu yake."

Tukamuambia: "Ole wako, nani wewe?"

Akasema: "Mumekwishazijua habari zangu, nihadithieni juu yenu. Ni nani nyinyi?"

Wakasema: "Sisi ni watu katika waarabu, tulisafiri kwa merikebu na ikasadifu bahari kuchafuka. Mawimbi yakatucheza muda wa mwezi kisha tukateremka katika kisiwa chako hiki. Tukakaa ukingoni mwa merikebu na tulipoingia kisiwani tukakutana na mnyama mwingi wa nywele hajulikani wapi mbele wapi nyuma kwa wingi wa nywele tukamuuliza, 'Ole wako, Nani wewe?' Akasema: 'Mimi ni Jassaasah', tukamuuliza: 'Nini Jassaasah?' Akatuambia nendeni kwa mtu huyu kijijini atakuwa na hamu ya kujua habari zenu. Ndipo tulipokujia wewe haraka na tulimuogopa, tukidhania kuwa anaweza kuwa shetani.'

Akasema: Nipeni habari za mitende ya Biysan.'

Tukamuuliza: 'Nini katika habari zake unataka kujua?'

Akasema: 'Nataka kujua juu ya tende zake. Zishamea? Tukamuambia: 'Ndio'.

Akasema: "Hivi karibuni zitaacha kumea."

Akasema: "Nipeni habari za bahari ya At Twabariyah."

Tukamuuliza: "Nini katika habari zake unataka kujua?"

Akasema: "Yamo maji ndani yake?"

Wakasema: "Maji mengi sana."

Akasema: "Hakika hivi karibuni maji yake yatatoweka."

Akasema: "Nipeni habari za Ain Zaatar."

Wakasema: "Nini katika habari zake unataka kujua?'

Akasema: "Katika chemchem yake yamo maji?

Wakasema: "Ndiyo, maji mengi sana, na watu wake wanayatumia kwa kilimo chao."

Akasema: "Nipeni habari za Mtume wa wasiojua kusoma wala kuandika amefanya nini?"

Wakasema: "Ameondoka Makka na kuhamia Yathrib (Madina)."

Akasema: "Wamempiga vita waarabu?"

Tukasema: "Ndiyo.'

Akasema: "Na yeye amewafanya nini.?

Tukamjulisha kuwa amehamia kwa waarabu wengine wenye kumuunga mkono na kumtii."

Akawaambia: "Yashatokea hayo?"

Tukasema: "Ndiyo."

Akasema: "Ama ni bora kwao kumtii. Na mimi nitakupeni khabari zangu. Mimi ndiye Al Masiy'h, na hivi karibuni nitapewa idhini ya kutoka na nitatoka na kutembea juu ya ardhi, na wala sitoacha kijiji ila lazima nikipitie katika muda wa siku arubaini isipokuwa Makkah na Tiybah (Madina), miji hii ni haramu kwangu kuingia ndani yake. Kila ninapotaka kuingia katika mojawapo ya miji hiyo, ananikabili Malaika aliyeshika mkononi mwake upanga ulionolewa akinizuwia. Hakika katika kila pembe yupo Malaika mwenye kuilinda miji hiyo.

 

Akasema Fatimah: Fatima binti Qays (Radhiya Llahu an'ha) "Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Laahu alayhi wa sallam) alisema huku akichocha gongo lake katika membari: "Hii ndiyo Tiybah hii jdiyo Tiybah hii ndiyo Tiybah (akimaanisha Madina). Si nilikuhadithieni haya?" Watu wakasema: "Ndiyo."

Akasema: "Kwa hakika imenifurahisha hadithi ya Tamiym kwa kuwa inakubaliana na yale niliyokuhadithieni na juu ya Madina na Makkah. Hakika atatokea katika bahari ya Syria au bahari ya Yemen, hapana bali kutoka upande wa Mashariki. Hakika ni upande wa Mashariki, hakika ni upande wa Mashariki." Akaashiria kwa mkono wake upande wa Mashariki."

Akasema: Fatima binti Qays (Radhiya Llahu an'ha) "Nikayahifadhi haya kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Laahu alayhi wa sallam)

 

Maimamu na maulamaa wamekiingiza kisa hiki ndani ya vitabu vyao katika milango ya sifa za Tamiym (Radhiya Llahu an'hu) kama alivyofanya Ibnu Hajar katika kitabu chake

'Al Iswaabah' 1/368 na katika Fathil Bari 12/46 na Imam Annawawiy katika Sharhi ya Muslim.

Amesema Ibnu Hajar katika Al Iswaabah: "Ni mashuhuri miongoni mwa Masahaba, alikuwa katika dini ya Manasara akenda Madina kusilimu."

