UHUSIANO WA BABA NA MTOTO WA ZINA AU NA MTOTO WA KULAANI

Anasema Sayed Sabeq katika Fiqhil Sunnah;

"Mwana wa zina ni yule aliyezaliwa nje ya ndoa ya kisheria, na mtoto wa kulaani ni yule ambaye mume ameikataa mimba kuwa si yake".

Mume anaweza kuikataa mimba kuwa si yake ikiwa atakuwa na mashahidi wanaoweza kuthibitisha hayo, au ikiwa ataapa viapo vinne kuwa yeye anasema kweli na mara ya tano aape kuwa laana ya Mwenyezi Mungu iwe juu yake ikiwa anasema uongo.

Mwenyezi Mungu anasema;

"Na wale wanaowasingizia wake zao (kuwa wamezini) na hawana mashahidhi ila nafsi zao, basi ushahidi wa mmoja wao utakuwa kushuhudia mara nne kwa kiapo cha Mwenyezi Mungu ; ya kwamba bila shaka yeye ni mmoja wa wanaosema kweli.

Na mara ya tano (aape) kwamba laana ya Mwenyezi Mungu iwe juu yake ikiwa ni miongoni mwa waongo.

Na (mke) itamuondokea adhabu kwa kutoa shahada mara nne kwa kiapo cha Mwenyezi Mungu ya kwamba (huyu mume) ni miongoni mwa waongo.

Na mara ya tano (aape) ya kwamba hasira ya Mwenyezi Mungu iwe juu yake kama (mumewe) yu miongoni mwa wanosema kweli, (na yeye mke ndiye muongo)".

ANNUR-6-9

Mwana wa zina (aliyezaliwa nje ya ndoa na mwana wa kulaani ambaye mzee wake amemkataa, hawa hawarithiani na baba zao, yaani baba hamrithi mwana wala mwana hamrithi baba, na mtoto huyo anaungana na mama yake moja kwa moja na kurithiana naye.

Kuhusu hukumu hii hakuna hitilafu baina ya maulamaa wa Kiislam, kutokana na kutokuwepo kwa uhusiano wa kisheria baina yao.

Kutoka kwa Ibni Omar (RA) kuwa katika wakati wa Mtume (SAW) mtu mmoja aliapa kwa njia ya kulaani kuwa mtoto si wake, na Mtume (SAW) akawatenganisha baina yao na kumhusisha mtoto huyo moja kwa moja na mama yake.

Bukhari na Abu Daud

Lafdhi ya hadithi inasema hivi;

"Mtume (SAW) amehukumu kuwa mtoto aliyekataliwa na baba yake kwa njia ya kulaani kuwa (hatorithiana na babake, bali) atarithiana na mamake na atarithiana pia na wale wanaoweza kumrithi mama yake".

Kifungu nabari 47 cha sheria ya mirathi ya nchi ya Misri kinasema;

"Mwana aliyezaliwa nje ya ndoa, na mwana aliyekataliwa kwa njia ya kulaani, anarithiana na mamake na jamaa za mamake".

Muhammad Faraj Salem