Assalaam Alaykum,
Ufuatao ni utenzi unaoeleza kisa cha mtume wa Mwenyezi Mungu, Sayyidna Yusuf
ALAYHI SALAAM. Utenzi huu umetungwa na Sh. Said Karama kutoka Lamu.
UTENZI WA KISA CHA NABII
YUSUF (A.S.)
Mtungaji : Said Karama - Lamu
1. Bisimilahi Kahari, Ya Rabi Mola Jabari, Mmoja uso akhiri,
Wala mwanzo kuanzia
2. Naanza kwa lako jina, Mola wetu Subuhana, Mtukufu wetu
Bwana, Wa pili asotokea
3. Twamsalia kaumu, Sote ndugu Isilamu, Mtume Bani Hashimu,
Sayyidil Arabia
4. Sote Rabi Ya Rahimu, Twamsalia Hashimu, Na tunu nyingi
salamu, Twamtakia nabiya
5. Nina kisa maarufu, Cha tumwa wake Latifu, Mtume mwema
Yusufu, Wao Isirailia
6. Mtume wake Wahabu, Yusufu tumwa Habibu, Baba yake
Yaakubu, Jinale tawatajia
7. Mzazi wake wa pili, Jinale ni kama hili, Aitwa bibi
Rahili, Mtukufu wa muruwa
8. Yusufu ndie Rasuli, Aloletwa na Jalali, Kwa bani
Isiraili, Kaumu isosikia
9. Nduguze kuwahisabu, Kwa majina ni taabu, Samahani
masahibu, Idadi tawatajia
10. Ana kumi wa awali, Kwa baba na mama mbali, Na mdogo ni
Rakili, Kwa baba na mama pia
11. Walikuwa majabari, Wasiogopa shari, Shujaa walo hodari,
Dhiki ikiwafikia
12. Alipokwisha kuzawa, Na ndugu wakachukiwa, Wamuhasidi na
ngowa, Maradhi yalokomaa
13. Sababu yeye kwa kweli, Alikua na jamali, Uzuri wake
rasuli, Akipendeza nabiya
14. Ni mrembo mtulivu, Mwenye busara mwerevu, Na mwilini
hana kovu, Uzuri umezidia
15. Yusufu alipokaza, Kwa wazazi kupendeza, Ndugu
yakawachukiza, Mabaya kukusudia
16. Ndugu walifanya wivu, Na kila la uwerevu, Wamtendee
uovu, Kumwangamiza dunia
17. Siku moja ya utoto, Amelala hako mato, Yusufu kaota
ndoto, Ajabu nawaambia
18. Ndoto hiyo ya kioja, Jua na mwezi pamoja, Na nyota kumi
na moja, Vyote kumsujudia
19. Muda alipogutuka, Hapo alipoamka, Alikimbia haraka, Kwa
baba kumwelezea
20. baba kwa wake ujuzi, Akaifahamu wazi, Ndoto ya jua na
mwezi, Na nyota kumi na moya
21. Na baba asinyamaze, Ndipo amsisitize, Mwanangu
siwaeleze, Nduguzo nakuusia
22. Mwanangu stahamili, Siwaambie asili, Yusufu usikubali,
Siri ya ndoto zuwia
23. Mungu atakukhitari, Akufunze tahariri, Ya ndoto na ya
khabari, Waja wasizozijua
24. Hapo ndipo auladi, Hao kumi mahasidi, Ikashtadi hasadi,
Wakawa na jicho baya
25. Hasadi ya jicho ovu, Kwa kumuonea wivu, Ili wamtenze
nguvu, Yusufu mwema nabiya
26. Ndio waliokutana, Wote ashara vijana, Wasijizuie tena, Moyoni
kuvumilia
27. Faragha walionana, Wote kushauriana, Mwisho wakasikizana, Maovu
kuazimia
28. Wakatoka taratibu, Vijana hao kidhabu, Wakenda kwa
Yaakubu, Baba yao kumwambia
29. Wakafika pasi khofu, Maneno kumuarifu, Kwa kumtaka
Yusufu, Ruhusa kumuombea
30. Wamtaka ndugu yao, Yusufu mdogo wao, Ili asafiri nao,
Huko wanakokwendea
31. Hila waliyoisema, Kwa wao mtu mzima, Ni Yusufu kuandama,
Kwenda kucheza pamoya
32. Hapo baba kashangaa, Na kwanza akakataa, Akajua ni
hadaa, Wana walomwelezea
33. Maana alitambua, Hila yao kuijua, Yusufu wamchukua,
Lakini hatarejea
34. Mola aliyoandika, Ni uongo kufutika, Ni lazima
kutendeka, Kwani yote yamwelea
35. Na baba kwa takilifu, Ya wanawe wapotofu, Moyo ukafanya khofu, Lakini
kavumilia
36. Ikawa hapana budi, Baba yao kuburudi, Akamtoa fuadi,
Yusufu kuwaachia
37. Vijana wakaondoka, Na mji wakautoka, Pamoja na
muhibbuka, Yusufu tumwa Jalia
38. Wakawa wasafarini, Wapotelea porini, Na huku
wamachungani, Walisha katika njia
39. Wakawasili makini, Kando ya mji njiani, Kwenye mji
Dausani, Mji walioingia
40. Kufikia kisimani, Mmoja wa ikhiwani, Ambae ni wa
mwanzoni, Umri alozidia
41. Akalitoa shauri, Kuwapa ndugu khabari, Akasema jambo
zuri, Yusufu kumtendea
42. Mimi katu sikubali, Tulivyowaza awali, Ni lazima liwe
hili, Jengine sitoridhia
43. Yusufu tusimuweni, Sote na tumshikeni, Tumtupe kisimani,
Haya kwake ni kifaya
44. Ikawa budi hawana, Asili kutoshindana, Mkubwa aloyasema,
Wadogo wakatikiya
45. Hapo tena kwa upesi, Wakamvua libasi, Ambayo ndio
khalisi, Yusufu alovalia
46. Na kisha wakamshika, Wakamtupa haraka, Kwenye kisima cha
nyoka, Kirefu chenye udhia
47. Kwa uwezo wa Rabuka, Hata si robo dakika, Jibrili
akashuka, Ajabu ilotokea
48. Kufumba na kufumbua, Jibrili keshatua, Yusufu kumuokoa,
Kabla hajaumia
49. Jibrili kamnyaka, Kabla chini kufika, Taratibu kamuweka,
Mahali pema nabiya
50. Baada ya kutendeka, Kisa hiki kufanyika, Nduguze
wakatoroka, Wakaanza kukimbia
51. Wenda wakifurahika, Waongea wakicheka, Wakajua kwa
hakika, Yusufu keshajifia
52. Kumbe wamehadaika, Na bure kuadhirika, Na Yusufu hana
shaka, Bukheri kajikalia
