1.      Utangulizi 1

2.      Mashia wanavyowagawa Masahaba. 3

3.      Nani Sahaba – kilugha na kidini 4

4.      Nani Mnafiki – kilugha na kidini 4

5.      Pili - Ugawaji wa kweli wa Masahaba Kishia (Ithnaasheri) 5

6.      Majibu juu ya itikadi ya ugawaji wa Masahaba Kishia. 7

7.      Sulhu ya Hudaybiya. 19

8.      Tukio la siku ya Alkhamis. 28

 

BALI UMEPOTOKA

 

Kitabu kinachofichua uongo wa Attiygany uliomo ndani ya kitabu chake alichokiita (ثم اهتديت)  'Kisha Nikaongoka'

Kimeandikwa na Khaled al Asqalaani

Kimetafsiriwa na Muhammad Faraj

Utangulizi

Abdullahi bin Saba-a aliyekuwa Myahudi kutoka mji wa Sana-a - Yemen, aliingia katika dini ya Kiislamu akiwa na nia ya kuwatenganisha na kuwafitinisha Waislamu kwa kisingizio cha kuwapenda sana Ahlul Bayt (Watu wa nyumba ya Mtume wa Mwenyezi Mungu wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam).

Mtu huyu alifanikiwa kiasi kikubwa kulifanya kundi kubwa la Waislam liamini kuwa Qurani Tukufu ina makosa, haikukamilika, na kwamba imebadilishwa na kupunguzwa. Alifanikiwa pia kulifaya kundi hilo liwatuhumu Masahaba wakubwa wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) kuwa ni Wanafiki pamoja na kuwatuhumu Maimam wakubwa wa Kiislam kuwa ni watu wajinga, pamoja na kuvituhumu vitabu vya hadithi Sahihi kama vile Bukhari na Muslim na venginevyo kuwa ni vya uongo.

Abdillahi bin Saba- a huyu, ni mtu wa mwanzo kuueneza uongo wa kufaridhisha Uimamu wa Sayiduna Aly  (Radhiya Llahu anhu), na kwamba anayeukataa Uimamu huo anakuwa kafiri na hatoingia Peponi, pamoja na kuwatukana na kuwakufurisha Makhalifa watatu wa mwanzo, Abubakar, Omar na Othman (Radhiya Llahu anhum).

Aliweza kupata wafuasi wengi kiasi walioyameza na kuyakubali maneno hayo, na kuueneza ufisadi huo kwa kusudi la kuwagawa Waislam kwa bidhaa yake hiyo ovu.

Bidhaa yenyewe ni madai kuwa Makhalifa wa mwanzo hawakuwa na haki ya kutawala na kwamba wamemdhulumu Aly (Radhiya Llahu anhu) , na kwamba Aly (Radhiya Llahu anhu) aliteuliwa na Mwenyezi Mungu kuwa Khalifa wa Waislam kwa ushahidi wa Qurani na Sunnah, na kwamba kwenda kiyume na hayo ni kufru.

Wafuasi hawa wa Abdullahi bin Saba-a Myahudi wanasema kuwa; Aly (Radhiya Llahu anhu) ni bora kupita Masahaba wote (Radhiya Llahu anhum), bali wengine wanasema kuwa Aly (Radhiya Llahu anhu) ni bora kuliko hata Mitume wa Mwenyezi Mungu (Alayhimu ssalaam).

Kwa ajili ya kuziendeleza fikra hizo, kisa cha kuuliwa kwa Al Husayn (Radhiya Llahu anhu) kikageuzwa kuwa ni matanga yanayofanywa kila mwaka. Haya ni mambo ya ajabu kabisa, kwani tatizo hili limekwisha malizika tokea karne nyingi zilizopita lakini kwa makusudi wanaihuisha kila mwaka siku hii wa ajili ya kuiendeleza fikra hii ya Uimam.

Wanaendelea kujiadhibisha kwa kujipiga vifua, kujitoa damu tena kwa visu na minyororo huku wakilizana, wakati kulia na kujitesa kwa ajili ya kifo kilichotokea miaka elfu moja mia nne iliyopita, bali hata kwa kifo kilichotokea leo, ni haramu kubwa na haijuzu kwa kila Muislam mwenye akili timam na mwenye kufuata maamrisho ya dini na mafundisho ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Laahu alayhi wa sallam).

Mtume wa Mwenyezi Mungu(Swalla Llahu alayhi wa sallam) amesema:

“Hayuko pamoja nasi anayepiga mashavu na kuchana nguo na kuomboleza kama (walivyokuwa wakiomboleza) wakati wa Jahilia."

Bukhari na Muslim

Na akasema;

“Atakayelia kwa kuomboleza kisha asitubu, basi atavishwa nguo za moto Siku ya Kiama.”

Bukhari na Muslim

Na hadithi za namna hii ziko nyingi sana.

Mitume wangapi (Alayhimus Salaam) wameuliwa. Masahaba walio bora kuliko Al Husayn (Radhiya Llahu anhu) wameuliwa, akiwemo baba yake - Aly, pamoja na Othman bin Affan (Radhiya Llah anhum), bila shaka Aly na Othman ni bora kuliko Al Husayn (Radhiya Llahu anhum). Wote hawa waliuliwa kwa dhulma na kuonewa lakini hatujawaona wakifanya misiba na maombolezi.

Isitoshe, ikiwa sisi tunaamini kuwa Al Husayn (Radhiya Llahu anhu) yuko Peponi akineemeka, kama alivyotujulisha Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) kuwa ndugu hao wawili; Al Hassan na Al Husayn ni mabwana wa vijana wa Peponi. Sasa ikiwa wao wako huko katika neema za Mola wao, kwa hekima gani sisi tunajitesa kwa ajili ya kifo kilichowafikisha huko?

 

Wanayahuisha matendo yao haya kila mwaka na kuyapulizia pulizia kwa sababu moja tu, nayo ni kuendelea kuupulizia pulizia na kuuwasha moto wa Fitna. Na walipoona kuwa hoja zao hazikubaliki, wakaanza kuleta mvurugano mwengine wa kuwakufurisha Masahaba wote isipokuwa watatu tu au saba. Wakaanza kuwaambia watu kuwa Maimam wa Kishia ni watu waliokingwa na kufanya makosa (hawafanyi makosa yoyote), na kwamba wanafunuliwa Wahyi na kwamba wanajiwa na Malaika walio bora kuliko Jibril na Mikail na kwamba wao ni bora kuliko baadhi ya Mitume wa Mwenyezi Mungu (Alayhimus Salaam), na kwamba wanajua yaliyokuwa, yanayokuwa na yatakayokuwa, na kwamba asiyewaamini Maimam hao ni kafir. Na tatizo ni kwamba bado wanao wafuasi wengi wanaowajaza sumu hizo na kujaza chuki nyoyoni mwao.

Chuki za kuwachukia nani? Mayahudi au Manasara? La, bali chuki za kuwachukia watukufu wa Umma huu na Masahaba wa Mtume wa Mwenyezi Mungu Muhammad bin Abdillah (Swalla Llahu alayhi wa sallam) walioinyanyua bendera ya Mwenyezi Mungu na kuieneza kila pembe ya dunia, mara tu baada ya kufariki kwa kipenzi chao, Mtume wa Mwenyezi Mungu wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam).

 

Mashia wanavyowagawa Masahaba

Mashia wanawagawa Masahaba (Radhiya Llahu anhu) katika makundi matatu:

La kwanza ni wale wanaowaita kuwa ni wema waliomjua Mwenyezi Mungu Subhanahu wa Taala na kumjua Mtume wa Mwenyezi Mungu wake (Swalla Llahu alayhi wa sallam) kama inavyopaswa, wakafungamana naye na kuwa Masahaba wa kweli katika kauli zao na kuwa wakweli katika matendo yao na baada ya kufa kwake hawakugeuka, bali walithibiti; hata Mwenyezi Mungu aliwasifia katika kitabu chake kitukufu katika aya nyingi, na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) pia aliwasifia katika hadithi nyingi.

Mashia wanapowataja Masahaba hawa, huwataja kwa heshima na kuwapa utukufu mkubwa kama vile Masunni wanavyowaheshimu na kuwapa heshima kubwa.

 

La pili ni Mashaba (Radhiya Llahu anhum) walioingia katika dini na kumfuata Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) ama kwa hiari zao au kwa uoga, lakini walikuwa wakijivunia kusilimu kwao mbele ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), na baadhi ya wakati walikuwa wakimuudhi Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), na hawakuwa wakifuata maamrisho na makatazo yake sawasawa, bali walikuwa wakizitanguliza rai zao mbele ya maamrisho yaliyo wazi ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) mpaka pale zinapoteremshwa aya za Qurani zikiwakemea au kuwatisha, ndipo wanapokubali kufuata maamrisho.

Na wanaamini kuwa Mwenyezi Mungu amekwisha wafedhehesha Masahaba hao katika aya nyingi za Qurani, na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) pia alikiwisha waonya katika hadithi nyingi, na Masahaba hawa hawatajwi na Mashia isipokuwa kwa matendo yao tu, na huwataja bila ya kuwaheshimu.

La  tatu, ni wale wanaowaita Wanafiki waliomfuata Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) kwa ajili ya kumfanyia inda tu, na kwamba waliufanyia inda Uislam na Waislam na kwamba Mwenyezi Mungu ameteremsha Sura kamili na kuwataja katika mwahali mwingi na kuwapa ahadi ya kuwaingiza katika tabaka za chini za Motoni. Wanasema kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) keshawataja na kuwaonya watu juu yao na kwamba baadhi ya Masahaba walikuwa wakiyajua majina yao na wasfu wao.

 

Fungu hili la tatu ni wale ambao Masunni na Mashia wanakubaliana juu ya unafiki wao.

Huu ndio ugawaji wa Mashia kwa Masahaba, ukilitenga fungu la Masahaba ambao ni watu wa nyumba ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) ambao wana fadhila zaidi za kinafsi na za kimaumbile kuliko Masahaba waliobaki.

Kuhusu Masunni, wao wanasema yafuatayo:

“Juu ya Masunni kuwaheshimu kwao Ahli l Bayt na kukubali fadhila zao, lakini hawaukubali ugawaji huu na wala hawakubali kuwa baadhi ya Masahaba ni wanafiki, bali kwao wao Masahaba wote ni watu walio bora baada ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam). Na ikiwa wanawagawa basi ni kwa ajili ya kutangulia kwao katika Uislam na kwa ajili ya mitihani waliyokumbana nayo, na wanawafadhilisha Makhalifa waongofu na kuwaweka katika daraja la mbele, kisha Masahaba sita waliobaki katika wale waliokwisha bashiriwa Pepo kama wanavyowaona wao’.

Hii ni kauli ya Mashia ju ya Masunni.

 

Majibu:

Kwanza kabisa kabla sijaanza kujibu na kuuchambua ugawaji huu wa Masahaba katika Itikadi ya Mashia (Ithnaasheri) na kuonesha ubatilifu wake, sina budi kueleza; Nani Sahaba na nani mnafiki, Kilugha na kidini, kisha itatubidi tujulishe kusudi la Mashia (Ithnaasheri) katika ugawaji huu kama walivyoandika katika vitabu vyao wanavyovikubali, ili iwepesike kwa msomaji kuijua haki iko wapi na batili iko wapi, ikiwa msomaji huyo ni Sunni au Shia.

Kisha nitajibu juu ya ugawaji wao huo ili aelewe kila mtu kuwa ugawaji huo uko mbali na haki.

 

Nani Sahaba – kilugha na kidini

Katika kamusi la lugha ya kiarabu, neno ‘Sahaba’, maana yake Rafiki, Mwenzi wake, Sahibu nk.

Katika kamusi la dini neno ‘Sahaba’ maana yake ni Mwislam aliyemuona Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), akawa pamoja naye na kumfuata na kumuamini mpaka kufa kwake.

Na hii ina maana kuwa, yeyote aliyewahi kumouna Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) na asimuamini, basi hawezi kuingia katika maana ya neno ‘Sahaba’.

(Maelezo haya utayapata katika kitabu cha Ibni Qudama kiitwacho ‘Lam-atul Itiqad’.

 

Nani Mnafiki – kilugha na kidini

Katika kamusi la lugha ya kiarabu, neno ‘Mnafiki’ maana yake ni mtu mwenye kigeugeu au mwenye kuwa na sura mbali mbali: Leo hivi kesho vile.

Katika kamusi ya dini, Mnafiki ni yule anayejidhihirisha kuwa ni Muislam na kumfuata Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) wakati undani wake ni kafiri na adui wa Mwenyezi Mungu na adui wa Mtume wa Mwenyezi Mungu wake (Swalla Llahu alayhi wa sallam).

(Tafsiri hii utaipata katika kitabu kiitwacho; Tariyqul hijratayn wa baabul saadatayn’ kilichoandikwa na Ibnul Qayim).

Baada ya tafsiri hii fupi ya nani Sahaba na nani Mnafiki, tutakubaliana kuwa maneno hayo mawili hayawezi kukubaliana (hayawezi kwenda sambamba) hata siku moja Kilugha wala Kidini.

Kwa sababu Sahaba ni yule aliyemuamini Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) na akafa akiwa Muislam, wakati Mnafiki ni yule mwenye kujidhihirisha kama ni Mwislam wakati ndani ya nafsi yake ni kafiri.

Kwa hivyo maneno haya mawili hayakubaliani, na haiwezekani Sahaba akawa Mnafiki na wala Mnafiki hawezi akawa Sahaba.

Sasa Mtu anaweza kuuliza:

'Vipi tutaweza kutofautisha baina ya Sahaba na Mnafiki'

 

Majibu:

Mnafiki ana sifa na alama maalum tulizojulishwa katika Qurani na katika Mafundisho ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), na kwa ajili hiyo tunaweza kutofautisha baina yake na Sahaba. Tutayaelezea yote kila tukiendelea mbele huku tukizijibu hoja za Mashia (Ithnasheri).

 

Pili - Ugawaji wa kweli wa Masahaba Kishia (Ithnaasheri)

Ingawaje kama tulivyoona hapo mwanzo kuwa baadhi ya Mashia wanadai kuwa wao wanawagawa Masahaba mafungu (makundi) matatu, lakini ukweli ni kuwa wanawagawa mafungu Mawili tu na wala hakuna la tatu, na haya ni kutokana na kauli mbali mbali za maulamaa wao na katika vitabu vyao kama tutavyobainisha kila tukiendelea mbele.

Kundi la kwanza la Masahaba (Radhiya Llahu anhu,) katika itikadi ya Kishia, ni lile waliloridhika nalo wenyewe ambao idadi yao hawazidi watu saba.

Al Koshy, ambaye ni Mwanachuoni wa Kishia katika elimu ya wapokezi wa hadithi (Ilmu rijaal), ameelezea kuwa; “ Imam Al Baaqer amesema:

‘Watu wote walirtadi (baada ya kufariki Mtume wa Mwenyezi Mungu - Swalla Llahu alayhi wa sallam), isipokuwa Salman na Abu Dhar na Al Miqdad (Radhiya Llahu anhum)’.

Anayesimulia hadithi hii anaendelea kusema:

‘Nilimuuliza; 'Na Ammar je?’

AkanijibuM

‘Alikuwa akitia na kutoa kisha akarudi’.

(Maelezo haya utayapata katika kitabu kiitwacho ‘Haqul yaqiin fiy maarifat usuul uddin’ kilichoandikwa na Abdulla Shiyr – aalim wa Kishia - juzuu ya kwanza ukurasa 370 hadi 371, na katika kitabu ‘Rijalul Koshy’ ukurasa 17 na ‘Tafsiyr al Abbasy’ juzuu 1 ukurasa 223).

Na katika mapokezi mengine anasema:

‘Kisha wakarudi (baadhi ya) watu, na wa mwanzo katika waliorudi ni Abu Sasan Al Ansari na Ammar na Abu Umeira na Shateera. Walikuwa watu saba, na Amiril Muuminin hakuwa akiwajuwa isipokuwa hawa saba”.

(Utayakuta haya katika vitabu hivyo tulivyovitaja).

