KUTHIBITISHA KUONEKANA ALLAH
(SUB’HAANAHU WATA’ALAA) KWA MACHO HUKO AKHERA
MAJIBU NA MAELEZO
Muandishi: Abul Fadhl Kassim Mafuta Kassim
Yaliyomo
Vipi Tutamfahamu Mola Wetu Na
Wapi Tuichukue Imani Ya Dini Yetu?
Uchambuzi Yakinifu Juu Ya Elimu
Ya Hadithi.
Mashar’ti Ya Usahihi Wa Hadithi
Tuhuma Za Uwongo Dhidi Ya Ahli
Sunna
Historia Ya Abul-Hasan Kwa
Ufupi
Yaliyomo Katika Kitabu
“Al-Ibana”
Uchambuzi Yakinifu Juu Ya Suala
La Majazi
“Chanzo Cha Kutumbukia Katika
Itikadi Batili
Je Wenye Kupinga Majazi Wana
Hoja Za Kielimu?
Hoja Za Wenye Kuthibitisha
Majazi
Hoja Za Wenye Kuitakidi
Kuonekana Allah Huko Akhera.
Jaribio La Kwanza La Kuipotosha
Hoja Hii
Jaribio La Pili La Kupotosha
Hoja Hii
Jaribio La Kwanza La Kuipotosha
Hoja Ya Pili
Juma Na Sheikh Wake Al-Qannubi
Wamzulia Uwongo Sheikh Al-Bani.
Hata Mufti Wao Pia Asema
Uwongo!
“Kasoro Ya Pili Ya Hadithi Hii:
Maana Sahihi Ya Neno
“Al-Ziyadah”
Jaribio La Kwanza La Kupotosha
Hadithi Hii
Tuhuma Yake Ya Pili Dhidi Ya
Qais:
Ufahamu Wake Mbaya Juu Ya
Hadithi Hii
Jaribio La Kwanza La Upotoshaji
Hoja Za Wenye Kupinga Kuonekana
Allah Kwa Macho Huko Akhera.
Jaribio Lake Jingine La
Upotoshaji
Kauli Za Baadhi Ya Maimamu Juu
Ya Suala Hili.
Jaribio La Kuipotosha Kauli Hii
© 2008-02-25 Haki ya uchapishaji inamilikiwa na muandishi.
Ni ruhusa kwa mtu yoyote kukitoa copy na kukisambaza kitabu hiki
kwa dhumuni la kufikisha ujumbe kwa waislamu kokote walipo.
Lakini hairuhusiwi kubadilisha chochote bila ruhusa ya muandishi
wa kitabu hiki.
Abul-Fadhli Kassim Mafuta Kassim
KITABU HOJA ZENYE NGUVU KATIKA KUTHIBITISHA KUONEKANA ALLAH KWA
MACHO HUKO AKHERA, MAJIBU NA MAELEZO.
MARKAZ SHEIKHIL-ISLAMI IBN TAYMIYYAH AL-SALAFIY,
P.O.BOX 398 TANGA,
MOBILE: 0715 615645 / 0784 615645.
BARUA PEPE: kassimmafuta@yahoo.com
PONGWE-TANGA.
TANZANIA.
بسم الله الرحمن الرحيم
إنَّ الحمْدَ للهِ نَحْمَدُهُ ونستعينُ بهِ
ونَستَغْفِرُهُ، ونعوذُ باللهِ من شرورِ أنفُسِنا وسيِّئاتِ أعمالِنا من يهْدِهِ
اللهُ فلا مضل له ، ومن يُضْلِلْ فلا هاديَ
له. وأشهد أن لا إلهَ إلاّ اللهُ وحدَهُ لا شريكَ له. وأشهَدُ أنَّ مُحمَّداً
عبْدُهُ ورَسولُهُ، ارسله بالهدى ودين الحق ليظهره على الدين كله ولو كره
الكافرون.
(يَا
أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا اتَّقُوا اللَّهَ حَقَّ تُقَاتِهِ وَلا تَمُوتُنَّ
إِلَّا وَأَنْتُمْ مُسْلِمُونَ)([1])
[سورة آل عمران: الآية: 102]. (يَا أَيُّهَا النَّاسُ اتَّقُوا رَبَّكُمُ الَّذِي
خَلَقَكُمْ مِنْ نَفْسٍ وَاحِدَةٍ وَخَلَقَ مِنْهَا زَوْجَهَا وَبَثَّ مِنْهُمَا
رِجَالاً كَثِيراً وَنِسَاءً وَاتَّقُوا اللَّهَ الَّذِي تَسَـاءَلُونَ بِهِ
وَالْأَرْحَامَ إِنَّ اللَّهَ كَانَ عَلَيْكُمْ رَقِيباً)([2])
[سورة النساء، الآية: 1].
(يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا اتَّقُوا
اللَّهَ وَقُولُوا قَوْلاً سَدِيداً يُصْلِحْ لَكُمْ أَعْمَالَكُمْ وَيَغْفِرْ
لَكُمْ ذُنُوبَكُمْ وَمَنْ يُطِعِ اللَّهَ وَرَسُولَهُ فَقَدْ فَازَ فَوْزاً
عَظِيماً)([3])
[سورة الأحزاب، الآيتان: 70، 71].
أما بعد فإنَّ أصدَقَ الحَديثِ كِتَابُ اللهِ
تعالى، وخَيرَ الهَدْيِ هَدْيُ مُحَمدٍ صلى الله عليه وسلَّمَ، وشَّرَّ الأمورِ
محدثاتُها، وكُلَّ مُحْدَثَةٍ بِدْعَه
وكُلَّ بدعةٍ ضلالةٌ، وكُلَّ ضلالَةٍ في النار.
Ama baada ya kumsifia mola wetu kwa sifa njema, sina budi
kumswalia Mtukufu Mtume wetu Muhammad –swalla llaahu alayhi wasallam-, na swala
na salamu hizo pia ziwafikie Aali zake, wake zake, maswahaba zake na wale wote
walioiandama njia yao kwa wema mpaka siku ya malipo.
Kwanza, napenda kusema machache kuhusu kitabu hiki, sababu za
kuandikwa kwake na madhumuni yake.
Sababu kuu na asili ya kitabu hiki ni majibu na maelezo dhidi ya kitabu
kiitwacho; “HOJA ZENYE NGUVU JUU YA KUTOONEKANA MWENYEZI MUNGU KWA MACHO” cha
Ndugu JUMA M. Al-Mazrui.
Maudhui ya kitabu hicho ni kama kinavyojieleza chenyewe katika
anwani yake, nayo ni kupinga kuonekana kwa Allah kwa macho huko akhera, na hiyo
ndiyo itikadi ya makundi mengi ya batili kama vile: Mu’tazila, Khawariji
(Ibadhi), Shia, na wengineo.
Ndugu Juma M. Al-Mazrui muandishi wa kitabu hicho hakuleta jambo
jipya, bali amejikakamua kwa kiasi kikubwa mno kuitetea itikadi hiyo batili
inayopingana na mafundisho sahihi ya Qur’an na Sunna za Mtume wetu
Muhammad-swalla llaahu alayhi wasallam-.
Baada ya kukisoma kwa utulivu na umakini kitabu hicho chenye
kurasa 339 kutoka mwanzo hadi mwisho, sikuweza kuuvumilia upotoshaji
alioufanya, ndipo nilipoamua kukirudia tena na tena kwa lengo la kuyadhibiti
yale ambayo nimeyaona kuwa ndio mambo ya msingi aliyoyategemea muandishi huyo
kwenye kitabu chake hicho kwa lengo la kutaka kuhakiki zaidi.
Baada ya kufanya utafiti wa kielimu ambao lengo lake lilikuwa ni
kupata faida, nikaona kuwa ninaowajibu wa kuzitawanya faida hizi ili ziwafikie
wengineo katika waislamu ambao wengi wao hawana uwezo wa kufanya utafiti wa
kielimu kwa kutumia misingi sahihi mpaka kuufikia ukweli.
Kutokana na majukumu niliyonayo pamoja na ufinyu wa wakati, kazi
hii niliiona kuwa ni ngumu mno hivyo nilikata tamaa, kwa sababu shughuli hii si
ndogo na inahitaji muda wa kutosha, lakini mambo makuu manne ndiyo yaliyonipa
moyo wa kukiandika kitabu hiki:
i) Amri zilizokuja kuhimiza kuibainisha haki, na makatazo
yaliyokuja kuharamisha kuinyamazia batili.
ii) Hali ya hatari ambayo inayowakabili waislamu wengi hasa wale
wasio na uwezo wa kufanya utafiti wa kielimu; ima kwa sababu ya udhaifu wa
kielimu au kwa sababu ya uvivu wa kutafiti au kukosa nyenzo za kufanyia utafiti
huo au kwa sababu nyinginezo, hivyo hawataweza kukabiliana kielimu dhidi ya
ubabaishaji alioufanya ndugu Juma, na hatima yake wataingia kwenye dimbwi la
batili kwa kudhania kuwa upotoshaji alioufanya ndugu Juma Mazrui kuwa ni haki.
iii) Kupambana kwa kalamu dhidi ya watu wa bid’a na wapotoshaji
wote ni moja katika amali njema za kumweka mtu karibu na Mola wake kwa sababu
ni katika sampuli za Jihadi.
iv) Na kwa kuwa suala hili linafungamana na kuhusiana na mambo ya
itikadi, ambayo ndiyo msingi wa dini, bado tuna wajibu wa kuielimisha jamii
hata kama hakujitokeza mpotoshaji.
Kwa kuyazingatia yote hayo, nilipata ari na hima ya kulikabili
jambo hili kwa umakini, na kwa Tawfeeq
ya Allah nikafanikiwa kukikamilisha kitabu hiki kwa salama.
Na zote hizo ni miongoni mwa fadhila nyingi za Mola wangu juu
yangu, ninamuomba anijaalie niwe miongoni mwa wenye kumshukuru.
Muandishi.
Abul-Fadhli Kassim Mafuta Kassim.
كلمة شكر وتقدير
بسم الله الرحمن الرحيم
الحمد لله رب العالمين والصلاة
والسلام على اشرف الانبياء والمرسلين وعلى آله واصحابه والتابعين لهم باحسان الى
يوم الدين.
فقد اطلعت على كتاب الأخ الفاضل
ابى الفاضل قاسم مفوتا فاسم فوجدته كتابا مفيدا فياثبات رؤية الله تعالى في الآخرة
وكشف فيه عن كذب الأخ جمعة المزروعي وشوخه وتلبيسهم في تلك الحجج الظاهرة كالشمس
في رابعة النهار. فجزى الله المؤلف عنا وعن المسلمين خير، وبارك الله له في علمه
وفي جهوده الجبارة في نشر عقيدة السلف الصالح والذب عنها.
وصلى الله وسلم على نبينا محمد
وعلى آله وصحبه أجمعين.
كتبه الفقير الى رحمة الله:
ابوهاشم
عبدالقادر بن هاشم بن عبدالقادر المساوي
13/جمادي
الأولى/1430 هـ
8/مايو/2009
Sifa njema zote ni za Allah Bwana wa viumbe wote, na swala na salamu
zimshukie mtukufu wa Manabii na Mitume, na Jamaa zake na Swahaba zake na
waliowafuatia hao kwa wema mpaka siku ya malipo.
Ama baada ya yaliyotangulia.