53. Hata kwa muda saghiri, Wakazuka wasafiri, Wenda mji wa
Misiri, Wa katika yao njia
54. Ulikua msafara, Ulotimia imara, Wafanyaji biashara,
Wasafiri wa ngamia
55. Hapo bila ya kungoja, Maji ndio yao haja, Wakamtuma
mmoja, Maji kwenda watekea
56. Ndoo ikashika papo, Yusufu hapo alipo, Akashika papo
hapo, Kamba ilomlekea
57. Kamba alipoipata, Akawa yuwaivuta, Na aliyeikamata, Uoga
ukamwingia
58. Uoga na taharuki, Kwa kamba yake kusaki, Ndoo
haitaharuki, Yusufu ameigwia
59. Katizama kutafiti, Kujua kilo tiati, Mara ikaja sauti,
Kisimani kutokea
60. Kwa nguvu zake Kahari, Ndipo tena wasafiri, Hapo pasi
kusubiri, Kutafuta kila ndia
61. Ikawa ni pata shika, Waume kushughulika, Kamba
zimekusanyika, Kisimani zangojea
62. Yusufu kwenye kisima, Akatolewa mzima, Ameokoka salama,
Kama hakutumbukia
63. Basi hapo mtukufu, Mtume mwema Yusufu, Akawa yukwenye
safu, Na wasafiri pamoya
64. Wakawa wasafarini, Na Yusufu yukundini, Hadi Misiri
mjini, Wendako kuwasilia
65. Nduguze bila kungoja, Wote kumi kwa umoja, Kutimia yao
haja, Walianza kurejea
66. Wenda bila wasiwasi, Ndiani wakihadisi, Pamoja nayo
qamisi, Walomvua nabiya
67. Na mipango walofanya, Ya hila na kudanganya, Ili kwamba
kuwaponya, Baba wanapomwambia
68. Walingia kwenye kazi, Ya kumkamata mbuzi, Kumchinja kwa
ukuzi, Ovu lao kufidia
69. Wakaipaka libasi, Yusufu yake qamisi, Kwa hiyo damu
najisi, Ya mbuzi walomuua
70. Nyumbani wakawasili, Na baba kumkabili, Na la kwanza ni
ajali, Ilowakumba na njia
71. Wakazidi kutongoa, Na qamisi kuitoa, Ilokua na madoa, Ya
damu iloingia
72. Uongo walouzuwa, Walosema ndugu hawa, Yusufu ameuawa,
Kwa mbwa kumrukia
73. Baba kusikia yale, Ya wanawe muda ule, Na huzuni pale
pale, Alianza na kulia
74. Baba alisema kua, Kwa mwanangu yalokua, Si mbwa alomuua,
Wallahi nawaapia
75. Ni uongo uso shaka, Wa kanzu kutoraruka, Hata tundu
kutoboka, Na mwenyewe akalia
76. Yusufu kumdhulumu, Nawaachia Rahimu, Ndie mwenye
kuhukumu, Yote Mola yamwelea
77. Sasa Yusufu Misiri, Kafika na wasafiri, Maliki
akaghairi, Na Yusufu kubakia
78. Kampeleka makani, Mtume wa Rahamani, Ambapo ni mnadani,
Ili kwamba kunadiwa
79. Na kwa bahati nzuri, Akatokea waziri, Kadawaa kwa uzuri,
Aliopewa nabiya
80. Kamnunua Yusufu, Kwa bei ilo pungufu, Kama mtumwa
dhaifu, Asiye na manufaa
81. Waziri akamtwaa, Yusufu nae kukaa, Kama mwana wa kuzaa,
Mahaba yalomwingia
82. Baadae atamke, Kumwambia mke wake, Zulekha mwana mshike,
Mola katujaalia
83. Waziri bila ya khofu, Akaishi na Yusufu, Asimpe taklifu,
Kwa kila lenye udhia
84. Waziri akamsifu, Kwa wake uaminifu, Akimpa maalufu, Mali
kuyasimamia
85. Sasa hapa tufahamu, Umri aliotimu, Ndiyo apewa ilimu, Na
hikima zote pia
86. Ili kufunzwa khabari, Ya ndoto kuzibashiri, Na akawa ni
hodari, Kujua mambo ya ruya
87. Hata kwa muda fulani, Hapo Zulekha nyumbani, Ndipo
yuwaanza zani, Maovu kuazimia
88. Kila siku yamoyoni, Iwapo mili ya ndani, Yusufu
kumtamani, Kumuwazia mabaya
89. Zulekha yalikithiri, Mapenzi kumuathiri, Na hapo
akamghuri, Ibilisi kumwingia
90. Kukicha azidi huba, Vitendo vya ukahaba, Ili yake
matilaba, Yapate kumnyokea
91. Tangu akipenda siri, Na mwisho asisubiri, Mambo yakawa
dhahiri, Kwa huba kumtokea
92. Na siku hiyo yakini, Waziri hako nyumbani, Mumewe
yusafarini, Ndipo aanza udhia
93. Na ndiyo siku hakika, Zulekha kufedheheka, Na yake
kutotendeka, Aliyoyaazimia
94. Wakati ulipofika, Hiyo siku aloweka, Zulekha akatamka,
Na Yusufu kusikia
95. Alimwita faraghani, Zulekha kwake chumbani, Amueleze
kanuni, Hilo alokusudia
96. Yusufu akamwitika, Zulekha bibi labeka, Kwa upesi
akatoka, Alikoitwa kungia
97. Hata akifika ndani, Akasubiri makini, Asikize jambo
gani, Bibi alilomwitia
98. Ndipo basi atamke, Huyu baa mwanamke, Amwambie haja
yake, Yusufu kumwelezea
99. Akatamka machafu, Zulekha bila kukhofu, Yusufu
kumuarifu, Na nguvu kumtilia
100. Kasema kwa yake dhati, Zulekha muhasharati, Kila njia
kutafiti, Amghilibu rasua
101. Akazidi ubazazi, Akanena ya upuzi, Kumpa Yusufu wazi,
Lake alohitajia
102. Moyo wako burudika, Niridhi ninalotaka, Na huna la
kukufika, Lolote lenye udhia
103. Yusufu hapo rasuli, Kupata hino kauli, Ilimdhuru akili,
Na moyo kushitukia
104. Moyo ukabadilika, Yusufu kukasirika, Akaanza kumwepuka,
Kabisa kutoridhia
105. Kasema Yusufu katu, Jambo hilo sithubutu, Sitendi yaso
na utu, Ya kumuudhi Jalia
106. Basi ndipo hapo hapo, Zulekha pake alipo, Katambua
yaliyopo, Yake kutomnyokea
107. Akainuka haraka, Ili kutaka mshika, Na Yusufu kaepuka,
