MATOKEO YA MWEZI WA RAMADHANI

 

Sameer Zulfikar Ramzan

 

FAT-HI MAKKA

Fat-hi Makka ni kule kuuingiza mji wa Makka katika mikono mwa waislam kama inavyoeleweka kuwa Bwana Mtume Muhammad (Swallah Llahu alayhi wa sallam) baada ya kupewa utume alipata bughdha tele ikambidi kuuhama mji wa Makka na kuhamia mji wa Madinah, na mji wa Makka ni mji mtakatifu na mji ulio bora koliko mji yote duniani.

 

Zimekuja hadithi nyingi zenye kutuelezea utukufu wa mji wa Makka mji aliozaliwa Bwana wetu Muhammad (Swallah Llahu alayhi wa sallam), na mji huu ndio uliokuwa ni  kitovu cha ushirikina kwa wakati huo ujulikanao wakati wa ujinga, na ndio sababu kuu ya kuteremshwa Mtume Makka katikati ya ujinga ili aweze kupambana nao kwa ufanisi zaidi, lakini matokeo yake Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) alifukuzwa na kutaka kuuliwa na ndipo ikajiri kwa amri ya Allah kuuhama mji wa Makka na kuhamia Madinah mji wa jirani yake.

Bwana Mtume alihama Makka akiwa na huzuni kubwa kwani alikuwa akiupenda mno mji huo na Allah (Subhaanahu wa Ta’ala) akahakikisha ndoto ya Mtume wake kwa kuutia mkononi mji huo hali ya kuwa yupo

hai.

Tarehe ya Fat-hu Makka na sababu zake

Ilikuwa katika mwezi wa Ramadhani mwaka wa nane tokea Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) kuhamia Madinah na ilikuwa katika  kumi la pili, na sababu ya kutekwa huko ilikuwa ni kutokana na Makafiri wa Makka kutengua mkataba walioekeana  na Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) katika mwaka wa sita yaani miaka miwili kabla ya tokeo hili. Mkataba huo ulikuwa moja katika mikataba maarufu katika uislam ukijulikana kama Sulhu ya Hudaibia, na ndani ya  mkataba huu kuna mafunzo mengi lakini tutayazungumzia katika makalo zinazofwata inshaallah.

 

Makafiri katika kila zama wanakuwa ni walalamishi na wenye kuvunja mikataba, Makafiri wa Makka walikiuka kipengele kimoja cha mkataba ambacho kinasema kuwa 'pasiwepo na mapambano baina ya waislam na makafiri kwa muda wa miaka kumi'.

Na kipengele chengine walichoki khalifu kilikuwa kinasema;

"kwa yeyote anayetaka kuungana na Mtume katika makabila ya warabu basi ni ruhusa, na yeyote anaye taka kuungana na Makureshi wa Makka ni ruhusa na  watakuwa na hukumu sawa na watakaoungana nao kwa kufanya kazi vipengele vyote vya  mkataba huo.

Sasa hebu na tuangalie matokeo ya ubabaishaji kutoka  upande wa makafiri.

Watu wa kabila la Bani Bakri wakaungana na Makureshi na Bani Khuzaah wakaungana  na Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam), na ikijulikana kuwa makabila haya mawili yalikuwa na gomvi lisilo kwisha. Hapo tena Bani Bakri wakawafanyia uadui bani Khuzaah na kuwavamia usiku na kuwauwa wenzao waliokubaliana kuwacha uadui ndani ya mkataba, na baya zaidi ni kwamba badhi ya viongozi wa Makurshi walishiriki wakitoa msaada wa kila wa aina kwa Bani  Bakri katika dhulma hii.

Mmoja kati ya hao Bani Khuzaah alisalimika na akawahi kwenda kwa Mtum (Swallah Llahu alayhi wa sallam) kutoa khabari na kuomba kunisuriwa, hapo tena Bwna Mtume akaazimia kuiteka Makka kwa hali yoyote ikiwa kwa vita au kwa njia nyengine yeyote ile. Wakati huo Mtume Muhammad (Swallah Llahu alayhi wa sallam) alikuwa na wafuasi wengii walioingia katika islam.

