USIA

 

Mtungaji : Sh. Abdulla Bakathir (Kadara) Mola amrehemu  

                Lamu . Mwaka unakadiriwa 1960  

 

Kwa jina la Mwenyezi Mungu , mwingi wa rehema mwenye kurehemu

  

1.    Bisimillahi kutubu - Ina la Mola Qaribu - Alompesi kujibu - Alomoumba kwa niya.

 

2.    Nandike na Rahamani - Mrahamu masikini - Na matajiri bengini - Kwa mali kuwayaziya

 

3.    Nandike na Arrahimu - Wema alowakirimu - Kuwapa njema ilimu - Wakaweza kutumiya

 

4.    Kisa naleta himdi - Kwa neema na kuzidi - Umati wa Muhamadi - Nami nikawa mmoya

 

5.    Ninashukuru kwa haki - Alonipa tawfiki - Wanangu na marafiki - Kuwapa huu wasiya

 

6.    Ina Bahiya Durari - Yenye na tabia nzuri - Mimi nimeifasiri - Ipate kuwaeleya

 

7.    Na mukisa kuipata - Somani bila matata - Pamoya na kufuata - Yote nalowandikiya

 

8.    Maradhi yamenishika - Siku sita zimefika - Siyaweza kutamka - Maneno kukuuswiya

 

9.    Watu wakidirikana - Henenda wakiagana - Ghafula huepukana - Pasi na kukusudiya

 

10.    Mengi nimekuuswiya - Ila sikukwandikiya - Sasa hini nipokeya - Mwanangu utatumiya

 

11.    Mauti kwetu ni haki - Wala usingiye dhiki - Na ikiwa nimebaki - Na mengine takwambiya

 

12.    Kwani mimi si wachuma - Kuna siku nitakoma - Ni sasa kwa hini huma - Awtani tatembeya

 

13.    Lakini naomba Mungu - Nishike wano wanangu - Nizike na mama zangu - Kisa yapo taifiya

 

14.    Ikiwa nimeondoka - Usipende kuzunguka - Baraza zenye dhihaka - Sio nzuri kuongeya

 

15.    Wanenapo masikini - Tukuonapo ndiyani - Twamkumbuka fulani - Mayondi yatakwingiya

 

16.    Wakikwalika harusi - Ukiwa nayo nafasi - Nenda ungiye upesi - Palo pema kukaliya

 

17.    Pindi wakubwa wayapo - Nafasai tena haipo - Huinika wewe hapo - Heshima ukamwekeya

 

18.    Ule alokualika - Mno atafurahika - Takua kihangaika - Nafasi kuizengeya

 

19.    Usiketi ziatuni - Wala tini mlangoni - Itiye uwandazini - Nafasi itatokeya

 

20.    Wenendapo karamuni - Usiswifu ya fulani - Kunena si kama hini - Nla takachokwekeya

 

21.    Kama nyama imekwisha - Mtuzi haujafisha - Wata kumuhangaisha - Kumwambiya nieteya

 

22.    Pengine huwa hakuna - Nae hawezi kunena - Hutahayari maana - Si uzuri kumwambiya

 

23.    Mahala usoalikwa - Tahadhari na kufika - Japo kwa mjomba kaka - Kwenenda nakuzuwiya

 

24.    Akiwa alisahau - Hakika hakudharau - Kikuiliya hiyau - Inika andama ndiya

 

25.    Ukitoka hadharani - Sikae mabarazani - Fuliza kwako nyumbani - Pija hodi kisa ngiya

 

26.    Uchambiwa ningojeza - Usingie na kufuza - Wala kisa kuuliza - Ni mtu gani nambiya

 

27.    Situngie mivunguni - Maghala za zipembeni - Kufuli zimo nyoyoni - Wata fafani kungiya

 

28.    Kiwa wewe wapoteza - Na yeye zake tauza - Ukiwa unatengeza - Naye atakuwekeya

 

29.    Siulize majirani - Ayao kwangu ni nyani - Kweli haipatikani - Wasiwasi utangiya

 

30.    Kufuli ya mwanamke - Huwa nayo mume wake - Isha akirudi kwake - Mke hendi kutembeya

 

31.    Mume kenda senemani - Mke henda kwa jirani - Arudipo hatamani - Kuzungumza na ndiya

 

32.    Yule yamempendeza - Alikokwenda kuteza - Jirani huku meyaza - Maovu amemwambiya

 