Zulekha kumkimbia
108. Zulekha kwa zake kasi, Asimshike khalisi, Ila kugwia
qamisi, Muda alimtapiya
109. Alimshika kwa nyuma, Akaivuta kwa hima, Libasi
ikamwandama, Qamisi kuipasua
110. Ikawa kuchoropoka, Yusufu akaokoka, Na vazi limepasuka,
Wakati ajitetea
111. Zulekha uchungu wake, Kwa Yusufu amwepuke, Kapasua nguo
zake, Na makucha kujitia
112. Maana ya hiki kisa, Nguo zake kuzitesa, Ilikua ni
siasa, Yusufu kumchongea
113. Kusudio ni kunena, Arudipo wake bwana, Kumtilia fitina,
Yusufu kumzulia
114. Ghafula mara waziri, Karudi kwenye safari, Akingia yake
dari, Mlangoni kufikia
115. Ndipo kuwahi matata, Mwenyewe akayakuta, Kwa kushuhudia
vita, Vya mkewe na nabiya
116. Moyowe ulishituka, Kwa mambo kubadilika, Si kama
alivyotoka, Mbele ya kusafiria
117. Moyo mengi ukahisi, Khofu ndani ya nafusi, Akazidi wasi
wasi, Kuona yalivyokua
118. Waziri kumtangaza, Zulekha kumueleza, Hebu bibi
nieleza, Ni vipi umechukiwa
119. Niambia tafadhali, Ijapokuwa qalili, Niondowe
mushikili, Zulekha bibi nambiya
120. Na Zulekha akajibu, Kwa nyingi zake ghadhabu. Kumpa
mume jawabu, Kisa kilomfikia
121. Bwana unavyoniona, Wala sina la kunena, Ni mambo ajabu
sana , Mtu akiyasikiya
122. Akaanza kwa mpango, Zulekha wake uongo, Kumtakia
kifungo, Yusufu pasi na njia
123. Alimwambia mumewe, Yalonikumba ujuwe, Yote dhamana ni
wewe, Bwana ulonitakia
124. Nimetendewa vituko, Mume wangu nawe huko, Na Yusufu mtu
wako, Huyo uloniletea
125. Ni jambo la kipumbavu, La kunishika kwa nguvu, Anifanye
tendo ovu, Nami nikakatalia
126. Tena akanisumbuwa, Ni lazima lake kuwa, Nguo zangu
kupasuwa, Kutaka nigeukia
127. Na mara bila ajizi, Kijana kasema wazi, Mbele yao
kubarizi, Na wote wakasikia
128. Kwa nguvu zake Karima, Mola mwingi wa rehema, Mwana
mchanga kasema, Bila khofu kumwingia
129. Alinena hivi sasa, Sote tufanye siasa, Tutamjua mkosa,
Ni yupi alokosea
130. Tuliyopo hapa sisi, Tupeleleze tukisi, Tuitazame
qamisi, Kwa ilivyonyanyuliwa
131. Upande ulopasuka, Nguo hio kunyanyuka, Tutamjua hakika,
Vita alotangulia
132. Na qamisi ndio ile, Nyanyuko likiwa mbele, Hapo hapana
kelele, Yusufu amekosea
133. Au tukiitazama, Imepasuka kwa nyuma, Zulekha ana
lawama, Na ndie mwenye khatia
134. Kijana alipokoma, Mwana mchanga kusema, Ikawa ni rai
njema, Ushahidi alotoa
135. Hata walipochungua, Qamisi kuangaliwa, Nyuma
imepasuliwa, Wote kuishuhudia
136. Basi kwa hichi kiwango, Tushaujua mpango, Zulekha ndie
muongo, Yusufu kumzulia
137. Mwishowe kimtangaza, Wanawake kueleza, Zulekha ni
miujiza, Kwa yeye kutenda haya
138. Kwani hawajaamini, Banati hao yakini, Kujua yuhali
gani, Uzuri wake nabiya
139. Khalafu wakatamka, Banati wakamtaka, Ili Yusufu kufika,
Wapate mshuhudia
140. Hapo Zulekha mwenyewe, Akasikia mwishowe, Kwa kumsema
wenziwe, Khabari kumtokea
141. Ndipo ghera kumshika, Kwake akawaalika, Na vyakula
akaweka, Wote wakahudhuria
142. Akapitisha sharuti, Mbele yao mabanati, Wakayakubali
dhati, Zulekha alowambia
143. Yusufu alipopita, Banati wakamkuta, Kwa visu
wakajikata, Bila ya kufahamia
144. Wote kodo macho mbele, Ajabu ya maumbile, Wakakatika
vidole, Kwa urembo wa nabiya
145. Ni hapo kujulikana, Hapo walipomuona, Kuwa ni mzuri
sana, Yusufu wameridhia
146. Mwanena lawama kwangu, Kwa hasira na uchungu,
Jitizameni wenzangu, Nanyi yalowafikia
147. Nanyi mumeadhirika, Kushinda yalonifika, Na vidole
kukatika, Bila ya kuzingatia
148. Wakazidi kina mama, Waeleza kua kama, Zulekha hana
lawama, Yusufu katimilia
149. Basi mwisho akapuza, Kwa hasira kumkaza, Zulekha
kuwaeleza, Wenziwe kuwaambia
150. Yakuwa asipoweza, Yusufu kunisikiza, Nyumba yake ni
gereza, Lazima ataingia
151. Namweleza ya muanga, Yangu anapoyapinga, Hakika
nitamfunga, Kiapo namuapia
152. Kisha tena awambiye, Hao mabibi wenziye, Na nyinyi
semeni naye, Huenda akasikia
153. Zulekha kumpa nguvu, Kwa alosema maovu, Wakafanya
uerevu, Tumwa kumkazania
154. Ndipo wakamuarifu, Kwa nguvu na takilifu, Wakamwmbia
Yusufu, Ya bibi yako ridhia
155. Ikawa asitamke, Yusufu asiyashike, Maneno ya wanawake,
Hayo waliyomwambia
156. Kwa hayo aloambiwa, Akaona hana dawa, Ila ya kuomba
dua, Kwa Mola wake Jalia
157. Na Yusufu dua yake, Ni machafu yamwepuke, Kalingana
Mola wake, Hapo akaombolea
158. Ya Rabi Mola ujuwe, Yashanishinda mwenyewe, Uiwezae ni
Wewe, Shida yangu yakwelea
159. Nihifadhi Bwana Mola, Kwani sina tena hila, Kwangu
kheri kwenda jela, Kuliko huno udhia
160. Mungu aliyakubali, Maombi yake rasuli, Kwa mujibu
wa kauli, Ya dua yake nabiya