 

Juu ya tendo la kukhalifu mkataba waliowekeana pande mbili, baadhi ya viongozi wa ki-kureshi wakajuta na kujuwa kuwa kitendo walichokifanya kitasababisha kutenguka kwa mkataba wao hapo tena wakamtuma Abu Sufyani aende Madinah akautilie nguvu mkataba huo na kuonyesha kwamba wao hawaungani na hao wenzao walio wauwa Waislam. Lakini kwenda kwake Madina kulikuwa bure pasipo na maana pesa mbili  maana Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) hakumjibu kitu na alinyamza kimya kwani Bwana Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) alikuwa akisubiri kwa hamu fursa hii ili aweze kuitia mkononi Makka na kumaliza nguvu za Makureshi na kiburi chao.

 

Maandalizi ya kuuteka mji wa makka

Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) alifanya maandalizi katika hali ya siri mno kiasi cha kwamba hata Waislam hawakujuwa Mtume anakusudia kwenda wapi? Kwani alikuwa hajawaambia lolote lile zaidi ya kuwa wawe tayari kujiandaa na vita, na kulikuwa hakuna anayethubutu kumuuliza, na Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) akamuambia bibi Aisha  (Radhiya Llahu anha) kuwa amuandalie vifaa vya kivita na akamkataza asimwambie mtu wapi anakokusudia kwenda.

Hii ilikuwa ni hikma ya kivita, kwani  Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) hakutaka Makureshi wagundue azma  yake, na iwe nikuwateka kwa kuwashitukizia tu ikiwa ni moja ya mbinu za kivita inayotumika hata nyakati hizi za sasa.

Tena hapo Bwana Mtume akatuma kikosi cha Waislam kuelekea mbali na mji wa Madinah kujifanya wanapeleleza kitu, bila ya wanaotumwa kujuwa lengo, na majamedari wa siku hizi nao waitumia mbinu hii vile vile, Bwana  Mtume kafanya hivi ili waarabu washughulishwe na kikosi hiki na waone kuwa Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) azma yake ni kupambana na watu wa miji mengine.

 

Maandalizi ya Waislam yalipotimia Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) akawaelezea Masahaba  (Radhiya Llahu anhum) anakusudia kuelekea wapi na akaomba dua;

“Ewe Mola wadhibiti majasusi wasije kuwafikishia Makureshi khabari hizi”.

Na  kabla hawakutoka Madinah, uliteremka wahyi kumjulisha Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) yale aliyoyafanya Hatib ya kutuma barua kwa Makuresh ikuwaajulisha jambo hili. Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) akamtuma Sahaba Ali na Sahaba Zubair na Mikdadi (Radhiyallahu anhum), wamfuate huyo mjumbe mwenye barua nae ni mwanamke, na watamkuta sehemu kaadha.

Wakatoka hadi hiyo sehemu na wakamkuta bibi huyo na kumtaka awape hiyo barua aliyotumwa, na yule bibi akasema kuwa yeye hana kitu, na baada ya mjadala mrefu wakamuambia;

"Imma utowe mwenyewe au tutakuvua nguo", wakimaanisha kuwa wapo tayari kuitowa kwa nguvu, na walikuwa na yakini kuwa bibi huyu anayo barua kwani amri ikishatoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa sallam) basi inakuwa haina shaka.

Yule bibi alipoona kuwa  ataadhirika, akaitoa barua hiyo kwenye misuko yake ya nywele, na wakaichukuwa na kumpelekea Mtume barua hiyo, na Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) alipoamrisha ifunguliwe na isomwe ikagundulika kuwa kumenukuliwa kuhusu kuuvamia mji wa Makka kama alivyopanga.