33.    Watu huhishimiyana - Ndipo hapo hupendana - Ukali kujibizana - Hupitisha kupoteya

 

34.    Simtukane mkeo - Kiwa mbele ya wanao - Au watu wangiyao - Wakawa watasikiya

 

35.    Kikuudhi hadhirani - Sidhihirishe usoni - Ngoja mkingiya ndani - Nena kwa kutaradhiya

 

36.    Kiwa mekuwa mkali - Sinene mara ya pili - Epuka wenende mbali - Tasahau mara moya

 

37.    Si aibu usishike - Kumrai mke wake - Mtume ni kazi yake - Kwa wote wake tisiya

 

38.    Na upatapo kijana - Teza nae wewe sana - Maboi sipende sana - Zijana kukuyeleya

 

39.    Shika mwanangu mpenzi - Kijana kuwa azizi - Twabiya ni ya muyezi - Ndiyo takayotumiya

 

40.    Boi akiwa mpevu - Khaswa likiwa na nguvu - Afadhali mpe livu - Mngine wewe zengeya

 

41.    Nguo zako matambara - Usimpe hata mara - Zikiwa hazina sura - Kheri zungu kupuliya

 

42.    Boi akiwa nyumbani - Nasivae leso tini - Kheri umpe kiguni - Au kitambi kipiya

 

43.    Boi kiwa na maneno - Mazuri yaso mfano - Muyuwe hafai neno - Ni mpuzi nakwambiya

 

44.    Mtafute mtatufu - Asokuwa na harufu - Wala asiwe mchafu - Wa mwili na wa tabiya

 

45.    Akiwa mtu mzima - Kumi na tatu mekoma - Mfukuze kwa salama - Wewe mngine zengeya

 

46.    Na ulalako chumbani - Sikaribishe mgeni - Na ukiwa kitandani - Siwate mtu kungiya

 

47.    Kitanda cha mke wako - Kukiona waliyoko - Mama hata ndugu zako - Ni aibu nakwambiya

 

48.    Ila ukosapo budi - Kuna mambo yamezidi - Kula ayao harudi - Lazima ataingiya

 

49.    Na ungiyapo chumbani - Sauti na iwe tini - Aliyoko ukumbini - Asiwe wa kusikiya

 

50.    Ukiwa na mtumishi - Sifanye nae ubishi - Usizidishe uteshi - Walau kumrukiya

 

51.    Nasiyuwe siri zako - Walau aibu yako - Atakuondolea mbeko - Ni swalaha takwambiya

 

52.    Siri siweke moyoni - Wala sitie bengini - Wala simpe jirani - Fahamu itaeneya

 

53.    Siri isipite kanwa - Wala kwa mato kuonwa - Siri ni isiyonenwa - Inenwapo hueneya

 

54.    Mtu nasikupe siri - Kisa akakukariri - Simpe mtu khabari - Kataa kuisikiya

 

55.    Mwambiye alokuyuza - Mbona wewe hukuweza - Kwangu umeitangaza - Nami watu tawambiya

 

56.    Boi akija chumbani - Nasimame mlangoni - Nasitie guu ndani - Hata kukufagiliya

 

57.    Alfajiri amka - Wakati usiyatoka - Kuku achanda kuwika - Muwe mwawika pamoya

 

58.    Inuka ungie choni - Uswali rakaateni - Usome arubaini - Ya hayyu Ya Qayyumiya

 

59.    Uchelewapo kwamka - Yuwa mbele limetoka - Watu wametiarika - Nyumbani wameeneya

 

60.    Kwanda sitoke chumbani - Imunike kiyooni - Uchafu ulo usoni - Uoshe ulokungiya

 

61.    Usipite kwa ziyatu - Penye hadhara ya watu - Za miti huwa si mtu - Hishima huwavundiya

 

62.    Ila kwa kuzoweyana - Au wawe ni zijana - Hapo makosa hapana - Waweza kuivaliya

 

63.    Shai kunwa ukumbini - Sipende kunwa chumbani - Paka tungu mivunguni - Fahamu wataeneya

 

64.    Saa itie majira - Ijaribu kula mara - Ukichelewa si sura - Kazini kwenda kungiya

 

65.    Uingiyapo kazini - Wape watu gudi moni - Kwa furaha za usoni - Pamoya na kutekeya

 

66.    Wote waite mabwana - Au waite manana - Furaha ukiziona - Kila siku endeleya

 