161. Akamkinga Jalali, Na wa Zulekha muhali, Rabi
akatakabali, Na gerezani kungia
162. Ikawa si muda tena, Zulekha kungoja sana, Ndipo aanze
fitina, Uongo kuuchochea
163. Maana alipojuwa, Atakalo halikuwa, Tena ameadhiriwa,
Khabari zimeenea
164. Akamwambia waziri, Mume wake kasisiri, Bwana nnayo
khabari, Tafadhali nisikiya
165. Nakuomba kwa hisani, Yusufu mtie ndani, Mpeleke
gerezani, Kwani amenikosea
166. Mji wote ni sherehe, Yusufu kunifedhehe, Katu
usimsamehe, Idhara imeenea
167. Na kwa hapo ndipo mume, Asijibu asiseme, Ya mkewe
aandame, Bila ya kufikiria
168. Waziri akawa radhi, Ili bibi amridhi, Mkewe asimuudhi,
Ijapo ni jambo baya
169. Kamtia kifungoni, Yusufu korokoroni, Hali hako
makosani, Badili kumuonea
170. Yusufu akenda ndani, Na wawili ithinani, Walokua
khatiani, Kwa yao walokosea
171. Walifanya ukhalifu, Mfalume kaarifu, Wafungwe wawe
madufu, Na adabu kuwatia
172. Kwa kutokea ubishi, Kwa ndoto za ushawishi, Waloota
watumishi, Jela walikofungiwa
173. Na wakenda kwa Yusufu, Kwa shaka na takilifu, Kwani
ashawaarifu, Kua ndoto zamwelea
174. Saiki ndie wa kwanza, Aliyejitanguliza, Ndoto yake
kueleza, Yusufu kuisikia
175. Akasema jana kua, Nimeota kuchukua, Sinia iliyokua, Na
vinywaji vimetiwa
176. Na mwendo wangu wa shime, Njiani nisisimame, Nenda
kwake mfalume, Vinywaji kumwandalia
177. Yusufu akamjibu, Kama ilivyo wajibu, Kumpa njema
jawabu, Ndoto kumfasiria
178. Saiki akajibiwa, Ndoto ikaaguliwa, Kifungoni kutolewa,
Tumwa kumbashiria
179. Akanena langu shika, Wala usifanye shaka, Wewe jela
utatoka, Kazi yako kurejea
180. Mara hapo akaruka, Mpishi akatamka, Ili hakika kutaka,
Kumjaribu nabiya
181. Asifikiri ni nini, Yakamwingia kichwani, Akaanza
ubishani, Kujifanya yamwelea
182. Na hapo bila kusita, Ndoto yake kufuata, Kusema
aliyoota, Yote yalomfikia
183. Yusufu kabwaga shingo, Kuusikiza uongo, Upangwavyo kwa
mpango, Bila ya kuona haya
184. Ewe nabii wa Mungu, Yusufu mkubwa wangu, Nimeota ndoto
yangu, Nimejitweka sinia
185. Nimejitweka kichwani, Na mikate imo ndani, Naipeleka
nyumbani, Kwa mkuu wa raiya
186. Nilipokuwa njiani, Kaja ndege wa angani, Kaudona
siniyani, Mkate kauchukua
187. Mkate akaudona, Kabaki nimedangana, Ndipo Yusufu
kanena, Ndoto kumfumbulia
188. Fasiri ya ndoto yako, Haina salama kwako, Utakatwa
kichwa chako, Lazima utauwawa
189. Mpishi akaduwaa, Akawa ataataa, Ikawa hana tamaa, Kwa
alivyobashiriwa
190. Akamwambia mwalimu, Yusufu bwana fahamu, Hayo
nilotakalamu, Ni dhihaka nakwambia
191. Yusufu ndipo kusema, Ujuwe huna salama, Utauliwa
lazima, Kama nilokwelezea
192. Siku nyingi zisitimu, Kwa rehema za Karimu, Mungu
akamrehemu, Saiki kafunguliwa
193. Mwenziwe yule laimu, Aliyengiwa na hamu, Ikatolewa
hukumu, Akenda akauwawa
194. Na siku ya kuachana, Na Yusufu kuagana, Hapo Yusufu
kanena, Saiki kumwashiria
195. Akamba leo watoka, Kwako nnalolitaka, Siwache
kunikumbuka, Yakumbuke mazoweya
196. Ewe wangu muhisani, Sinisahau mwendani, Na kunitaja
nyumbani, Kwake mfalume pia
197. Saiki kenda kuanza, Kazi yake kufanyiza, Shetani
kamsauza, Kutekeleza wasia
198. Ikatukia azizi, Maliki kwenye malazi, Alipitiwa na
njozi, Mno kaigutulia
199. Muda alipogutuka, Malazini kuamka, Akangiwa na wahaka,
Wasiwasi kumwingia
200. Akawataka Maliki, Watumiao falaki, Watizame kisa hiki,
Cha ndoto ilomjia
201. Kawaita makuhani, Wakuu wanavyuoni, Wote walio mjini,
Kuja kumbashiria
202. Nimewaita wajuzi, Muifanye yangu kazi, Ya ndoto munipe
wazi, Jawabu ilo na njia
203. Bidii munavyoweza, Munipe ya muangaza, Kwani
yamenishangaza, Sasa nawatamkia
204. Nimeota waungwana, Usingizini kuona, N'gombe walodhofu
sana, Sabaa katika ruwiya
205. Huwala walionona, N'gombe sabaa mabwana, Kisha nikaota
tena, Baada ya mambo haya
206. Nikayaota mashuke, Yaso kitu ndani yake, Na mengine
yalo pweke, Sabaa yaliyojaa
207. Ikabidi makuhani, Kutazama vitabuni, Kuiona hawaoni,
Akili zimewashia
208. Kushindwa kwa watu hao, Maliki kazidi mwao, Akawa hana
makao, Wasiwasi kuzidia
209. Saiki akagutuka, Ghafula kamkumbuka, Yusufu akatamka,
Maliki kumwelezea
210. Saiki katakalamu, Kumwambia muadhamu, Mimi bwana
nafahamu, Wakati nilipokuwa
211. Nimefungwa gerezani, Nilimkuta mwendani, Mfadhila na
hisani, Ajuaye mambo haya
212. Na Yusufu kakariri, Bila ya kuyafikiri, Ndoto
akaibashiri, Alivyombashiria
213. Ni miaka ya neema, Sabaa ya wakulima, Watavuna vuno
jema, Chakula cha kuzidia
214. Ikisha miaka hiyo, Yenye shibe iso choyo, Itakuja
mengineyo, Saba ya watu kulia