Bwana Mtume akamgomba sahaba huyu nae akajitetea na kuthibitisha kwamba hakufanya hayo kwa kutoka katika uislamu na Bwana Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) akamsadiki aliyoyasema, lakini kama tunavyoisoma tarekhe ya kiislam mara zote Syd Umar  (Radhiya Llahu anhu) alikuwa ni mtu wa kuchukua maamuzi makali na yakutisha na safari hii ikawa kama ilivyokuwa desturi yake akamuomba Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) amruhusu amuuwe kwani ni jasusi, lakini Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) akamkataza kwa sababu huyo sahaba alipigana vita vya Badri.

 

MSAFARA UKIWA NJIANI

Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) akiwa yumo njiani  kuelekea Makka akakutanaa na ami yake bwana Abbas akiwa na aila yake wanaelekea Madinah wakiwa washasilimu. Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) akafurahishwa sana na tukio hilo la kusilimu kwa ami yake.

Upande mwengine Abu Sufyan aliamua kutoka Makka kupeleleza khabari, kwani kimya kilikuwa kirefu wala hawakuwa wakifahamu Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) anaazimia kufanya nini? Akatoka Abu Sufyan hadi kufika sehemu ambayo akaja akapambana na Bwana Abbas  (Radhiya Llahu anhu) nae akiwa anamtafuta mtu wa kumpa khabari ili aweze kawapelekea Makureshi ya kwamba wajisalimishe na alifanya hivyo baada ya kuomba kwa Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) na kuruhusiwa kufanya hivyo na baada ya hapo bwana Abbas  (Radhiya Llahu anhu) akampakia Abu Sufyan katika farasi wake hadi kwa Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam),  kwa bahati wakati huo sahaba Umar bin Khattab  (Radhiya Llahu anhu) alikuweko huku anatetemeka kumuona Abu Sufyani, na bila ya kusita akamuomba Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) amruhusu amkate kichwa chake,  Bwana Abbas  (Radhiya Llahu anhu) akasema kuwa yeye ndiye aliyekuja na Abu Sufyan, na Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) alipoona kuwa Omar amekuja juu akamuamrisha bwana Abbas aondoke na Abu Sufyan na arudi  nae asubuhi ya siku ya pili yake.

Ilipofika siku ya pili bwana Abbas  (Radhiya Llahu anhu) alikwenda pamoja na Abu Sufyan na Abu Sufyan akasilimu mbele ya Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam), na Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) akasema kuwaambia kina Abu Sufyan akawambie watu wake kwamba;

Atakaefunga  mlango wa nyumba yake akabaki ndani basi atakuwa na amani, na atakaeingia msikiti wa Makka atakuwa katika amani, na atakaeingia nyumba ya Abu Sufyan atakuwa na amani.”

Na hili la mwisho bwana Abbas  (Radhiya Llahu anhu) ndie aliyemuomba Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) ampe kipaumbele Abu Sufyan kwa sababu alikuwa mtu mwenye kupenda fakhari. Kisha Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) akamtaka bwana Abbas  (Radhiya Llahu anhu) apande nae kwenye kijabali ili awaone waislam wote pamoja na nguvu walizokuwa nazo. Hapo tena wakawa wanapita makundi kwa makundi, na kwa kufanywa hivyo ilikuwa ni kumfahamisha Abu Sufyan kuwa watu wa Makka hawatoweza kupambana nao kutokana na nguvu kubwa walizokuwa nazo waislam kwa wakati  huo.

Abu Sufyan akarudi Makka na akawapa khabari watu wa Makka na akawatahadharisha  na kufanya ukaidi, kwani waislam wana nguvu kubwa zisizo kifani ikiwa idadi yao ni kubwa sana. Watu wa Makka waliposikia hivyo wakakimbilia majumbani mwao na wengine kukaa msikitini kama walivyoambiwa kuwa watakuwa na amani wakikaa sehemu hizo.   

 

Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) akaingia Makka hali ya kuwa nimwenye ushindi, na akaingia sehemu iliyo ya juu na huku akamuamrisha Khalid bin Walid  (Radhiya Llahu anhu) aingilie sehemu ya chini yaani upande mwengine akiwa pamoja na waislam wengine na Mtume aliwakataza waislam wasipigane, lakini sahaba khalid alipambana na baadhi ya makafiri ambao waliamua kutotii amri ya Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) na wakaanza kuwapiga waislam, hapo dipo sahabi Khalid  (Radhiya Llahu anhu) nae akaamua kupambana nao hadi kuwashinda.