Ama Al Kulayni ambaye ni katika wakuu wa Maulamaa wa Kiithnaasheri, katika kitabu chake kiitwacho ‘Usool mina l Kafi’ (na kitabu hiki ni katika vitabu kumi na nne ambavyo ni marejeo makubwa ya Madhehebu ya Kishia) anasema:

“Humran bin Ayun anasema: "Nilimuambia Aba Jaafar alayhi salaam:

"Tuko wachache sana, hata tukijumuika kwa ajili ya kumla mbuzi mdogo, basi hatotoweza kummaliza kwa uchache wetu.”

Akaniambia:

’Nitakuhadithia ya ajabu kupita hayo; Muhajirina (Watu wa Makka) na Answaar (Watu wa Madina) wote wameangamia isipokuwa ---‘akaniashiria kwa vidole vyake vitatu…..”

(Usul minal Kafi – juzu ya 2 ukurasa 191)

Kitabu cha Al Iman wal Kufr – mlango wa Upungufu wa idadi ya Waislam.

Rijal l Koshy uk.13

Tafsir al Safi – juzu 1 uk. 359

 

Na katika kitabu kiitwacho Al Rawdha anasema:

“Kutoka kwa Abdul Rahim al Qasiyr, kasema:

‘Nilimuambia Aba Jaafar alayhi salaam ‘Watu huwa wanaogopa pale tunapowaambia kuwa watu wote wamertadi’, akaniambia:

"Ewe Aba Abdurahim, watu walirudi ‘kuwa makafirikama walivyokuwa wakati wa Ujahilia mara baada ya kufa kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu. Watu wa Madina waligeuka na hawakugeuka katika kheri, wakawa wanafungamana na Saad huku wakiharibika uharibifu wa kijahilia wakimuambia:

“Ewe Saad wewe ndiye tunayekutegemea ….”

(Al Raudha ya Al Kafi juzuu ya 8 uk.246)

 

Hii ni sehemu ya kwanza ya Masahaba wanaokubalika na Mashia wa Ithnaasheri.

Ama kundi la pili la Masahaba katika Itikadi ya Kishia, ni Masahaba wote waliobaki wasiotajwa katika kundi la mwanzo, na wote hao kwao ni Wanafiki na wamertadi na wenye kigeugeu. Wote wakiongozwa na Makhalifa walioongoka (Al Al Khulafaa Arrashidun), kisha wale kumi waliobashiriwa Pepo, kisha Masahaba waliobaki.

Hii ni itikadi ya Mashia Ithnaasheri juu ya Masahaba wa Mtume wa Mwenyezi Mungu wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) kutoka katika vitabu vyao wanavyovitegemea.

Lakini nini hasa sababu ya ugawaji wao ule wa makundi matatu (uliotajwa hapo mwanzoni) wa Masahaba?

Sababu yake ni kujaribu kuwopotosha watu, hasa katika Masunni ili pale unapoanza kusoma katika vitabu vyao kuwa Masahaba hawakurtadi isipokuwa tu walikuwa wakiipenda dunia na kwa ajili hiyo walimfuata Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) ama kwa ajili ya kuitaka dunia au kwa ajili ya kumuogopa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), (yaani walikuwa wanafiq) na msomaji kila anapoendelea kusoma inakuwa rahisi kwake kukubali kila wanachoandika juu ya Masahaba hao, na mwisho inakuwa rahisi kukubali kuwa Masahaba walirtadi. Na kila msomaji anapoendelea kusoma juu ya kundi la pili, kisha la tatu ambao ni wanafiki na kumfanya msomaji ayameze yote anayoyasoma kisha anajikuta anawachanganya wale walio katika kundi la pili pamoja na wa kundi la tatu na kuwaunganisha kuwa ni kundi moja na hatimaye Masahaba wanageuka kuwa makundi mawili; Kundi moja lenye kuridhisha na lingine lililogeuka na kurtadi, na mwisho inakuwa rahisi kwa msomaji kuukubali ugawaji halisi wa Kishia wa kuwagawa Masahaba makundi mawili tu.

Mtu anapoanza kusoma atadhani kuwa wanafiki waliokusudiwa ni Abdillahi bin Ubay bin Salool, ambaye ni mkuu wa wanafiki pamoja na kundi lake, lakini jambo la kushangaza ni kuwa utawaona huyo wanamtetea, na hasa pale Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alipomsalia, wakati Umar (Radhiya Llahu anhu) alipomtaka Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) asimsalie. Kisha wanapinga msimamo wa Masahaba juu ya wanafiki hao.

 

Majibu juu ya itikadi ya ugawaji wa Masahaba Kishia

Ikiwa wanafiki pia watawaita Masahaba, hii itakuwa na maana kuwa yeyote aliyemuona Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) aitwe Sahaba hata kama hakumuamini na kufa katika imani hiyo. Lakini kwa vile wanafiki ni miongoni mwa makafiri, basi hawezi kuwa Sahaba.

Lakini Mashia hawaongezi sharti hii; ya kuwa ‘Sahaba lazima awe yule aliyemuamini Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam)’.

Iwapo tutafuata mantiki hiyo, kwa hivyo Mayahudi, Manasara na Washirikina wa Makka waliomuona Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) nao pia wataitwa masahaba kwa sababu ili mtu aitwe Sahaba halazimiki kuwa amemuamini Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam).

Maneno haya hasema isipokuwa mtu aliyeshiba ujinga.

Wao wanasema hivyo bila ya kuweka sharti hiyo, kwa sababu ikiwa watasema kuwa; Sahaba ni yule aliyemuona Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) na sharti awe amemuamini na afe katika imani hiyo, basi madai yao kuwa wanafiki nao pia ni Masahaba yatabatilika kwa sababu wanafiki si katika watu waliomuamini Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam). Na jambo hili limekubaliwa na Maulamaa wote wa Kishia na Kisunni. (Kuwa Wanafiki si katika watu Walioamini).

Aly (Radhiya Llahu anhu) pamoja na wale Masahaba walioridhika nao Mashia, nao pia wataweza kuingizwa katika kundi la wanafiki (Astaghfirullah), kwa sababu wao wenyewe watakuwa wameufungua mlango wa kukufurishana bila ya kuweka vipimo vya kumjua nani Sahaba na nani Mnafiki, na kwa ajili hiyo kila mtu atakuwa na haki ya kuamini atakavyo juu ya Masahaba wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam). Wote wataweza kuitwa wanafiki kwa sababu wanafiki ni miongoni mwa Masahaba (Radhiya Llahu anhum).

Na kwa mlango huu wamepita wale wasioamini Mungu, wazandiki na wale wazungu wenye elimu za mambo ya Mashariki (Orientalists), ili kuushambulia Uislamu na watu wake.

Msomaji wa vitabu vya Kishia (Ithnaasheri) ataona kuwa wanafiki ndio waliokuwa wengi miongoni mwa Masahaba (Radhiya Llahu anhum), bali wao ndio walioukamata uongozi wa Waislamu mara baada ya kufa kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), (na hii ni itikadi ya Kishia), na wao (Mashia) ndio wanaosema kuwa wanafiki ndio walioshika hatamu mara baada ya kufa kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) na wakauendea kinyume Uislam pamoja na Waislam.

 

Sasa ikiwa kweli hao wanaowaita kuwa ni wanafiki walio wengi walioshika hatamu za Uislamu lengo lao lilikuwa kuwaendea kinyume Waislam, basi kwa nini wasingemzunguka Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) pamoja na Masahaba wake wazuri (hao Masahaba watatu au sita tu) na kuwaua na kuiangamiza Dola ya Kiislamu tokea mwanzo? Kwa nini wakangoja mpaka Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) afariki?

Lakini anayechunguza hali ya mambo, ataona kinyume na madai hayo. Ataona kuwa; Masahaba (Radhiya Llahu anhum) wanowaita kuwa ni wanafiki, waliposhika hatamu, Uislam ulishinda na kusonga mbele na kuenea katika kila pembe ya dunia. Na bendera yake ilinyanyuka juu na kuziangusha bendera za kikafiri Mashariki ya ardhi na Magharibi yake.

Tizameni ndugu zangu vipi hoja zao zinavyogongana na uhakika wa mambo na uhakika wa kiakili pamoja na uhakika wa historia.

Hapo Madina, wale wanafiki wa kweli walikuwa ni watu wachache waliokuwa wakijulikana na kila mtu kutokana na wasfu wao, maana Qurani mara nyingi ilikuwa ikizungumza juu yao, na ushahidi wa kauli hii unapatikana katika hadithi ya Kaab bin Malik (Radhiya Llahu anhu), ambaye ni mmoja katika wale Masahaba watatu (Radhiya Llahu anhum) waliotakiwa wasubiri baada ya kutohudhuria kwao vita vya Tabuk, pale Kaab bin Malik aliposema

“Nikawa kila ninapotoka nje ya nyumba yangu na kuonana na watu, ninahuzunika sana na kuona uchungu kwa vile sikuwa nikimwona hata mmoja aliye kufu yangu. Sikuwa nikiwaona isipokuwa wale watu waliokuwa wakijulikana kuwa ni wanafiki au wale waliokuwa na udhuru wa kutokwenda vitani kwa sababu ya umasikini, udhaifu wa hali zao au maradhi”.

(Bukhari juzuu ya 4 uk.1604 nayo ni sehemu ya hadithi ndefu ya Kaab bin Malik (Radhiya Llahu anhu)).

Zifuatazo ni baadhi tu ya sifa za wanafiki kama alivyowaelezea Mwenyezi Mungu katika kitabu chake, na pia Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) katika mafundisho yake;

Wanafiki ni watu;

‘Wanaoeneza ufisadi ardhini, kuifanyia istihzai dini, kuwafanyia istihzai wacha Mungu, wavukaji mipaka katika maasia na kuwa wao wanaununua upotofu (upotevu) kwa uongofu, viziwi, mabubu na vipofu (sumun bukmun umyun), waliotahayari, wavivu katika kufanya ibada, hugeuka geuka, mara Waislamu mara makafiri, kama alivyosema Mwenyezi Mungu:

“Wanayumba yumba baina ya huku (kwa Waislam) na huko (kwa makafiri). Huku hawako wala huko hawako)”.

Annisaa-143

Wanafiki wanapenda kuapa uongo kwa jina la Mwenyezi Mungu, hawaijui dini na kwamba wao ni waoga.

Na katika sifa za wanafiki pia ni;

‘Kuwa hawamwamini Mwenyezi Mungu wala Siku ya Akhera na kwamba Waislam wanapopata kheri yoyote au mafanikio wao wanahuzunika, na huwa wanafurahi pale Waislamu wanapopata tabu na mitihani na kwamba kazi yao ni kuwavizia Waislam, na pia huchukizwa katika kutoa mali zao katika njia ya Mwenyezi Mungu na hufurahi wanaporudi nyuma na kumuacha Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) peke yake aende vitani na kwamba wao ni watu waovu kabisa mbele ya Mwenyezi Mungu na wameingia katika dini yake ili wajikinge wasiambiwe kuwa wao ni makafiri na wanapenda kuwadhuru Waislam na kuwafarikisha na hupindukia mipaka pale wanapohasimiana na kwamba wanaiahirisha sala mpaka nyakati zake za mwisho na hawahudhurii Sala za jamaa na kwamba wanaionea uzito kabisa Sala ya Alfajiri na ya Ishaa’.

 

Hizi ni baadhi tu ya sifa za Wanafiki alizozitaja Mwenyezi Mungu katika Qurani tukufu, na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) katika mafundisho yake.

Ndugu zangu Waislam, hivyo kweli hizi ni sifa wanazostahiki kupewa Masahaba wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam)?

Bila shaka Masahaba wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) ni watu walio mbali kabisa na sifa kama hizi. Masahaba (Radhiya Llahu anhum) waliostahiki kupata radhi za Mwenyezi Mungu pamoja na sifa nzuri nzuri, hata Mwenyezi Mungu akawaita kuwa;

“Nyinyi ndio umma bora kuliko umma zote zilizodhihirishiwa watu (ulimwenguni) mnaamrisha yaliyo mema na mnakataza yaliyo maovu, na mnamwamini Mwenyezi Mungu”.

Aali Imran- 110

Na akasema juu yao:

“Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Mwenyezi Mungu anakutoshelezea wewe na wale walokufuata katika hao walioamini”.

Al Anfal-64

Na akasema juu yao:

“Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu . Na walio pamoja naye ni wenye nyoyo thabiti mbele ya makafiri na wenye kuhurumiana wao kwa wao. Utawaona wakiinama kwa kurukuu na kusujudu (pamoja), wakitafuta fadhila za Mwenyezi Mungu na radhi (yake).”

Al Fat-h- 29

Na akasema:

“Na wale walioamini wakahama (kuja Madina) na wakaipigania dini ya Mwenyezi Mungu (Nao ni Muhajir); na wale waliowapa (Muhajir) mahala pa kukaa na wakainusuru dini (ya Mwenyezi Mungu na Mtume wake).(nao ni Ansar) Hao ndio Waislam wa kweli. Watapata msamaha (wa Mwenyezi Mungu) na kuruzukiwa kuzuri (kabisa huko Akhera)”.

Al Anfal – 74.

Kwa hivyo wale Walioamini, Wakahama, Wakapigana jihadi ni Wahajir (Masahaba wa Makka). Na wale Waliowapa mahala pa kukaa na Kuwanusuru nao ni Maanswar (Masahaba wa Madina), Mwenyezi Mungu amewapa wote hao sifa kuwa ni Waislam wa kweli. Kisha aje mtu atuambie kuwa Masahaba na wanafik ni kitu kimoja!!!?

 

Katika mambo yanayokubaliwa na Maulamaa wote ni kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) aliwajulisha baadhi ya Masahaba (Radhiya Llahu anhum)  majina ya baadhi ya wanafiki, na haya yanakubaliwa na maulamaa wa Kishia pia kama yanavyokubaliwa na Masunni.

Na katika mambo wanayokubaliana pia ni kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) amezungumza juu ya kuridhika kwake na Masahaba wake (Radhiya Llahu anhum)  na akasema:

"Msiwatukane masahaba wangu. Ninaapa kwa jina la Yule ambaye nafsi yangu imo mikononi mwake, hata mmoja wenu akijitolea katika njia ya MwenyeziMungu kugawa dhahabu ukubwa wake mfano wa jabali Uhud, basi hatofikia gao lao wala hata nusu ya gao lao".

Bukhari na Muslim

Kuwatia Masahaba na wanafiki katika kundi moja ni katika matusi makubwa kabisa.

Na Mtume wa Mwenyezi Mungu(Swalla Llahu alayhi wa sallam) pia akasema:

“Atakayewatukana Masahaba wangu, basi itampata laana ya Mwenyezi Mungu na (laana ya) Malaika na (laana ya) watu wote”.

((Attabariy, katika kitabu chake kiitwacho ‘Al Kabeer’, Abi Naeem katika ‘Al Hiliya’ na Abi Asim, na hadithi hii pia inapatikana katika ‘Silsila za hadithi sahihi kilichoandikwa na Sheikh Al Albani)).

Na akasema:

“Nihifadhieni Masahaba wangu, kisha wale waliowafuatilia kisha wale waliofuatilia”.

Imam Ahmad, Ibni Majah, na Al Haakim.

Sifa hizi lazima wapewe Masahaba wote kwa uadilifu na haiwezekani kuwaingiza wanafiki katika sifa hizi, wanafiki ambao Mwenyezi Mungu anasema juu yao;

“Bila shaka wanafiki watakuwa katika tabaka za chini kabisa katika moto”.

An Nisaa- 145

 

Kisha tunauliza:

Ikiwa tutafuata ugawaji wao (Mashia) wa Masahaba wa makundi matatu na kuyahesabu yale makundi mawili, la pili na la tatu kuwa ni hao waliomfuata Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) kwa maslahi yao au kwa kuogopa na kwamba walikuwa na kigeu geu wakarudi nyuma baada ya kufa kwake (Swalla Llahu alayhi wa sallam), pamoja na kuwa wanafiki.