Nimekitalii kitabu cha ndugu mbora Abul-Fadhli Kassim Mafuta
Kassim, nikakikuta kuwa ni kitabu kilicho na faida kwa sampuli yake, katika
kuwajibu Makhawariji wa Kiibadhi, pale mtunzi alipozileta HOJA ZENYE NGUVU
katika kuthibitisha kuonekana Allah huko Akhera kwa macho, na akaufichua uwongo
wa ndugu Juma Al-Mazrui na masheikh zake pamoja na ubabaishaji wao kwa hoja za
wazi wazi kama vile jua lililokuwa katikati ya mchana.
Allah amlipe mtunzi kheri kwa sababu ya kuwatumikia waislamu, na
ambariki katika elimu yake na juhudi zake kubwa katika kuitangaza itikadi ya
Salaf na kuitetea.
Na swala na salamu zimshukie Mtume wetu Muhammad na Jamaa zake na
Maswahaba zake wote.
Al-Akhi Sheikh Abu Hashim Abdul-Qadir Ibn Hashim Ibn Abdul-Qadir
Al-Musawaa
13 /Jumadal-Ulaa /1430 H.
8 /Mei / 2009 M.
Ama baada ya kukipitia kitabu cha ndugu yetu Abul fadhli Kassim
Mafuta, kitabu chenye anuani ya kitabu HOJA ZENYE NGUVU katika kuthibitisha
kuonekena Allah kwa macho huko akhera, majibu na maelezo, kitabu hiki
nimekipitia chote kwa uwangalifu na insaafu, ni kitabu madhubuti kinacholingana
na jina lake kwani makusudio yake makubwa ni kutetea itikadi sahihi ya Manabii
na Mitume wote, itikadi ya AHLI SUNNATI WAL-JAMAA dhidi ya waandishi wa uwongo,
walio dhidi ya itikadi hii safi, kwani kitabu hiki kimebainisha waziwazi kwa
hoja sahihi juu ya upotovu wa mtunzi wa
kitabu kiitwacho HOJA ZENYE NGUVU JUU YA KUTOONEKANA MWENYEZI MUNGU KWA MACHO
cha ndugu JUMA AL-MAZRUI ambae ni miongoni mwa wafuasi wa mapote ya matamanio
kwani ndugu Juma ndani ya kitabu chake hicho amemsingizia uwongo Mwenyezi Mungu
na Mtume wake kama kawaida ya watu wa matamanio kumsifu Allah sub’haanahu
wata’alaa kwa sifa ambazo ametakasika nazo za kutoonekana, ilhali Mwenyezi Mungu Sub’haanahu wata’alaa amejisifu
yeye mwenyewe nafsi yake kwa sifa ya kuonekana huko akhera na pia akasifiwa na
Mtume wake Muhammad swalla llaahu alaihi wasallam kwa sifa hiyo hiyo ya
kuonekana na hii ndio itikadi ya Maswahaba wa Mtume Muhammad swalla llaahu alaihi wasallam na ndio itikadi
ya Taabiina na wema waliofuata baada yao itikadi ya Ahli-Sunnat Wal-Jamaa.
Ndugu Juma Al-Mazrui ameandika kitabu hicho ili atetee itikadi
yake ya kikhawarij kama ilivyo kawaida ya watu wa matamanio kabla ya kusoma na
kufahamu jambo, wao kwanza ni kutetea itikadi zao vyovyote iwavyo kama vile
walivyoipokea toka kwa mababu zao, lakini kwa rehema za Mwenyezi Mungu
sub’haanahu wata’alaa amejaalia katika umma huu kama anavyosema Mtume katika
hadithi sahihi kwamba: HALITAACHA KUWEPO KUNDI KATIKA UMMA WANGU LENYE
KUPIGANIA HAKI HAWATADHURIWA NA WASIOWASAIDIA NA WALA HATADHURIWA NA
WANAOWAPINGA MPAKA KITAKAPO SIMAMA
KIYAMA na watu hawa ni AHLI-SUNNAT WAL-JAMAA.
Ama ndugu Juma Mazrui mimi namlaumu sana kwa kufanya haraka
kuandika kitabu hicho bila ujuzi wa dini, lakini baada ya lawama namuomba Mwenyezi
Mungu amuongoze ndugu Juma na ampe maarifa na amtoe katika hali ya itikadi
potofu, kwani kubwa la Juma ni kumuamini sana Said Mabruk Al-Qanuubi bila
kumuelewa elimu yake na uwadilifu wake kwani inaonyesha bwana Juma hamfahamu
bwana huyu Qannubi na ndio maana akampachika majina makubwa ya kielimu ambayo
hastahiki jinsi alivyo, kwani Said Qannubi si mwengine zaidi ya kuwa ni
mwanakasumba wa kikhawariji si mkweli, angelikuwa ni mkweli asingelifikia hali
ya kunukuu hoja hai za ndani ya vitabu vya wanakasumba na watu wa matamanio na
yeye kuzifanya hoja za kuwarudi Ahli-Sunnat wal-Jamaa.
Ama marudio anayorudiwa ndugu Juma ndani ya kitabu hiki ni malipo
yatokanayo na chumo la mikono yake iliyoandika maandiko ya Qannubi ambaye
ni mwanakasumba wa kikhawariji
aliyeiajiri mikono yake juu ya kunukuu maneno ya watu wa matamanio wenye chuki
dhidi ya wanasunnah, na maimamu wa Ahli-Sunnat.
Miongoni mwa watu anaowaiga Qannubi maandiko yao ni kama
Al-kauthari, na Abuu Ghudah na Jamal-din Af’ghani ambaye si Muaf’ghani bali ni
Muirani, na Butwi na Al-Maliki katika watu wa hivi karibu na pia miongoni mwao
hao ni pote la Muutazilah kwani wao ndio wanaopinga sana kuonekana kwa Mwenyezi
Mungu sub’haanahu wata’alaa kwani pote hili elimu yao yote imejengeka juu ya
misingi ya mijadala ambayo asili yake ni vipimo vilivyo juu ya kufananisha
kisichopo kwa kilicho kuwepo na miongoni mwa maigizo ya Qannubi ni pote la
Jahmiyyah, Baatiniyya, Mashia Imamiyyah ndio maana utayakuta maandishi yao yote
juu ya kutoonekana Mwenyezi Mungu sub’haanahu
wata’alaa wanayanukuu kwa mwana matamanio mkubwa adui wa Mwenyezi Mungu
sub’haanahu wata’alaa Abdul Jabbar al-Muutazili kwenye kitabu chake almughni,
hasa katika zile hoja za kiakili alizozitaja Alkhalili kama alivyomnukuu Juma
Mazrui katika kitabu chake Al-Haqu Addamigh ukurasa 67, kwamba kuona kwa macho
ni kuingia sura …., na kadhalika amefananisha kuonekana Mwenyezi Mungu
sub’haanahu wata’alaa na kuonekana viumbe, ametakasika Mwenyezi Mungu na dhana
zao.
Na vilevile Qannubi si mwenye elimu ya vitendea kazi (Qawaid) vya elimu za waislamu kama somo la hadithi na
ala zake na usuli na misingi ya fiqhi na lugha ya waarabu, lakini ni shujaa
asiye na uwoga wala aibu na ndio maana utakuta mara nyingi hutoa hukumu juu ya
hadithi kutokana na ushujaa wake mfano;- anasema kwamba hadithi ambazo
zimepokewa zenye kuifasiri aya ya 22 na ya 23 za surat Al-Qiyamah ni dhaifu na
za uwongo, na Juma Al-Mazrui akamfuata kiongozi wake Qannubi na ilhali hadithi
hizo zote zilizokuja kutafsiri aya hizo ni Mutawatir kwa mujibu wa majio yake
na kwa mujibu wa ushuhuda wa wanazuoni wa somo la hadithi, pia Qannubi kutokana
na kutoelewa somo hili utakuta anamtia ila (dosari) mpokezi wa hadithi pasi na
kuielewa ila ile kwamba haiwi hadithi ya mpokezi yule ni dhaifu, mfano amemwita
imamu Zuhri kwamba ni Mudalis ili aidhoofishe hadithi zake bila kubainisha ni
tadlis ipi ili muradi atetee matamanio yake.
Haya nimeyataja machache, lakini makosa ya namna hii ni mengi juu
ya Qannubi na mfano wa hayo, na yote haya yanatokana na kasumba za kimadhehebu
zinazompelekea Qannubi na mfano wake kuandika mambo wasioyajua ili watetee
madhehebu yao kwa hali na mali, mfano Juma Mazrui, nikisema kwamba hana ujuzi
katika somo la hadithi sitakosea, lakini hebu tumsikilize yeye mwenyewe
anavyojieleza katika kitabu chake “Hoja zenye nguvu” katika ukurasa wa 194 anamwita mpokezi wa
hadithi kwa jina ambalo sio lake, mpokezi huyu jina lake ni Ibn Halbas yeye
akamwita Abu Halbas, mfano mwingine katika kitabu chake hicho katika ukurasa wa
69 amemwita Al-Duuriy, Al-Dauri na haya ni mengi mno kwenye maandiko ya Juma na
haya ni kwa kuwa haja wahi kukaa na watu wa elimu hizi, labda aliwahi kukaa na
Qannubi kisha akamuiga porojo zake na ndio maana akasema Ibnu-Halbas ni
majhulil-ayn bila ya kubainisha ni majhul wa vipi, lakini yeye katika uibadhi
wake Imamu wake aitwae Abuu Ubaidah Muslim Ibni Abi Karimah yeye ndiye Majhuli
tena ni Majhulil-Ayn, mtu huyu ni kigano, lakini kwa kutojua kwao wanadhania
yupo, sitaeleza mengi bali mengi yameshaelezwa ndani ya kitabu hiki na mwenye
kutaka haya arudi kuangalia vitabu vya watu wa Sunnah kama kitabu Assunnah,
Arrisalatu alhamawiyyatu alkubraa, Al-Aqidatu Atwahawiyah, na Minhaju Assunnah
na vinginevyo.
Ama kitabu hiki cha ndugu yetu Abul-Fadhli ni kitabu
kilichokusanya faida nyingi sana haswa katika somo azizi la hadithi na pia
katika somo la lugha ya waarabu, faida ambazo hazipatikani katika vitabu vingi
vilivyokwisha andikwa kwa lugha ya waswahili. Mwenyezi Mungu sub’haanahu
wata’alaa amlipe ndugu yetu huyu kheri na amzidishie elimu na uongofu na
kulingania dini ya Mwenyezi Mungu sub’hanahu wata’alaa kwa hekima na elimu,
kwani Mwenyezi Mungu ndiye mwenye kutakabali dua za watu wake na rehema na
amani zimfikie Mtume wetu Muhammad swalla llaahu alaihi wasallam na Aali zake na
Maswahaba zake.
Al-Akhi Sheikh Abuu Saam Seif .S. Al-Ghafriy.
Ni Allaah peke yake ndiye wa kuhimidiwa na kushukuriwa, kwa hiyo
sina budi kusema:
الحمد لله (Al-Hamdu lillaahi) kwa kuniwezesha kukiandika kitabu hiki na
ninamuomba Allaah akijaalie kitabu hiki kiwe ni chenye kheri, faida na manufaa
kwa waislamu wote hasa wasomi wa mambo ya dini na wale wenye kuitafuta elimu ya
dini na kuyafuatilia mambo ya dini kwa ukaribu na wakawa wako tayari kutoa
wakati wao na hali na mali zao kwa ajili ya elimu ya kuutafuta ukweli kupitia
elimu ya dini.