Kwa kweli hivyo hatuwezi kuvita kuwa vilikuwa ni vita ila tu kuna watu wachache ambao walikuwa ni wakarofi na kutaka kuonyesha ukaidi wao nakutaka kuonyesha kuwa wao wana nguvu, wakauliwa wakaidi hao ikiwa idadi yao ni ipatayo ishirini na nne. Baada ya kuwa hakuna kipingamizi chochote kile hapo tena Bwana Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) na masahaba  (Radhiya Llahu anhum) wakaingia Makka kweupe, hakuna pingamizi ya aina yeyote ile.

 

Kuvunjwa kwa masanamu

Baada ya waislam kuingia Makka nakufika kwenye Al-Kaaba, Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) akamuagizia mshika ufunguo wa Makka bwana Othman bin Talha aulete ufunguo huo nae akatii na kuusalimisha pasi na pingamizi,  bwana huyu alikuwa katika makafiri shupavu (mkereketwa) na aliwahi kumtukana Mtume wakati alipokuwepo Makka na mara moja Bwana Mtume alimtaka ampe ufunguo wa Al-Kaaba na alimkatalia kumpa funguo na Bwana Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) akamuambia itafika siku nitauchukuwa ufunguo huo nawe utakuwa huna nguvu, na siku ilipowadia akautoa, na hapo tena ndipo Bwana Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) akaingia ndani ya Al-Kaaba na kuanza kuyavunja masanamu yote na kuyatupwa nje.

Yasemekana kuwa yalikuwemo masanamu mia tatu na sitini, na Bwana Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) aliyavunja masanamu hayo kwa gongo lake na kuamrisha yavunjwe masanamu yote yaliyokuwepo ndani ya mji wa Makka.

Mshika ufunguo siku hiyo alikuwa ni mtu dhalili kabisa na wakati huo akiwa bado ni kafiri Mtume akamwambia;

"Hakika Allah  (Subhaanahu wa Ta’ala) ameniaamrisha nikurejesheeni ufunguo na hatokunyanganyeni isipokuwa dhalimu”.

Kutoka siku hiyo ufunguo wa Al-Kaaba ukabaki mikononi mwa kabila la mshika funguo huyo. Bwana huyu kuona hali hii ikamuingia imani na akasilimu hapo hapo. Tena ikatoka amri kwa sahaba Bilal  (Radhiya Llahu anhu) apande juu ya Al-Kaaba ili aadhini, na lengo ni kudhihirisha uislamu mbele ya makafiri.

 

Baada ya adhana Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) akahutubia, na mwisho akawauliza watu wa Makka alowateka; “Jee mnafikiri nitakufanyeni nini leo ?

"Wakajibu;

"Wewe ni ndugu mwema na ni mtoto wa ndugu yetu hivyo tunadhani utatufanyia wema tu”.

Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) akawaambia;

“Nendeni hakika nyinyi mpo huru”.

Kutokana na maneno haya wengi kati yao wakasilimu, na wakabaki wachache lakini ikawa kila kukicha husilimu kidogo kidogo hadi Makka nzima ikawa ni waislam watupu.

 

Baada ya hapo wakaja watu makundi kwa makundi  kutoa ahadi Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) ya kumtii na kuwa pamoja naye. Na Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) alipokuwa akitufu Al-Kaaba alitokezea bwana mmoja akawa anataka kumuuwa Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam), akamvizia mpaka akamfikia na hapo tena Bwana  Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) akamgeukia na kumuuliza;

“Nani wewe, Fadhalah?”,

yule bwana akajibu

“Ndiye ni mimi”,

akaulizwa;

“Ulikuwa unakusudia nini kwenye nafsi yako”,

akajibu;

“Nilikuwa namtaja Mola wangu”,

yaani alimdanyanya Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam), na Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam)akacheka kisha akamuambia; “Muombe msamaha Mola wako”.