Kwa vile wao ndio waliokuwa wengi sana, na kundi lingine ambalo ni la Masahaba wachache mno walioridhika nao Mashia kama ilivyobainika hapo mwanzo, iwapo tutafuata na kuukubali ugawaji wao huo, utaleta maana gani?

Ikiwa wengi wa Masahaba walikuwa ni watu waliokuwa na kigeugeu na unafiki, hii italeta maana kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) hakuweza kuwalea na kuwafundishsa vizuri Masahaba wake (Radhiya Llahu anhum)  wakaijuwa haki, na kwamba yeye ni mlezi asiyefanikiwa, aliyefeli katika kazi yake ya kuwalea Masahaba (Radhiya Llahu anhum).

Baada ya kuishi nao muda mrefu wote huo amefanikiwa kuwalea na kuwafundisha Mashaba watatu tu au wasiozidi saba?

Sisi tunakanusha kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alifikia daraja hii ya kuangushwa na kuwa alishindwa kuwalea Masahaba wake (Radhiya Llahu anhum).

Nawauliza ndugu zangu Waislam:

‘Je! Huku si kumshutumu hata Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa Sallam)?’

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alikuwa akifanya nini miaka yote aliyoishi na Masahaba wake (Radhiya Llahu anhum)?

 

Subhanallah! Hivyo kweli Mtume wa Mwenyezi Mungu huyu mtukufu ambaye ni kipenzi cha Mola wake na mbora wa viumbe vyote (Swalla Llahu alayhi wa sallam), aliyelea vizazi vitukufu, na Mwenyezi Mungu akamfungulia dunia yote akaweza kuwaokoa watu kutoka katika kuwaabudu viumbe na kuwafanya wamuabudu Mungu wa viumbe; akawatoa katika dini za dhulma na kuwatia katika Uadilifu wa Uislam, na akaweza kuwatoa katika viza vya dini za kijahilia na kuwaingia katika nuru ya Uislam, na watu wakaingia makundi kwa makundi katika dini hii kutoka katika kila pembe ya dunia mpaka wanavyuoni wa Kiyahudi na Manasara waliukubali ukweli huu.

Leo na baada ya kupita karne kumi na tano, waje wajukuu wa Abdillahi bin Saba-a - Myahudi, na kutustua kuwa eti Masahaba walikuwa wanafiki na kwamba walirudi nyuma?

Kila anayesoma na kuidurusu sira (historia) ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), anaelewa kwamba wakati Waislam walipokuwa Makka hapakuwa na unafiki, na hii ni kwa ajili ya adhabu kali walizokuwa wakipata wale waliosilimu, na kwamba unafiki ulianza kujitokeza baada ya Waislam kuhamia Madina na baada ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) kupata nguvu, na dini ya Mwenyezi Mungu kuanza kutambulika kila mahala.

Na inaeleweka pia kwa kila mwenye kudurusu sira (historia) ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) kuwa Abubakar, Umar na Uthman na wengineo ni miongoni mwa Masahaba (Radhiya Llahu anhum)  walioingia katika dini ya Mwenyezi Mungu tokea siku za mwanzo, wakapata tabu na shida kama walivyopata wenzao, na hii ni dalili wazi kabisa kuwa walikuwa mbali kabisa na unafiki.

Mwenyezi Mungu amewafedhehesha wanafiki kwa kuwateremshia Suratul Munafiqun na At Tawba; akaelezea  ndani sura hizo juu ya hali zao na vitimbi vyao; na akatuelezea yale yaliyofichika nyoyoni mwao katika kuwachukia Waislam, na hii ndiyo maana Surat at Tawba ikaitwa 'Sura ya Kufedhehesha'. Katika sura hiyo Mwenyezi Mungu alitaja sifa za Masahaba (Radhiya Llahu anhum)  na akatujulisha kuridhika kwake nao. Na huu ni ushahidi utokao Kwake Subhanahu wa Taala.

Ama Suratul Munafiqun, hii imeteremshwa kwa ajili ya kutujulisha juu ya mkubwa wa wanafiki na kiongozi wao aitwae Abdillahi bin Ubay bin Salool na wenzake.

Anasema Zayd bin Al Arqam (Radhiya Llahu anhu):

"Nilikuwa vitani, nikamsikia Abdillahi bin Ubay akisema:

“Msitoe mali kuwasaidia waliokuwa na Mtume wa Mwenyezi Mungu mpaka watakapomwondokea pale alipo, na tutakaporudi Madina yule mtukufu (akimaanisha yeye Abdillahi bin Ubay ‘mkuu wa wanafiki’) atamtoa (katika mji wa Madina) yule aliyedhalilika (akimaanisha Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam)”.

Nikamhadithia hayo niliyoyasikia Ami yangu (au Umar) naye akamhadithia Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam): Akaniita na mimi nikamhadithia. Kisha Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akamtuma mtu amuite Abdillahi bin Ubay pamoja na wenzake, wakaapa na kukanusha yale waliyosema, na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) hakunisadiki na akamsadiki yeye. Nikaona dhiki sijapata kuona mfano wake. Nikakaa nyumbani kwangu, lakini haujapita muda Mwenyezi Mungu akateremsha Suratul Munafiqun (Idhaa jaaa-aka l Munafiqun), Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akamtuma mtu aniite, akanisomea (Sura hiyo) kisha akaniambia:

“Mwenyezi Mungu amesadikisha maneno yako ewe Zeyd”.

Bukhari.

Tafsiri hii pia inapatikana katika kitabu cha tafsiri cha Mashia kiitwacho ‘Maj maa l bayan fiy tafsiyri l Quran’, kilichoandikwa na Imam Al Tubrusy ambaye ni miongoni mwa maulamaa wakubwa wa Kishia. Na katika kitabu hicho, ameelezea sababu ya kuteremshwa Suratul Munafiqun kuwa ni juu ya Abdillahi bin Ubay ‘mnafiki’ na wenzake …..

(Maj maa l bayan fiy tafsiyr l Qur an ukurasa 85)

Kisha Mwanachuoni huyu wa Kishia akazitaja riwaya zile zile alizozielezea Imam Bukhari zinazothibitisha hoja hiyo.

Inajulikana wazi kuwa Abdillahi bin Ubay pamoja na wafuasi wake walikuwa wakijulikana wazi wazi na Masahaba wote (Radhiya Llahu anhum) kuwa ni wanafiki, na mtu yeyote anaposoma Surat at Tawba ataona kuwa sura hiyo imeelezea juu ya vituko mbali mbali walivyokuwa wakivifanya wanafiki hao kiasi ambacho ilikuwa wazi kabisa mbele ya kila mtu kuwa wao ndio waliokusudiwa.

Kwa mfano katika kuanzia aya ya 44 hadi 49 ya sura hiyo Mwenyezi Mungu anasema:

“Hawatakuomba ruhusa wale wanao muamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho, wasende kupigana Jihadi kwa mali yao na nafsi zao. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kuwajua wachaMungu.

Wasio muamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho na nyoyo zao zikatia shaka, hao tu ndio wanao kutaka ruhusa. Basi hao wanataradadi katika shaka zao.

Na ingeli kuwa kweli walitaka kutoka bila ya shaka wangeli jiandalia maandalio, lakini Mwenyezi Mungu kachukia kutoka kwao, na kwa hivyo akawazuia na ikasemwa: Kaeni pamoja na wanao kaa!

Lau wangeli toka nanyi wasingeli kuzidishieni ila mchafuko, na wange tanga tanga kati yenu kukutilieni fitna. Na miongoni mwenu wapo wanao wasikiliza. Na Mwenyezi Mungu anawajua madhaalimu.

Tangu zamani walitaka kukutilieni fitna, na wakakupindulia mambo juu chini, mpaka ikaja Haki na ikadhihirika amri ya Mwenyezi Mungu, na wao wamechukia”.

Na miongoni mwao wapo wanao sema: ‘Niruhusu wala usinitie katika fitina’. Kwa yakini wao hivyo wamekwisha tumbukia katika fitina. Na hakika Jahannamu imewazunguka.”

Inaeleweka na kila mtu kuwa Masahaba wote walitoka na kwenda vitani siku hiyo ya vita vya Tabuk (vita ambavyo aya hizo zinazungumzia juu yake), na waliobaki nyuma ni Abi Dhar na Abu Khaythamah (Radhiya Llahu anhum), kisha nao pia wakenda kujiunga na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) pamoja na wenzao, na waliwawahi njiani kabla vita kuanza.

Na ineleweka pia kuwa miongoni mwa waliobaki nyuma ni Kaab bin Malik, Hilal bin Umayya na Mirara bin Rabia (Radhiya Llahu anhum), nao ni katika watu wa Madina na inajulikana na kila mtu kuwa Mwenyezi Mungu aliwasamehe Masahaba hao kama ilivyoelezwa katika kisa cha ‘Wale watatu waliongojeshwa’.

Ama wengine waliobaki Madina na wasende vitani walikuwa wakijulikana kuwa ni katika wale wanafiki waliomuendea Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) na kuomba udhuru wa uongo, au wale waliokuwa na udhuru wa kutopigana Jihad kwa ajili ya ugonjwa au udhuru mwingine unaokubalika.

Na haya tulieleza hapo mwanzo katika kisa cha Kaab (Radhiya Llahu anhu)  kuwa katika waliobaki pale Madina wasende vitani hakuwa akimuona aliye kufu yake isipokuwa wenye udhuru au wale waliokuwa wakijulikana kuwa ni Wanafiki.

Na hii ni dalili kuwa wanafiki walikuwa wakijulikana na Masahaba.

Ama katika kauli yake Subahanahu wa Taala katika Sura hiyo hiyo ya At Tawba aya ya 64, Mwenyezi Mungu anasema:

“Wanafiki wanaogopa isije teremshwa Sura itakayo watajia yaliyomo katika nyoyo zao. Sema: ‘Fanyeni mzaha! Hakika Mwenyezi Mungu atayatoa nje hayo mnayo yaogopa.”

Anasema Ibni Kathiyr katika kuifasiri aya hii:

“Kasema Mujahid: ‘Walikuwa wakizungumza baina yao, kisha wanasema: ‘Pengine Mwenyezi Mungu hatoificha siri yetu hii’.

Na hii inasadikisha kauli ya Mwenyezi Mungu isemayo:

“Na wafikapo kwako wanakuamkia kwa (maamkio) ambayo siyo maamkio aliyoamrisha Mwenyezi Mungu uamkiwe kwa maamkio hayo, na husema katika nyoyo zao; ‘Mbona Mwenyezi Mungu hatuadhibu kwa haya tunayoyasema?’ Basi Moto wa jahannam utawatosha kuwatia adhabu, watauingia, napo ni mahali pabaya sana pa kurudia (kiumbe)”.

Al Mujadalah - 8

Na maana yake ni kuwa Mwenyezi Mungu atamteremshia Mtume wake (Swalla Llahu alayhi wa sallam) yale yatakayowafedhehesha na kubainisha juu yenu.

Na mfano wake ni mfano wa kauli ya Mwenyezi Mungu isemayo:

“Je! Wale wenye maradhi nyoyoni mwao wanadhani kwamba Mwenyezi Mungu hataidhihirisha bughudha yao?

Na kama tungependa tungekuonyesha (watu hao wenye bughudha na Uislam) na ungewatambua kwa alama zo, lakini utaweza kuwafahamu kwa namna ya msemo (wao). Na Mwenyezi Mungu anavijua vitendo vyema (vyote).”

Muhammad – 29 – 30

Na kwa sababu hii Qatada amesema:

“Sura hii ilikuwa ikiitwa kashfa iliyowafedhehesha Wanafiki.”

(Tafsiri ya Ibni Kathiry)

Na hii ni kwa sababu Mwenyezi Mungu amewafedhehesha ili watu wawajue, wakati kabla ya hapo hapana aliyekuwa akiwajua, na walikuwa wakifanya vitimbi vyao kwa siri.

Kisha baada ya yote hayo aje mtu awatie moja wao katika fungu la Masahaba watukufu (Radhiya Llahu anhum).

Ama katika kauli ya Mwenyezi Mungu isemayo:

“Watakuapieni kwa Mwenyezi Mungu mtakapo rudi kwao ili muwaachilie mbali. Basi waachilieni mbali. Hakika hao ni najsi, na makaazi yao ni Jahannamu, kuwa ni malipo kwa waliyo kuwa wakiyachuma.

Wanakuapieni ili muwe radhi nao. Basi hata mkiwa radhi nao nyiye, Mwenyezi Mungu hawi radhi na watu wapotofu”.

Al Tawba – 95-96

Aya hizi ziliteremshwa juu ya wale wanafiki waliobaki nyuma wasiende kupigana katika vita vya Tabuk kisha wakaja kutoa udhuru wa uongo kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) na idadi yao ilikuwa wanaume wapatao themanini na kidogo hivi, na hakuwa miongoni mwao hata mmoja katika Sahaba wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam).

Anayetaka maelezo zaidi na asome kisa CHA WALE WATATU WALIONGOJESHWA, kilichomo katika Sahihul Bukhari, kisa kinachoelezea sababu za kuteremshwa aya hizi.

 

Ama kuhusu kauli ya Mwenyezi Mungu katika sura hiyo hiyo ya Al Tawba kuanzia aya ya 107 hadi 108 isemayo:

“Na wapo walio jenga msikiti kwa ajili ya madhara na ukafiri na kuwafarikisha Waumini, na pa kuvizia kwa walio mpiga vita Mwenyezi Mungu na Mtume wake hapo kabla. Na bila ya shaka wataapa kwamba: Hatukukusudia ila wema tu. Na Mwenyezi Mungu anashuhudia kuwa wao ni waongo.

Usisimame kwenye msikiti huo kabisa. Msikiti ulio jengwa juu ya msingi wa uchaMungu tangu siku ya mwanzo unastahiki zaidi wewe usimame ndani yake. Humo wamo watu wanao penda kujitakasa. Na Mwenyezi Mungu anawapenda wanao jitakasa”.

At Tawba -107-108

Aya hizi pia ni miongoni mwa aya zilizowafedhehesha wanafiki walipojenga msikiti kwa kusudi la kuwatakia Waislam madhara, na msikiti huo ulikuwa wa Abu Amer aliyekuwa mtu asi. Alijenga msikiti huo kwa kusudi la kuwapiga vita Waislam, kisha akamtaka Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) aswali katika msikiti huo, lakini Jibril (Alayhi Ssalaam) akamteremshia Wahyi Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) kutoka kwa Mola wake kuwa asende kusali mahali hapo, na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akawaamrisha baadhi ya Masahaba (Radhiya Llahu anhu) kuubomoa msikiti huo na wasali katika msikiti uliojengwa juu ya msingi wa uchaMungu (Masjid Qubaa).

Bila shaka wanafiki hao waliotaka kuudhuru Uislam walikuwa wakijulikana na Masahaba (Radhiya Llahu anhu), lakini Mashia wanasema kuwa eti Masahaba wengi walikuwa wanafiki.

Mtu yeyote akitumia akili yake kidogo tu, ataona kuwa ule msikiti aliosali ndani yake Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) ‘Masjid Qubaa’, ndio uliojengwa na Masahaba (Radhiya Llahu anhum), na ule ambao Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) aliamrisha ubomolewe ni msikiti wa wanafiki.

Sasa ikiwa Masahaba walio wengi ni wanafiki (waliomo katika kundi la kwanza na la pili – kutokana na ugawaji wao Mashia), na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alisali katika msikiti wa Masahaba wanafiki (kama wasemavyo wao). Je! Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) aliamrisha ubomolewe ule wa Masahaba ambao ni wachache, kisha akasali katika msikiti wa wanafiki walio wengi?

Wakati katika sura hiyo hiyo Mwenyezi Mungu anatuelezea juu ya kuridhika kwake juu ya Sahaba waliotangulia wa kwanza katika Wahajir (watu wa Makka waliohamia Madina) na Ansar (Watu wa Madina waliowapokea Wahajir wa Makka) na akawatayarishia Bustani zipitazo mito kati yake, wadumu humo milele.