Pamoja na hayo, pia ninawashukuru wale wote ambao wametoa juhudi
zao kwa njia mbali mbali kwa ajili ya kufanikisha kutoka kwa kitabu hiki, ima
kwa kutoa nasaha na ushauri wao, au kwa kuutumia wakati na mali zao.
Pia ninawashukuru ndugu zangu wapenzi:
Sheikh Abu Hashim Abdul-Qadir Hashim Al-Musawaa Al-Hashimiy.
Na Sheikh Abu Saam Seif .S. Said Al-Ghafriy.
Kwa kazi yao kubwa waliyoifanya ya kukipitia kitabu hiki na kwa
nasaha zao na ushauri wao walioutoa. Pia ninamshukuru ndugu yangu mpenzi Sheikh
Abu Ar’qam Abdallah Muhsin kwa kunishajiisha na kunipa moyo wa kukichapisha
kitabu hiki wakati nilipomuonyesha nuskha ya kitabu hiki kabla ya kukichapa.
Mwisho ninamshukuru Ahli yangu Ummul-Fadhli kwa ustahamilivu wake
na uzito alioubeba mpaka nikaweza kukimaliza kitabu hiki.
Abul-Fadhli Kassim Mafuta Kassim
Markaz Sheikhil-Islami Ibn Taymiyyah, Pongwe-Tanga Tanzania
25/SHAABAN/1428 H = 26/08/08 M.
Nimekianza kitabu hiki kwa kumsifia Allah sub’haanahu wata’alaa
Mola wetu mkarimu na kumswalia Mtume wetu Muhammad swalla llaahu alaihi
wasallam pamoja na Aali zake na Maswahaba zake wote.
Kisha nikalazimika kuzijibu baadhi ya tuhuma za uwongo ambazo
amezileta ndugu Juma dhidi ya maulamaa wa kiislamu kama vile Ibnu Taymiyyah, na
Ibnul-Qayyim Allah awarehemu kwa lengo la kutaka kuwachafua.
Kisha nikaweka mlango maalumu kwa ajili ya kuelezea kwa muhtasari
uchambuzi wa elimu ya hadithi, na kanuni za upokezi wa habari.
Pia tukabainisha sababu za msingi za upotevu wa watu, na
kuyabatilisha madai ya uwongo ya ndugu Juma pale alipodai kuwa chanzo na sababu
ya upotevu ni kukataa kuwepo kwa majazi ndani ya Qur’ani.
Pia tumelazimika kujadili kielimu tena kwa muhtasari suala la
Majazi kuwepo kwake na kutokuwepo na tofauti za maulamaa wa kiislamu juu ya
suala hilo.
Kisha ndio tukaanza kuubainisha msimamo sahihi wa AHLI-SUNNA
WALJAMAA, juu ya mas’ala ya kuonekena
Allah kwa macho huko akhera, na suala hili ndiyo maudhui mama ya kitabu hiki.
Na tumelizungumzia suala hili kwa namna tatu:
i) Kuithibitisha itikadi hii kupitia maandiko matakatifu ya dini yetu
kama vile; Qur’an na Hadithi sahihi za Mtume Muhammad -swalla llaahu alayhi
wasallam- pamoja na kutoa maelezo kwa muhtasari juu ya maandiko hayo.
ii) Pia nimetumia kauli za Maswahaba na wanafunzi wa Maswahaba
(Taabiina) na Maimamu wakubwa wa kiislamu kama vile Imamu Malik, Imamu Shaafiy,
Imamu Ah’mad bin Hanbal na wengineo kwa lengo la kuutilia nguvu msimamo wetu,
na kuibatilisha dhana ya kwamba itikadi ya kuonekana Allah akhera kwa macho ni
itikadi ya wale ambao ndugu Juma na kaumu yake anawaita kuwa ni Mawahabi.
iii) Kuzivunja baadhi ya hoja batili zilizotolewa na muandishi
huyo hasa zile ambazo ndiyo msingi aliojengea juu yake itikadi yake hiyo
potofu.
iv) Mwisho tukamalizia kwa kuweka Khatima.
Hayo yote nimeyafanya kwa ufupi mno, na sikutaka kumjibu hoja
baada ya hoja au neno kwa neno kwa kuhofia kurefusha, hasa ukizingatia kuwa
ndugu Juma Mazrui amekijaza kitabu chake maneno mengi ambayo si ya kweli na
yasiyo na uzito katika misingi ya kielimu.
Hili ni swali muhimu mno na jawabu sahihi la swali hili ndiyo
ufumbuzi wa matatizo mengi yaliyojitokeza katika umma wa kiislamu, kwa sababu
waislamu wengi hawajui vipi watamfahamu mola wao muumba, na wapi wanatakiwa
kuichukua dini yao !
Ama Ahlu Sunna wal Jama’a wao wanaitakidi kwamba:
Tutamjua mola wetu kwa vile alivyojielezea yeye mwenyewe katika
kitabu chake (Qur’an tukufu) na vile alivyotuelezea mjumbe wake mtukufu katika
mafundisho yake yaliyo sahihi.
Kwa kuyathibitisha yale yote ambayo Allah amejithibitishia
mwenyewe au ambayo ameyathibitisha Mtume wake -swalla llaahu alayhi wasallam-,
na kuzikanusha sifa ambazo Allah na Mtume wake swalla llaahu alaihi wasallam
wamezikanusha, bila ya kupotosha, wala kupinga, wala kumfananisha yeye na
chochote katika viumbe vyake, pamoja na kufuta dhana ya kwamba kuyathibitisha
yale ambayo Allah amejisifia nayo kuwa ni kumfananisha yeye –Jalla Jalaaluh- na
viumbe vyake.
Na tunaichukua imani ya dini yetu kutoka kwenye Qur’an na Sunna
(mafundisho) sahihi ya Mtume wetu Muhammad -swalla llaahu alayhi wasallam-
pamoja na kuuzingatia ufahamu wa Salaf Swaalih (wema waliotangulia) kama vile;
Maswahaba na Taabi’ina (wanafunzi wa Maswahaba) na maulamaa waliokuja baada
yao.
Na hivi ndivyo tulivyoamrishwa na Qur’an kadhalika Sunna sahihi za
Mtume swalla llaahu alayhi wasallam.
Amesema Allah -azza wajalla-:
وَإِذَا قِيلَ
لَهُمْ آمِنُواْ كَمَا آمَنَ النَّاسُ قَالُواْ أَنُؤْمِنُ كَمَا آمَنَ
السُّفَهَاء أَلا إِنَّهُمْ هُمُ السُّفَهَاء وَلَـكِن لاَّ يَعْلَمُونَ
البقرة13
“Na wanapoambiwa:aminini
KAMA WALIVYOAMINI WATU wanasema;
Tuamini kama walivyoamini
wapumbavu?...”.
Suratul-Baqarah aya ya 13.
Imepokewa kutoka kwa Ibnu Mas’oud na Ibn Abbaas kwamba wamesema:
“Watu waliokusudiwa hapa ni maswahaba”.
Tazama tafsiri al-Durrul-Manthuur juzuu ya 1 ukurasa 70-71.
Na maana ya aya hii ni kwamba makafiri na wanafiki walikuwa
wakiambiwa kwamba wamuamini Allah kama walivyoamini Maswahaba wa Mtume Muhammad
-swalla llaahu alayhi wasallam- wao kwa sababu ya kiburi, na jeuri zao walikuwa
wakiwatukana Maswahaba kwa kuwaita wapumbavu, na hali ya kuwa wapumbavu ni wao
!
Na amesema tena Allah:
فَإِنْ
آمَنُواْ بِمِثْلِ مَا آمَنتُم بِهِ فَقَدِ اهْتَدَواْ وَّإِن تَوَلَّوْاْ
فَإِنَّمَا هُمْ فِي شِقَاقٍ فَسَيَكْفِيكَهُمُ اللّهُ وَهُوَ السَّمِيعُ
الْعَلِيمُ
“Basi wakiamini KAMA
MLIVYOAMINI NYINYI (maswahaba) basi watakuwa wameongoka.Na wakikengeuka basi
wao wamo katika upinzani”.
Suratul Baqarah aya ya 137.
Katika aya hii Allah anawataka Ahlul-kitabi (Mayahudi na Wakristo)
wamuamini Allah kama walivyoamini Maswahaba na waislamu wote kwa ujumla walio na
imani kama ya Maswahaba, na kama wataasi wakenda kinyume na Amri hiyo, basi wao
watakuwa ni waasi na ni wapinzani wa Allah.
Na amesema tena Allah:
وَمَن يُشَاقِقِ الرَّسُولَ مِن
بَعْدِ مَا تَبَيَّنَ لَهُ الْهُدَى وَيَتَّبِعْ غَيْرَ سَبِيلِ الْمُؤْمِنِينَ
نُوَلِّهِ مَا تَوَلَّى وَنُصْلِهِ جَهَنَّمَ وَسَاءتْ مَصِيرًا
“Na anaye mpinga Mtume
baada ya kumdhihirikia uwongofu na AKAFUATA NJIA ISIYOKUWA YA
WAUMINI,tutamuelekeza alikoelekea mwenyewe,na tutamuingiza katika
Jahannamu....”.
Surat An Nisaa aya ya 115.
Amesema Allah:
وَالسَّابِقُونَ
الأَوَّلُونَ مِنَ الْمُهَاجِرِينَ وَالأَنصَارِ وَالَّذِينَ اتَّبَعُوهُم
بِإِحْسَانٍ رَّضِيَ اللّهُ عَنْهُمْ وَرَضُواْ عَنْهُ
“Na wale waliotangulia,
wakwanza katika Muhajirina na Answaari,na wale
waliowafuata kwa wema, Allah ameridhika nao, na wao wameridhika
naye....”.
Suratut Tawba aya ya 100.
Kwa mujibu wa aya hizo zote tulizozitaja, tunatakiwa waislamu wote
kuamini kama walivyoamini maswahaba wa Mtume Muhammad -swalla llaahu alayhi
wasallam- pamoja na kuifuata njia waliyoipita.
Na kama imani zetu zitatofautiana na imani zao na njia yetu
ikitofautiana na njia yao, basi tutakuwa ndani ya mashaka makubwa mno na
upotevu uliowazi kama zilivyoeleza aya tulizozitaja.
Hivyo basi, tunapolizungumzia suala zima la kumuamini Allah
–Sub’haanahu Wata’alaa- ni lazima tujiulize maswali yafuatayo:
Je imani zetu zinaendana na mafundisho ya Qur’an na Sunna kama
walivyofahamu wema waliotangulia (Salaf Swalih)?
Je hivi tunavyoitakidi ndivyo walivyoitakidi hao Salafu Swalihi (wema
waliotangulia) au la?
Na kama jawabu likiwa la, basi tujue kwamba tumo ndani ya upotevu
kwa kuifuata njia isiyokuwa ya hao waumini wa mwanzo.
Na bila shaka, wao wameifahamu vizuri Qur’an na walimfahamu vizuri
Mtume -swalla llaahu alayhi wasallam- kuliko walivyomfahamu na wanavyomfahamu
na watakavyofahamu watakaokuja baada yao, ndiyo maana Allah akawasifia wao na
wale walioifuata njia yao kwa wema, na akawaahidi mambo mazuri.
Na wakati huo huo akawasema vibaya wale waliyoihalifu njia hiyo,
na kuwaandalia makazi mabaya motoni
-Allah atuepushe na adhabu zake-.