215. Kilio kiso nyamaa, Kwa kungiliwa na njaa, Iwe ni kuu
balaa, Chakula kuwashilia
216. Kupata hayo Saiki, Mambo yakamuafiki, Akamwambia
rafiki, Yusufu tuonye njia
217. Yusufu yake kalima, Kampa jawabu njema, Nawalime
wakulima, Mavuno yakiwadia
218. Mupatafute mahala, Muvitie kwenye ghala, Shida ikija
ghafula, Mupate cha kutumia
219. Basi hapo ikabidi, Bwana Saiki karudi, Na kamili
ushahidi, Wa kwenda kuwaridhia
220. Hata akifika ndani, Kwa mfalume nyumbani, Akaeleza
makini, Yote yaliyotukia
221. Alimpa tafsiri, Ya ndoto yake dhahiri, Mambo
yatakayojiri, Ambayo yatatokea
222. Papo kastaajabu, Mfalume kwa jawabu, Mno kaona ajabu,
Kwa ujuzi wa nabiya
223. Na pale pale kwa hamu, Maliki katakalamu, Saiki
kumlazimu, Upesi jela rejea
224. Mwite Yusufu haraka, Umwambie ukifika, Mfalume akutaka,
Haraka akungojea
225. Kufika kwenye kizimba, Asingoje akamwamba, Yusufu bwana
aomba, Wende kwake akwambia
226. Kukangiya walakini, Kuwa haiwezekani, La kutoka
gerezani, Yusufu kakatalia
227. Akasema kumjuza, Saiki kumueleza, Mimi katika gereza,
Sitaondoka sikia
228. Salamu zangu zifishe, Mfalume mjulishe, Mpaka
athubutishe, Yakua sikukosea
229. Na kisha kwa hiki kisa, Awajuze watu khasa, Yakuwa sina
makosa, Zulekha ndie mbaya
230. Awaite vilevile, Banati wa siku ile, Walojikata vidole,
Na Zulekha wote pia
231. Ni kua apeleleze, Maliki awaulize, Wanawake wamweleze,
Ni yupi alokosea
232. Saiki akaushika, Ujumbe kaupeleka, Yote aliyotamka,
Yusufu kumwaridhia
233. Alipokwisha ambiwa, Maliki kuelezewa, Maneno yakamtuwa,
Pingamizi kutotia
234. Ndipo hapo apeleke, Mfalume mtu wake, Wakaitwe
wanawake, Na wote wakafika
235. Banati wakiwasili, Maliki kawakabili, Kisha akawasaili,
Mfalume kuwambia
236. Musiogope muhali, Baina hawa wawili, Mwenye makosa kwa
kweli, Mwaweza kunitajia
237. Ni Zulekha na Yusufu, Mkosa muniarifu, Yupi alo
mpotofu, Huyo alo na hatia
238. Wanawake wakasema, Kwa upole na heshima, Bwana mwenye
na lawama, Zulekha ndie mbaya
239. Na Zulekha baadae, Akiulizwa na yeye, Asili asikatae,
Akajibu ya sharia
240. Yakua wangu ulimi, Leo uongo sisemi, Mwenye makosa ni
mimi, Hakika nakubalia
241. Mfalume ufahamu, Yusufu simlaumu, Bali niememdhulumu,
Na tena kumzulia
242. Zulekha akalingana, Ya Ilahi Subhana, Nakubali mimi
Bwana, Yakua nimekosea
243. Na makosa kua kwangu, Nakuomba Bwana Mungu, Nisamehe
dhambi zangu, Ya Rabbi Mola Jalia
244. Yote maneno ya watu, Yusufu imethubutu, Si mkosa huyu
mtu, Hakika imetokea
245. Imethubutu Yusufu, Kua mtu mtukufu, Sababu hana
machafu, Maovu kujizuiya
246. Zulekha alitamka, Kua alighilibika, Ndie aliemtaka,
Sasa amekubalia
247. Tushafahamu Yusufu, Kwamba hana ukhalifu, Zulekha ndie
mchafu, Kosa lilomwelemea
248. Alipopata ukweli, Maliki kwa jambo hili, Ikawa
yastahili, Yusufu kwenda tolewa
249. Ndipo Saiki atoka, Kwa furaha na kucheka, Kwa Yusufu
akifika, Akawa atmwambia
250. Itunze yako nafusi, Usiwe na wasiwasi, Zulekha ndie
mkosi, Makosa ameridhia
251. Wameitwa watu tele, Kaulizwa mambo yale, Akajibu yale
yale, Kama yalivyotokea
252. Yusufu iliyobaki, Sasa twende kwa Maliki, Usiwe mwenye
hamaki, Kufikiri mambo haya
253. Yusufu akaitika, Gerezani akatoka, Kwa Maliki akafika,
Vizuri akapokewa
254. Maliki akasimama, Mtukufu wa heshima, Akampa taadhima,
Sitaha kumfanyia
255. Maliki kamkubali, Kuwa ni mtu wa kweli, Tena ni mwenye
akili, Yusufu kajaaliwa
256. Yusufu akataraji, Awe waziri wa mji, Awe ni mtazamaji,
Neema ikitokea
257. Mfalme karidhia, Na kumsafia nia, Akamba nakuachia,
Fanya litakalofaa
258. Yusufu asighairi, Wala asitaakhiri, Akashika uwaziri,
Cheo hicho kupokea
259. Ndipo yaanza neema, Chakula mji mzima, Furaha kwa
wakulima, Hadi waliobakia
260. Wala vyema wakishiba, Na vyengine kwa akiba, Muda wa
miaka saba, Njaa kuwaepukia
261. Kwa furaha wakakaa, Muda wa myaka sabaa, Hapo ikangia
njaa, Raha kuwapungukia
262. Lakini wao hakika, Japo njaa imefika, Waliishi pasi
shaka, Wakila bila udhia
263. Ila ilizidi dhiki, Kwa miji iliyobaki, Kwa majirani
rafiki, Njaa ikawafikia
264. Ndipo ilipomsibu, Njaa kuu Yaakubu, Kumfikia taabu, Ya
wanawe wote pia
265. Yaakubu hapo basi, Akazidi wasiwasi, Wakati alipohisi,
Chakula kimeishia
266. Na baba yeye mwenyewe, Akawajuza wanawe, Kuwaambia
wajuwe, Njaa ile ilongia
267. Ili kwamba wasafiri, Wende mji wa Misiri, Na wana
wakakhiari, Baba kumkubalia
268. Wakenda wana ashara, Ila wa hidaashara, Hakua na
msafara, Nyumbani akabakia
269. Aliebaki nyumbani, Kutokua safarini, Ni huyu Binyamini,