Mwenyezi Mungu anasema:

“Na wale walio tangulia, wa kwanza, katika Wahajiri na Ansari, na walio wafuata kwa wema, Mwenyezi Mungu ameridhika nao, na wao wameridhika naye; na amewaandalia Bustani zipitazo mito kati yake, wadumu humo milele. Huko ndiko kufuzu kukubwa.”

At Tawba 100

Sasa tizameni ndugu zangu vipi Mwenyezi Mungu anatuelezea juu ya kuridhika kwake na Masahaba katika Muhajir na Ansar na vipi wenzetu wanatuambia kuwa wao ni wanafiki na kwamba walirudi nyuma na kukufuru, akiwemo mbora wa Masahaba wote Abubakar Al Siddique (Radhiya Llahu anhu).

Ama Masunni wanaridhika na wote Mwenyezi Mungu aloridhika nao, na wanawafanyia uadui wale maadui wa Mwenyezi Mungu tu, na wanafuata yale waliyofundishwa na Mwenyezi Mungu pamoja na mafundisho ya Mtume wa Mwenyezi Mungu wake (Swalla Llahu alayhi wa sallam), na wala hawavumbui mambo katika vichwa vyao.

Na katika kauli yake Mwenyezi Mungu pale aliposema:

“Mwenyezi Mungu amekwisha pokea toba ya Nabii na Wahajiri na Ansari walio mfuata katika saa ya dhiki, pale baada ya kukaribia nyoyo za baadhi yao kugeuka. Basi akapokea toba yao, kwani hakika Yeye kwao wao ni Mpole na ni Mwenye kuwarehemu.”

Attawba 117

Katika aya hii na aya iliyotangulia nambari 100 inaonyesha wazi namna gani Mwenyezi Mungu alivyoridhika nao na anavyowasifia Muhajir na Ansar waliomfuata katika ile saa ya dhiki (vita vya Tabuk), na pia Mwenyezi Mungu anatujulisha juu ya usafi wa yale yaliyofichika nyoyoni mwao.

Huu ni ushahidi utokao kwa Mwenyezi Mungu asiye mshirika.

Ksha Mwenyezi Mungu anatujulisha juu ya kuridhika kwake na wale watatu walioambiwa wangoje ambao ni miongoni mwa Masahaba (Radhiya Llahu anhum)  kinyume na wale wanafiki ambao Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alikubali udhuru wao bila kujua undani wao, lakini hatimae Mwenyezi Mungu akawafedhehesha. Na hii ni dalili kubwa kabisa kuwa ipo tofauti baina ya Masahaba JUU YA KUKOSEA KWAO BAADHI YA WAKATI na WANAFIKI aliowafedhehesha Mwenyezi Mungu katika kitabu chake kitukufu.

 

Hapa tutaleta dalili kutoka kwa Wanavyuoni wakubwa wa Kishia (Ithnaasheri) ambao Mwenyezi Mungu atakayekifanya kila kitu kiseme siku ya Kiama, aliwafanya wanavyuoni hao kuutamka ukweli wakitaka wasitake. Na wameyasema haya katika vitabu vyao vinavyoaminika na kutambulika.

Anasema Abu Nasr Muhammad bin Masaud, anayejulikana kwa jina la ‘Al Iyashi’ katika tafsiri yake juu ya kauli ya Mwenyezi Mungu isemayo:

“Hakika Mwenyezi Mungu huwapenda wanaotubu na huwapenda wanaojitakasa’

Al Baqarah – 222

Mwanachuoni huyu wa Kishia ametamka kauli inayokanusha wazi wazi kuwa Masahaba wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) walikuwa wanafiki.

Na kauli hii imetamkwa na Muhammad al Baqer (Radhiya Llahu anhu)  ambae ni Imam wa tano katika Maimam waliokingwa kwa Mashia.

Anasema Al Iyashi:

‘Kutoka kwa Salam anasema: ‘Nilikuwa kwa Abu Jaafar (AS) akaingia Hamran bin Ayun akamuuliza baadhi ya mambo na alipotaka kuondoka, Ayun akamuuliza Abu Jaafar:

'Tuelezee Mwenyezi Mungu akupe umri mrefu, sisi tunapokuwa nawe nyoyo zetu hulainika na nafsi zenu zinakuwa mbali na dunia, tunadharau kila kilichomo mikononi mwa watu katika hizi mali, lakini tunapotoka na kuchanganyika na watu na kufanya biashara tunaanza kuipenda tena dunia.’

Anasema, Abu Jaafar akasema:

"Nyoyo zinashindwa na mambo baadhi ya wakati, na wakati mwengine mambo yanakuwa mepesi’, kisha Abu Jaafar (AS) akaendela kusema: ‘Kwa hakika Masahaba wa Mtume wa Mwenyezi Mungu walisema:

‘Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, tunajiogopea unafiki’ akasema: “Kwa nini mnaogopa?”

Wakasema:

“Sisi tunapokuwa nawe ukatukumbusha, huwa na uoga na nyoyo zetu zinalainika tukaisahau dunia, hatuitamani, hata hufikia kuwa tunaiona akhera, Pepo na Moto mbele yetu. Lakini mara tunapotoka kwako na kuingia majumbani mwetu na kuanza kuwabusu watoto wetu na kuonana na wake zetu na mali zetu, tunaanza kubadilika hali zetu kinyume na pale tunapokuwa nawe, kama kwamba hatukuwa na kitu. Je! Hutuogopei unafiki?"

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akawaambia:

“Kabisa sikuogopeeni hilo, kwani hizi ni katika hatua za shetani akijaribu kukupendezesheni dunia, Wallahi lau kama mungebaki katika hali ile mliyokuwa nayo pale mlipokuwa kwangu, basi Malaika wangekusalimieni barabarani na mungekuwa mnatembea juu ya maji, na kama mungelikuwa hamtendi madhambi na kumuomba Maghfira Mwenyezi Mungu, basi Mwenyezi Mungu angeliumba viumbe ili wafanye madhambi kisha wamuombe maghfira ili apate kuwaghufiria, kwani Muislam siku zote yupo katika mtihani, kwani hukuisikia kauli ya Mwenyezi Mungu isemayo;

‘Hakika Mwenyezi Mungu huwapenda wanaotubu?’ na isemayo;

“Na ili muombe msamaha kwa Mola wenu kisha mtubie (mrejee)?"

Hud 3

(Tafsir Al Iyashi Juz1 uk.128)

 

Ama Imam Al Hassan Al Askari, ambaye ni Imam wao wa kumi na moja alipokuwa akiwafahamisha watu daraja ya Masahaba (Radhiya Llahu anhum)  mbele ya Mwenyezi Mungu alisema:

‘Miongoni wa masuala aliyouliza Musa (Alayhi Ssalaam) kumuuliza Mwenyezi Mungu alisema:

‘Je! Wapo Masahaba wa Mtume wa Mwenyezi Mungu yeyote walio bora kuliko Masahaba wangu?'

Mwenyezi Mungu akamjibu:

“Ewe Musa kwani hujui kuwa ubora wa Masahaba wa Mtume wa Mwenyezi Mungu Muhammad juu ya Masahaba wa Mitume yote ni sawa na ubora wa Aali ya Muhammad juu ya Aali za Mitume yote, na mfano wa ubora wa Muhammad juu Mitume yote?”

 

Kwa kumalizia tutizame nini anasema Imam Aly bin Abu Talib (Radhiya Llahu anhu) juu ya Masahaba hawa watukufu.

Imam Aly ni Imam wao wa mwanzo na kwetu sisi ni Khalifa wa nne aliyeongoka. Tutanukuu kauli yake kutoka katika kitabu kitukufu sana kwa Mashia kiitwacho ‘Nahaj al Balaghah’, Sharhi ya Muhammad Abdo Uk. 225, pale Imam Aly aliposema:

“Nimewaona Masahaba wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Laahu alayhi wa sallam), na sioni yeyote kati yenu aliyeshabihiana nao. Walikuwa wakati wa asubuhi utawaona nywele zimetimka kwa sababu ya kusimama kwao usiku kucha wakisujudu na kusimama (kwa kusali), wanaomba huku wakisujudu, na wanapolala na wanapokumbuka akhera yao utawaona wanasimama kama kwamba wamesimamia makaa ya moto. Na anapotajwa Allah basi macho yao yanatoa machozi mpaka nyuso zao zinaroa, na wanainamisha vichwa vyao chini mfano wa miti iliyopinda kwa upepo mkali wa kimbunga kwa kuhofia adhabu na kutarajia thawabu”.

 

Ama Ibarahim Al Thaqafi ambaye ni katika maulamaa wakubwa wa Kishia, katika kitabu chake kiitwacho ‘Al Ghaaraat’ Juzuu ya 1 Uk.177 akimnukuu Aly (Radhiya Llahu anhu)  anasema:

“Aliulizwa Aly: ‘Ewe Amiri wa Waislam, tuelezee juu ya Sahibu zako.’

Akauliza:

“Juu ya sahibu zangu wepi?”

Wakamwambia:

“Juu ya Sahaba wa Muhammad (Swalla Llahu alayhi wa sallam).”

Akasema:

“Masahaba wa Muhammad wote  ni sahibu zangu”.

Hizi ni kauli za Imam Ali (Radhiya Llahu anhu) juu ya Masahaba ambao wao wanadai kuwa wengi wao au karibu wote ni Wanafiki.

 

Tunamuomba msomaji arudie marejeo yote tuliyonukuu ushahidi wetu huu ili imbainikie wapi ukweli upo, na ili aelewe uovu wa msimamo wa ndugu zetu hawa juu ya Masahaba wakiwemo Makhalifa watatu wa mwanzo wa Waislam.

 

Mlango wa pili

Atakayesoma kitabu hiki au makala haya ataona kuwa ushahidi wote unaegemezwa kutoka katika yale yaliyokubaliwa na pande zote mbili kutoka katika Qurani na Sunnah na ushahidi mwengine ni wa kutumia akili na mantiki.

 

Kwanza

Sulhu ya Hudaybiya

Kisa cha Hudaybiya kilikuwa kama ifuatavyo:-

Katika mwaka wa sita baada ya Hijra, Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alitoka pamoja na Masahaba wapatao elfu moja na mia nne kuelekea Makka, wakiwa na nia ya kufanya Umra, na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) aliwataka Masahaba (Radhiya Llahu an'hum) waziache panga zao ndani ya ala zake. (yaani wasitoe panga zao nje)

Wakavaa nguo zao za Ihram katika Miyqaat, hapo Dhul Hulayfa (Abyaar Aly), kisha wakaondoka pamoja na mbuzi wao, ili Maqureshi wajue kuwa wamekuja kwa nia ya kufanya Umra na si kivita. Lakini Maqureshi wakafanya kiburi kwa kuogopa watu wakisikia kuwa Muhammad ameingia Makka bila bila ya kufanyiwa tabu yoyote, na akafanya Umra, watu watawadharau na kuona kwamba labda wameshindwa kumzuwia.

Wakatuma ujumbe ulioongozwa na Suhail bin Amru bin Wud Al Amry aliyemtaka Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) pamoja na alokuja nao warudi Madina mwaka huu bila ya kufanya Umra na kamba mwaka ujao watamruhusu aje kufanya Umra kwa muda wa siku tatu.

Wakamwekea Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) masharti mazito aliyoyakubali.

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) aliyakubali masharti yao kwa ajili ya kutaka sulhu - kama alivyofunuliwa na Mola wake, lakini baadhi ya Masahaba (Radhiya Llah anhum) waliyakataa masharti hayo, na Umar (Radhiya Llahu anhu)  alimwendea Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) na kumuuliza:

“Kwani wewe si Mtume wa Mwenyezi Mungu wa kweli?”

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akamuambia:

“Ndiyo.”

Umar (Radhiya Llahu anhu) akamuuliza:

“Sisi si tuko katika haki na adui zetu wako katika batil?”

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akamuambia:

“Ndiyo.”

Umar (Radhiya Llahu anhu) akasema:

“Kwa nini basi tunakubali dini yetu idhalilike?”

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akamuambia:

“Mimi ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, na sitomuasi, na Yeye ndiye mwenye kuninusuru”.

Umar (Radhiya Llahu anhu) akamuuliza tena:

“Si ulituambia kuwa tutakwenda (Makka) na tutatufu penye nyumba?”

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akamuambia:

“Ndiyo, lakini nilikuambia kuwa tutakwenda mwaka huu?”

Umar (Radhiya Llahu anhu) akasema:

“La, sivyo.”

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akasema:

“Hakika utakwenda na utatufu penye nyumba.”.

Kisha Umar (Radhiya Llahu anhu)  akamuendea Abubakar (Radhiya Llahu anhu)  na kumuambia:

“Abubakar, kwani yeye si Mtume wa Mwenyezi Mungu kweli?”

Abubakar (Radhiya Llahu an'hu)  akamuambia:

“Ndiyo.”

Kisha akamuuliza msuali yale yale aliyomuuliza Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) na Abubakar (Radhiya Llahu anhu) akamjibu majibu yale yale aliyojibiwa na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), kisha akamuambia:

“Ewe mwanamume, huyu ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, na hatomuasi, kwa hivyo shikamana naye vizuri."

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alipomaliza kuandikiana mkataba wa Mapatano, akawaambia Masahaba wake:

“Inukeni mchinje kisha nyoweni nywele.”

Alisema hivyo mara tatu na hapana hata Sahaba mmoja aliyeinuka na kufanya kama walivyotakiwa na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam). Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akaingia ndani ya hema lake na baada ya kutoka nje na bila ya kumsemesha yeyote kati yao, akamchinja mnyama wake kisha akamwita kinyozi wake na kunyoa nywele zake.

Masahaba nao (Radhiya Llahu anhum) walipoona vile, wote wakainuka na kuanza kuchinja wanyama wao na kunyoana nywele.

Hiki ni kisa cha Sulhu ya Hudaybiya ambacho Mashia na Masunni wote wanakubaliana kuwa hivi ndivyo ilivyokuwa na haya ndiyo yaliyotokea.

Na hivi ndivyo kilivyoelezwa na maulamaa wa historia kama vile Attabary na Ibni l Athiyr na Ibni Saad na Maulamaa wa hadithi wengineo kama vile Bukhari na Muslim.

Katika kisa hiki ndugu zetu Mashia wanawatuhumu Mashaba kuwa walipinga amri ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) wakakataa kufuata amri pale alipowaambia wachinje na wanyoe na kwamba kuchelewa kufuata amri ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) ni dhambi kubwa sana hasa kwa vile Mwenyezi Mungu anasema:

“Naapa kwa (haki ya) Mola wako. Wao hawawi wenye kuamini (kweli kweli) mpaka wakufanye (wewe ndiye) hakim (mwamuzi) kati ya yale wanayokhitilafiana, kisha wasione uzito nyoyoni mwao juu ya hukumu uliyoitoa, na wanyenyekee kabisa”.

Annisaa 65

Inaelekea ndugu zetu wanasahau kuwa katika kisa hiki pana sehemu muhimu sana wasiopenda kuizungumzia na hii ni kwa sababu ya kuwachukia kwao Masahaba wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam).

Na sehemu hiyo ni pale Urwa bin Masaood (aliyekuwa miongoni mwa washirikina), alipotamka kuwaambia Maqureshi:

"Huyu Muhammad, (Swalla Llahu alayhi wa sallam) amekupeni fikra nzuri, bora muikubali na muniache mimi nimuendee."

Wakamuambia; ‘Muendee’. Akamuendea na akawa anamsemesha Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akamuambia maneno yale yale aliyomuambia hapo mwanzo.

Urwa, baada ya kuyasikia hayo akasema:

‘Ewe Muhammad unaonaje ikiwa nitawamaliza watu wako wote, (niwauwe), Kwa sababu mimi sioni nyuso, bali naona makundi ya watu waliokuwa tayari kukukimbia na kukuacha peke yako.” (huku akijaribu kutaka kuzichezea ndevu za Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam).

Abubakar (Radhiya Llahu anhu)  akasema:

“Nenda kabusu utupu wa (Mungu wako) Lata. Sisi tumkimbie na kumuacha?”

Urwa akauliza:

“Nani huyu?”