Hivyo basi, katika suala hili la kuonekana au kutokuonekana Allah
kwa macho huko akhera pia tunatakiwa pale tunapozitazama aya na hadithi zinazo
lizungumzia suala hili tuutangulize mbele ufahamu wa hao wema waliotutangulia
(Salafu Swalihi) katika imani, vipi wao walizifahamu aya na hadithi hizo?
Na ilikuwaje imani yao juu ya suala hilo?
Je waliamini kwamba Allah ataonekena kwa macho huko akhera kama
wanavyo amini Ahli Sunna?
Au Allah hataonekana kwa macho huko akhera kama ilivyokuwa itikadi
ya makundi mengine kama vile: Jah’miyyah, Mu’tazila na wajukuu zao kama vile
Shia, Ibadhi na wengineo miongoni mwa watu wa bid’a?
Inshaallah swali hili litajibiwa na kitabu chetu hiki, tafadhali
fuatilia kwa makini na insafu utagundua ukweli juu ya suala hili.
Huenda mtu akatatizika au akatatizwa kwa kuambiwa: vipi tufuate
njia ya hao waliotangulia (Maswahaba,Taabi’ina, na Maimamu waliokuja baada yao)
na hali yakuwa wao wenyewe wametofautiana katika mambo mbalimbali?
Jawabu ni kwamba; tutashikamana na ufahamu wao katika mambo ambayo
wameafikiana, na yale waliyotofautiana sisi tutaichukua kauli iliyoungwa mkono
na maandiko sahihi, na wala haifai kuzusha kauli ya tatu zaidi ya kauli zao
mbili zilizo tofauti.
Ama mambo ambayo hayakuwepo katika wakati wao katika yale ambayo
yanafaa kutumia akili na rai, basi huo ndiyo uwanja wa kuogelea maulamaa katika
kufanya ijtihadi na kutumia rai zao kwa mujibu wa kanuni na misingi ya kielimu.
Swali la kujiuliza ni; Je hao wema waliotangulia wametofautiana
juu ya suala la kumuona Allah kwa macho huko akhera?
Jawabu ni kwamba:
Maswahaba Hawakutofautiana katika suala hili, bali wote
waliafikiana kwamba watu wema watamuona mola wao kwa macho huko akhera kama
lilivyo thibitishwa suala hilo na Qur’an na Sunna sahihi za Mtume –swalla
llaahu alayhi wasallam-.
Na hakuna mtu yeyote aliyemuona, wala atakayemuona Allah kwa macho
yake hapa duniani, na hivyo ndivyo wanavyoamini na kuitakidi Ah’lu Sunna
Wal-jamaa.
Lakini tofauti imekuja katika jambo ambalo ni nje ya maudhui yetu
hii, jambo lenyewe ni: Je bwana Mtume –swalla llaahu alayhi wasallam- alimuona
Mola wake katika usiku aliokwenda mbinguni (Miraji) ?
Jawabu ni kwamba, kuna kauli iliyopokewa kutoka kwa Ibn Abbas
-Allah amridhie- kwamba; bwana Mtume –swalla llaahu alayhi wasallam- alimuona
Mola wake katika usiku huo.
Wengi katika wanavyuoni wakayachukulia maneno yake hayo kwamba,
makusudio yake ni kuwa bwana Mtume alimuona Mola wake kwa moyo wake, na
wakategemea riwaya nyingine zilizopokewa kutoka kwa huyo huyo Ibn Abbas.
Ama kuhusu suala la kumuona Allah usingizini hili pia si katika
maudhui ya kitabu hiki.
Kabla ya kuanza kuzitaja hoja na dalili wanazozitegemea Ahli sunna
wal- Jamaa juu ya kuonekana Allah kwa macho huko akhera, kwanza napenda
kuzungumzia suala linalofungamana na elimu ya istilahi ya upokezi wa riwaya za
hadithi za bwana Mtume -swalla llaahu alayhi wasallam- na suala hili
litakuwa katika nukta zifuatazo:
i) Kwanza, tufahamu kuwa mafundisho yote ya bwana Mtume -swalla
llaahu alayhi wasallam- ni wah’yi (ufunuo) utokao kwa Allah, na Mtume -swalla
llaahu alayhi wasallam- hazungumzi kwa matashi wala matamanio ya nafsi yake.
ii) Pili, mafundisho yote ya Mtume wetu Muhammad -swalla llaahu
alayhi wasallam- yamehifadhiwa katika vitabu vya maulamaa wa Ahlu Sunna
wal-Jamaa kwa ufanisi mkubwa mno kiasi ambacho hakuna jambo lolote
linalohitajika kubainisha itikadi au hukumu ya mambo ya dini ya kiislamu
isipokuwa jambo hilo limedhibitiwa kwa
ufanisi wa hali ya juu.
iii) Tatu, katika kuhakikisha kuwa mafundisho hayo sahihi ya dini
ya kiislamu yanahifadhiwa na hayachanganyiki na upotofu wowote, maulamaa wa
Ahli Sunna wal Jamaa wameweka misingi madhubuti
juu ya usahihi wa mapokezi hayo ya riwaya za hadithi za bwana Mtume
-swalla llaahu alayhi wasallam- na ukweli wa wapokezi hao kama tulivyofundishwa
na Qur’an tukufu pale aliposema Allah:
يَا
أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا إِن جَاءكُمْ فَاسِقٌ بِنَبَأٍ فَتَبَيَّنُوا
“Enyi mlioamini ! akikujilieni mwovu (fasiki)
na habari yoyote ichunguzeni basi.”
al Hujraat (49) aya 6.
Kwa mujibu wa aya hii ni kwamba, si kila asemaye; amesema Mtume
-swalla llaahu alayhi wasallam- atakuwa msemaji huyo ni mkweli, na atakayo
yanukuu yatakuwa ni kweli maneno ya Mtume, bali ni lazima uchunguzi wa kina
ufanyike ili kujua usahihi wa habari hiyo aliyoileta na udhaifu wake.
Kwa sababu hiyo, maulamaa wa hadithi baada ya kufanya utafiti wa
kina pamoja na kutumia uzoefu wao wa muda mrefu, wakaweka misingi madhubuti
inayowahusu wapokezi wa hadithi.
Pia wakaweka kanuni maalumu kwa ajili ya udhibiti wa njia sahihi
za kukubaliwa hadithi na kurudishwa.
Na pia yakatumika maneno ya kiistalahi ambayo yanaleta maana
maalumu na hayo yamejaa kwa wingi katika vitabu vyao.
Kwa mantiki hiyo, yeyote
anayetaka kuzungumzia masuala yanayofungamana na elimu ya hadithi;
usahihi wake na udhaifu wake, hana budi kuzijua kanuni hizo na maneno hayo ya
kiistilahi.
Na kama hatafanya hivyo, basi lililobora kwake ni kunyamaza kuliko
kusema, kwa sababu hatima yake ni kupotosha watu kwa kuzisahihisha hadithi
zisizo sahihi au kuzidhoofisha hadithi zilizo sahihi na yote mawili ni balaa,
hasa ukizingatia kwamba maneno ya Mtume Muhammad -swalla llaahu alayhi
wasallam- ni sheria.
1) العدالة Uadilifu, ni lazima kila
mpokezi wa hadithi za Mtume -swalla llaahu alayhi wasallam- awe ni mtu mwenye
akili timamu,mwenye uwezo wa kupambanua mambo hata kama ni mtoto mdogo, awe
mkweli, mcha mungu na wala asiwe mwongo, wala asiwe mwenye kufanya maasia kwa
dhahiri wala asiwe na tabia mbaya zenye kuvunja heshima.
2) لضبطا تمام Hifdhi
nzuri, mpokezi awe na uwezo wa kudhibiti maneno aliyo yapokea, bila ya
kubadilisha chochote katika maana yake,au kukosea sana,au kubabaika
kulikopetuka mipaka wakati wa kusimulia mapokezi hayo.
3) السند اتصال Kuungana kwa sanadi (msururu wa wapokezi)
kwa kuwa kila mpokezi awe amepokea kutoka kwa aliye juu yake mpaka mwisho wake
(kwa huyo ambaye habari hiyo imenasibishwa kwake, ima bwana -Mtume swalla
llaahu alayhi wasallam-, au swahaba, n.k.
4) الشذوذ عدم Isiwe
habari aliyoileta mpokezi huyo ni “SHAADHUN” (ni yenye kupingana na habari
ya mpokezi mwingine aliye madhubuti au wengi zaidi kuliko yeye).
5) القادحة الخفية العلة
عدم Wala isiwe na ila (kasoro iliyojificha) kama vile Idh’tiraabu
(mgongano baina ya wapokezi n.k) au kuwa ni habari Maq’luub (yenye kugeuzwa)
Katika masharti haya tuliyoyataja, yako ambayo likikosekana moja
tu basi hadithi haitakubaliwa,kama vile:
1-Kuwa mpokezi si muadilifu,kwa kuwa ni mwongo au asherati n.k.
2-Kupatikana kasoro kama vile mgongano katika sanadi (njia) au
mgongano wa maneno katika habari hiyo, kisha ikawa imeshindikana kuziunganisha
au kuipa nguvu njia moja juu ya nyingine.
Tanbihi:
Habari inaweza kuwa na njia nyingi, na katika njia hizo
wakawepo wapokezi wasio madhubuti kwa
kuwa wanakosea kiasi, au silsila (mtiririko) wa wapokezi haukuungana, kutokana
na wingi wa njia hizo habari hiyo itapata uzito na kuhesabiwa kuwa ni sahihi,
na kwa lugha ya kitaalamu huwa wanaiita “HASANUN-LIGHAIRIHI”.
Amesema Imamu An-Nawawiy:
بل ما كان ضعفه لضعف حفظ رواية الصدوق الأمين من وجه آخر
وصار حسنا وكذا اذا كان ضعفها لارسال زال بمجيئة من وجه آخر
“Bali ile hadithi ambayo imekuwa ni dhaifu kwa
sababu ya udhaifu wa mpokezi wake ambaye ni mkweli mwaminifu utaondoka (udhaifu
huo) kwa kuja kwake kupitia njia nyingine na itakuwa ni HASAN (sahihi)
Na vile vile ukiwa udhaifu wake ni kwa sababu ya Ir’saal
(atakaposema Taabi’I amesema Mtume -swalla llaahu alayhi wasallam-) pia udhaifu
huo utaondoka kwa kuja (kupokewa) kwa njia nyingine…”.
Hivyo basi, inawezekana ukaifuatilia hadithi kisha ukazikuta takriban
njia zake zote zina udhaifu, hapo hutakiwi kuwa na pupa na kuanza kuihukumu
hadithi yote kuwa ni dhaifu, bali unatakiwa kuihukumu sanad husika tu, na useme
kwamba sanad ya hadithi hii ni dhaifu.
Kwa sababu udhaifu wa sanad moja tu, si ushahidi wa udhaifu wa
hadithi yote yenye njia nyingi.
Na kama ukitaka kuihukumu hadithi yote kwa njia zake zote
unatakiwa ufanye kazi ya kuzikusanya sanad (njia) zote kisha ndiyo uichambue
sanad moja baada ya nyingine kwa kufuata kanuni na taratibu za elimu ya hadithi
(mustalahul-hadithi).
Na kama itakubainikia kuwa njia zote zina udhaifu, basi pia
unatakiwa kuangalia sababu za udhaifu wake.