Ndie aliesalia
270. Mwana huyu mtukufu, Na tena nawaarifu, Ni mdogo wa
Yusufu, Kwa baba na mama pia
271. Basi kumi walobaki, Wakenda na yao dhiki, Kuitafuta
riziki, Misiri wakafikia
272. Wakawasili vijana, Hata walipopambana, Yusufu akawaona,
Kwake walipoingia
273. Walipofika ikawa, Yusufu kuwatambuwa, Na wao kutomjuwa,
Yakuwa ni ndugu moya
274. Yusufu akafuliza, Na wao kuzungumza, Na hali kuwauliza,
Na wao kumwelezea
275. Yusufu yakamtosha, Nduguze walompasha, Nae
akayakinisha, Ni nduguze wote pia
276. Khalafu mwisho akaze, Yusufu awaeleze, Awaambie
nduguze, Hao walomjilia
277. Katamka akanena, Enyi ashara vijana, Munaporejea tena,
Hapa mukifikilia
278. Ndugu yenu muje nae, Aandamane na nyie, Ili hapa
afikie, Nipate mshuhudia
279. Hilo hakika nawapa, Nisipomuona hapa, Na chakula
sitawapa, Munachokihitajia
280. Wala musinifikie, Kwangu musikaribie, Huko huko
mubakie, Sitaki washuhudia
281. Ikangia tafauti, La kusema hawapati, Ikawa kwao
sharuti, Ndugu hao kurejea
282. Wakapakiliwa tweka, Za chakula walotaka, Ili wapate
ondoka, Makwao kurejelea
283. Walipowasili kwao, Kufikia ndugu hao, Wakampa baba yao,
Khabari ilotukia
284. Walipofungua tweka, Nyoyo ziliwapasuka, Kwa furaha
kuwafika, Ya mali kuregezewa
285. Hata chakula kikisha, Ndiyo siku ikatisha, Wana
kujitayarisha, Safari kuandalia
286. Baba wakamshauri, Ili wao kwa uzuri, Kwa huyo mwana
saghiri, Ili wende nae pia
287. Na watoto wakasema, Kumpa baba kalima, Baba hakuna
hekima, Tutakayokufanyia
288. Utupe Binyamini, Awe nasi safarini, Usiwaze asilani,
Salama atarejea
289. Na baba yakamtanza, Halijui la kufanza, Akakumbuka la
kwanza, La Yusufu kupotea
290. Baba alifanya khofu, Akidhania machafu, Yalomkumba
Yusufu, Na huyu atatendewa
291. Khalafu akakariri, Kuwapa wana khabari, Akasema
mwafikiri, Kua nitakubalia
292. Na wana yao kauli, Kumtoa mushikili, Wakasema ilo
kweli, Baba yao kumwambia
293. Hakika amtakae, Ili sisi twende nae, Ni waziri asemae,
Ndiyo alotwelezea
294. Kwa nyingi mno taabu, Akanena Yaakubu, Wanawe
akawajibu, Kwa hilo sitaridhia
295. Hendi hadi ushahidi, Munipe kweli ahadi, Yake Ilahi
Wadudi, Yakuwa atarejea
296. Na ijapo ni ajali, Jambo lisokua hili, Siwalaumu asili,
Apendalo Mungu huwa
297. Na wana wote walipo, Ikawa kula kiapo, Wakasema papo
hapo, Kwa Mungu kushahidia
298. Wallahi twenda na yeye, Khofu isikuingiye, Baba
tutakuja nae, Mwanayo atarejea
299. Baba kwa hino ahadi, Ya ashara auladi, Moyowe
uliburudi, Imani ikamwingia
300. Basi baba akaridhi, Moyo wake kuwa radhi, Mwanawe
kuwakabidhi, Wanawe walosalia
301. Ndipo baba amtake, Binyamini afike, Na alipokuja kwake,
Mara kamkumbatia
302. Yaakubu akanena, Na mwanawe kuagana, Kwaheri ya
kuonana, Na kheri nakutakia
303. Safiri Binyamini, Kwa salama salmini, Na urudi mara
thani, Kwa umri na afiya
304. Hapo muda ukajiri, Hapana tena shauri, Vijana
wakasafiri, Hidaashara pamoya
305. Wakenda mara ya pili, Vijana kama awali, Kwa Yusufu
kuwasili, Misiri wakafikia
306. Kuwasili ikhiwani, Yusufu kwake nyumbani, Kawapanga
ithineni, Wawili chumba kimoya
307. Yusufu yake akili, Kawatenga mbalimbali, Ndugu wawili
wawili, Mdogo akasalia
308. Ndipo basi masikini, Kabaki pweke mwendani, Yaani
Binyamini, Hapo kaanza kulia
309. Mambo yakamtatiza, Yusufu kumshangaza, Kisha
akamuuliza, Mdogowe kumwambia
310. Nieleze kwa makini, Likulizalo ni nini, Walizwa na
jambo gani, Nambia nipate juwa
311. Binyamini kasema, Kwa sauti ya huruma, Kumpa yake
kalima, Yusufu kumwadithia
312. Lau yuhai Yusufu, Leo mimi pasi khofu, Singepata
takilifu, Kwa haya kunifikia
313. Yusufu nae kajibu, Wasemaje mahabubu, Leo ni wako
sahibu, Binyamini sikia
314. Yusufu na ndugu yake, Wakangia chumba pweke, Na Yusufu
atamke, Siri hapo kuitoa
315. Kampa la burudiko, Biyamini tamko, Mimi ndie ndugu
yako, Yusufu alopotea
316. Na muda ulipofika, Ndugu chakula kutaka, Ili wapate
ondoka, Kwa haraka kurejea
317. Wote wakamiminiwa, Magunia kujaziwa, Bila ya kulia
ngowa, Na Binyamini pia
318. Lakini gunia lake, La Yusufu ndugu yake, Yaani mdogo
wake, Huyo aliyeletewa
319. Humo mwake guniani, Kwa huyo Binyamini, Kaificha pishi
ndani, Yusufu kumtilia
320. Ndipo ndugu wakafisha, Safari kutayarisha, Mizigo
kuipandisha, Kuwabebesha ngamia
321. Na mara kwa muda huo, Kuepuka ndugu hao, Katika safari
yao, Wanjiani warejea
322. Askari nae basi, Akakimbia upesi, Akawakuta khalisi,
Bado wangali na njia
323. Muda alipowapata, Asikari, kuwakuta, Kwa kelele
kawaita, Mkono kuwapungia