Wakamjibu; “ Huyu ni Abubakar”

Akasema:

"Naapa kwa yule ambaye nafsi yangu ipo mikononi mwake, kama si wema ulionifanyia zamani na mimi mpaka leo bado sijakulipa, basi ningekujibu”.

Kisha akaendelea kumsemesha Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), na kila anapomsemesha hujaribu kuzishika ndevu za Mtume wa Mwenyezi Mungu na Al Mughiyra bin Shuuba (Radhiya Llahu anhu) aliyekuwa amesimama mbele ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akiwa ameshika upanga wake na ngao, humpiga mikono yake kwa mkono wa upanga na kumwambia:

“Ondoa mkono wako na uweke mbali na ndevu za Mtume wa Mwenyezi Mungu wa Mwenyezi Mungu”.

Urwa akaunyanyua uso wake na kuuliza:

“Ni nani huyu?”

Akamjibu: “Mughiyra bin Shuuba.”

Akasema:

“Ah! Haini, mimi bado nakutafuta kwa ajili ya uhaini wako.”

Mughiyra huyu, wakati alipokuwa kafiri alifuatana na kundi la watu akawaua na kuwanyang’anya mali zao kama walivyokuwa wengi wakifanya wakati ule, lakini baadae akatubu na kusilimu.

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akasema:

“Ama Kusilimu kwake nimekukubali, lakini hiyo mali sina haja nayo hata kidogo”.

Kisha Urwa akawa anawatizama Masahaba wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) machoni pao mmoja mmoja.

Kisa akaondoka na kurudi kwa wenzake, akawaambia:

“Wallahi Muhammad huyu hata anapotema mate, basi Sahaba zake wanayapokea kwa mikono yao na kujipaka nayo. Anapotawadha, wanafanya kila njia ili watawadhe kama yeye, anaposema, wote wanazishusha sauti zao chini (ili wamsikilize), na hawamkodolei macho kwa kumtizama moja kwa moja (bali wanamtizama) kwa heshima kubwa.

‘Watu wa aina gani hawa, Wallahi nishawahi kuwatembelea wafalme na nishamtembelea Qaysar (mfalme wa Warumi) na Kisraa (mfalme wa Wafursi) na Annajashi (mfalme wa Wahabeshi), Wallahi sikumuona hata mfalme mmoja anayeheshimiwa kama anavyoheshimiwa Muhammad na Sahibu zake."

 

Hivyo ndivyo Masahaba wanavyomuheshimu Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akishuhudia mmoja katika washirikina.

 

Sehemu hii wao hawaitaji, na hii ni kwa sababu wakiitaja basi ushahidi wao kuwa Mashaba walikuwa waasi ungetoweka.

Masahaba hawakumbishia Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) kwa nia ya kumuasi pale walipochelewa kufuata amri ya kuchinja na kukata nywele, na wala hapana dalili yoyote ile katika hadithi kuwa walikuwa na nia ya kwenda kinyume na maamrisho ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), bali walifanya waliyofanya na kutamka waliyotamka kwa sababu ya kuionea wivu dini yao na kuona uchungu kuwa makafiri wamekubaliwa masharti yao yote, na wakaona kama vile mtu yeyote wa kawaida angeliona, kuwa masharti yaliyokuwemo ndani ya mkataba huo kama kwamba Waislamu wamejidhalilisha. Na hivi ndivyo ilivyokuwa katika dhahiri ya mkataba huo, na wao ni wanadamu wa kawaida, hawapokei wahyi kama Mtume wao (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alivyokuwa.

Masahaba wangelikuwa wamekwenda kinyume na maamrisho ya Mtume wao (Swalla Llahu alayhi wa sallam), vipi basi baada ya tukio hilo ingeteremka aya juu yao isemayo;

"Kwa hakika Mwenyezi Mungu amewapa radhi Waislamu walipofungamana nawe chini ya mti na alijua yaliyomo nyoyoni mwao. Basi akateremsha utulivu juu yao , na akawapa kushinda kwa zama za karibu".

Al Fath – 18

Vipi Mwenyezi Mungu anayejua ya ghaibu na ya dhahiri angeridhika nao na kuwapa ushindi wa katika zama za karibu, kama si kujua Kwake juu ya utiifu wao kwa Mtume wao na ukweli wao juu yake.?

Ili ieleweke vizuri nitanukuu kisa hiki cha Sulhuya Hudaybiya kama ilivyoandikwa katika Sahih Muslim;

 

Katika Sahih Muslim inaelezwa vizuri zaidi ni nani katika Masahaba waliokataa kufuata amri ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam):-

Kutoka kwa Al Bara -a bin Aazib (Radhiya Llahu anhu)  anasema:

“Ilipombidi Mtume wa Mwenyezi Mungu(Swalla Llahu alayhi wa sallam) kuandikiana mkataba wa Sulhu na watu wa Makka kwamba wataruhusiwa kuingia Makka (mwaka ujao) na kubaki hapo siku tatu, na kwamba wasichukue silaha isipokuwa panga na ala zao tu, na asiruhusiwe Muislam yeyote katika watu wa Makka kuondoka nao na kwamba yeyote katika Waislam anayetaka kubaki Makka asizuiliwe. Akamuambia Aly bin Abi Talib:

‘Andika masharti yaliyokubaliwa baina yetu; Bismillahi Rahmani Rahiym, haya yaliyokubaliwa na Muhammad Mtume wa Mwenyezi Mungu ….”

Makafiri wakasema:

“Tungekuwa tunaamini kuwa wewe ni Mtume wa Mwenyezi Mungu basi tungelikufuata. (usiandike hivyo) Bali andika Muhammad bin Abdillah”.

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akamuamrisha Aly afute, lakini Aly akamjibu:

“La wallahi sitofuta”

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akamuambia:

“Nionyeshe mimi wapi ilipoandikwa.”

Akamuonyesha, akafuta na akaandika badala yake ‘Ibnu Abdullah’ badala ya ‘Rasulu Llah’, na akabaki hapo siku tatu.

Muslim

Ikiwa tutatumia mantiki yao ya kulifanya kila tukio baina ya Sahaba (Radhiya Llahu anhu) na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) kuwa ni kutotii amri yake na kwamba hii haijuzu na kwamba huu ni unafiki na uhaini, basi hapa tungemlaumu Aly (Radhiya Llahu anhu) kwa sababu Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alipomtaka afute akajibu:

“Wallahi sitofuta”.

Na kwa njia hii tungefungua mlango kwa kila mtu kuanza kuwashambulia Masahaba (Radhiya Llahu anhu) kuwa ni watu waliokuwa wakimuasi Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam).

Tuwaulize ndugu zetu hapa;

‘Je mtakubali kukifasiri kitendo hiki cha Aly (Radhiya Llahu anhu) kuwa ni kutotii amri za Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam)? Ikiwa wataikubali hukmu hii basi itakuwa wamemhukumia Aly (Radhiya Llahu anhu) pia kuwa ameshindwa kutii amri ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), na kwa ajili hiyo itabidi wamtie katika kundi la Masahaba wenzake wanaodai kuwa huwa hawatii amri za Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam).

Kisha wanasema kuwa Umar (Radhiya Llahu anhu) hakusalimu amri na kutii pale alipotakiwa kufanya hivyo na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), bali alimwendea Abubakar (Radhiya Llahu anhu) na kumuuliza maswali yale yale aliyokuwa akimuuliza Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam):

“Kwani wewe si Mtume wa Mwenyezi Mungu kweli?”.

“Si ulituambia kuwa ………”. Kisha akaendelea kusema:

“Nikafanya mambo siku hiyo”.

Mashia wanasema kuwa hawajui mambo gani hayo, kisha wanaendelea kuwatuhumu Masahaba (Radhiya Llahu anhum) kuwa hawakufuata amri ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) pale walipoambiwa wachinje na kunyoa juu ya kuwakariria mara tatu; wakati wanaelewa kwamba Mwenyezi Mungu ametuamrisha kufuata amri ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam).

 

Majibu:

Hapana shaka yo yote kuwa Umar (Radhiya Llahu anhu) alisalimu amri na kuyakubali maneno ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) isipokuwa tu alionyesha kutoridhika kwake kwa yale yaliyokuwemo ndani ya mkataba ule kwa sababu hakuelewa undani wake wakati ule, hasa tukikumbuka kuwa alimuuliza maswali yale yale Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) kisha Abubakar (Radhiya Llahu anhu) baada ya kuwekewa masharti mazito sana yakiwemo (Mtu ye yote wa Makka atakayesilimu asiruhusiwe kukimbia na kuwafuata watakaporudi Madina).

Kwa sababu hadithi inasema hivi:

“Waislamu walisema Subhanallah, vipi arudishwe kwa washirikina yule aliyesilimu na kukimbilia kwetu?”

Hapo ndipo alipotokea Aba Jundul bin Suheil bin Amr akiwa amefungwa minyororo kwa sababu amekimbia kutoka Makka, akajitupa mbele ya Waislamu na kuwaomba wamchukuwe Madina, mbali na mateso ya Makafiri.

Suheil aliyekuwa kiongozi wa washirikina na pia ni baba yake huyo Aba Jundul akasema:

"Huyu ewe Muhammad ni mtu wa mwanzo ambaye huna budi kumrudisha kwetu."

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akasema:

‘Lakini bado hatukumaliza kutia saini (kutia sahihi) mkataba.’

Suheil akasema:

‘Kwa hivyo hakutokuwa na mapatano yoyote baina yetu’.

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akasema:

‘Nakuomba umruhusu huyu tu’.

Suheil akasema:

‘Sitofanya hivyo’.

Ikambidi Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akubali kuwaache makafiri wale wamchukue, ndipo Abu Jundul aliponyanyua sauti na kusema:

‘Enyi Waislam, mnaniacha nirudishwe kwa Makafiri na mimi ni Muislam mwenzenu nakimbilia kwenu. Hamuoni jinsi gani wameniadhibisha?’

Aba Jundul alikua ameadhibishwa adhabu kali sana na makafiri.

 

Sasa ukiichunguza kauli ya Umar (Radhiya Llahu anhu) pale alipomuuliza Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam):

“Si ulituambia kuwa tutakwenda (Makka) na tutatufu penye nyumba…….nk.?”

Utaona kuwa alimuuliza kwa sababu Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) aliwaambia hapo mwanzo kuwa aliota kuwa wanafanya Umra yeye na Masahaba zake na kutufu Al Kaaba, na Masahaba walipoona mambo yanachelewa wakaona uzito kidogo.

(Fathi l Bari – Sharhi ya Sahihul Bukhari – Juzu ya 5 uk.408).

Kwa ajili hiyo Umar (Radhiya Llahu anhu) alimuendea na kumuuliza Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam). Na hii ni kwa sababu ya Umar (Radhiya Llahu anhu) alitaka kuwaona washrikina wakidhalilika na kuinusuru dini ya Mwenyezi Mungu.

Hata ukiyachunguza masuali yake utaona kuwa hayabebi isipokuwa maana hiyo.

Hapana shaka yoyote kuwa Umar (Radhiya Llahu anhu) alikuwa akiamini kuwa Muhammad (Swalla Llahu alayhi wa sallam) ni Mtume wa Mwenyezi Mungu wa kweli.

Ukiisoma riwaya iliyonukuliwa kutoka kwa Is-haq (Radhiya Llahu anhu) na kutolewa na Imam Bukhari (Fathi l Bari Juz.5 uk.409) inayosema:

“Pale Abubakar (Radhiya Llahu anhu)  alipomuambia Umar (Radhiya Llahu anhu):

“Shikamana naye kwani huyu ni Mtume wa Mwenyezi Mungu wa Mwenyezi Mungu”.

Umar akajibu:

“Mimi nashuhudia kuwa yeye ni Mtume wa Mwenyezi Mungu”.

Na kwa ajili hii Imam Ibni Hajar Al Asqalani anasema:

‘Ni wazi kuwa Umar alipokuwa akiuliza masuali yale, alikuwa na nia ya kutaka kujua hekima ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) kuyakubali masharti yale ili umdhihirikie ukweli na asibabaike. Na mfano wake ni mfano wa kisa chake pale aliposimama mbele ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), wakati Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alipotaka kumsalia mnafiki maarufu aitwae Abdillahi bin Ubay, isipokuwa siku hiyo hakufanya mambo kama aliyoyafanya siku ya Hudaybiya. Kwa hivyo lolote alilotamka siku hiyo atasameheka, bali atapata thawabu kwa ajili yake, kwa sababu alikuwa akifanya Ijtihad”

(Al Fat h- ju. 5 uk 409)

Ni kweli kabisa kuwa Umar (Radhiya Llahu anhu), siku hiyo alikuwa na msimamo wa kutaka kuijua hekima ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) ya kukubali masharti yale ya makafiri, na haya yanadhihirika katika hadithi iliyopokelewa kutoka kwa Imam Muslim akielezea kisa cha Hudaybiya baada ya Umar (Radhiya Llahu anhu) kuuliza masuali.

Hadithi hiyo inasema hivi:

“Kisha ikateremshwa Suratul Fat-h, (Sura ya Ufunguzi), na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akamwita Umar (Radhiya Llahu anhu) na kumsomea sura hiyo. Umar (Radhiya Llahu anhu) akamuuliza Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam):

“Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, huu ndio ufunguzi?”

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akajibu:

“Naam (Ndiyo).”

Umar akafurahi na kuridhika.”

(Muslim na Sharhi yake Juz. 12 Uk.194 (Kitabu cha Jihad na Sira No.1784)

Na ni katika sura hii ya Al Fathi (Ufunguzi), iliteremka kauli Yake Subahanahu wa Taala isemayo:

"Kwa hakika Mwenyezi Mungu amewapa radhi Waislamu walipofungamana nawe chini ya mti na alijua yaliyomo nyoyoni mwao. Basi akateremsha utulivu juu yao , na akawapa kushinda kwa zama za karibu".

Al Fathi  - 18

Na katika Musnad ya Imam Ahmed kutoka kwa Jabir bin Abdillah amesema:

“Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) amesema:

“Hatoingia Motoni kamwe yeyote aliyepigana vita vya Badar na (yeyote) aliyefungamana (na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam)) siku ya Hudaybiya”.

(Musnad Imam Ahmed Juz. 5 No.15262 na hadithi hii imesahihishwa na Sheikh Al Albani katika Silsila Sahiha No.2160).

Mwenyezi Mungu katika aya iliyotangulia anatujulisha juu ya kuridhika kwake na Waislam waliofungamana na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) chini ya mti siku hiyo na anashuhudia kuwa atawaingiza Peponi.

Kwa ajili gani Mwenyezi Mungu atawaingiza Peponi?

Kwa ajili ya usafi wa yaliyomo nyoyoni mwao, na hii ni kauli ya Mwenyezi Mungu na ushahidi Wake Subuhanahu wa Taala katika Sura hiyo.

Sasa vipi tena aje mtu atuambie kuwa hawa ni wanafiki, makafiri na ni watu wa Motoni?

Tufuate maneno ya Mwenye Kujua siri za moyoni na yaliyodhihiri au tufuate kauli za binadamu?

Wengine wanaichukulia ile kauli ya Umar (Radhiya Llahu anhu), aliposema:

“Nilifanya mambo siku hiyo”

Na kauli yake katika hadithi iliyopokelewa kutoka kwa Bukhari na kusimuliwa na Is-haq (Radhiya Llahu anhu) kuwa:

“Umar alikuwa akisema:

‘Niliendelea kutoa Sadaka, Kufunga, Kuswali na kununua watumwa na kuwaacha huru ili Mwenyezi Mungu anisamehe kwa yale niliyotenda siku hiyo, nikiogopa juu ya maneno niliyotamka siku hiyo”.

Na katika hadithi nyingine:

“Kwa ajili yake nilinunua na kuwaacha huru watumwa wengi sana na nilifunga miaka mingi sana”.

(Bukhari – Fathi l Bari – Juz.5 Uk. 408).

Wanazichukulia kauli hizi kama ni dalili kuwa Umar (Radhiya Llahu anhu)  alitamka maneno mabaya sana siku hiyo na wengine wakabuni kauli mbali mbali na kuzinasibisha na Umar (Radhiya Llahu anhu) kuwa alizitamka siku hiyo.