67.    Yaliyokhusu siyasa - Sizungumze kabisa - Ngojeya kazi ikisa - Na wengine endeleya

 

68.    Mno siifanye tamu - Utakuwa maadumu - Kanwani usiwe sumu - Watu watakutukiya

 

69.    Itiye mwao matoni - Itowe mwao ndimini - Barizi mwao nyumbani - Shikiyo utakaliya

 

70.    Siiza uitiwalo - Sikiza uambiwalo - Teuwa ulitakalo - Yesapo kukueleya

 

71.    Ukenda nyumba ya mtu - Ukaona kuna zitu - Usinene nami kwetu - Yako mambo kama haya

 

72.    Uwate kumuuliza - Kitu hiki wewe huza - Mno kimenipendeza - Au kuomba kimoya

 

73.    Wala sikae kitini - Kilokabili chumbani - Na uketipo mezani - Wata zitu kutezeya

 

74.    Mzungu akikwalika - Mezani akakuweka - Chakula boi kaweka - Na mai kuwatiliya

 

75.    Uma shika kushotoni - Kisu shika kivulini - Kijiko kiwe yamini - Ni uzuri wa kuliya

 

76.    Kitambaa kushotoni - Kiwe mwako mkononi - Zambatazo mdomoni - Ukawa utafutiya 

 

77.    Kiwa ni Mtaliani - Huifunga na shingoni - Na nta moya mezani - Uchafu kuzuwiliya

 

78.    Wakikweteya khamri - Usinwe wambiye sori - Atafahamu uzuri - Huipendi kutumiya

 

79.    Tahadhari siteuke - Katika hadhara yake - Afadhali uondoke - Faraghani kimbilya

 

80.    Kuteuka ni aibu - Ni kama shuzi swahibu - Wahindi na Waarabu - Wao wanaifanyiya

 

81.    Ila wasitaarabu - Ambao wana adabu - Mve kwao ni aibu - Zitabuni wametiya

 

82.    Kuteuka hadhirani - Ni kama shuzi mwendani - Khususa kwa Ungujani - Na Maka na Misiriya

 

83.    Ukiweko hadhirani - Sitie zanda puani - Sitiye masikiyoni - Na meno kutotoleya

 

84.    Usiikune matako - Usishike mbele yako - Ziwiya mikono yako - Hadhirani kutezeya

 

85.    Muhindi akikwalika - Kawa chumbi akaweka - Kwanda kwa chanda andika - Na ulimini kutiya

 

86.    Ladu tamu huya kisa - Usile hata zikesa - Wali huya kwa matasa - Hula ukiengezewa

 

87.    Ukiwako hadhirani - Ndi akaya usoni - Sighadhibike mwandani - Makofi ukaitiya

 

88.    Mtatuwe kwa raufu - Utowe yako hanchifu - Usoni futa uchafu - Mara moya takimbiya

 

89.    Ukiwako hadhirani - Au ukawa mgeni - Chakula kiko mezani - Na paka tini huliya

 

90.    Chakula kilichowekwa - Tonge usimpe paka - Na kuku wa kuzunguka - Hufai kuwatiliya

 

91.    Wewe walikusudiwa - Kula tonge uchambuwa - Kuku wake awayuwa - Mwenyewe tawatiliya

 

92.    Nyumba ya watu swahibu - Kiwa mekuya gharibu - Usimwambiye karibu - Kiwa umetanguliya

 

93.    Kwako akiya mgeni - Mpe mai gilasini - Kisa muoneshe choni - Na pa kupumzikiya

 

94.    Kiyeta simu mgeni - Simngojee nyumbani - Mfuatiye stani - Au mtu kumwekeya

 

95.    Kiwa mtu wa barani - Simbo una mkononi - Pokeya uweke ndani - Ndipo naye taingiya

 

96.    Kiwa ni wa Mambasani - Tanga na Uungujani - Begi una mkononi - Boi au wewe pokeya

 

97.    Wageni furaha kwao - Ni kupata nyumba yao - Ufunguo wawe nao -  Bila ya hodi kungiya

 

98.    Nyumba ikiwa na hodi - Mgeni siku hazidi - Huwa si yake kasidi - Ni dhiki zimemngiya

 

99.    Ukiwa wewe mgeni - Umeshukiya nyumbani - Sichelewe chakulani - Ni yambo lina udhiya

 

100.    Sichelewe kwenda kula - Na wakati wa kulala - Na uchalikwa mahala - Na mapema humwambiya

 