324. Askari akanena, Kuwajulisha vijana, Nasema kwenu
mabwana, Jambo nilowaitia
325. Nimeambiwa nifike, Na Maliki niwashike, Imeibwa pishi
yake, Ya chakula kupimia
326. Na vijana wakafika, Kwa khofu kutetemeka, Khalafu
wakatamka, Askari kumwambia
327. Twaapa kwa Mwenye enzi, Twakupa iliyo wazi, Sisi bwana
sio wezi, Pishi tulowaibia
328. Yusufu kasisitiza, Mwishowe kuwauliza, Ni nini yake
majaza, Pishi aliyeitwaa
329. Walipoulizwa hayo, Wakamjibu kwa payo, Jaza yake mtu
huyo, Adhabu kumfikiya
330. Ikatazamwa vizuri, Kwa ndugu hao kabiri, Na ikawa
asikari, Pishi hakuivumbuwa
331. Basi akawa imara, Askari kuchakura, Hadi vijana ashara,
Kwenye yao magunia
332. Askari kakazana, Hata wa kumi kijana, Na pia hakuiona,
Pishi kuishuhudia
333. Kuja kutizama ndani, Kwa huyo Binyamini, Humo mwake
guniani, Pishi hio ikagwiwa
334. Kufika wakatongowa, Uongo wakauzuwa, Kwamba huyu hana
dawa, Si mwanzo kufanya haya
335. Na huyo ndugu wa mbele, Alimwivi vile vile, Hata tembe
ya mchele, Akiona huitwaa
336. Yusufu katabasamu, Moyoni katakalamu, Ni uovu ulotimu,
Machoni kunizulia
337. Bwana ufanye imani, Twakuomba kwa hisani, Muwache
Binyamini, Tafadhali twakwambia
338. Twaomba kwako Maliki, Na sote kutuafiki, Mmoja wetu
kubaki, Badili kumfidia
339. Yusufu yake kauli, La ndugu asikubali, Kushika mtu
badali, Hilo hakukubalia
340. Hapo akazidi chuki, Ndugu mkubwa hataki, Kanena mimi
sitoki, Misri nitabakia
341. Kuwasili kwa mzazi, Na mema maamkuzi, Kisha lao
simulizi, Baba kumuhadithia
342. Siri hawakuiziba, Wakampa wazi baba, Baba mwanao kaiba,
Nasi kumshuhudia
343. Na baba yake kauli, Kajibu hili si kweli, Hilo ni yenu
nakili, Ni hila mwaniletea
344. Kwa yote haya madhara, Inshalla niko imara, Mungu
tanipa subira, Njema ya kuvumilia
345. Kisa hiki kumfika, Ndipo alipokumbuka, Yale ya kwanza
mashaka, Ya Yusufu kupotea
346. Akanena kwa uchungu, Rudini enyi wanangu, Kwenye aridhi
ya Mungu, Musiogope udhia
347. Nendeni pasi nakhofu, Musijali takilifu, Mumtafute
Yusufu, Na Binyamini pamoya
348. Wakafika kwa heshima, Kwake Yusufu salama, Na wote
wakainama, Hishima kumfanyia
349. Khalafu kisha waanze, Wakatamka nduguze, Yusufu
wamueleze, Wanalolihitajia
350. Ewe mwingi wa fadhila, Tuna haja ya chakula, Sisi na
yetu aila, Tusije kufa na njaa
351. Nasi hatuna thamani, Wala kitu mkononi, Ila ni bidhaa
duni, Isiyo na manufaa
352. Yusufu kasikitika, Wazazi kawakumbuka, Machozi
yakamtoka, Hawezi kuvumilia
353. Sasa ndio wapambana, Yusufu na hao wana, Maswali
kujibizana, Siri Yusufu atoa
354. Yote mambo ya zamani, Ya kutupwa kisimani, Ndipo hapo
yabaini, Yusufu alotendewa
355. Yusufu awaambie, Ni nani wapili yeye, Alofarikana nae,
Baba alompotea
356. Ndugu wakamuarifu, Wakasema bila khofu, Jina lake ni
Yusufu, Mwana aloangamia
357. Na ndugu wakatongowa, Yusufu akajibiwa, Mwana huyo
kauawa, Na mbwa mwitu kuliwa
358. Yusufu akatamka, Kweli mbwa kamshika, Au nyinyi kwa
hakika, Kisa mumemtendea
359. Yusufu kasema tena, Na ndugu kujibishana, Hamukufanya
khiana, Kisimani kumtia
360. Na papo wakajibiwa, Na Yusufu kuambiwa, Jee aliemuuwa,
Ni nyinyi wenu mmoya
361. Ndugu nao kwa upesi, Wakanena kua sisi, Tutauwaje
nafusi, Bila kisa kutokea
362. Basi Yusufu kakaza, Kuzidi kuwaeleza, Yote
waloyafanyiza, Mpaka kuishilia
363. Na hiyo si dhambi katu, Kwa huyo mbwa wa mwitu, Hiyo ni
dhambi ya watu, Yenu mulokusudia
364. Ajabu yao ni kua, Vipi Yusufu kujua, Ni kama aliekua,
Yuko na wao pamoya
365. Baadae ndipo tena, Mmoja wao vijana, Alama akaiona,
Yusufu kamtambua
366. Na hapo kwa nyingi khofu, Kanena kwa takilifu, Wewe
kwani ni Yusufu, Bwana hebu niambia
367. Yusufu nae haraka, Na mara akatamka, Mimi ndie pasi
shaka, Yusufu alopotea
368. Ndie Yusufu wenzangu, Mimi mtume wa Mungu, Na huyu ni
ndugu yangu, Aliyeniandamia
369. Akazidi kukariri, Kuwapa ndugu khabari, Hakika
ukisubiri, Mja kwa kila udhia
370. Nao ndugu wakaanza, Yusufu wakamweleza, Mola
amekutukuza, Kwa dhiki kuvumilia
371. Kwa hili Yusufu kuwa, Mungu akujaze sawa, Kwa
uliyoyachukuwa, Mambo tulokufanyia
372. Yusufu nae kasema, Kuwajibu ndugu vyema, Leo hakuna
lawama, Kwenu nyinyi ndugu pia
373. Na Mola wetu Karimu, Tawasamehe Rahimu, Ndie mwenye
kurehemu, Viumbe wake Jalia
374. Kisha nae atamke, Yusufu kwa ndugu zake, Qamisi
muipeleke, Nawatuma nyote pia
375. Twaeni yangu libasi, Tena haraka upesi, Mufikapo
na qamisi, Kwa baba mukiingia
376. Musimpe mkononi, Nitakavyo ikhiwani, Mumbwagie usoni,
Macho yatamrudia