Anayechunguza ataona kuwa kule Kufunga kwake, Kusali, Kutoa Sadaka na Kuwaacha huru watumwa kwa ajili ya kutaka kusamehewa na Mola wake, ni dalili ya UchaMungu wake kwa kuogopa kwake kwa yale masuali aliyokuwa akimuuliza Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), na dalili nyingine ya ucha Mungu wake ni kule kuielekea kwake haki mara anapoitambua ilipo, na kwamba hakutaka isipokuwa Uislam uwe na utukufu mbele ya makafiri na kuwadhalilisha makafiri hao, na haya yote yako wazi kabisa katika hadithi zilizotangulia.

Wengine wanasema:

“Hata hao Waislam wengine pia hawakutii amri ya Mtume wa Mwenyezi Mungu siku hiyo.”

Jawabu:

Tulieleza hapo mwanzo kuwa na Aly (Radhiya Llahu anhu) alikuwepo siku hiyo, na pale Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alipowaambia:

Inukeni chinjeni na nyoeni nywele”, hapana hata Sahaba mmoja aliyeinuka, basi kwa vile hata Aly (Radhiya Llahu anhu) hakuinuka, hii inaleta maana kuwa hata Aly (Radhiya Llahu anhu) hakuridhika na masharti hayo kama vile alivyokuwa Umar bin Khatab (Radhiya Llahu anhu).

Zipo sababu nyingi zilizowafanya Masahaba (Radhiya Llahu anhum) wachelewe kutii amri ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) siku hiyo. Ibni Hajar katika Fat h Juz. 5 Uk. 409 na 410 anasema:

“Inaelekea kwamba Masahaba (Radhiya Llahu anhum) walisubiri kwa kutegemea wasifaridhishiwe amri hiyo, huku wakitamani iteremke aya kutoka kwa Mwenyezi Mungu itakayoubatilisha mkataba huo wa Sulhu, au Aya itakayowahusisha kuingia Makka na kufanya Umra waliyoikusudia. Na hii ni kwa sababu wakati huo zilikuwa zikiteremka aya za kufuta ‘Nas'kh’.

Huenda pia pale walipotakiwa wachinje na kunyoa walikuwa wamezama katika kutafakari juu ya hali zao kwa mshangao waliopigwa nao wakihisi kuwa wamedhalilishwa na makafiri hasa kwa vile wao walikuwa na nguvu za kutosha kuweza kuingia Makka na kufanya Umra.

Au huenda ikawa walichelewa kutii amri hiyo wakidhani kuwa amri waliyopewa haikubeba maana ya kulazimika kuitimiza hapo hapo, na hivi ndivyo ilivyo, kuwa zipo dalili nyingi zinazowapa Masahaba (Radhiya Llahu anhum) kila aina ya udhuru wa kuchelewa kufuata amri hiyo”.

Mfano wake ni mfano wa vita vya kuuteka mji wa Makka vilivyokuwa katika Mwezi wa Ramadhani, pale walipotakiwa kufungulia Saumu zao, na walipochelewa kufungulia kwa kufikiria kuwa huenda amri hiyo ikawa ni hiari na sio lazima kwao. Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akaamrisha aletewe birika na kunywa mbele yao. Masahaba (Radhiya Llahu anhum)  walipomuona akinywa, nao pia wakanywa.

(Bukhari).

Hizi ni sababu mbali mbali walizoziweka Maulamaa katika kutoa udhuru wa kuchelewa kwa Masahaba (Radhiya Llahu anhum) kunyoa na kuchinja, pale walipotakiwa na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) kufanya hayo. Lakini mara Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alipotoka na kuanza kunyoa na kuchinja mnyama wake, Masahaba wote (Radhiya Llahu anhum) wakafanya kama alivyofanya Mtume wao (Swalla Llahu alayhi wa sallam) bila kuchelewa.

 

Tukio la siku ya Alkhamis

Mashia wanasema kuwa hiyo ndiyo siku ambayo Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alitaka kumchagua Aly (Radhiya Llahu anhu)  awe ndiye Imam wa Waislam baada ya kufa kwake. Wakazua mengi kutokana na yaliyotokea siku hiyo wakijaribu kuuthibitisha uongo wao huo.

Wanasema hivi:

“Masahaba wote walikuwepo nyumbani kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) siku ya Alkhamis, siku tatu kabla ya kufariki kwake, na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akasema:

“Leteni kidawati na kalamu nikuandikieni maneno yatakayokukingeni na upotovu baada yangu”.

Umar akasema: “Mtume wa Mwenyezi Mungu anasema bila fahamu (hii ni kauli ya Mashia). Munayo Qurani, kinatutosha kitabu cha Mwenyezi Mungu”.

Masahaba wakaasi amri, na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), akuwafukuza nyumbani kwake bila ya kuwaandikia chochote”.

Katika vitabu vyao, wanakielezea kisa hiki kwa ufupi na kwa kubadilisha badilisha maneno.

Katika vitabu vingine wanasema:

Ibni Abbas (Radhiya Llahu anhum) alisema:

“Siku ya Alkhamisi, na kipi kitakachokujulisha hiyo siku ya Al Khamis, siku hiyo maumivu yalimzidi Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), akasema:

“Ngojeni nikuandikieni maandishi, hamtopotoka baada yake”.

Umar  akasema:

“Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) anasema bila fahamu, na tunayo Qurani, kinatutosha kitabu cha Mwenyezi Mungu.”

Wakakhtilafiana na watu wa nyumba ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Laahu alayhi wa sallam) na kukasirikiana, na kwamba wapo waliokuwa wakisema:

“Jisogezeni ili aandike yale ambayo baada yake hamtapotea tena”

Na wapo waliokuwa wakisema yale aliyosema Umar. Na mazungumzo na khitilafu zilipozidi, Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akawaambia:

“Ondokeni karibu yangu”.

Ibni Abbas akawa anasema:

“Msiba wa kweli hasa ni kule Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) kutoweza kuwaandikia maandishi yale kutokana na kukhitilafiana kwao”.

Tukio hili lilitokea kweli na limenukuliwa na Maulamaa wa Kishia pamoja na Maulamaa wa Kisunni, kwa hivyo halina shaka yoyote kuwa lilitokea.

Mashia wanajaribu kulifasiri tukio hili kama kwamba jambo jipya litakalokata mzizi wa fitna baina ya Waislam ambalo Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) siku hiyo alitaka kuwaandikia Masahaba (Radhiya Llahu anhum), ni usia wa kumchagua Ali (Radhiya Llahu anhu) kuwa Khalifa wa Waislam baada ya kufa kwake na kwamba Umar (Radhiya Llahu anhu) aliyajua hayo, ndio maana akawaambia watu kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) hajui nini anasema na kwamba tunayo Qurani inatutosha.

 

Atakayeichunguza hadithi hii kwa njia zake zote zilizopokelewa ataona kuwa ndugu zetu wanajaribu kuchanganya maneno na kuacha maneno.

Kwa mfano, katika hadithi iliyotolewa na Bukhari katika Kitabu cha Al Maghazi hadithi Nambari 4168 inasema hivi:-

“Wakasema: Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) hana fahamu juu ya anayoyasema, jamani hebu msikilizeni vizuri." wakamuendea huku wakimuuliza.

Akawaambia:

“Niacheni, maana haya niliyonayo ni bora kuliko mnayoniitia”, kisha akawausia mambo matatu; akasema:

“Watoeni washirikina nje ya Bara ya Arabu na wapokeeni vizuri wageni kama nilivyokuwa nikiwapokea”. (kisha msimulizi wa hadithi hii Ibni Abbas, hakusema juu ya jambo la tatu au alisema; ‘nimelisahau’)”

Sahih Bukhari (Kitabul Maghazi)

Anasema Imam Annawawiy:

“Itikadi ya kila Muislam kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) hawezi kusema neno la uongo wala hawezi kubadilisha yale aliyotakiwa kutufikishia ikiwa yu mgonjwa au mzima na afya yake. Na iwapo tushayajua hayo, basi inatubainikia kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) angekuwa ametumwa na Mola wake kutufikishia jambo, basi lazima atatufikishia akiwa anaumwa au akiwa na afya yake.

Na kwa ajili hiyo angekuwa ametumwa kutufikishia jambo la lazima ambalo baada yake hatutopotoka, basi hata Waislam wangekhitilafiana namna gani, lazima angelifikisha neno hilo., na hii inatokana na kauli Yake Subhanahu wa Taala pale aliposema:

“Wafikishie yale uliyofunuliwa” (Balligh maa unzila ilayka)."

 

Kama vile alivyokuwa hakuacha kuyafikisha aliyoteremshiwa kabla ya hapo juu ya inadi, mateso, inda na zogo alokuwa akifanyiwa na makafiri.

Kutokana na sababu hizi inatubainikia kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alikuwa anataka kuwaandikia juu ya mwenendo mzuri wa kuufuata na siyo amri iliyowajibika.

Kwa sababu Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) baada ya tukio hilo aliishi siku nne nyingine, na katka siku zote hizo hakuwaamrisha tena wamletee kitabu na kalamu.

Kisha katika riwaya, pana kauli isemayo:

“Akawausia mambo matatu”.

Na hii ni dalili kuwa aliyotaka yaandikwe ni usia na si amri, kwa sababu angetaka kuandika maamrisho basi asingeacha kwa sababu ya kukhitilafiana kwa Masahaba (Radhiya Llahu anhum). Na Mwenyezi Mungu angemtia adabu yule aliyekuwa kizuizi katika kuifikisha amri hiyo. Na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) angeliifikisha hata kwa matamshi kama alivyowausia wakati wa maradhi yake juu ya kuwaondoa washirikina na wenye mfano wao.

 

Katika riwaya zao wanasema kuwa eti siku hiyo Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alikasirka sana na Masahaba (Radhiya Llahu anhu) .

Atakayechunguza maneno aliyotamka Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) wakati ule, ataona kuwa hapakuwa na dalili yoyote kuwa alikasirika nao, isipokuwa tu pale alipoona maradhi yanamzidi akawataka waondoke. Na yanabainika haya zaidi pale Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alipowausia juu ya mambo yale matatu.

Hata tukichukulia kwa ajili ya mjadala kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alikasirika nao, hii haina maana kuwa daraja yao mbele ya Mtume wao imepungua, kwani wao ni wanadamu, wanaweza kufanya kosa la kumkasirisha Mtume wao wakati wowote. Bali kinyume cha hivyo huenda kukasirika kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) juu yao (kama kweli amekasirika) kukawa ni kheri kwao, kwa sababau katika hadithi iliyotolewa na Bukhari, anasema Abu Huraira (Radhiya Llahu anhu) kuwa alimsikia Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akisema:

“Mola wangu! Muislam yeyote niliyemtukana, basi mjaalie tusi hilo liwe ni kurubisho lake kwako siku ya Kiama”.

Bukhari Mlango wa Daawat – hadithi nambari 6000

Na kutoka kwa Attabarani katika Al Kabeer na Imam Ahmed katika Musnad yake imepokelewa kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) amesema:

“…….Yeyote katika umati wangu niliyemtukana au kumlani wakati nimeghadhibika, kwani mimi ni katika wana wa Adam, ninaghadhibika kama wanavyoghadhibika isipokuwa mimi nimeletwa niwe Rehema kwa walimwengu. Kwa hivyo mjaalie (matusi yangu wakati wa ghadhabu zangu hizo) yawe shifaa kwake siku ya Kiama".

Attabarani, Ahmed na Abu Daud

Iwapo wao wanaona kuwa pale Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) anapomkasirikia mtu, basi mtu huyo anageuka kuwa mnafiki au kafiri, kama wanavyoelezea katika vitabu vyao. Basi siku moja Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alimkasirikia Sayiduna Aly (Radhiya Llahu anhu), sasa naye pia wanaweza kumpa sifa kama hizo? (Astaghfirullah).

Imepokelewa kutoka kwa Bukhari katika hadithi iliyosimuliwa na Imam Aly (Radhiya Llahu anhu) kuwa usiku mmoja Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alipita nje ya nyumba yao akawagongea na kuwauliza:

“Mbona hamsali?”

Anasema Aly (Radhiya Llahu anhu), nikasema:

“Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, nafsi zetu zimo mikononi mwa Mwenyezi Mungu, angetaka tuamke tungeamka”.

Aly (Radhiya Llahu anhu)  anasema:

“Nilipomuambia vile, Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akaondoka bila kunijibu huku akilipigapiga paja lake na kusema:

“Wa kaan l insaanu ak' thara shay in jadala”.

“Binadamu kwa ubishi hawezekani”

Bukhari mlango wa Tahajjud – Hadithi nambari 1075

 

Sasa hapa watasema nini juu ya Imam Aly (Radhiya Llahu anhu) ambaye ni Imam wao wa mwanzo aliyekingwa (asiyekosea) na Khalifa wa nne wa Waislam?

Wanapoambiwa kuwa sababu iliyomfanya Umar (Radhiya Llahu anhu) kutaka Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) asiandike wakati ule ni baada ya kumuona kuwa alikuwa taabani sana, wao (Mashia) hushangaa na kubisha.

Tunawauliza;

“Umar  (Radhiya Llahu anhu) ambaye ni Al Farook wa Umma huu (Mwenye kutenganisha haki na batil), na hii ni sifa aliyopewa na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), na ni mbora wa Masahaba baada ya Abubakar (Radhiya Llah anhu), hivyo mnataka kusema kuwa alikusudia kumuudhi Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam)?"

Wallahi hayasemi haya isipokuwa yule aliyechagua ujinga kuwa ni muongozo wake na ujahili kuwa ni Mantiki yake.

Hasa pale tunaposoma katika hadithi kuwa:

"Alizidiwa na maradhi".

Si hivyo tu, bali ilimbainikia Umar (Radhiya Llahu anhu) kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) hakukusudia kufaridhisha kitu, bali alikusudia kupendekeza tu.

Mfano wake ni mfano wa usiku ule wakati Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alipomwamsha Aly (Radhiya Llahu anhu) na kumtaka aswali. Ilimbainikia Ali (Radhiya Llahu anhu) kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) hakutaka kumfaradhishia jambo, bali alikusudia kupendekeza tu tendo lile, ndiyo maana akajitetea kwa kusema kuwa hakujaaliwa kuamka.

 

ITAENDELEA INSHAALLAH

ثانياً: الرد على التيجاني في موقفه من الصحابة في رزيَّة يوم الخميس:

يقول التيجاني (( ومجمل القصة أن الصحابة كانوا مجتمعين في بيت رسول الله قبل وفاته بثلاثة أيام فأمرهم أن يحضروا له الكتف والدواة ليكتب لهم كتابا يعصمهم من الضلالة، ولكن الصحابة اختلفوا ومنهم من عصى أمره واتهمه بالهجر، فغضب رسول الله وأخرجهم من بيته دون أن يكتب لهم شيئا، وإليك شيئا من التفصيل، قال ابن عباس: يوم الخميس وما يوم الخميس اشتد برسول الله وجعه، فقال: هلم أكتب لكم كتابا لا تضلوا بعده، فقال عمر إن النبي قد غلبه الوجع، وعندكم القرآن حسبنا كتاب الله، فاختلف أهل البيت واختصموا، منهم من يقول قربوا يكتب لكم النبي كتابا لا تضلوا بعده، ومنهم من يقول ما قال عمر، فلمّا أكثروا اللغو والإختلاف عند النبي، قال لهم رسول الله (ص) قوموا عني، فكان ابن عباس يقول: إن الرزيّة كل الرزيّة ما حال بين رسول الله وبين أن يكتب لهم ذلك الكتاب من اختلافهم ولغطهم، هذه الحادثة صحيحة لا شك فيها، فقد نقلها علماء الشيعة ومحدثوهم في كتبهم، كما نقلها علماء السنة ومحدثوهم ومؤرخوهم، وهي ملزمة لي على ما ألزمت به نفسي، ومن هنا أقف حائراً في تفسير الموقف الذي وقفه عمر بن الخطاب من أمر رسول الله، وأي أمر هو؟ أمر عاصم من الضلالة لهذه الأمة، ولا شك أن هذا الكتاب فيه شيء جديد بالنسبة للمسلمين سوف يقطع عليهم كل شيء ... ثم يتابع فيقول ... ولنترك قول الشيعة بأن الرسول أراد أن يكتب إسم علي خليفة له، وتفطن عمر لذلك فمنعه فلعلهم لا يقنعوننا بهذا الزعم الذي لا يرضينا مبدئياً ولكن هل تجد تفسيراً لهذه الحادثة المؤلمة التي أغضبت الرسول حتى طردهم وجعلت ابن عباس يبكي حتى يبلَّ دمعه الحصى ويسميها رزية، أهل السنة يقولون بأن عمر أحس بشدة مرض النبي فأشفق عليه وأراد أن يريحه، وهذا التعليل لا يقبله بسطاء العقول فضلاً عن العلماء، وقد حاولت مراراً وتكراراً التماس بعض الأعذار لعمر ولكن وقع الحادثة يأبى علـي ذلك، وحتى لو أبدلت كلمة يهجـر ( والعياذ بالله ) بلفظة ( غلبه الوجع ) فسوف لن نجد مبرراً لقول عمر ( عندكم القرآن ) حسبنا كتاب الله، أوكان هو أعلم بالقرآن من رسول اللـه الذي أنزل عليه، أم أن رسول اللـه لا يعي ما يقول (حـاشـاه) أم أنـه أراد بأمـره ذلك أن يبعث فيهـم الاختـلاف والفـرقة  أستغفـر الله ))(1).