Je udhaifu wake ni mwepesi
au mzito?
Kama ni mwepesi basi hadithi hiyo kwa kuzijumuisha njia zote hizo
itakuwa ni “Hasanun-Lighayrihi” (sahihi) na itafaa kuifanya kuwa ni hoja ya
kisheria, na wala haitohesabiwa kuwa ni dhaifu.
Hili ni jambo muhimu sana katika elimu ya hadithi kulifahamu na
kulizingatia, lakini ndugu Juma kwa makusudi hakuuzingatia utaratibu huu kwenye
kitabu chake “Hoja zenye Nguvu” kwa sababu anazozijua mwenyewe, kwani yeye
ndiye aliyesema hivi:
“kitaalamu ikiwa hadithi imepokewa na wapokezi wengine kabisa,
lakini hadithi ni ile ile, basi huambiwa kuwa hadithi hiyo ina shahidi.”
Mwisho wa kunukuu.
Tazama “Hoja zenye Nguvu” ukurasa 70.
Lakini huko mbele
-Inshaallah- utazigumdua sababu zilizomfanya ndugu Juma aupuuze utaratibu huu.
Kama ilivyokuwa kawaida ya watu wanaofuata matamanio ya nafsi zao
katika mambo ya dini kama vile: Mayahudi, Manasara, Washirikina na kadhalika
watu wa bid’a, huwa hawaachi kuwasema vibaya wale walioshikamana na njia sahihi
na kuwataja kwa kebehi na uovu, tena mpaka kufikia kuwazulia uwongo.
Huu ndiyo mwenendo wao na sera yao tangu zamani, jambo la
kusikitisha zaidi ni kuwa hata ndugu Juma naye ameifuata njia hiyo ovu dhidi ya
Ahli Sunna wal-Jama’a.
Amekianza kitabu chake kwa mashambulizi yasiyo na ukweli dhidi ya
Ah’li Sunna na maulamaa wao, tena bila ya kuwa na insafu wala uadilifu, bali
chuki binafsi na uadui ndivyo
vilivyomuongoza na kumsababishia kuacha kuyahakiki mambo kwa njia za
kielimu, kwa mfano:
1-Hakuna kitu kingine zaidi ya chuki kilichomfanya awaite Ah’lu
Sunna kwa jina la Mawahabi, au Hashawiya, au Mujasima.
2- Hakuna kitu kingine zaidi ya chuki dhidi ya Ah’li Sunna
kilichomfanya awatie kasoro kwa mambo ambayo hayakuthibiti kuwa ndiyo itikadi
yao, kama suala la kuwa Allah ana sura
ya kijana, au ana viatu vya dhahabu na mengineyo.
3-Hakuna jambo jingine zaidi ya chuki na uadui lililompelekea
kuwatuhumu baadhi ya wanavyuoni wa Ah’li Sunna kama vile Ibn Taymiyyah na Ibn
Al-Qayyim kwa sababu ya misimamo yao na
kuwaita kuwa ni wanavyuoni wa kiwahabi! Maimamu wa Hashawiya! Mujasima! Na hali
yakuwa hakuna tofauti yoyote baina ya misimamo yao hiyo na misimamo ya Maimamu
wakubwa wa Ahli Sunna kama vile: Abu Hanifa, Imamu Malik, Imamu Shaafiy, Imamu
Ah’mad Ibn Hanbal, Imamu Bukhari, Imamu Muslimu, Imamu Abu Daud, Imamu
Tirmidhiy, Imamu Abul-Hasan Al-Ash’ariy, Imamu Abdul-Qadir Jaylaaniy !!!
Kwamfano katika suala la sifa za Allah: kuwa Allah ana mikono
miwili, ana macho mawili, ana uso, anacheka, ana mguu na nyinginezo katika sifa
za Allah za ukamilifu ambazo amejisifia nazo au amesifiwa na Mtume wake –swalla
llaahu alayhi wasallam- utawakuta maimamu hawa wakubwa wanazithibitisha sifa
hizo kama zilivyopokewa, na hivyo ndivyo anavyofanya Ibn Taymiyya na Ibn
al-Qayyim.
Lakini Juma kwa sababu ya chuki zake dhidi ya Ibn Taymiyya na Ibn
al-Qayyim akalizungumzia suala hilo kwa
sura ambayo msomaji anaweza kudhania kuwa Ibn Taymiyya na Ibn al-Qayyim wana
itikadi ambayo si ya kiislamu na wala hakuna muislamu yeyote mwenye itikadi
hiyo ila Ibn Taymiyya na mwanafunzi wake Ibnul-Qayyim.
Kwa mfano amesema Juma:
“Na itikadi hizi ambazo nitakutajia sasa hivi (Inshala) zimo hasa
katika madhehebu ya kiwahabi na wao
wamezirithi kutoka kwa maimamu wa madhehebu za Al-hashawiya Al-mujasima kama
Ibn Taymiyya Ibn Qayyim Al-jawziya na wengineo”.Mwisho wa kunukuu. Tazama
kitabu chake “Hoja zenye Nguvu” ukurasa wa 23.
Sisi tunasema kwamba msimamo wa Sheikhul-Islami Ibn Taymiyya na
mwanafunzi wake Ibn al-Qayyim katika mas’ala ya sifa za Allah hauna tofauti na
msimamo wa Qur’an na Sunna, bali ndiyo msimamo wa maswahaba na wanafunzi wao,
na ndiyo msimamo wa maulamaa wakubwa waliokuja baada ya wanafunzi wa maswahaba,
kama vile: Abu Hanifa, Malik, Shaafiy, Ah’mad bin Hanbal, Abul-Hasan
al-Ash’ariy na wengineo katika maimamu wakubwa, kwa hiyo kumuita Ibn Taymiyya
na mwanafunzi wake Ibn al-Qayyim kuwa ni maimamu wa Hashawiya Mujasima ni
matusi dhidi maimamu hao wote waliotangulia kama tutakavyoona hapo mbeleni
Inshaallah.
Kisha akasema ndugu Juma katika ukurasa wa 23:
“Falsafa ya Ibn Taymiyya kuhusu maumbile ni kuwa ulimwengu una
sifa ya kutangulia kama alivyosema haya katika kitabu chake NAQDU MARATIBIL
AL-IJMAA.
Nini maana ya sifa ya kutangulia? Sisi waislamu tunaamini kuwa
Mwenyezi Mungu tu ndiye mwenye sifa ya kutangulia, yaani kabla yake hapakuwa na
kitu chochote: kila kilichopo tunapopajua na tusipopajua, tunapopaona na
tusipopaona basi ni kiumbe cha Mwenyezi Mungu.
Lakini itikadi ya Ibn Taymiyya wanaemwita Sheikh wa waislamu ni
kuwa Mwenyezi Mungu alikuwa navyo vitu ambavyo kutokana na hivyo ndio kaanzia
kuumba maumbile yote.
Sasa suala ni kuwa hivi vitu vya nani? Je haoni yeye huyu Ibn
Taymiyya kuwa falsafa hii inapelekea kurudi kwenye itikadi ya kuwepo kwa
Mwenyezi Mungu zaidi ya mmoja?
Huyu ndiye ambaye Mawahabi wanamwita Sheikh Al-islam……”.
Mwisho wa kunukuu.
Maneno yote haya ya ndugu Juma ni maneno ya uwongo yaliyojaa chuki
dhidi ya mwanachuoni huyu mkubwa wa kiislamu, si kweli kwamba itikadi ya Ibn
Taymiyya ni kuwa ulimwengu una sifa ya kutangulia.
Na wala maneno ya Ibn Taymiyya katika suala hili hayapelekei
kwenye dhana ya kuwepo Mungu zaidi ya mmoja, lakini huo ni ufahamu mbaya wa
ndugu yetu Juma uliosababishwa na chuki binafsi dhidi ya maulamaa wa Ah’li
Sunna hasa Ibn Taymiyya.
Katika kubatilisha madai haya ya uwongo ya Juma, hebu tukunukulie
kidogo ndugu msomaji maneno ya Ibn
taymiyya yanayohusu masuala haya ya maumbile, amesema Ibn Taymiyya:
كل ما سوى الرب حادث كائن بعد أن لم يكن وهو - سبحانه - المختص
بالقدم والأزلية، فليس في مغعولاته قديم وإن قدر أنه لم يزل فاعلا وليس معه شيء
قديم بقدمه، بل ليس في المفعولات قديم ألبته، بل لا قديم إلا هو - سبحانه - وهو
وحده الخالق لكل ما سواه وكل ما سواه مخلوق كما قال – سبحانه ((الله خالق كل شيء))
الزمر26
“KILA KISICHOKUWA MOLA NI CHENYE KUZUKA KIMEPATIKANA BAADA YA
KUTOKUWEPO, ay eye (Allah) –Sub’hanah- ndiye mwenye kuhusishwa na kutangulia na
azal, hakuna kitu katika viumbe vyake kilichokuwa ni chenye kutangulia, hata
kama ikikadiriwa kuwa yeye (Allah) hakuacha kuwa ni mwenye kutenda, (lakini)
hakuna kitu kilichotangulia kwa kutangulia kwake, bali hakuna kabisa katika
viumbe (vyake ambavyo ) ni vyenye kutangulia, BALI HAKUNA KILICHOTANGULIA ILA
YEYE (ALLAH) – Sub’haanah-.
Na yeye pekeyake ndiye
mwenye kukiumba kila kisichokuwa yeye, kila kisichokuwa yeye ni chenye kuumbwa
kama alivyosema –Sub’ahaanah-:
((Allah ni muumba wa kila kitu))”. Surat Zumar aya ya 26.
Tazama kitabu Dar’u Ta’arudh juzuu ya 8 ukurasa wa 272 cha Ibn
Taymiyya.
Ndugu msomaji, je kwa maneno haya umefahamu kwamba Ibn Taymiyya
ana itikadi ya kuwa ulimwengu una sifa ya kutangulia kama anavyodai Juma?
Au umefahamu kwamba Ibn Taymiyya anasema kuwa kila kisichokuwa Allah
ni chenye kuzuka na kimepatikana baada ya kutokuwepo?
Je kwa maneno haya ya Ibn
Taymiyya umefahamu kwamba ana itikadi ya kuwepo Mungu zaidi ya mmoja kama
anavyodai ndugu Juma kuwa sheikhul islam Ibn Taymiyya ana itikadi hiyo?
Au umefahamu kwamba ndugu Juma si mkweli?
Hebu yatupie jicho maneno mengine ya Sheikul-Islam Ibn Taymiyya
tuone anavyosema:
"كل
واحد من أفعاله لا بد أن يكون مسبوقا بالفاعل وأن يكون مسبوقا بالعدم، ويمنتع كون
الفعل المعين مع الفاعل أزلا وأبدا .. فافاعل يتقدم على كل فعل من أفعاله وذلك
يوجب أن كل ما سواه محدث مخلوق"
مجموع الفتاوي 18/227-228
“Kila kitu katika vitendo
vyake hakuna budi kuwa ni chenye kutanguliwa na mwenye kutenda na ni chenye
KUTANGULIWA NA KUTOKUWEPO. NA HAIWEZEKANI KUWA KITENDO FULANI KILIKUWEPO PAMOJA
NA MTENDAJI TANGU MWANZO NA AZAL…..
Mwenye kutenda (ambaye ni Allah) anakitangulia kila kitendo katika
vitendo vyake na hilo linawajibisha kuwa KILA KISICHOKUWA YEYE (ALLAH) NI
CHENYE KUZUKA NA NI CHENYE KUUMBWA”.