377. Na khalafu baadae, Murudi pamoja nae, Nyote kwangu
mugurie, Pasi mtu kubakia
378. Muje na wote jamaa, Na wala kutokataa, Tuje pamoja
kukaa, Hapa kwangu kuguria
379. Walipotoka nyumbani, Kwa Yusufu ikhiwani, Wakali bado
ndiani, Muda wakisafiria
380. Yaakubu mtukufu, Akasikia harufu, Ya qamisi ya Yusufu,
Puani kumuingia
381. Ilokwenda kwa upepo, Muda huo hapo hapo, Kwa Yaakubu
alipo, Harufu kumfikia
382. Yaakubu kabashiri, Kwa walokua hadhiri, Akawapasha
khabari, Akasema kuwambiya
383. Naisikia harufu, Ya mwanangu maarufu, Al-waladi Yusufu,
Fuadi alopotea
384. Jamaa wakamjibu, Kumweleza Yaakubu, Yuko wapi aloghibu, Alokufa kurejea
385. Mara kwa chache dakika, Saa kutomalizika, Hapo wana
wakafika, Kwa shangwe wakatokea
386. Na mbele ya kujilisi, Ili wapate marisi, Waliibwaga
qamisi,Usoni kumtupia
387. Akarejea kuona, Kama zama za ujana, Na kisha ndipo
kanena, Yaakubu kutongowa
388. Kujuza wale mabwana, Mbele ya kuja vijana, Kwa harufu
kushindana, Wakati wakiongea
389. Yaakubu katongowa, Mambo nnayoelewa, Najuwa musoyajuwa,
Mimi sikuwaambia
390. Kwa kufupisha maneno, Mambo yakawa manono, Furaha iso
mfano, Kwa baba na wana pia
391. Na hapo baba na wana, Wote kukumbatiana, Dhambi
kusameheana, Wana waloyakosea
392. Ikawa baba kuhama, Wana pamoja na mama, Wakawasili
salama, Kwa Yusufu kuguria
393. Kawakaribisha vyema, Aila ilomwandama, Kwa adabu na
heshima, Yusufu kuwapokea
394. Furaha ikawa kuu, Wana hadi wajukuu, Si shangwe mambo
makuu, Furaha kuwazidia
395. Kisha ndipo kawaweka, Wazazi wake katika, Kiti chenye
mamlaka, Heshima kuwafanyia
396. Na mara baba na mama, Na wana wakaandama, Kwa furaha
kuinama, Wakasujudu pamoya
397. Walipokwisha pumuka, Kwa furaha na kucheka, Wakashukuru
Rabuka, Kumhimidi Jalia
398. Na muda huo haraka, Yusufu papo kafika, Ndoto yake
kakumbuka,Ya zama zilopitia
399. Akamweleza mzazi, Babake kumpa wazi, Huno ndio uwaguzi,
Wa ndoto nilokwambia
400. Alizidi akinena, Wa ndoto niloiona, Katika wangu ujana,
Leo yatufunukia
401. Siku leo imefisha, Ya Mola kutonyesha, Haki
amehakikisha, Ilahi Pweke Mmoya
402. Tena Ilahi Karima, Kanitendea na wema, Kuniokoa salama,
Jela kunifungulia
403. Na nyinyi akawaleta, Niliko kunifuata, Mukaja
mukanikuta, Kwa salama na afiya
404. Kwa uwezo wa Rabbana, Kawaleta nyinyi tena, Tukaja
tukaonana, Kujumuika pamoya
405. Na mwisho wake khalafu, Mtume mwema Yusufu, Kamshukuru
Latifu, Huku akiombolea
406. Ewe Bwana Mtukufu, Uliyenipa sharafu, Ufalme uso khofu,
Bwana Ulotimilia
407. Ukanipa na uweza, Ndoto za kimiujiza, Uwaguzi
kunifunza, Tafsiri kuzijua
408. Ewe Mwenye enzi Mungu, Ya Ilahi Mola wangu, Uloumba
ulimwengu, Na ardhi zote pia
409. Ya ilahi niongowa, Nipite hali ya kuwa, Kila haki
kuijuwa, Na kwako kunyenyekea
410. Njia njema nionyeshe, Na wema nilahikishe, Yaani
nikutanishe, Na wetu wema Jalia
411. Na hapo akamaliza, Yusufu aloeleza, Pasi moja kulisaza,
Shukurani kutumia
412. Kwa hivyo wote wendani, Wakakutana yakini, Kama zama za
zamani, Siku zilizopitia
413. Kufikia kwa Yusufu, Aila ilo tukufu, Wakaishi bila
khofu, Kusahau yote pia
414, Kwa furaha wakadumu, Kwenye makao timamu, Nyoyo
zikatabasamu, Hadi kuaga dunia
415. Kwa kufupisha niseme, Yusufu kawa mtume, Kapata na
ufalume, Mola kumjaalia
416. Basi hapa waungwana, Yatosha niloyanena, Ya zaidi tena
sina, Samahani ila haya
417. Sasa ndio nasimama, Kisa chetu kimekoma, Na dua kwake
Karima, Naanza kuombolea
418. Ni wewe Mola Mmoja, Muumba wa sote waja, Itimize yetu
haja, Ilahi watusikia
419. Twakuomba Ya Manani, Isilamu ikhiwani, Tuongoze kwenye
dini, Imani kutuzidia
420. Tupe nguvu za nafusi, Tumshinde Ibilisi, Asiipate
nafasi, Njia mbovu kututia
421. Twakuomba Ya Wadudi, Machafu yawe baidi, Na waovu
mahasidi, Yao kutowanyokea
422. Ya Ilahi Ya Karimu, Tupe akili timamu, Ya dini na ya
ilimu, Tushike bila udhiya
423. Tulinde tuwe wekevu, Tuyaepuke maovu, Na nyoyo ziwe na
nguvu, Machafu kuyakimbia
424. Tuepushie na dhara, Kwa dini tuwe imara, Twaiomba na
sitara, Ya akhera na dunia
425. Dua ifike ulipo, Na kabuli ije papo, Utupe na njema
pepo, Hiyo ulotwandalia
426. Amina Rabi amina, Amina Mola amina, Utukabalie Bwana,
Kwa baraka za nabiya
427. Na hapa ninamsifu, Mola wetu Mtukufu, Mkubwa Mtakatifu,
Taala Rabi Jaliya
428. Na mtume Muhammadi, Mjumbe wake Wadudi, Kila siku
turadidi, Swala na salamu pia
429. Bwana Saidi Karama, Mungu takwegesha pema, Akupe na
nyingi hima, Malenga usiye doa
430. Nimekisoma kitabu, Hakuna moja aibu, Yote haya ni
thawabu, Uliyotuhadithia