وللرد على ما سبق أقول:

1ـ خلط التيجاني في هذا الحديث يبن أكثر من رواية مختلفة فقد ذكر أن الصحابة اتهموا النبي صلى الله عليه وآله وسلم ( بالهجر ) وفي الحديث الذي ذكره في كتابه لا وجود لهذه الكلمة وفي الحديث أيضاً نقل قول ابن عباس ( يوم الخميس وما يوم الخميس اشتد برسول الله وجعه ) فهذه الجملة ليست من الحديث المذكور والذي يعزوه للبخاري في بـاب المـرض ( بـاب قول المـريض قـوموا عني  ) بهـامش كتـابه ولكنـها وكلمـة ( يهجر ) جزء من رواية أخرى تجاهلها هذا التيجاني لأنها توضح أموراً هامة في هذه الحادثة وهي رواية سعيد ابن جبير قال (( قال ابن عباس: يوم الخميس وما يوم الخميس، اشتد برسول الله صلى الله عليه وآله وسلم وجعه فقال: ائتوني أكتب لكم كتاباً لن تضلوا بعده أبداً، فتنازعوا، ولا ينبغي عند نبي نزاع، فقالوا ماشأنه؟ أهجر، استفهموه، فذهبوا يَرُدُّون عليه، فقال: دعوني، فالذي أنا فيه خيرٌ مما تدعونني أليه، وأوصاهم بثلاث قال: أخـرجوا المشركين من جزيرة العرب، وأجيزوا الوفد بنحو ما كنت أجيزهم، وسكت عن الثالثة أو قال فَنَسِيتُها ))(2).

2ـ إذا أراد هـذا التيجـاني  أن يفسر  أحاديث المصطفى صلى الله عليه وآله وسلم لقلب الموازين، فالكاتب الفاضل يدعي أن الرسول صلى الله عليه وآله وسلم أراد  أن يكتب لهم كتاباً يعصمهم من ( الضلالة )! هكذا بإطلاق، ومعلوم أن للضلالة معاني مختلفة، والصحيح أن النبي صلى الله عليه وآله وسلم بقوله ( لن تضلوا بعده  ) فإنه يخصه بأمر محدد كأن ينص على تعيين خليفة أو كتابة كتاب في الأحكام ليرتفع النزاع في الأمة وإلا فبالله كيف يترك النبي صلى الله عليه وآله وسلم أن يكتب أمراً يعصم الأمة به من الضلالة؟! فإن دل هذا على شيء فإنه يدل على أن الأمر ليس للوجوب فتركه.

3ـ يجب أن يعتقد كل مسلم (( أن النبي صلى الله عليه وآله وسلم معصوم من الكذب ومن تغيير شيء من الأحكام الشرعية في حال صحته وحال مرضه ومعصوم من ترك بيان ما أمر ببيانه وتبليغ ما أوجب الله عليه تبليغه ))(3) فإذا عرفنا ذلك تبين لدينا أنه لو أمر بتبليغ شىء حال مرضه وصحته فإنه يبلغه لامحالة  فــ(( لو كان مراده صلى الله عليه وآله وسلم أن يكتب مـالا يستغنون عنه لم يتركـه لاختلافهم ولا لغيره، لقوله تعالى { بلغ ما أنزل إليك } كما لم يترك تبليغ غير ذلك لمخالفة من خـالفه ومعاداة من عاداه ))(4) فدل ذلك على أن ما أراد النبي صلى الله عليه وآله وسلم كتابته يحمل على الندب لا على الوجـوب وقد عـاش صلوات الله وسلامه عليه أربعة أيام بعـد ذلك ولم يأمـرهم بإعـادة الكتابة، وقوله في الرواية التى أخفاها الكاتب ( وأوصاهم بثلاث ) يدل على أن الذى أراد أن يكتبه لم يكن أمراً محتّماً لأنه لو كان مما أمر بتبليغه لم يكن يتركه لوقوع الاختلاف، ولعاقب الله من حـال بينه وبين تبليغه، ولبلغه لهـم لفظاً كما أوصاهم بإخـراج المشركين وغير ذلك(5).

4- أمّا ادعاؤه بقوله ( ولكن هل تجد تفسيراً معقولاً لهذه الحادثة المؤلمة التي أغضبت الرسول حتى طردهم )،   قلت:

لم يظهر على النبي صلى الله عليه وآله وسلم أي غضب على صحابته أو أمر بطردهم (هكذا ) ولم يرد هذا المعنى في أيٍ من روايات الحديث السبع التي ذكرها البخاري في صحيحه، ولكنه لشدة إحساسه بالمرض طلب منهم الكف عن الجدال فيما بينهم، ويظهر هذا واضحاً في الرواية التي أوصاهم فيها بثلاثة أمور وذلك بعد جدالهم فلا دليل على أنه غضب منهم أو طردهم ولو فرضنا جدلاً أنه غضب منهم فليس في هذا قدح بهم لأنهم ليسوا معصومين من الوقوع بذلك والرسول صلى الله عليه وآله وسلم يغضب ويرضى بل لعل غضبه على أصحابه يكون خيراً لهم فقد أخرج البخاري في صحيحه عن أبي هـريرة رضي اللـه عنه أنه سمع النبي صلى الله عليه وآله وسلم يقول (( اللهم فأيما مؤمن سببته فاجعل ذلك له قربة إليك يوم القيامة ))(6) وروى الطبراني في الكبير وأحمد في المسند قوله صلى الله عليه وآله وسلم في جزء من الحديث (( أيما رجل من أمتي سببته سُبة أو لعنته لعنة في غضبي فإنما أنا من ولد آدم، أغضب كما يغضبون، وإنما بعثني رحمة للعالمين فاجعلها عليهم صلاة يوم القيامة ))(7) ثم أقول لهذا التيجاني ( المهتدي ) إذا لم تستطع أن تجد تفسيراً معقولاً ( لغضب ) النبي صلى الله عليه وآله وسلم على الصحابة كما تدعي فأقول لك أخرج البخاري عن علي بن أبي طالب قوله (( أن رسول الله صلى الله عليه وآله وسلم طرقه وفاطمة بنت النبي عليه السلام ليلة فقال: ألا تصليان؟ فقلت: يارسول الله أنفسنا بيد الله، فإذا شاء أن يبعثنا بعثنا، فانصرف حين قلت ذلك ولم يرجع إليّ شيئاً، ثم سمعته وهومول يضرب فخذه وهـو يقول { وكـان الإنسان أكثر شيء جدلا }))(8)! فهل يجد التيجاني تفسيراً معقـولاً لمخـالفة  (علي) أمر الرسول صلى الله عليه وآله وسلم واحتجـاجه بالقـدر حتـى جـعل النبي صلى الله عليه وآله وسلم يضرب علـى فخـذه ويقول معترضاً ( وكان الإنسان أكثر شيء جدلا ) فإن وجد تفسيراً معقولاً لجدال علي ففعل الرسول صلى الله عليه وآله وسلم لجدال الصحابة معقول جداً؟!

5ـ أما عن بكاء ابن عباس حتى بل دمعه الحصى وتسميته ذلك رزيّة فلست أدري والله ما الحجة التي فيه على أهل السنة فابن عباس كان يقول ذلك عندما يروي الحديث وليس عندما حدثت الحادثة، والروايات كلها تدل على ذلك ويحتمل أنه تذكر وفاة النبي صلى الله عليه وآله وسلم فزاد في حزنه بالإضافة إلى أن عدم كتابة الكتاب كان هذا رزية في حق من شك في خلافة أبي بكر فلو كتب الكتاب لزال الشك وكذلك سمـى تلك الحادثة رزية لأن ابن عباس كان ممن وافق على ترشيح أبـي بكر، وعلـى كل حـال إذا اعتقد أحـد أن قول ابن عباس حـق في خـلافه مع عمـر فأقـول لا شك عندنا أن عمر كان أفقه من ابن عبـاس والحمد اللـه.

6ـ وقوله ( أهل السنة يقولون بأن عمر أحس بشدة مرض النبي فأشفق عليه وأراد أن يريحـه، وهـذا التعليل لا يقبله بسطاء العقـول فضلاً عن العلماء )

فأقـول:

سبحان الله على هذا العقلاني فإذا كان قول العلماء أن عمر أراد إراحة النبي صلى الله عليه وآله وسلم تعليل لا يقبله بسطاء العقول؟! فهل القول بأن عمر وهو فاروق الأمة ومن خيرة الصحابة بعد أبي بكر تعمد إيذاء الرسول صلى الله عليه وآله وسلم واتهامه بالهجر تعليل يقبله عظماء العقول يا تيجاني؟! فوالله لا يقول هذا إلامن جعل الجهل منهجه وطريقه، ولا شك لدينا أن هذا التعليل مقبول منطقياً خصوصاً إذا عرفنا أنه في الحديث اشتد برسول الله صلى الله عليه وآله وسلم وجعه، ولكن ليس هذا هو السبب وحده الذي جعل عمر يقول ما قال بل لأنه ظهرت لديه قرينة تدل على أن الرسول صلى الله عليه وآله وسلملم يجزم بالكتابة فقال ما قال وهذا من اجتهاده،..كما تبين لعلي عندما دعاه النبي صلى الله عليه وآله وسلم  للصلاة فاحتج بالقدر لأنه تبين أن النبي عليه السلام لم يقل هذا على سبيل الجزم أى بالوحي، والكاتب يدعي أن أهل السنة يتعللون عن عمر بأنه أراد أن يريح النبي صلى الله عليه وآله وسلم شفقة عليه وبما أنه نقل جزءاً من كلام أهل السنة مبتوراً فسأضطر لنقل بعض من أقوال علماء أهل السنة ليظهر للقارئ مدى قوة حجج أهل السنة في تعليل موقف عمر ومدى الفرق بين تعليل جاهل مفرط في جهله وبين عالم راسخ في علمه، يقول المازري عن هذه الحادثة (( إنما جاز للصحابة الاختلاف في هذا الكتاب مع صريح أمره لهم بذلك لأن الأوامر قد يقارنها ما ينقلها من الوجوب، فكأنه ظهرت منه قرينة دلت على أن الأمر ليس على التحتم بل على الاختيار فاختلف اجتهادهم، وصمم عمر على الامتناع لما قام عنده من القرائن بأنه صلى الله عليه وآله وسلم قال ذلك عن غير قصد جازم، وعزمه صلى الله عليه وآله وسلم  كان إما بالوحي وإما بالاجتهاد وكذلك تركه إن كان بالوحي فبالوحي وإلا فبالاجتهاد أيضاً....))(9)

 وقال الإمام البيهقي في أواخر كتابه  دلائل النبوة (( إنما قصد عمر التخفيف على رسول الله صلى الله عليه وآله وسلم حين غلبه الوجع ولو كان مراده صلى الله عليه وآله وسلم  أن يكتب ما لايستغنون عنه لم يتركه لاختلافهم ولا لغيره لقوله تعالى { بلغ ما أنزل إليك } كما لم يترك تبليغ غير ذلك لمخالفة من خالفه ومعاداة من عاداه وكما أمر في ذلك الحال بإخراج اليهود من جزيرة العرب وغير ذلك مما ذكره في الحديث ))(10) ويقول الإمام القرطبي (( ائتوني أمر، وكان حق المأمور أن يبادر للإمتثال لكن ظهر لعمر رضي الله عنه مع طائفة أنه ليس على الوجوب، وأنه من باب الإرشاد للأصلح فكرهوا أن يكلفوه من ذلك مايشق عليه في تلك الحالة مع استحضارهم قوله تعالى { ما فرطنا في الكتاب من شيء } وقوله تعالى { تبياناً لكل شيء } ولهذا قال عمر: حسبنا كتاب الله، وظهر لطائفة أخرى أن الأولى أن يكتب لما فيه من زيادة الإيضاح، ودلّ أمره لهم بالقيام على أن أمره الأول كان على الاختيار، ولهذا عاش صلى الله عليه وآله وسلم بعد ذلك أياماً ولم يعاود أمرهم بذلك ولو كان واجباً لم يتركه لاختلافهم لأنه لم يترك التبليغ لمخالفة من خالف، وقد كان الصحابة يراجعونه في بعض الأمور مالم يجزم بالأمر فإذا عزم امتثلوا ))(11)

 وقـال الخطابي (( لم يتوهم عمر الغلط فيما كان النبي صلى الله عليه وآله وسلم يريد كتابته، بل امتناعه محمول على أنه لما رأى ما هو فيه من الكرب وحضور الموت خشي أن يجد المنافقون سبيلاً إلى الطعن فيما يكتبه وإلى حمله على تلك الحـالة التي جرت العـادة فيها بوقوع بعض مايـخالف الاتفاق فكان ذلك سبب توقف عمر، لا أنه تعمد مخالفة النبي صلى الله عليه وآله وسلم ولا جواز الغلط عليه حاشا وكلا ))(12)

 ويقول النووي في شرحه لمسلم (( أما كلام عمر رضي الله عنه فقد اتفق العلماء المتكلمون في شرح الحديث على أنه من دلائل فقه عمر وفضائله ودقيق نظره، لأنه خشي أن يكتب صلى الله عليه وآله وسلم أموراً ربما عجزوا عنها واستحقوا العقوبة عليها لأنها منصوصة لامحالة للاجتهاد فيها فقال عمر: حسبنا كتاب اللـه لقوله تعالى { مافرطنا في الكتاب من شيء } وقوله تعالى { اليوم أكملت لكم دينكم } فعلم أن اللـه تعالى أكمل دينه فأمن الضلالة على الأمـة وأراد الترفيه على رسول الله صلى الله عليه وآله وسلم فكان عمر أفقه من ابن عباس وموافقيه ))(13) ومما يدلل على فقه وعلم عمر ما رواه مسلم في صحيحه عن عائشة أن النبي صلى الله عليه وآله وسلم قال (( قـد كان في الأمم قبلكم محدثـون، فـإن يكن في أمتي أحد فعمر ))(14)

 وعن أبي سعيد الخدري قال: قال رسول الله صلى الله عليه وآله وسلم (( بينما أنا نائم رأيت الناس يعرضون علي وعليهم قمص، منها مايبلغ الثدي، ومنها ما يبلغ دون ذلك، ومر عمر بن الخطاب وعليه قميص يجره. قالوا: ماأولت ذلك يارسول الله؟ قال الدين ))(15)

 وأخرج البخاري في صحيحه عن ابن عمر أن النبي صلى الله عليه وآله وسلم قال ((بينما أنا نائم إذ رأيت قدحاً أتيت به فيه لبن فشربت منه حتى أني لأرى الرَّيَّ يخرج من أظافري، ثم أعطيت فضلي عمر بن الخطاب فقالوا: فما أولته يارسول الله؟ قال العلـم ))(16)

 وهذا علي بن أبي طالب يمدح عمر بن الخطاب ويشهد بعدالته واستقـامته وذلك من كتاب الإمامية الحجة ( نهج البلاغة ) الذي جمعـه إمامهم (الشريف الرَّضى ) حيث يقول في جزء من خطبته (( ووليهم والٍ فأقام واستقام حتى ضرب الدين بجرانه ))(17) ويقول ابن أبي الحديد الشيعي شارح نهج البلاغة ((...هذا الوالي هو عمر بن الخطاب ))(18)

 فأقول للتيجاني المهتدي كما يقول الشاعر:

وكم من عائبٍ قولاً صحيحاً..........وآفته من الفهم السقيم.