Tazama Maj’muul-Fatawa juzuu ya 18 ukurasa wa 227-228.
Bila shaka maneno haya yako wazi katika kuufichua uwongo wa ndugu
Juma na wala hayahitajii maelezo.
Kisha ndugu Juma akaleta tuhuma nyingine dhidi ya Ibn Taymiyya na
mwanafunzi wake (Ibn al-qayyim) kuhusiana na suala la sifa za Allah akasema:
“Anasema Ibn Al-qayyim katika kitabu chake “HADI AL-ARWAAH”
ukurasa wa 13 akitaja sifa za Mwenyezi Mungu anasema:
“na kwamba yeye (Mwenyezi Mungu) ana mikono miwili bila ya mfano
na ana macho mawili na ana uso”. Naye Ibn Al-qayyim anasema kuwa kayanukuu
maneno haya kutoka kwa Abul-hasan Al-ash’ari….
Lakini kudai kwamba maneno haya ni maneno ya Al-imamu Al-ash’ari
ni kitu cha kutazama zaidi kwani wafuasi wa Al-imamu Al-ash’ari nao ni masuni
kama mashafi hawakubaliani na haya”.
Mwisho wa kunukuu.
Tazama ukurasa wa 24-25 katika kitabu chake “Hoja zenye Nguvu”.
Majibu yetu dhidi ya maneno haya ya ndugu Juma yatakuwa katika
nukta kuu tatu:
Nukta ya kwanza:
Suala kuwa Allah ana Mikono miwili bila ya mfano.
Ana Macho mawili bila ya mfano.
Ana Uso bila ya kuwa na mfano.
Hii si itikadi ya Ibn Taymiyya na mwanafunzi wake peke yao, hiyo
ndiyo itikadi iliyo elezewa na Qur’an na Sunna na ndiyo itikadi ya maswahaba na
wanafunzi wao na ndiyo itikadi ya maimamu wakubwa wa kiislamu.
Amesema Imamu Shaafiy –Allah amrehemu-:
"لله تبارك وتعالى أسماء وصفات جاء بها كتابه وأخبر بها نبيه صلى
الله عليه وسلم أمته.......أتانا أنه سميع وأن له يدين بقوله ((بل يداه مبسوطتان)).
وقال رحمه الله :
"........وأن له وجهاً بقوله ((كل شيئ هالك إلاّ وجهه)).
“Allah –Tabaaraka Wata’alaah- ana majina na sifa ambazo zimetajwa
na kitabu chake na amezielezea Mtume wake –swalla llaahu alayhi wasallam- kwa
uma wake…… zimetufikia (habari) kuwa yeye ni mwenye kusikia na ana mikono
miwili kwa kauli yake (Allah) : “Bali mikono yake (Mwenyezi Mungu) iwazi”.
Na akasema tena (Imamu Shaafiy) –Allah amrehemu-:
“…..Na yeye (Allah) ana Uso kwa sababu ya kauli yake (Allah):
((Kila kitu ni chenye kuangamia isipokuwa Uso wake))”.
Tazama kitabu “Twabaaqatul-Hanabila” juzuu ya 1 ukurasa wa 283-284
cha Imamu Ibn Abi Ya’ala.
Pia tazama kitabu “Man’haju Imami Shaafiy fi Ith’batil-Aqidah”
ukurasa wa 370-378. cha Dkt. Muhammad al-Aqil.
قَالَ أَبُو عِيسَى رحمه الله:
وَقَدْ قَالَ غَيْرُ وَاحِدٍ
مِنْ أَهْلِ الْعِلْمِ فِي هَذَا الْحَدِيثِ وَمَا يُشْبِهُ هَذَا مِنْ الرِّوَايَاتِ
مِنْ الصِّفَاتِ وَنُزُولِ الرَّبِّ تَبَارَكَ وَتَعَالَى كُلَّ لَيْلَةٍ إِلَى السَّمَاءِ
الدُّنْيَا قَالُوا قَدْ تَثْبُتُ الرِّوَايَاتُ فِي هَذَا وَيُؤْمَنُ بِهَا وَلَا
يُتَوَهَّمُ وَلَا يُقَالُ كَيْفَ هَكَذَا رُوِيَ عَنْ مَالِكٍ وَسُفْيَانَ بْنِ عُيَيْنَةَ
وَعَبْدِ اللَّهِ بْنِ الْمُبَارَكِ أَنَّهُمْ قَالُوا فِي هَذِهِ الْأَحَادِيثِ أَمِرُّوهَا
بِلَا كَيْفٍ وَهَكَذَا قَوْلُ أَهْلِ الْعِلْمِ مِنْ أَهْلِ السُّنَّةِ وَالْجَمَاعَةِ.
وَأَمَّا الْجَهْمِيَّةُ فَأَنْكَرَتْ
هَذِهِ الرِّوَايَاتِ وَقَالُوا هَذَا تَشْبِيهٌ وَقَدْ ذَكَرَ اللَّهُ عَزَّ وَجَلَّ
فِي غَيْرِ مَوْضِعٍ مِنْ كِتَابهِ : الْيَدَ وَالسَّمْعَ وَالْبَصَرَ فَتَأَوَّلَتْ
الْجَهْمِيَّةُ هَذِهِ الْآيَاتِ فَفَسَّرُوهَا عَلَى غَيْرِ مَا فَسَّرَ أَهْلُ الْعِلْمِ
وَقَالُوا إِنَّ اللَّهَ لَمْ يَخْلُقْ آدَمَ بِيَدِهِ وَقَالُوا إِنَّ مَعْنَى الْيَدِ
هَاهُنَا الْقُوَّةُ.
و قَالَ إِسْحَقُ بْنُ إِبْرَاهِيمَ
إِنَّمَا يَكُونُ التَّشْبِيهُ إِذَا قَالَ يَدٌ كَيَدٍ أَوْ مِثْلُ يَدٍ
......".
انظر جامع الترمذي 1/ 166 رقم الحديث 772.
Amesema Imamu Abu Issa Al-Tirmidhiy –Allah amrehemu- alipoitaja hadithi namba
772:
“Na wamesema wengi katika wanavyuoni kuhusu hadithi hii na
inayofanana na hii katika mambo ya sifa (za Allah) na kushuka Mola katika
mbingu (iliyokaribu na) dunia, wamesema: zimethibiti riwaya nyingi kuhusu suala
hili, na sisi tunaliamini na wala hatusemi kwa dhana na wala hatusemi vipi? Na
hivi ndivyo ilivyopokelewa kutoka kwa Malik,Ibn Uyaina, na Abdullahi bin
Mubarak kuwa wamesema kuhusu hadithi hizi: zipitisheni bila ya kuzipa namna.
Na hii ndiyo kauli ya wanavyuoni wa Ah’li Sunna wal-Jamaa. Ama
Jah’miya wao wamezipinga riwaya hizi na wakasema: huko ni kumfananisha Allah
(na viumbe).
Na hali yakuwa ametaja Allah katika kitabu chake katika sehemu
nyingi: (ametaja kuwa ana) Mkono, Usikivu, Uoni.
Lakini Jah’miya wakazitafsiri aya hizi tofauti na wanavyuoni,
wakasema: Allah hakumuumba Adam kwa mkono wake, na (wakasema kuwa) maana ya
mkono hapa ni nguvu.
Na amesema Is’haq bin Ibrahim: inakuwa ni kumfananisha Allah (na
viumbe) atakaposema: Mkono (wa Allah) ni kama mkono au mfano wa mkono (wa
kiumbe).
Tazama kitabu chake Jamiul-Tir’midhiy/Sunan Tir’midhiy hadithi
namba 772.
قال الإمام أبو جعفر محمد بن جرير الطبري [224-310]:
"القول فيما أدرك علمه من الصفات خبراً, وذلك نحو إخباره عز وجل
أنه سميع بصير , وأن له يدين بقوله: ((بل يداه مبسوطتان))
وأن له وجهاً بقوله: ((ويبقى وجه ربك)) وأن له قدماً بقول النبي صلى الله
عليه وسلم: ((حتى يضع الرب فيها قدمه)) وأنه يضحك بقوله: ((لقي الله وهو يضحك إليه))......".
مختصر العلو للعلي الغفار ص 224.
Amesema Imamu Abu Ja’far Muhammad bin Jarir al-Tabariy aliyefariki
mwaka [310 H]:
“Kauli katika yale yaliyofahamika ujuzi wake katika sifa (za
Allah) kwa habari, ni mfano wa kuelezea kwake (Allah) -Azza wajalla- kuwa yeye
(Allah) ni mwenye kusikia mwenye kuona, na kwamba yeye (Allah) ana mikono
miwili aliposema:
“Bali mikono yake (Mwenyezi Mungu) iwazi”.
Na kwamba yeye (Allah) ana Uso pale aliposema:
“Na utabakia Uso wa Mola wako”
Na kwamba yeye Allah ana Mguu, kwa kauli ya Mtume –swalla llaahu
alayhi wasallam-: “Mpaka atakapo weka Mola ndani yake Mguu wake”
Na kwamba yeye (Allah) anacheka kwa kauli yake Mtume:
“Na atakutana na Allah na hali ya kuwa anamchekea”.
Tazama kitabu Mukh’tasarul-Uluwi ukurasa wa 224.
قال الإمام أبو بكر الخطيب البغدادي
[392-463]:
"فإذا قلنا : يد , وسمع, وبصر ,فإنما هو إثبات صفات أثبتها الله
لنفسه , ولا نقول : إن معنى اليد القدرة....".
انظر كتاب " الصفات" للخطيب 16/ 43-44. بواسطة مختصر العلو
ص 272.
Amesema Imamu Abu Bakar al-Khatib al-Bagh’dadiy aliyefariki mwaka
[463 H]:
“Sisi tunaposema: (kuwa Allah ana) Mkono, Usikivu,na Uoni ni
kuthibitisha sifa za Allah kama alivyo jithibitishia mwenyewe, na wala hatusemi
maana ya mkono ni uwezo…..”.
Tazama Mukh’tasarul-Uluwi ukurasa 272.
Hizi ni baadhi ya kauli za maulamaa wa Ah’li Sunna ambao
wamemtangulia Ibn Taymiyya kwa kar’ne nyingi.
Wao wanasema kuwa Allah ana Macho, Mikono miwili, Mguu, n.k. na
hiyo ndiyo itikadi ya maimamu wote wanne: Abu Hanifa, Malik, Shaafiy, na Ah’mad
bin Habal, sasa kwanini ndugu Juma ainasibishe itikadi hii sahihi na Ibn
Taymiyya na mwanafunzi wake Ibn al-Qayyim peke yao?
Kwani kuna kioja gani kwa mtu kumsifia Allah kwa sifa ambazo
amejisifia nazo mwenyewe katika Qur’an na amesifiwa na Mtume wake –swalla
llaahu alayhi wasallam-?
Je wakumshangaa ni yule aliyehalifu hilo au yule aliyetii? Ama
kweli walimwengu wana mambo !
Amesema tena Juma:
“Lakini kudai kwamba haya ni maneno ya Al-imamu Al-ash’ari ni kitu
cha kutazamwa zaidi kwani wafuasi wa Al-imamu Al-ash’ari nao ni masuni kama
mashafi hawakubaliani na haya”.
Kwa maneno haya ya ndugu Juma anatuwekea wazi zaidi namna
asivyokuwa mtafiti mzuri wa mambo na huwa hukumu zake ni za kubuni.