101.    Huu ni wangu waswiya - Mwanangu nakuusiya - Iwapo utaugwiya - Utaepuka balaya

 

102.    Na mtu akikutaka - Nende kule waloshuka - Kwao yakimalizika - Na wewe watakwambiya

 

103.    Akikwambiya mwendani - Hapa mekuya fulani - Amekutaka fulani - Mwende mukale pamoya

 

104.    Nguo zako piga pasi - Teuwa njema libasi - Sita wa robo jilisi - Tayari wa kumwendeya

 

105.    Ukenda kwake nyumbani - Simwandame hata ndani - Kwanda kaa barazani - Mpaka wambiwe ingiya

 

106.    Hapo kikuweka ndani - Kikuweka kitandani - Au ukiwa kitini - Sikatae nakwambiya

 

107.    Sinene ukiitesha - Kunena hapa patosha - Sikiza akikwamrisha - Ni kwake umeingiya

 

108.    Tena uwazungumze - Maneno yawapendeze - Urongo usiuzuze - Ya kweli ukiwambiya

 

109.    Kiwa wamekupulika - Kwa furaha na kuteka - Kuwengeza wametaka - Ni bora kuendeleya

 

110.    Kiwa hawakusikiza - Ni heri ukanyamaza - Si bora kuwaengeza - Asotaka kusikiya

 

111.    Usiwe kutetemeka - Kwa wakati wa kuteka - Heh tatu zikifika - Kiteko kimetimiya

 

112.    Wala sifunuwe kanwa - Watu ndani wakaona - Wala usiteke sana - Hadhirani nakwambiya  

 

113.    Towa salamu mwendani - Wenendapo barazani - Upite ukae ndani - Wakikwambiya kungiya

 

114.    Wakitonena karibu - Sikae nao swahibu - Wala sione ajabu -  Wana siri nakwambiya

 

115.    Wakiwa wazungumza - Kwanda nenda pulikiza - Mpaka wakiuliza - Khabari utawambiya

 

116.    Usende ukaitiya - Maneno kwa kukatiya - Wao wametanguliya - Sizungumze sikiya

 

117.    Unenapo barazani - Siakie mayamini - Wallahi tena fulani - Ni kweli nalokwambiya

 

118.    Wendapo taaziyani - Popote na karamuni - Sitoke mbele mwandani - Ila wakikuambiya

 

119.    Waandazi wakikoma - Mwenyewe atasimama - Hasanta atasema - Hapo utaitokeya

 

120    Ikiwa utaondoka - Kabula kumalizika - Asopata atatoka - Kwa wandazi ni udhiya

 

121.    Ukiwa huna makini - Sitoke kwako nyumbani - Ukenda makaramuni - Watu kuwaharibiya

 

122.    Wenendapo karamuni - Nyama ngumu ya kanwani - Sirudishe sahanini - Ni uchafu nakwambiya

 

123.    Ukiweko chakulani - Mifupa kibakulini - Duhu lilomifupani - Usiigonge sikiya

 

124.    Usisonde zilizomo - Ukatongowa midomo - Au kurudisha mumo - Wesapo kuutumiya

 

125.    Karamu iliyo nzuri - Yenye mai ya sukari - Ziwili sinwe khatari - Hutosha kunwa kimoya

 

126.    Yatiwapo gilasini - Zanda usitie ndani - Tumiya kwa kushotoni - Kiwa wavuli huliya

 

127.    Utumiya wa vulini - Ukiwa swafi mwandani - Pumzi sitie ndani - Gilasi ukitumiya

 

128.    Utotowazo menoni - Zisirudi matumboni - Wala sishike zandani - Kisa ukazangaliya

 

129.    Sende kwa mtu mtana - Kwa siku za joto sana - Ukamwita ewe bwana - Haya nimekuiliya

 

130.    Ingoje kumi na nusu - Ufanye kwake julusu - Haikupati nuhusu - Waweza kuikaliya

 

131.    Kwa mtu sende mtana - Au asubuhi sana - Na isha sikiza sana - Qur-ani yatwambiya

 

132.    Baada hapo nendani - Kwa swahibu na jirani - Imenena Qur-ani - Ilahi ametwambiya

 

133.    Na safarini ukiwa - Kwenu peleka baruwa - Hali wapate kuyuwa - Yote yalokujiriya

 

134.    Kwa mama mwenye jamali - Na mkeo wa halali - Kwa bashasha mbalimbali - Usitanganye pamoya

 