7ـ وقـوله ( وحتـى لـو أبدلت كلمة يهجـر ـ والعياذ باللـه ـ بلفظة غلبـه الوجـع فسوف لـن نجـد مبرراً لقـول عمر ـ عندكم القرآن ـ حسبنا كتاب الله ) فأقول:

لا يوجد في أي من روايات الحديث بأن قائل هذه الكلمة هو عمر فقوله أنه لو أبدل كلمة ( يهجر ، بغلبه الوجع ) إيهام من هذا التيجاني بأن عمر القائل غلبه الوجع قد قال أيضا بأنه يهجر وهذا من الكذب البين على عمر لفروق المعنى بين الكلمتين ومن يجـد الكاتب وهو يقول وحتى لو أبدلت كلمة يهجر( والعيـاذ بالله ) يظن أنه أكثر ورعـاً وتورّعا من صحابة رسول الله صلى الله عليه وآله وسلم فيالسخافاته الجاهلية !! .

وأما بالنسبة لكمة ( أهَجَرَ ) فإنها جاءت بصيغة الجمع وسبب قولهم ذلك إنكاراً لمن قال لاتكتبوا فقالوا كيف نتوقف هل تظن أنه كغيره يقول الهذيان في مرضه ثم قالوا: إستفهموا للإنكار، وإن فرض صدور هذا الكلام عن بعضهم فلعل أحدهم اشتبه عليه الأمر فشك في ذلك لأنه ليس معصوماً والشك جائز عليه ولكن يستبعد ذلك لأنه لا بد أن ينكره الباقون، أو لعل قائل هذا القول هو من قرب دخوله في الإسلام  أو أن أحدهم أصيب بالحيرة لدى مشاهدته النبي  في حالته هذه فقال ما قال و (( الهجر في اللغة هو اختلاط الكلام بوجه غير مفهِم وهو على قسمين: قسم لا نزاع لأحد في عروضه للأنبياء عليهم السلام وهو عدم تبيين الكلام لبحَّة الصوت وغلبة اليبس بالحرارة على اللسان كما في الحميات الحارة، وقد ثبت بإجماع أهل السير أن نبينا صلى الله عليه وآله وسلم كانت بحة الصوت عارضة له في مرض موته صلى الله عليه وآله وسلم، والقسم الآخر جريان الكلام غير المنتظم أو المخالف للمقصود على اللسان بسبب الغشي العارض بسبب الحميات المحرقة في الأكثر، وهذا القسم وإن كان ناشئاً من العوارض البدنية ولكن قد اختلف العلماء في جواز عروضه للأنبياء، فجوزه بعضهم قياسا على النوم، ومنعه آخرون، فلعل القائل بذلك القول أراد القسم الأول، يعني أنَّا نرى هذا الكلام خلاف عادته صلى الله عليه وآله وسلم فلعلنا لم نفهم كلامه بسبب وجود الضعف في ناطقته فلا إشكال ))(19) فعلى العموم كل ما صدر عن الصحابة من أقوال لا تفيد الطعن بالنبي صلى الله عليه وآله وسلم بيقين وليس فيها ما يقدح بعدالتهم.

8ـ وقوله (( أوكان هو أعلم بالقرآن من رسول الله.....الخ )) فقوله هذا لا يدل إلا على جهله المركب لأن قول عمر حسبنا كتاب الله هو رد على من نازعه لا رداً على رسول الله صلى الله عليه وآله وسلم بالإضافـة إلى أنـه تبين لديه أن الرسـول صلى الله عليه وآله وسلم لم يجـزم على الكتـابة فقال عمر قولته اعتماداً على قوله { اليوم أكملت لكم دينكم } وقوله { ما فرطنا في الكتاب من شيء } وهذا كما بينت سابقاً يدل على عميق فقهه وعلمه، والرسول صلى الله عليه وآله وسلم يعي ما يقوله هو وما يقوله عمر، لذلك لم ينكر عليه قالته تلك تدليلاً على استصوابه ويعلم النبي صلى الله عليه وآله وسلم أن هذا لن يبعث فيهم الاختلاف والفرقة وهو ما حدث بالفعل فقد رشح المسلمون ( أبا بكر الصديق ) فقطع الخلاف وكتب الله لصحابته في عهد أبي بكر حب الإئتلاف وبغض الاختلاف.

ثم يقول التيجاني ( ثم لو كان تعليل أهل السنة صحيحاً، فلم يكن ليخفى على رسول الله حسن نية عمر، ولشكره رسول الله على ذلك وقربه بدلاً من أن يغضب عليه ويقول أخرجوا عني ) أقول: يأبى هذا التيجاني إلا أن يبرهن على سوء فهمه وقلة حيلته فيعيد كلامه تكراراً ولله در القائل:

إذا لم يكن لك حسن فهم............أسأت إجابةً وأسأت فهماً!؟

فلو كانت حججك العقلانية صحيحة أن تقول سكوت النبي صلى الله عليه وآله وسلم  على قول عمر ثم توقفه عن الكتابة يدل على موافقته له، ثم يجازف نحوياً فيقول ( بدلاً من أن يغضب عليه ويقول أخرجوا عني ) عجباً فالهاء في ( عليه ) عائدة على عمر والواو في (أخرجوا ) واو الجمع فكيف تستقيم الجملة هكذا؟ فالأصل أن يقال ( أن يغضب عليه ويقول أخرج عني ) ولو قال ذلك فلعلها كانت شبهة له وقول التيجاني هذا أعظم دليل على أن النبي صلى الله عليه وآله وسلم سكت عن قول عمر ولم يعترض عليه ولكن لما كثر اللغط والاختلاف قال ( دعوني ) وليس فيها ما يفيد الطرد والإخراج خاصةً إذا ما عرفنا أنه أوصاهم بعدها بثلاثة وصايا.

ثم يهذي التيجاني فيقول (( وهل لي أن أتساءل لماذا امتثلوا أمره عندما طردهم من الحجرة النبوية، ولم يقولوا بأنه يهجر؟ ألأنهم نجحوا بمخططهم في منع الرسول من الكتابة، فلا داعـي بعد ذلك لبقائهم، والدليل على أنهم أكثروا اللغـط والاختـلاف بحضرته (ص)، وانقسموا إلى حـزبين منهم من يقول: قربـوا إلى رسـول اللـه يكتب لكـم ذلك الكتاب ومنهم من يقول ما قال عمر أي أنه يهجر ))(20).

الله أكبر!؟ آلصحابة يخططون ضد محمد بن عبد الله صلى الله عليه وآله وسلم  ليمنعوه من الكتابة!!! فهذا والله اعتقاد من لم يدخل في قلبه حب وتوقير لصحابة النبي صلى الله عليه وآله وسلم الذين آزروه ونصروه واتبعوا النور الذي أنزل عليه، وأفدَوهُ بأرواحهم وأهليهم بل وبكل ما يملكون ففتح الله لهم الدنيا وأذل لهم جبابرة الأرض من الفرس والروم بسبب نصرتهم للنبي صلى الله عليه وآله وسلم ثم يأتي هذا الأنوك ليدعي أن الصحابة يخططون ضد من؟! رسول الله صلى الله عليه وآله وسلم !!؟ فإنها والله لإحدى الكبر فهل هذا هو المنطق السليم والعقلاني الذي أوصله إلى ما يخالف المعقول والمنقول؟!... سبحان الله أكلّ هذا التحريف ليحاول أن يجعل النص يخدم أهداف الرافضة الشنيعة للحط من الصحابة ولكن أَنّى لهم، ثم يعيد ويكرر حجته الخاوية على عروشها بأن عمر يقول بأنه يهجر ودون إطالة أقول الحقيقة ظاهرة والحمد لله.

ثم يدلل هذا المهتدي على أسباب هدايته فيقول (( والأمر لم يعد بتلك البساطة يتعلق بشخص عمر وحده ولو كان كذلك لأسكته رسول الله وأقنعه (!) بأنه لا ينطق عن الهوى ولا يمكن أن يغلب عليه الوجع في هداية الأمة وعدم ضلالتها ولكن الأمـر استفحل واستشرى ووجد له أنصاراً كأنهم متفقون مسبقاً (!)، ولذلك أكثروا اللغط والاختلاف ونسوا أو تناسوا (!) قول اللـه تعالى { ياأيها الذين آمنوا لا ترفعوا أصواتكم فوق صوت النبي ولا تجهروا له بالقول كجهر بعضكم لبعض أن تحبط أعمالكم وأنتم لا تشعرون }

فإن تعجب فعجب قولهم! فإذا كان النبي صلى الله عليه وآله وسلم يغضب على عمر ويقول له وللباقين اخرجوا عني ألا يستطيع أن يسكت عمر؟ وفي الحديث أنه أوصاهم بثلاث وصايا، وعدم إسكاته دليل على الموافقة له والرضا بما قال، أما أنهم أكثروا اللغط ونسوا أو تناسوا ( هكذا ) قول اللـه سبحانه ( الآية ) فأقول لهـذا التيجـاني: الصحـابة لم يرفعـوا أصواتهم فوق صوت النبي صلى الله عليه وآله وسلم بل رفعوا أصواتهم على بعضهم البعض وهـذا جـائز بدلالة الآية وعلى هذا فاحتجاجك السقيم ردٌ عليك.

ثم يخرج التيجاني أوضاره فيقول (( وفي هذه الحادثة تعدوا حدود رفع الأصوات والجهر بالقول إلى رميه (ص) بالهجر والهذيان  والعياذ بالله (!!) ثم أكثروا اللغط والاختلاف وصارت معركة كلامية بحضرته وأكاد أعتقد بأن الأكثرية الساحقة كانت على قول عمر ولذلك رأى رسول الله (ص) عدم الجدوى من كتابة الكتاب لأنه علم بأنهم لم يحترموه (!!) ولم يمتثلوا لأمر الله فيه في عدم رفع أصواتهم بحضرته، وإذا كانوا لأمر الله عاصين فلن يكونوا لأمر رسوله طائعين (!)، واقتضت حكمة الرسول بأن لا يكتب لهم ذلك الكتاب لأنه طعن فيه في حياته فكيف يعمل بما فيه بعد وفاته، وسيقول الطاعنون: بأنه هجر من القول ولربما سيشككون في بعض الأحكام التي عقدها رسول الله في مرض وفاته (!)، إذا اعتقادهم بهجره ثابت، أستغفر الله (!) وأتوب إليه من هذا القول في حضرة الرسول الأكرم (!!)، كيف لي أن أقنع نفسي وضميري الحر(!) بأن عمر بن الخطاب كان عفوياً في حين أن أصحابه ومن حضروا محضره بكوا لما حصل حتى بل دمعهم الحصى وسموها رزية المسلمين، ولهذا فقد خلصت إلى أن أرفض كل التعليلات التي قدمت لتوجيه ذلك، ولقد حاولت أن أنكر هذه الحادثة وأكذبها لأستريح من مأساتها (!) ولكن كتب الصحاح نقلتها وأثبتتها وصححتها ولم تحسن تبريرها ))(21)!

هاهو التيجاني يدلي بوعائه ليخرج لنا قيحه الذي سود به صفحات كتابه، ولم يدر أنه بكلامه هذا قد خلع ربقة الإسلام من عنقه! فكيف يدعي أن رسول الله صلى الله عليه وآله وسلم رأى عدم الجدوى من كتابة الكتاب واقتضت حكمته ذلك (( هكذا!! )) بحجة أن الصحابة ( لن ) يحترموه و( لن ) يمتثلوا أمره بالإضافة إلى طعنهم به!! ولو فرضنا ( اعتباطاً ) أن هذا حق فكيف يتوقف النبي صلى الله عليه وآله وسلم عن كتابة ما أمر ببلاغه وهو الرسول المبلغ عن رب العالمين؟ وليس هو مخيرٌ في ذلك والله يقول { يأيها الرسول بلغ ما أنزل إليك من ربك، وإن لم تفعل فما بلغت رسالته، والله يعصمك من الناس ...} ( المائدة 67) ويقول سبحانه { وما ينطق عن الهوى إن هو إلا وحي يوحى } ( النجم 3ـ 4) فلا بد للنبي صلى الله عليه وآله وسلم من التبليغ سواءٌ بالكتابة أو بالقول كما أمرهم بإخراج المشركين من جزيرة العرب وغيره، وادعاء التيجاني هذا هو طعن بالنبي صلى الله عليه وآله وسلم إذ كيف يتوقف عن التبليغ لمجرد الطعن به؟! ومن قرأ كتاب الله يعلم مدى جهل هذا التيجاني بحقيقة الرسالة لأن الرسل جميعاً تعرضوا من أقوامهم لشتى أنواع التعذيب الجسدية والنفسية فلم تثنيهم هذه العذابات عن المضي قدماً بتبليغ رسالة الله، ونبينا محمد صلى الله عليه وآله وسلم خاتم الأنبياء قد تعرض لأنواع من الاغراءات ثم التهديدات والتعذيب ليثنيه المشركون عن تبليغ رسالة السماء، فقاموا بالاعتداء عليه وعلى أصحابه وتعذيبهم وحاصروه وقومه بشعاب مكة ورموه بألقاب السخرية والاستهزاء كالساحر والمجنون فلم تقف هذه الضغوط في طريقه ليبلغ دين الله كاملاً غير منقوص وجاهد في سبيل الله مع أصحابه حتى مكن الله له في الأرض وجعل دينه يعلوا على كل الأديان وبذلك استحق أن يكون خير رسل الله أجمعين، ثم يأتي هذا الرويبض ليدعي على نبي المرحمة صلوات الله وسلامه عليه أنه توقف عن تبليغ أمر الله عاصماً للأمة من الضلالة! لماذا؟ لمجرد عدم احترامه وإطاعة أمره أو الطعن به يتراجع عن تبليغ ما أمر ببيانه! فحاشا نبينا صلى الله عليه وآله وسلم ذلك، فلا بد من أن يبلغ الرسالة وأن يظهر الحق وإن حاربه أهل الأرض جميعاً وليظهر أهل الحق من أهل الباطل ويعرف أولياءه من أعدائه، فمن اتبع أمر الله ورسوله نجا ومن خالف فقد هلك ولذلك أنزل الله الرسل مبشرين للناس ومنذرين، ومن هنا نعلم أن الذي أراد النبي صلى الله عليه وآله وسلم كتابته ليس وحياً بل على سبيل الاختيار ذلك لمن كان له قلب أو ألقى السمع وهوشهيد، ثم يدعي هذا التيجاني على الصحابة بأنهم لم يحترموا النبي صلى الله عليه وآله وسلم ولم يمتثلوا لأمره وطعنوا به!!؟ فيبدوا أن الكلام عند هذا التيجاني لا يشترى بالمال فلا غضاضة إذاً من تسويد الصفحات بالمجـازفات والافتراءات، فمرة يقول أن ابن عباس بكى وبل دمعه الحصى ومـرة يقول أن الصحابة بكوا حتى بل دمعهم الحصى وفي نفس الوقت يخططـون لمنـع النبي صلى الله عليه وآله وسلم من الكتابـة وأكثرهم كانوا على رأي عمر إلى آخر هذه التجنيات التيجانية!!