Tangu lini mtu akahukumiwa kwa matendo ya watu wengine?
Kuwa wafuasi wa Abul-Hasan al-Ash’ari wako kinyume na itikadi
yake, basi hiyo ndiyo hoja yakwamba hakusema maneno hayo?
Kwanini usiwashangae watu
wanaodai kuwa ni wafuasi wa Imamu Shaafiy katika mambo ya twahara na
swala lakini katika mambo la itikadi wamemfuata Abul-Hasan na wako kinyume na
Imamu wao?
Kwanini wamemkwepa Imamu Shaafiy aliyefariki mwaka 205 H na
kumfuata Abul-Hasan al-Ash’ariy aliyezaliwa mwaka 260 H na kufariki mwaka 324
H?
Abul-Hasan yeye amezaliwa
nusu karne baada ya Imamu Shaafiy kufariki, je Imamu Shaafiy hakuwa na
itikadi yoyote? Na je yeye alikuwa akimfuata nani?
Abul-Hasan al-Ash’ariy jina lake kamili ni: Aliy bin Ismail bin
Is’haq bin Salim bin Ismail bin Abdillahi bin Musa bin Abi Bur’da bin Abi Musa
al-Ash’ariy, amezaliwa mwaka 260 H.
Mwanzoni mwa uhai wake alikuwa na itikadi ya Mu’tazila kwa muda wa
miaka 40 na sababu yakuwa na itikadi hiyo ni sheikh wake aliyesoma kwake ambaye
ni baba yake wa kufikia (mume wa mamake) jina lake ni Abu Aliy al-Jubbai, yeye
alikuwa na itikadi potofu za Mu’tazila (itikadi za kupinga sifa za Allah) na hiyo ni itikadi iliyo anzishwa na Waasil
bin Atwaa.
Kisha Imamu Abul-Hasan akaiwacha itikadi hiyo ya Mu’tazila na
kuifuata itikadi ya Ibn Kullaabi kwa muda, na miongoni mwa itikadi za Ibn
Kullaabi ni kumthibitishia Allah sifa saba tu, sifa ya: Uhai, Elimu, Uwezo,
Utashi, Usikivu, Uoni, na kusema.
Na ama sifa nyingine zote kama vile Uso, Mikono miwili, Mguu na
mfano wa hizo alizipa tafsiri potofu.
Alijifungia ndani kwake kwa muda wa siku kumi na tano kisha
akatoka akaelekea msikiti mkuu wa Bas’ra akapanda juu ya mimbari baada ya swala
ya Ijumaa kisha akawaambia watu, nilijificha kwenu kwa muda kwa sababu
nimezitazama dalili lakini zikawa sawa kwangu na haikunipambanukia haki na
batili, nikamwomba Allah aniongoze ndipo akaniongoza kwenye haya niliyo yaweka
humu kwenye vitabu hivi, na nimejivua na yale yote niliyokuwa nikiyaitakidi
kama ninavyoivua kanzu yangu hii, kisha akaivua kanzu yake na akaitupa kwa
watu, kisha akavitoa vitabu vyake akawapa watu.
Na miongoni mwa vitabu vyake ni “al-Ibana an Usuli-Diyana” na
ndani ya kitabu hicho amesema wazi wazi kwamba msimamo wake huo ndiyo msimamo
wa Salaf Swalih msimamo wa maimamu wakubwa kama vile: Malik, Shaafiy, Ah’mad
bin Hanbal na wengineo na kuwalingania watu washikamane nao.
Na wanavyuoni walio lithibitisha suala hili la kutubia kwake,
kuacha misimamo hiyo potofu na kushikamana na msimamo wa Salaf Swalih na
kuandika kitabu “al-Ibana”, ni hawa wafuatao:
1- Abul-Qasim Aliy bin al-Hasan bin Hibatu-llaahi
Ibn Asaakir aliyefariki mwaka 571 H, katika kitabu chake “al-Tabyiin” ukurasa
wa 28.
2- Imamu al-Baihaqiy al-Shaafiy aliyefariki mwaka
458 katika kitabu chake al-I’tikad ukurasa wa 31na 32.
3- Imamu
al-Dhah’biy aliyefariki mwaka 748 H katika kitabu chake “al-Uluwu” ukurasa wa
160.
4- Imamu Ibn al-Imadi aliyefariki mwaka 1098 H
katika kitabu chake “Shadharaatul-Dha’hbi” ukurasa wa 303.
5- Imamu Abul-Hasan al-Sayyid Murtaza al-Zabidiy
katika kitabu chake “It’hafu Saadatil- Mutaqina” juzuu ya 2 ukurasa 2.
6- Imamu Ibn Kathir al-Qurashiy al-Shaafiy
aliyefariki mwaka 774H, katika kitabu chake “al-Bidayatu wal-Nihayah” juzuu ya
11 ukurasa wa 187.
7- Imamu Taaju-Din Abu Nasri Abdul-wahab bin
Taqiyu-Din al-Subkiy al-Shaafiy aliyefariki mwaka 771 H, katika kitabu chake
“Twabaqaatu al-Shaafi’iya al-Kubraa” juzuu ya 2 ukurasa 246.
Na wengi katika maulama ambao hatukuwataja, wote hao wamekiri na
kuthibitisha katika vitabu vyao tulivyo vitaja kuwa Abul-Hasan aliziwacha
itikadi zote hizo potofu na kushikamana na itikadi sahihi ya Salaf Swalih na
akatunga kitabu “al-Ibana”.
Hebu tunukuu baadhi ya maneno yake kutoka kwenye kitabu hicho ili
tuone je anayoyasema yeye yanatofauti yoyote na yale anayoyasema Ibn Taymiyya
na mwanafuzi wake?Au chuki binafsi inafanya kazi yake?
Anasema Abul-Hasan baada ya kuzitaja itikadi potofu za watu wa
bid’a na kuzipinga:
"الباب الثاني
فى إبانة قول أهل الحق والسنة
فإن قال لنا قائل : قد أنكرتم قولَ المعتزلة والقدرية والجهمية والحرورية
والرافضة والمرجئة , فعرِّفونا قولكم الذي به تقولون وديانتكم التي بها تدينون.
قيل له: قولنا الذي نقول به , وديانتنا التي ندين بها: التمسك بكتاب ربنا
عزّ وجل , وبسنَّة نبيِّنا صلى الله عليه وسلم وما روي عن السادة الصحابة والتابعين
وأئمة الحديث , ونحن بذلك معتصمون, وبما كان يقول به أبوعبدالله أحمد بن محمد بن حنبل
–نضَّر الله وجهه وفع درحته وأجزل مثوبته- قائلون.....
وجملة قولنا.....وأن الله استوى
على عرشه كما قال: ((الرحمن على العرش استوى)) طه 5.
وأن له سبحانه وجهاً بلا كيف كما قال: ((ويبقى وجه ربك ذوالجلال والإكرام))
الرحمن 27.
وأن له سبحانه يدين بلا كيف كما قال سبحانه: ((خلقتُ بِيَدَيَّ)) ص75.وكماقال:
((بل يداه مبسوطتان)) المائدة:64.
وأن له عيناً بلا كيف كما قال سبحانه : ((تجري بأعيننا)) القمر
14...".
“MLANGO WA PILI
Katika kuibainisha kauli ya watu wa haki na sunna Ikiwa atasema
mwenye kusema : mmeipinga kauli ya Mu’tazila, na kauli ya Qadariya (wenye kupinga
Qadari) na kauli ya Jah’miya na kauli ya Haruuriya (miongoni mwao ni maibadhi)
na kauli ya Raafidha (Shia) na kauli ya Mur’jia (wenye kuitakidi kuwa watu wote
ni sawa katika imani) basi hebu tuelezeeni kauli yenu na msimamo wenu ambao
mnaufuata.
Ataambiwa: Kauli yetu tunayoisema na msimamo wetu tunaoufuata ni
kushikamana na kitabu cha Mola wetu na Sunna za Mtume wetu –swalla llaahu
alayhi wasallam- na yale yaliyopokelewa kutoka kwa mabwana wakubwa katika
maswahaba na Taabi’ina (wanafunzi wa maswahaba) na maimamu wa hadithi, sisi ni
wenye kushikamana na hilo na yale anayoyasema Abu Abdillahi Ah’mad bin Muhammad
bin Hanbal –Allah autie nuru Uso wake na ainyanyue daraja yake na ampe thawabu
kwa wingi- sisi ni wenye kuyasema…..
Na jumla ya kauli ni kuwa sisi tunakiri kwamba ….Allah yuko juu ya
Arshi yake kama alivyosema: ((Allah mwingi wa reh’ma yuko juu ya Ar’shi)) Twaha
aya ya 5.
Na kwamba yeye Allah ana uso bila kuwa na namna kama alivyosema:
((Na utabakia Uso wa Mola wako wenye utukufu)).
Al-Rah’man aya ya 27.
Na kwamba yeye ana mikono miwili bila ya kuwa na namna kama
alivyosema Allah: ((…Niliye muumba kwa mikono yangu miwili?)) surat Saad (38)
aya ya 75.
Na akasema ((Bali mikono yake (Allah) iwazi)) al-Maida aya ya 64.
Na kwamba yeye ana jicho bila kuwa na namna kama alivyosema:
((Linakwenda(jahazi la Nuh) kwa uwangalizi wa macho yetu)) al-Qamar aya ya 14.”
Tazama katika kitabu chake “al-Ibana” kuanzia ukurasa wa 38-44,
chapa ya Daarul-Bayaan Damascus - Syria ya mwaka 2004.
Bila shaka ndugu msomaji kwa mujibu wa nukuu hizi utakuwa
umefahamu kwamba itikadi anayoielezea Ibn Taymiyya ndiyo itikadi halisi ya Ahli
Sunna, itikadi ya maimamu wakubwa waliotangulia ambayo ndiyo itikadi
iliyoelezwa na kitabu kitukufu Qur’an na Sunna sahihi za Mtume Muhammad –swalla
llaahu alayhi wasallam-.
Na hiyo ndiyo itikadi ya Imamu Abul-Hasan al-Ash’ariy, kama
alivyojielezea mwenyewe katika kitabu chake, kwa hiyo maneno ya ndugu Juma
yanayotilia shaka maneno ya Ibn al-Qayyim na kudai kuwa ni maneno ya kutazamwa,
madai hayo hayana uzito wowote wa kielimu.
Ndugu Juma hakuchoka kusema uwongo na kuwatuhumu maulamaa wa Ah’li
Sunna, bali akaamua kumzushia Imamu Ibn al-Qayyim tuhuma nyingine nzito,
amesema ndugu Juma:
“katika kuifasiri aya ya Mwenyezi Mungu inayosema kwamba:
"نسوا الله فنسيهم"
“Wamemsahau Mwenyezi Mungu na yeye akawasahau.”
Sura ya 9 aya 67.
Kaifasiri aya hii kuwa ni kusahau kweli kweli akasema: “Zingatia
kauli yake Mwenyezi Mungu (katika aya hio na ilio mfano wa hio) namna
alivyofanya uadilifu kamili kwao akawasahau kama walivyo msahau !!!”.
Mwisho wa kunukuu.
Tazama ukurasa wa 25 wa kitabu chake.
Miongoni mwa mambo mabaya kabisa katika uislamu ni kumzulia mtu
jambo asilolifanya au asilosema, na kama mtu mwenyewe ni mwanachuoni basi ubaya
unakuwa maradufu.