135.    Baruwa na iwe tamu - Ya kuwatowa hamumu - Yale yatiayo hamu - Sipende kuwandikiya

 

136.    Watiliye ya furaha - Na maneno ya mzaha - Mazuri yenye nasaha - Ya faida kutumiya

 

137.    Siarifu ya huzuni - Kuwaweka kitandani - Umbali hawakuoni - Wakabaki na kuliya

 

138.    Usiwate mfukoni - Deri buku ndiyani - Yajiriyo duniyani - Upate kuwandikiya

 

139.    Andika uyatakao - Ya haraka na kituo - Ya kesho au ya yeo - Na uloazimiya

 

140.    Ukiweko safarini - Una kitu cha nyumbani - Rafiki simuamini - Kumpa kukupekeya

 

141.    Akiwa rafiki yako - Nawe una mke wako - Simtoleze ni miko - Au utaiyutiya

 

142.    Sinene namuamini - Hawezi huyu kukhini - Fahamu kuna shetani - Fitina tawatiliya

 

143.    Zulekha mkumbukeni - Ni mwanamke amini - Yusufu kungiya ndani - Kwa nguvu kaishikiya

 

144.    Kamtiya aibuni - Kafungwa na gerezani - Hata Mungu kabaini - Zulekha kaikiriya

 

145.    Mke wa rafiki yako - Mumewe kondowa miko - Usingie kama kwako - Ila na yeye pamoya

 

146.    Na mungiyapo nyumbani - Kitwa inamiya tini - Simtazame usoni - Mke wa nduyo sikiya

 

147.    Fahamu kutizamana - Kunako khatari sana - Mato kukabiliyana - Moyo hufanya udhiya

 

148.    Mambo yako ya nyumbani - Sizungumze ndiyani - Sishitaki majirani - Wala mamako akiya

 

149.    Kizere aso kuruba - Kwako asiwe suhuba - Tawatiliya mswiba - Wa kuteta mara moya

 

150.    Huwa hana la kunena - Ila kutiya fitina - Na kukumbuka ujana - Wake alokitumiya

 

151.    Uonapo amefuza - Kuya kuizungumza - Ni kheri mkampuza - Musende kumsikiya

 

152.    Angiyapo ondokani - Muingiliye chumbani - Mumuwate ukumbini - Kwa uzuri kumwambiya

 

153.    Simrukiye kizere - Wala simteze shere - Wala simtume bure - Na wewe yatakujiya

 

154.    Kizere ni mabruki - Kiwa kizere cha haki - Zingine ni zishiriki - Simuamini mmoya

 

155.    Lakini siwatukiye - Maneno siwaambiye - Iwa na hadhari naye - Mambo kukuharibiya

 

156.    Jirani tumeusiwa - Yataka kuwangaliwa - Haifai kuudhiwa - Mtume ameziwiya

 

157.    Zigari sinunuweni - Kuwapa wano nyumbani - Fahamu wako jirani - Wane watamliliya

 

158.    Musikangeni mituzi - Kwa thaumu na ziyazi - Kama kumpa huwezi - Jirani kumpekeya

 

159.    Hufai kutamanisha - Kwa mituzi ya kupisha - Himtiya mshawasha - Na wane humliliya

 

160.    Umrahamu jirani - Akiwa ni masikini - Kwa wali kibakulini - Na wane kuwangaliya

 

161.    Hadhira yako nyumbani - Kwanda mwambie jirani - Kisa ngia mtaani - Kisa mbele endeleya

 

162    Sipende watu adhimu - Na suhuba za hakimu - Watakuzidisha hamu - Na dhiki zitakungiya

 

163.    Kiwa mumefuatana - Watu wote watanena - Apenda makuu sana - Kwa hakimu meitiya

 

164.    Kiwa watu wamenena - Siri ikijulikana - Hukutuhumu fitina - Ni wewe umeitiya

 

165.    Usipende matajiri - Katukiya mafakiri - Wenye twabiya nzuri - Suhuba zao zengeya

 

166.    Wagonjwa watizameni - Sipitali na nyumbani - Lakini musikaeni - Muda ukaendeleya

 

167.    Muwee kumkaliya - Mara dhiki humwingiya - Hawezi na kukwambiya - Twaa kiyasi sikiya

 

168.    Kwake ngiya mara moja - Ila kikwambiya ngoja - Pengine huwa na haja - Chooni ataka ngiya

 