 

Juu ya kuwa kuwemo hadithi hii ndani ya Sahih Muslim inatosheleza kulazimika kuikubali, kutokana na daraja yake na namna umma wote wa Kiislamu ulivyozipokea hadithi zake. Na wapokezi wote wa hadithi hii ni watu wenye kuaminika, hapana hata mmoja kati yao mwenye kutuhumiwa, hata hivyo hadithi hii imesimuliwa pia na Imam Ahmad na Abu Ya'ala na Ibnu Majah, na Abu Daud, na imepokelewa pia kwa njia ya Masahaba wengine wasiokuwa Fatima binti Qays (Radhiya Llahu an'ha) kama vile Abu Hurairah na Bibi Aisha na Jabir (Radhiya Llahu an'hum) ikiwa ni dalili ya kupokelewa kwa njia mbali mbali na wingi wa njia zake, kwa sababu hadithi hii haikutolewa na Imam Muslim peke  yake na wala haikusimuliwa na Fatima bint Al Qays peke yake.

 

Amesema Al Hafidh (Mwenyezi Mungu amrehemu) katika Al Fat'h  (13/323): "Wamekubaliana kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Laahu alayhi wa sallam) anapokubali linalotendwa au kutamkwa mbele yake asilipinge ni dalili kuwa jambo hilo linajuzu, kwa sababu hawezi kukubali kitendo au neno la uongo au kitendo batil."

 

Ama kudai kuwa haya si katika mambo ya dini ambayo Mitume haijakingwa katika kumsadiki mtu muongo, hilo si kweli, kwa sababu vipi jambo kama hili linalohusiana na dalili za Siku ya Kiama na Imani juu ya Siku ya Mwisho liwe si katika mambo ya yanayohusiana na dini.

 

Isitoshe, kama aliyohadithia Tamiym (Radhiya Llahu an'hu) ni kisa cha uongo ingewezekana kweli wahyi usiteremshwe kukikanusha kisa hicho na kuubainisha ukweli wake, kama ilivyowahi kutokea mara nyingi wakati wanafik na wenzao walipokuwa wakisema kinyume na waliyoficha nyoyoni mwao, na wahyi ukawa unateremka kuwafedhehesha na kubainisha uongo wao?

 

Juu ya kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Laahu alayhi wa sallam) kesha hadithia mara nyingi juu ya Ad Dajjal na kuteremka kwa Isa bin Maryam (Alayhis Salaam) katika zama za mwisho akihukumu kwa uadilifu kwa kutumia sheria ya Mtume wetu (Swalla Laahu alayhi wa sallam), na kwa mikono yake atamuua Ad Dajjal.

 

Yote haya yamesimuliwa kwa njia nyingi sana katika Sahihi mbili (Bukhari na Muslim) na katika vitabu mbali mbali vinavyoaminika. Kwa hivyo habari za dalili ya kukaribia kwa Siku ya Mwisho hazikusimuliwa na Tamiym peke yake(Radhiya Llahu an'hu), isipokuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa sallam) aliitumia fursa pale Tamiym alipohadithia kisa chake ili awabainishie watu kuwa aliyokuwa akiwaelezea ni kweli na uhakika usio na shaka.

 

Hata kama tutachukulia kuwa hadithi hii ni katika Israiliyat, basi ni katika zile sahihi zinazokubalika ambazo tunapaswa kuzikubali kutokana na kukubaliana na sheria yetu.

Dalili ya maneno haya ni kauli ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Laahu alayhi wa sallam) aliposema: "Na amenihadithia hadithi inayokubaliana na niliyokuwa nikikuhadithieni juu ya Masiyh Ad Dajjal…"

Na wengi katika wafasiri wameitafsiri kauli ya Mwenyezi Mungu:

"Na kauli (ya kuja kwa Kiama) itakapowathibitikia tutawatolea mnyama katika ardhi atakayewasemeza kwa sababu watu walikuwa hawaziyakinishi Aya zetu.'

An Naml - 82

Wanasema kuwa myama huyo ni huyu Al Jassaasah aliyetajwa katika hadithi ya Tamiym, kama ilivyosimuliwa na Abdullah bin Amru. Ikiwa ni hivyo, basi aya hiyo ni dalili ya kuisadikisha hadithi hii, hasa kwa vile aya haikanushi kuwepo kwake mnyama huyo kabla ya Siku ya Kiama, kwa sababu inaelezea juu ya kutokea kwa mnyama na si kuwepo kwake. Kwa hivyo anaweza kuwepo kabla ya haya.

 

Kwa kumaliza tunasema kuwa hadithi ni sahihi, na inazipa nguvu hadithi za Ad Dajjal na zile za dalili ya kukaribia kwa Siku ya Kiama.

Kwa hivyo kumtuhumu Tamiym (Radhiya Llahu an'hu) kuwa ni muongo na kwamba kaja kuuchafua uislamu ni tuhuma mbaya kwa sahaba huyu mtukufu (Radhiya Llahu an'hu) ambaye sira yake inashuhudia kuwa ni mcha Mungu na mwingi wa kufanya ibada na wema, bali ni kumtuhumu Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Laahu alayhi wa sallam) pamoja na ujumbe wake, na hili linatosha kuwa ni dhambi kubwa na uovu ulio dhahiri.