Kisha baada ya hapo akamuwekea mkono wake mtukufu kwenye kifua chake na akuondoa, na baada ya hapo bwana Fadhalah akawa anasema kuwa;

“Hakuunyanyua mkono wake Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa sallam) kutoka kifuani kwangu illa ikawa hakuna mtu nimpendaye katika dunia hii kama ninavyompenda Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam)".

Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) akakaa Makka siku kumi na tisa, kisha akawatazama Maansari (watu wa Madina) akawaona kuwa wana huzuni kubwa, walidhani kuwa Mtume hatorudi tena Madinah, Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) akawaambia;

"Mimi nitarudi Madinah na nitafia huko huko".

Wakafurahi kusikia hayo kwani huzuni zao ni kwamba watakosa kuishi nae. Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) akarudi Madina pamoja na Masahaba wake (RA) akiwa amefanikiwa kwa yale yaliyotokea na ahadi aliyopewa na Mola wake.

 

Baadhi ya mafunzo

Kuna mafunzo mengi katika matukio haya, lakini sisi tutagusia yale mazingatio yaliyo wazi zaidi.

Mbinu za kijeshi.

Tunaona katika matokeo haya namna gani Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) alivyokuwa akichunga maslahi ya kivita, hata ikawa haitaji sehemu wanayoikusudia isipokuwa siku za mwisho na hili linategemea ukubwa wa lile jambo lenyewe, kwa sababu angelilisimulia mapema pengine MaQureshi wangejiandaa kwa vita na baadae pangekuwa na hali nyengine siyo ile aliyoikusudia Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam)) nayo ni kuivamia Makka kwa amani.

 

Kusafika Makka na ushirikina

Hili halina ubishi kuwa Makka ilisafika na kushirikishwa Allah (Subhaanahu wa Ta’ala) wakati wa uhai wa Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) hadi kufikia kusema kuwa haingii Makka isipokuwa Muislam, na hii ni kutokana na utukufu wa mji huu. Pia kutakasika Al-Kaaba na masanamu yaliyokuwemo ndani yake, jambo ambalo lilikuwa likimuudhi mno Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swallah Llahu alayhi wa sallam) tokea ujanani mwake.

 

Upole wa Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) na usamehevu wake

Katika maisha ya Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) tunaweza tukathibitisha mengi kuhusiana na upole wake na usamehevu wake, na khasa katika matokeo kama haya ambayo yalichukuwa nafasi maalumu katika kuubadilisha ulimwengu huu. Itoshe kuielezea hali ya Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) kwa kuwasamehe Ma-Qureish wa Makka baada ya Fat-hi Makka, alipowauliza na kuwaambia nendeni hakika nyinyi mpo huru.

 

Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam) hakutaka kuyawaza yale yaliyopita kuanzia kuteswa waislam hadi kufukuzwa yeye na kupambana kwa vita pamoja na makafiri hao, yote hayo aliyaweka pembeni na akataka kudhihirisha shakhsiya (personality) yake uungwana wake ambao amesifiwa kwayo ndani ya Qurani kuwa;

“Hatuja kutuma wewe Muhammad isipokuwa uwe ni rehema kwa walimwengu wote”.

Wengine hudhani Mtume (Swallah Llahu alayhi wa sallam)kuja kwake ni rehma kwa waislam tu. Hapana, bali kuja kwake ni rehma hata kwa makafiri, kwani mara ngapi alitakiwa awaapize na uishe uonevu, lakini alikataa na hili lakuwasamehe ni kubwa zaidi maana alikuwa na uwezo wakuamrisha alitakalo. Kuuliwa, kupigwa n.k lakini yote hakuyataka.

Hii  ni kuonyesha usamehevu wake ulivyo na natija ya hatua yake hii ilikuwa ni kusilimu wengi katika Ma-Qureishi baada tu ya kuachiwa huru.

Mungu atujaalie tuwe ni wasamehevu kama alivyokuwa Kiongozi wetu Bwana Muhammad (Swallah Llahu alayhi wa sallam) rehema na amani ziwe juu yake pamoja na ali  zake na masahaba zake. “Amin”.