169.    Uwapo ni msafiri - Rafikiyo una gari - Nauli ikikaswiri - Usende ukarukiya

 

170.    Siteze na yake mali - Epuka ukae mbali - Kiwa swahibu wa kweli - Yeye atakuzengeya

 

171.    Na safari za malori - Kufunikwa tonobari - Usiingie si nzuri - Zina na mwingi udhiya

 

172.    Na ungiyapo relini - Tikiti kata sekani - Singie za rahisini - Kisa zitakutukiya

 

173.    Sasa nitatia koma - Siwezi tena kusema - Rabbi mnusuru mama - Na umbu langu pamoya

 

174.    Nina umbu masikini - Alomwingi wa imani - Uzito wangu kitwani - Yeye amenipokeya

 

175.    Muawini Ya Karima - Kwa zijana waso mama - Wao wanamsukuma - Na yeye huwatapiya

 

176.    Ilahi ndiwe muweza - Nina mamangu ajuza - Muhifadhi kwa kufuza - Na maisha ya afiya

 

177.    Nimechoka siyakoma - Mikono hunitetema - Siku nyingi nina huma - Hunu ni wangu wasiya

 

178.    Huu ni wasiya wangu - Kuwausiya wanangu - Kwani huona utungu - Kiwa mepotoka ndiya

 

179.    Penda awe mtukufu - Huyu mwanagu Yusufu - Na watu wamsharifu - Kiutumiya waswiya

 

180.    Waswiya si wake pweke - Ni yeye na ndugu zake - Na marafiki wandike - Pamoya na kutumiya

 

181.    Alotunga ina lake - Wamwita rafiki zake - Kadara ni yeye pweke - Alotangaa duniya

 

182.    Na lengine mashuhuri - Abdalla Bakathiri - Apenda mno safari - Hadiriki kutuliya

 

183.    Mtuze Rabbi Manani - Katika wake watani - Mpe kazi na makini - Za baraka na afiya

 

184.    Umondolee husuda - Tengeza zake ibada - Mrejeze kama ada - Imwekelee duniya

 

185.    Na jamii Isilamu - Walo kisiwa cha Amu - Na wengine walo humu - Kenya mwambao pamoya

 

186.    Na walio Tanganyika -  Uhuru walowafika - Rabi Mola tawaweka - Kwa furaha na afiya

 

187.    Na Waunguja Rabbana - Uwape kusikizana - Uhuru ukilingana - Wawe wote hali moya   

 

188.    Uwondolee fitina - Isilamu kupijana - Litetewalo hapana - Ni fitina zimengiya

 

189.    Swalla llahu  wasalama - Zishuke kwa wake tumwa - Nimedhoofu kwa huma -  Rabbi tatupa afiya.

  

MAANA

 

7.    Mukisa : mukisha

 

15.    Mayondi : majonzi   

 

17.    Huinika : wainukie

 

24.    Hiyau : sasa hivi ; Inika : inuka

 

26.    Uchambiwa : ukiambiwa ; Kufuza : kuingia moja kwa moja

 

27.    Situngie : usichungulie ; Fafani : kujipeleka mbelembele ( kujua sana)

 

39.    Muyezi : mlezi

 

42.    Kiguni : kikoi ; Kitambi : kikoi

 

44.    Mtatufu : mwenye makini ( mtulivu)

 

51.    Mbeko : heshima

 

53.    Kanwa : kinywa

 

57.    Achanza : akianza

 

59.    Yuwa : jua

 

60.    Imunike : jiangalie

 

63.    Tungu : chungu nzima (wengi , tele)

 

66.    Manana : mabibi

 

70.    Siize : usikatae

 

72.    Huza : unauza (kuuza)

 

75.    Kuvulini : kuliani ( mkono wa kulia , kuume)

 

81.    Mve : kuteuka

 

83.    Zanda : vidole

 

85.    chumbi : chumvi

 

86     Huja kisa : huja baadae

 

87.    Ndi : nzi

 

95.    Simbo : fimbo

 

107.    Ukiitesha : ukijichekesha

 

108.    Usiusuze : usiuzuwe

 

117.    Siaike : usiape

 

123.    Duhu : mafuta yaliyo ndani ya mfupa

 

135.    Yatiayo hamu : yatiayo wasi wasi

 

151.    Amefuza : amekuja moja kwa moja

 

157.    Zigari : vigari ( toys) ; Wano : wanao ; Wane : wanawe

 

167.    Muwee : mgonjwa