Vitendo vya ndugu Juma anavyovifanya dhidi ya maulamaa ni hiyana
na ni dhulma ambayo inamporomoshea mtu uadilifu wake na kumfanya asikubaliwe
maneno yake.
Je ni kweli Ibn al-Qayyim anasema kuwa Allah anasahau kweli kweli?
Au Juma amekusudia kusema uwongo ili kupotosha?
Jawabu ni kwamba, si kweli kuwa Ibn al-Qayyim anaitikadi kwamba
Allah anasahau, bali itikadi yake ni itikadi ya Qur’an na Sunna kuwa Allah
hasahau, lakini ndugu yetu Juma alikusudia kupotosha kama ilivyo kawaida ya
watu wa batili.
Na ushahidi wa kuwa Ibn al-Qayyim hana itikadi hiyo chafu ni pale
alipokuwa akiitafsiri kauli ya Allah isemayo:
" ((علمها عند الله)) طه 52 :
أي أعمال تلك القرون وكفرهم وشركهم معلوم لربي قد أحصاه وحفظه وأودعه
فى كتاب فيجازيهم عليه يوم القيامة, ولم يودعه فى كتاب خشية النسيان والضلال فإنه سبحانه
لا يضل ولا ينسى "!!!!!
انظر كتابه شفاء العليل ص 141 مطبعة دار الكتاب العربي بيروت – لبنان
الطبعة الأولى لعام 1424هـ
“[Ujuzi wake (karne hizo) uko kwa Allah] surat Twaha aya ya 52:
Makusudio ni kwamba matendo ya karne hizo (zilizopita) kufru zao
na shirki zao zote zinajulika kwa Mola wangu amezidhibiti, amezihifadhi na
ameziweka katika kitabu na atawalipa siku ya Qiyama, na hakuziweka katika
kitabu kwa sababu ya kuogopea kusahau na kupotea
KWA SABABU YEYE –SUB’HANAH- HAPOTEI WALA HASAHAU!!!!!
Tazama kitabu chake “Shifaul-Alili” ukurasa wa 141 chapa ya
Darul-kitabil- Arabi Beirut – Lebanon,chapa ya kwanza mwaka 2004.
Swali, kwa mujibu wa maneno haya, je ndugu msomaji umefahamu
kwamba Ibn al-Qayyim itikadi yake ni kuwa Allah anasahau au hasahau?
Je umegundua kwamba Juma al-Mazrui anaendelea kusema uwongo?
Pengine Juma mwenyewe au mtu mwengine katika wapenzi wake anaweza
kusema: lakini maneno hayo siyo aliyo yanukuu kutoka kwa Ibn al-qayyim bali
yeye amenukuu maneno mengine kwenye kitabu kingine ambayo Ibn al-Qayyim
anaelezea kwa uwazi kuwa Allah anasahau kweli kweli!
Sababu ya kunukuu kauli hiyo ya Imamu Ibn al-Qayyim ni kutaka
kukuthibitishia ndugu msomaji kwamba Ibn al-Qayyim hana itikadi hiyo ya
kikafiri ambayo ndugu Juma amembabatiza nayo.
Kisha ndiyo tutupie macho hayo maneno ya Ibn al-Qayyim aliyo yanukuu
Juma, na tutakapoyatazama tunakuta kwamba Ibn al-Qayyim hakutoka nje ya ibara
ya Qur’an na Sunna, na wala maneno yake hayamaanishi kuwa Allah anasahau kweli
kweli. Na kama maneno hayo yanaleta maana hiyo, basi hata Qur’an yenyewe na
Sunna zitakuwa zina maanisha hivyo.
Ibn al-Qayyim katika maneno yake ametumia ibara isemayo:
"بأن نسيهم كما نسوه"
“Bi an-nasiyahum kamaa nasuuhu”
Maana yake Kiswahili ni “kwa kuwa amewaacha (amewapuuza) wao kama
walivyo msahau (walivyompuuza)”
Na ibara hiyo hiyo ndiyo iliyotumika katika Qur’an amesema Allah:
"نسوا الله فنسيهم"
“Wamemsahau Allah naye akawaacha (akawapuuza) ”.
Na haya hapa ni maneno ya Ibn al-Qayyim kwa ukamilifu :
"وتأمل قوله الحق ((نسوا الله فنسيهم )) وقوله : ((ولا تكونوا كالذين
نسوا الله فأنساهم أنفسهم)) كيف عدل فيهم كل
العدل بأن نسيهم كما نسوه".
مختصر الصواعق المرسلة 1/210
“Izingatie kauli yake al-Haq (Allah) “Wamemsahau Allah na yeye
akawaacha wao (katika adhabu), na kauli yake “Wala msiwe kama wale ambao
wamemsahau Allah na yeye akawasahaulisha nafsi zao” (zingatia) namna alivyo
wafanyia wao uadilifu kwa kuwa walimsahau na yeye akawaacha (katika adhabu).”
Tazama kitabu “Mukh’tasaru Sawaaiqil-Mur’slah” juzuu ya 1 ukurasa
wa 210.
Hapa nataka kuelezea kitu kimoja muhimu kwa faida ya wasomaji:
Tulipo litafsiri neno “Nasiya hum” kwa maana ya kuacha, lengo si
kutaka kuleta taawili na kupotosha.
Bali neno hili la kiarabu “Nasiya” ambalo limetasuliwa
(limenyambuliwa) kutoka kwenye asili ya neno “Al-Nis’yaanu” lina maana mbili na zote ni za asili.
Amesema Imamu Abul-Husain Ah’mad bin Faaris aliyefariki mwaka 395
H, katika kamusi yake “Mu’jamu Maqaaisil-Lugha” ukurasa wa 987:
"نسي : النون والسين والياء أصلان صحيحان : يدل أحدهما على إغفال
الشيئ , والثاني على ترك شيئ".
معجم مقاييس اللغة ص987.
“Nasiya: Nuni, Siin, na Yaau ni asili mbili zilizo sahihi: moja
yao inafahamisha
“Kughafilika” na ya pili ni “Kuacha kitu”.
Kwa hiyo tumefahamu kuwa neno “Nasiya” lina maana mbili:
i)
Kughafilika.
ii)
Kuacha.
Na kwa mujibu wa kanuni na misingi ya elimu ya itikadi
linapotumika neno lolote lenye zaidi ya maana moja: Maana moja inalingana na
utukufu wa Allah, na maana ya nyingine hailingani na utukufu wake Allah, basi
neno hili litachukuliwa kwa maana ambayo inalingana na utukufu wake Allah.
Kwamfano hapa limetumika neno “Nasiyahum” ambalo maana yake ima
itakuwa :
“(Allah) Amewasahau wao” au “(Allah) Amewaacha wao”.
Tukitazama baina ya maana mbili hizi, ni ipi inayonasibiana na utukufu wake Allah –Jalla
Jalaaluh-?
Bila shaka kulitumia neno hili kwa maana ya “kuacha” ndiyo sahihi
bali ni wajibu kufanya hivyo kwa sababu Allah hasahau kama ilivyotuelezea
Qur’an na Sunna na alivyotuelezea Ibn al-Qayyim hapo nyuma.
Na hakuna shaka kwamba naye Ibn al-Qayyim amelitumia neno hili
hapa kwa maana inayolingana na utukufu wake Allah, nayo ni kwa maana ya
“kuacha”.
Na mtu akilitumia neno hili na jingine kama hili kwa utaratibu ule
ule uliotumika katika Qur’an au katika Sunna hatakuwa na hatia wala hastahiki
lawama, na hivyo ndivyo alivyofanya Ibn al-Qayyim, lakini kwa masikitiko
makubwa jambo hili halikumfurahisha ndugu Juma na kaumu yake na wakalifanya
hilo ni kosa kubwa lisilo na mfano !
Na -wali llaahil-hamdu- ukirejea sehemu mbali mbali katika vitabu
vya Ibn al-Qayyim utaona anavyosema kwa uwazi kabisa kwamba:
فإنه سبحانه لا يضل ولا ينسى "!
“KWA SABABU YEYE (ALLAH)
–SUB’HANAH- HAPOTEI WALA HASAHAU” !
Tazama kitabu chake “Shifaul-Alili” ukurasa wa 141 chapa ya
Darul-kitabil- Arabi Beirut – Lebanon,chapa ya kwanza mwaka 2004.
Lakini ah ! tutazifanya nini sisi nyoyo zilizonyweshwa chuki, husda na uadui mpaka
zikawa hazioni kwa waislamu wenzao ila shari tupu !
Lakini hii ndiyo sera ya watu wote wa bid’a tangu azal.
Ewe Mola wetu usijaalie ndani ya nyoyo zetu chuki na undani dhidi
ya ndugu zetu walio amini, Allaahumma Aamin!
Amesema Juma kuhusu Ibn al-Qayyim:
“Na Ibn Al-qayyim akafikia kusema kuwa moto wa akhera kuna siku adhabu
yake itakwisha kwa waislamu na wasio kuwa waislamu na utabaki mtupu bila ya mtu
yeyote.
Na akainasibisha kauli hii kwa Sheikh wake Ibn Taymiyya na
akaisifu kuwa kauli hii ndio inayokubaliana na Qur’an na suna.”
Mwisho wa kunukuu. Tazama katika kitabu chake “Hoja zenye Nguvu”
ukurasa wa 25.
Ibn al-Qayyim kwenye kitabu chake “Haadil-Ar’waahi” chapa ya
Daarul-Kitabil-Arabi amenukuu mjadala
ulio kuwa kati ya pande mbili: upande wa wasemao kuwa moto utakwisha na upande
wa wasemao kuwa moto hautakwisha, kwa hiyo yeye kazi yake ilikuwa kunukuu hoja
za pande mbili na ndiyo maana utaona anasema:
"والذين قطعوا بدوام النار لهم ست طرق"
“Na wale (wanaosema kwa) kukata kudumu kwa moto wana njia sita”.
Tazama “Haadil-Ar’waahi” ukurasa wa 232.
Kisha akasema tena:
"قال أصحاب الفناء....".
“Wamesema wenye kusema kwisha (kwa moto)….” Tazama kitabu
“Haadil-Ar’waahi” ukurasa 233.
Na mwisho alipofikia kuufunga mjadala huo akasema:
“Kama ukiulizwa ni wapi umefikia unyayo wenu katika mas’ala haya
makubwa, ambayo ni makubwa kuliko dunia kwa mara nyingi?
Ataambiwa : tumefikia kwenye kauli yake –Tabaaraka wata’alaa-:
((إنَّ ربَّك فعَّالٌ لمايريد)) هود:107.
“Kwa hakika Mola wako ni
mwenye kufanya analo litaka….”.
Surat Huud aya ya 107.
Tazama “Haadil-Ar’waahi” ukurasa wa 248.
Mpaka hapo inaonyesha kwamba Ibn al-Qayyim hakuunga mkono hoja ya
upande wowote ule.
Lakini ukweli ni kwamba Ibn al-Qayyim amebabaika sana katika
mas’ala haya, na hakuwa na kauli ya wazi katika suala hili kwenye kitabu hiki.
Lakini tulipo yafuatilia maneno yake yaliyomo kwenye vitabu vyake vingine tukakuta kuwa ameuweka wazi msimamo wake juu ya mas’ala haya kwa mfano kwenye kitabu chake “Al-Waabilu al-Sayibu” ukurasa wa 49 chapa ya “al-Na